SOMO LA 23
Kuonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia Habari
IWE unazungumza na mtu mmoja au watu wengi, si vizuri kudhani wasikilizaji watapenda habari yako eti kwa sababu unaipenda. Ingawa ujumbe wako ni muhimu, baada ya muda watu wanaweza kuacha kukusikiliza ikiwa huwaonyeshi faida yake.
Ndivyo ilivyo pia na wasikilizaji katika Jumba la Ufalme. Wanaweza kusikiliza unapotumia mfano au unaposimulia tukio ambalo hawajasikia. Lakini wanaweza kuacha kukusikiliza unapozungumzia mambo ambayo tayari wanajua, hasa ukikosa kujenga hotuba yako juu ya mambo hayo. Unahitaji kuwasaidia waone kwa nini habari hiyo ina faida na pia inawafaidi kwa njia gani.
Biblia inatuhimiza tufikiri kwa njia inayofaa. (Mit. 3:21) Yehova alimtumia Yohana Mbatizaji kuwaonyesha watu “hekima itumikayo ya walio waadilifu.” (Luka 1:17) Hekima hii inategemea kumcha Yehova. (Zab. 111:10) Wale wanaotambua hekima hii husaidiwa kukabiliana kwa mafanikio na maisha wakati huu, na kushika uhai halisi na wa milele wa wakati ujao.—1 Tim. 4:8; 6:19.
Kuwaonyesha Wasikilizaji Jinsi ya Kutumia Habari. Ili hotuba yako ifaidi wasikilizaji, mbali na kuifikiria hotuba hiyo wafikirie wasikilizaji. Usiwafikirie tu kwa ujumla. Miongoni mwa wasikilizaji hao mna watu mmoja-mmoja na familia tofauti-tofauti. Huenda kuna watoto wadogo sana, vijana, watu wazima, na wengine ambao ni wazee. Huenda pia miongoni mwao mna wale wanaopendezwa na wale ambao walianza kumtumikia Yehova kabla ya wewe kuzaliwa. Huenda wengine wamekomaa kiroho, na huenda wengine bado wana mielekeo na hali fulani za kilimwengu. Jiulize: ‘Hotuba hii itawasaidiaje wasikilizaji? Nawezaje kuwasaidia kuelewa jambo ambalo nitazungumzia?’ Unaweza kuamua kukazia akili kikundi kimoja au vikundi viwili kati ya vikundi ambavyo tumetaja. Lakini usiwasahau wengine kabisa.
Ufanyeje ukipewa hotuba inayozungumzia fundisho fulani la msingi la Biblia? Unaweza kufanya nini ili hotuba kama hiyo iwafaidi wasikilizaji ambao tayari wanafahamu fundisho hilo? Jaribu kuimarisha usadikisho wao kulihusu. Kwa njia gani? Kwa kutoa sababu za Maandiko zinazolithibitisha. Pia unaweza kuzidisha uthamini wao kuhusu fundisho hilo la Biblia. Unaweza kuzidisha uthamini wao kwa kuwaonyesha jinsi fundisho hilo linavyopatana na kweli nyinginezo za Biblia na jinsi linavyopatana na utu wa Yehova. Tumia mifano au ikiwezekana simulia matukio halisi maishani yanayoonyesha jinsi ambavyo watu wengine wamefaidika na kubadili maoni yao juu ya wakati ujao walipoelewa fundisho hilo.
Usieleze kwa ufupi tu jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo mwishoni mwa hotuba yako. Tangu mwanzoni kabisa, kila msikilizaji anapaswa kuona kwamba “habari hii inanihusu.” Baada ya kuweka msingi huo, endelea kuwaonyesha jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo unapokuza kila moja ya mambo makuu ya hotuba na pia unapomalizia hotuba.
