Vijana Wanaoangaza Kama Mianga
1 Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Ninyi ndio nuru ya ulimwengu.” (Mt. 5:14, 16) Wanafunzi hao wangeonekana wazi kama mji ulio juu ya mlima wakati wa mchana. Leo, vijana wengi Wakristo ‘wanaangaza kama mianga katika ulimwengu’ kwa mwenendo wao mzuri na bidii yao ya kuhubiri.—Flp. 2:15; Mal. 3:18.
2 Shuleni: Unaweza kuhubiri shuleni kwa njia gani? Vijana fulani wamehubiri wakati wa mazungumzo ya darasani wanapofundishwa kuhusu dawa za kulevya, mageuzi, yale maangamizi wakati wa utawala wa Nazi, na mambo mengineyo. Dada fulani alipoombwa aandike insha kuhusu ugaidi, aliandika kuhusu Ufalme wa Mungu na kuonyesha kwamba huo ndio tumaini pekee la wanadamu. Mwalimu alivutiwa sana na maelezo yake mazuri na hivyo dada huyo akapata nafasi ya kuhubiri.
3 Tunaweza pia kuangaza kama mianga kwa mwenendo wetu mzuri na kwa kuvaa na kujipamba kwa kiasi. (1 Kor. 4:9; 1 Tim. 2:9) Walimu na wanafunzi wanapoona mwenendo wako ulio tofauti, huenda baadhi yao wakavutiwa na mwenendo wako mzuri na unaweza kupata nafasi ya kuwahubiria kweli za Biblia. (1 Pet. 2:12; 3:1, 2) Kudumisha mwenendo mzuri wa Kikristo si jambo rahisi, lakini utabarikiwa sana na Yehova ukifanya hivyo. (1 Pet. 3:16, 17; 4:14) Ili kuwafanya wengine wapendezwe na habari njema, wakati wa mapumziko, unaweza kusoma vitabu vya kujifunzia Biblia au kuviweka mahali wanapoweza kuviona.
4 Kuacha nuru yako iangaze ukiwa shuleni kunaimarisha imani yako na kukufanya ujivunie kumtumikia Yehova. (Yer. 9:24) Pia, kufanya hivyo kunakulinda. Dada mmoja alisema: “Faida moja ya kuhubiri ni kwamba wanafunzi hawanishawishi nifanye mambo yasiyopatana na Biblia.”
5 Kupanua Utumishi: Vijana wanaangaza kama mianga kwa njia nyingine pia, yaani, kwa kupanua utumishi wao. Baada ya kumaliza shule ya sekondari, ndugu fulani alihamia eneo lenye uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Alishirikiana na kutaniko dogo lililokuwa na mzee mmoja tu. “Ninafurahia maisha kwelikweli,” akamwandikia rafikiye. “Utumishi unaburudisha sana! Kwa kuwa wenye nyumba wanataka sana kutusikiliza, kwa kawaida tunazungumza nao kwa dakika 20 hivi.” Anaongezea: “Laiti kila kijana angechukua hatua kama yangu na kuhisi jinsi ninavyohisi. Hakuna kitu kilicho bora kuliko kumtumikia Yehova kwa vyote tulivyo navyo.”
6 Tunajivunia sana ninyi vijana mnaoangaza kama mianga katika ulimwengu! (1 The. 2:20) Mkimtumikia Yehova kwa moyo wote, nafsi yote, akili yote, na nguvu zote, mtapata “mara mia sasa katika kipindi hiki cha wakati . . . na katika mfumo wa mambo unaokuja uzima wa milele.”—Marko 10:29, 30; 12:30.
[Maswali ya Funzo]
1. Biblia inaonyeshaje kwamba Wakristo wangeonekana wazi, na maneno hayo yanahusuje vijana Wakristo leo?
2. Unaweza kuwahubiria walimu na wanadarasa wenzako kwa njia gani?
3. Unaweza kuangazaje kwa mwenendo wako ukiwa shuleni?
4. Kuna faida gani za kuhubiri shuleni?
5. (a) Vijana fulani wanapanuaje huduma yao? (b) Una miradi gani ya kiroho?
6. Unajivunia jambo gani kuwahusu vijana wa kutaniko lenu?