Tunza
Mheshimu Yehova Katika Maisha Yako
Sehemu ya 2—Jihadhari na Mapokeo Yasiyo ya Kikristo
1, 2. Je, mapokeo yote ni mabaya? Eleza.
1 Mtume Petro aliandika hivi: “Wapendwa, kwa kuwa mnangojea mambo hayo, fanyeni yote mnayoweza ili mwishowe yeye awapate ninyi mkiwa bila doa na bila dosari na mkiwa katika amani.” (2 Pet. 3:14) Kwa kutii shauri hilo, Mashahidi wa Yehova hawajihusishi na mapokeo yasiyo ya Kikristo. Wale ambao sasa wanajifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova wanaweza kukumbuka baadhi ya mapokeo yanayotajwa katika Somo la 11 la broshua Mungu Anataka Tufanye Nini?
2 Kwa kweli, kuna mapokeo mazuri ambayo yanapatana na kanuni za Biblia. Baadhi yake ni, ukarimu, kuheshimu wazee, na kuwasaidia wenye uhitaji. Mara nyingi, mapokeo mengine kama vile mitindo fulani ya mavazi au salamu za aina fulani, hayavunji kanuni za Biblia. Hata hivyo, kuna mapokeo mengi ambayo humchukiza Mungu wa kweli. Mapokeo hayo yanaweza kuorodheshwa pamoja na ‘mwenendo usiozaa matunda ambao ulipokewa kwa njia ya mapokeo kutoka kwa mababu zenu,’ ambao Petro alionya Wakristo wa mapema wajihadhari nao. (1 Pet. 1:18) Tunapaswa kutii onyo hili la Paulo: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia . . . udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu . . . na si kulingana na Kristo.” (Kol. 2:8) Na tuzungumzie mapokeo machache katika eneo letu.
Tohara
3, 4. (a) Tohara ya wanaume ilikuwa na umuhimu gani katika Israeli la kale? (b) Taja baadhi ya tohara ambazo humchukiza Yehova.
3 Biblia haikatazi kuwapasha wanaume tohara. Kwa kweli, tohara ilikuwa sehemu ya Sheria ya Yehova kwa Waisraeli, na hadi kifo cha Yesu, mwanamume ambaye hakuwa ametahiriwa alionwa kuwa asiye safi. Hata hivyo, Sheria ilikuwa tu ‘mtunzaji wa kutuongoza kwa Kristo.’ Leo, tohara ya wanaume haina umuhimu wowote wa kipekee machoni pa Mungu na si takwa la Kikristo.—Gal. 3:24; 5:6.
4 Kwa hiyo, wazazi wakiamua kutahiri wana wao, labda kwa sababu za kiafya, huo ni uamuzi wa kibinafsi. Hata hivyo, katika maeneo fulani kunakuwa na wakati hususa wa kutahiri wavulana wa rika fulani. Karamu zenye nyimbo na dansi hupangwa ili kutukuza wavulana waliotahiriwa na kuonwa kuwa watu wazima. Sherehe hizo ni za kidini, na Mkristo hangependa kamwe kushiriki katika mazoea hayo yanayomvunjia Mungu heshima.
5. Kuwapasha wasichana tohara hutokeza hatari zipi?
5 Vipi kuwapasha wasichana tohara? Desturi hii ya kuondoa sehemu ya kiungo cha uzazi cha msichana, inaendelea katika nchi kadhaa za Afrika. Kuna njia mbalimbali za kuwapasha wanawake tohara. Vyovyote vile, tohara huwafanya wasichana wachanga wateseke vibaya sana bila sababu. Gazeti moja linaripoti hivi: “Matatizo ya kawaida ambayo huwapata wasichana mara tu baada ya kutahiriwa yanatia ndani maumivu makali, mshtuko, kuvuja damu, kujeruhiwa kwa viungo vilivyo karibu na viungo vya uzazi, maambukizo, na kifo.” Kwa kweli, wazazi Wakristo hawangetaka binti zao wapatwe na mambo hayo mabaya! Pia jambo la kufikiriwa hata zaidi ni kwamba zoea hilo linahusiana na ibada ya kipagani.