Unapowaeleza akina ndugu jinsi wanavyoweza kutumia habari hiyo, fuata kanuni za Biblia. Hiyo inamaanisha nini? Inamaanisha kuwa mwenye upendo na hisia-mwenzi unapowaeleza jinsi wanavyoweza kutumia habari unayozungumzia. (1 Pet. 3:8; 1 Yoh. 4:8) Hata mtume Paulo alipokuwa akishughulikia matatizo mazito katika Thesalonike, alihakikisha ametaja maendeleo mazuri ya kiroho ya ndugu na dada zake Wakristo waliokuwa huko. Pia alionyesha ana hakika kwamba wanataka kufanya yaliyo sawa kuhusu jambo alilokuwa akizungumzia. (1 The. 4:1-12) Huo ni mfano mzuri sana ambao tunaweza kuuiga.
Je, kusudi la hotuba yako ni kuchochea akina ndugu ili wahubiri na kufundisha wengine habari njema? Basi wasaidie wawe na shauku na kuthamini pendeleo hilo. Lakini wakati uo huo ukumbuke kwamba watu wana uwezo tofauti-tofauti, na hata Biblia inaonyesha hivyo. (Mt. 13:23) Usiwafanye akina ndugu wahisi hatia. Waebrania 10:24 linatuhimiza ‘tuchocheane kwenye upendo na kazi zilizo bora.’ Tukiwachochea kwenye upendo, watatenda kwa makusudio mazuri. Badala ya kuwaamuru-amuru, tambua kwamba Yehova anataka tuwachochee ‘watii kwa njia ya imani.’ (Rom. 16:26) Basi, tukikumbuka mambo haya tutajaribu kuimarisha imani yetu na imani ya wengine.
Kuwasaidia Wengine Kuona Faida ya Ujumbe Wetu. Unapohubiri, usisahau kuonyesha faida ya habari njema maishani mwao. Ili ufaulu, unahitaji kufahamu mambo yanayowahangaisha watu katika eneo lenu. Unawezaje kujua mambo hayo? Sikiliza habari kwenye redio au televisheni. Tazama ukurasa wa mbele wa gazeti la habari. Pia jaribu kuwafanya watu wazungumze, na uwasikilize wanapoongea. Unaweza kugundua wana matatizo makubwa kama vile kupoteza kazi, kulipa kodi ya nyumba, ugonjwa, kifo cha mshiriki wa familia, kupatwa na uhalifu, kutendwa isivyofaa na mtu mwenye mamlaka, kuvunjika kwa ndoa, kuwadhibiti watoto, na kadhalika. Je, Biblia inaweza kuwasaidia? Bila shaka, ndiyo.
Inaelekea kwamba unapoanzisha mazungumzo utakuwa na jambo fulani akilini unalotaka kusema. Lakini ukiona kwamba mtu huyo ana jambo jingine linalomhangaisha sana, usisite kuzungumza naye jambo hilo ikiwezekana, au mwambie utamletea habari ambazo zinaweza kumsaidia. Ingawa tunaepuka ‘kujiingiza katika lile lisilotuhusu,’ tunafurahi kuwapa wengine mashauri ya Biblia ambayo wanaweza kutumia. (2 The. 3:11) Ni wazi kwamba jambo linalowavutia watu zaidi ni shauri la Biblia linalohusu maisha yao.
Watu wasipoona jinsi ujumbe wetu unavyowahusu, wanaweza kukatiza mazungumzo haraka. Hata wakituruhusu tuendelee kuzungumza, tukikosa kuwaonyesha faida ya habari hiyo hawatafaidika. Lakini tukiwaonyesha faida ya ujumbe wetu, mazungumzo yetu yanaweza kubadili maisha yao.
Unapofundisha watu Biblia, endelea kukazia jinsi wanavyoweza kutumia habari wanayojifunza. (Mit. 4:7) Wasaidie wanafunzi waelewe shauri, kanuni, na mifano inayopatikana katika Maandiko ambayo inawaonyesha jinsi ya kufuata njia za Yehova. Kazia faida ambazo watapata. (Isa. 48:17, 18) Kufanya hivyo kutawachochea wanafunzi wafanye mabadiliko yanayotakikana katika maisha yao. Wasaidie wampende Yehova na kuwa na tamaa ya kumpendeza, na pia wasaidie wachochewe na moyo wao wenyewe kutumia shauri la Neno la Mungu.