Shule Ambayo Hutusaidia Kutumia Mambo Tunayojifunza
1 Tunapochunguza habari iliyoonyeshwa katika Ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya 2006, tunapaswa kujitahidi kunufaika na mafundisho ya Biblia yatakayotolewa kwa kuyatumia katika utumishi wetu mtakatifu na katika maisha yetu ya kila siku. Tunaazimia kutumia mambo tunayojifunza.—Yoh. 13:17; Flp. 4:9.
2 Kutoa Maelezo: Ratiba ya mwaka huu inawapa wasikilizaji dakika moja zaidi ya kutoa maelezo katika mambo makuu ya Biblia. Hii inamaanisha kwamba ndugu aliyepewa mgawo wa kutoa mambo makuu anapaswa kuwa mwangalifu amalize sehemu yake kwa dakika tano badala ya dakika sita. Wale wanaotoa maelezo wanapaswa kuwa waangalifu pia wasipitishe wakati. Kwa kufikiria maelezo yake kimbele, yule anayetoa maelezo anaweza kutaja habari muhimu kwa sekunde 30 hivi. Kufanya hivyo kutawawezesha watu kumi hivi watoe maelezo katika ule muda wa dakika tano uliotengwa kwa kusudi hilo.
3 Hotuba Zinazofundisha: Mambo makuu ya Biblia na hotuba ya maagizo inapaswa kukazia jinsi habari hiyo inavyohusu huduma yetu na sehemu nyingine za maisha yetu ya kila siku. Msemaji hapaswi tu kuwachochea wasikilizaji wake watende. Anapaswa kuonyesha waziwazi hatua inayopaswa kuchukuliwa, jinsi inavyoweza kuchukuliwa, na kuonyesha faida za kufanya hivyo. Anaweza kusema, “Andiko hili linatoa mwongozo huu,” au “Tunaweza kutumia mistari hii kwa njia hii katika huduma.” Wazee na watumishi wa huduma wanaofahamu hali za kwao wanapaswa kujitahidi kuonyesha kihususa jinsi habari hiyo inavyoweza kutumiwa.
4 Kutaja mifano iliyo katika Biblia kunaweza kuwa na matokeo sana katika kuonyesha jinsi mambo tunayojifunza yanavyoweza kutumiwa. Baada ya kutaja mfano fulani katika Biblia, msemaji anaweza kusema, “Huenda wewe pia ukajikuta katika hali kama hiyo.” Anapaswa kuhakikisha kwamba mfano wowote wa Biblia unapatana na muktadha, Biblia nzima, na pia habari ambayo imechapishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45.
5 Hekima ni uwezo wa kutumia ujuzi na uelewaji kwa mafanikio. “Hekima ndilo jambo kuu.” (Met. 4:7) Tunapoendelea kujipatia hekima kupitia mambo tunayojifunza katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, na tuboreshe pia uwezo wetu wa kuwapa wengine hekima.