6. Kuna kanuni gani za Biblia zinazohusu kuwapasha wanawake tohara?
6 Kuwapasha wanawake tohara hufanya wasifurahie ngono, hata ingawa Yehova alimuumba mwanamke afurahie ngono na mume wake. Inadaiwa kwamba kuwapasha wanawake tohara huwasaidia kulinda ubikira wao wakiwa waseja. Hata hivyo, msichana anaweza kulinda ubikira wake kwa kusitawisha maadili ya Kikristo na si kwa kukata sehemu fulani ya mwili wake. Toleo la Amkeni! la Aprili 8, 1993, lilisema hivi: “Matendo yasiyofaa yaweza kuzuiwa kwa elimu, si kwa kuchinja. Ili kutoa kielezi: Je! twapaswa kukata mikono ya watoto ili wasije kuwa wevi? Au tukate ndimi zao ili wasiseme mambo mabaya kamwe?” Kukata kiungo cha uzazi cha msichana ni hatari na kunaweza kumfanya mtu awe na hatia ya damu. (1 Nya. 11:17-19; Zab. 51:14) Mtu yeyote anayeunga mkono desturi hiyo ya kikatili hamheshimu Yehova, ambaye ndiye “chemchemi ya uhai” na Mpaji wa “kila zawadi njema.” Isitoshe, mahali ambapo desturi hiyo imepigwa marufuku na serikali, wazazi Wakristo wanapaswa kuheshimu sheria. (Zab. 36:9; Yak. 1:17; Rom. 13:1) Wazazi Wakristo ambao wanakubali binti zao wapashwe tohara huenda wasistahili mapendeleo ya pekee ya utumishi katika kutaniko. Vivyo hivyo, huenda dada mseja anayekubali kupashwa tohara asistahili kupewa mapendeleo.
Hirizi
7. Kuvaa hirizi kunahusianishwa na nini?
7 Katika historia yote, watu wamekuwa wakivaa hirizi ili kujilinda na maovu. Hirizi fulani hutengenezwa kwa manyoya ya wanyama, mifupa, meno, au kucha. Nyingine hutengenezwa kwa chuma, kitambaa, shanga, au mimea. Katika Misri ya kale, shanga na hirizi zilivaliwa kwa ukawaida kwa makusudi ya kuwasiliana na roho.
8. Ni maswali gani yanayotusaidia kuona hatari zinazohusiana na kuvaa hirizi?
8 Ikiwa Mkristo ana vitu kama hivyo, anaweza kujiuliza hivi: ‘Kwa nini nina hirizi? Je, ninaamini kwamba zinanilinda dhidi ya magonjwa, misiba, laana, au roho waovu? Wengine watakuwa na maoni gani wanaponiona nikivaa vitu hivyo? Watu wa ukoo wakiona watoto wangu wamevaa vitu hivyo, je, hilo halitawachochea wajaribu kunishirikisha katika mazoea mengine ya kipagani?’ Vitu hivyo havimlindi mtu. Badala yake, vinaweza kumfanya mtu ashambuliwe na mashetani au ajihusishe kabisa na roho waovu. Hirizi si mapambo tu. Zinahusianishwa na ibada ya roho waovu, jambo ambalo huathiri uhusiano wetu na Yehova.—Kum. 18:10-12; Gal. 5:19-21; Ufu. 21:8.
Mahari na Arusi
9. (a) Wazazi Wakristo wanapaswa kuongozwa na kanuni gani wanapojadiliana kuhusu mahari? (b) Kwa nini ndugu hapaswi kuruhusu watu wa ukoo wasioamini wapange mambo ya mahari binti yake anapoolewa?
9 Biblia inasema kwamba wazazi wa msichana walipewa zawadi. Walipokuwa wakijadiliana kuhusu ndoa ya Rebeka na Isaka, mtumishi wa Abrahamu ‘alianza kutoa vyombo vya fedha na vyombo vya dhahabu na mavazi.’ (Mwa. 24:53) Aliwapa Rebeka, mama yake, na ndugu yake vitu hivyo, kwani wao ndio waliokuwa washiriki wa karibu wa familia. Biblia haionyeshi kwamba watu wengine wa ukoo walipewa mahari. Basi, je, wazazi Wakristo wanapaswa kuruhusu washiriki wa familia wasioamini watawale majadiliano kuhusu mahari? Katika visa fulani, watu hao wamedai mahari kubwa sana au wamejaribu “kuuza” binti yao kwa mtu atakayewalipa kiasi kikubwa zaidi cha mahari. Wazazi wenye hekima huepuka mtazamo wa kufuatia vitu vya kimwili na hutafuta mwana-mkwe anayempenda Yehova na ambaye ni Mkristo mwenye bidii, anayeishi kupatana na kweli.
10. Taja desturi fulani zinazoweza kuchafua arusi ya Mkristo.
10 Arusi za Kikristo zinapaswa kumtukuza na kumheshimu Mwanzilishi wa ndoa, Yehova Mungu. Paulo aliwashauri hivi waamini: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.” (1 Kor. 10:31) Wakristo hawangependa arusi ya mshiriki wa familia ilete suto kwa Yehova au kutaniko lake. Arusi ya Mkristo haipaswi kuwa udhuru wa kujihusisha na sherehe zenye kelele za ulevi. Katika sehemu fulani za Afrika, arusi nyingi huwa na muziki au dansi zinazotukuza sherehe za ibada ya uzazi, kurushiwa mchele au desturi nyingine za kipagani. Desturi kama hizo hazipaswi kufanywa katika arusi za Wakristo.
11. Wazee wanapaswa kuwa waangalifu kuhusu nini sherehe ya arusi inapofanywa kwenye Jumba la Ufalme?
11 Ikiwa Jumba la Ufalme litatumiwa kwa ajili ya sherehe ya arusi, lazima wazee wawe waangalifu sana. Wazee wanapaswa kuhakikisha kwamba mipango ya arusi haipingani na kanuni za Kikristo. Kwa hiyo, gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1984 lilitoa shauri hili: “Kwenye Jumba hilo [la Ufalme], muziki wenye kujenga peke yake, kama ule unaopatikana katika kitabu cha nyimbo cha Mashahidi wa Yehova, ndio unaotumiwa. Maua yo yote au mapambo kama hayo yapasa kuwa ya kiasi, ndivyo pia na jinsi ambavyo msafara wa arusi unaingia kwenye Jumba na jinsi picha zinavyopigwa.—Wafilipi 4:5.” Vipi wale waliochaguliwa kuwa kwenye msafara wa arusi? Gazeti hilohilo liliongeza kusema hivi: “Hata hivyo, kiasi kinahitajiwa juu ya ni wangapi watakuwa kati ya washiriki hao, na pia jinsi wanavyovaa na kutenda. Haingefaa kuweka katika msafara wa arusi watu ambao wametengwa na ushirika au wale ambao mtindo wao wa maisha wenye kuudhi unapingana sana na kanuni za Biblia. (2 Wakorintho 6:14-16) Badala ya kuchagua watu ambao ni mashuhuri au ambao huenda wakatoa zawadi ya pesa nyingi, wenzi wengi Wakristo (na wasemaji) wanapendelea katika msafara kuwemo watu ambao wako karibu nao katika kumtumikia Yehova.”
12. Mtu anapopanga arusi anaweza kuonyeshaje sifa ya kiasi na usawaziko wa Kikristo?
12 Mwanamume na mwanamke watahitaji kufanya maamuzi mengi wanapopanga arusi yao. Maamuzi hayo yatatia ndani aina na rangi ya nguo watakazovaa, pete za arusi, au idadi ya watu watakaoalika kwenye arusi. Bila shaka, wahusika hao wataonyesha kiasi na usawaziko wa Kikristo kuhusiana na maamuzi hayo. Kwa mfano, ni jambo la kawaida kwa watu fulani wa ulimwengu kuwa na msafara wa magari yaliyopambwa na kuwa na vifijo na vigelegele. Mkristo anapaswa kuwa na maoni gani kuhusu hilo? Gazeti Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 1997, lilisema hivi: “Ijapokuwa Yesu alihudhuria arusi, hatuwezi kuwazia kwamba angekubali desturi ipendwayo ya kuwa na msafara wa magari kupitia mjini kwa kelele nyingi; polisi hata wamewatoza faini madereva kwa kupiga honi kwenye msafara wa arusi. (Ona Mathayo 22:21.) Kwa kifupi, badala ya kuiga wonyesho wa kujivuna au matendo ya kawaida ya watu wa mataifa, Wakristo hudhihirisha hekima iliyo mali ya mtu mwenye kiasi.”
Makesha na Mazishi
13. (a) Je, ni vibaya kuhuzunika au hata kulia mpendwa anapokufa? (b) Ni desturi gani za kuomboleza ambazo hazingemfaa mtu anayeamini ufufuo?
13 Sote huhisi tumepoteza rafiki mzuri mtu fulani tumpendaye anapokufa. Yaelekea kwa sababu ya kuhuzunika sana Mkristo anaweza kulia, kama vile tu mwanadamu mkamilifu Yesu ‘alivyotokwa na machozi’ alipoandamana na watu waliokuwa wakiomboleza kifo cha rafiki yake Lazaro. (Yoh. 11:35) Lakini, hata Wakristo wanapohuzunika, wanaepuka desturi za maombolezo ambazo hufanywa katika sehemu nyingi za Afrika. Desturi fulani zinatia ndani kung’oa nywele au kuinyoa kabisa, kuvaa nguo chafu na kujitupa chini, kufanya ishara kubwa kwa mikono, na kulia pamoja na wengine kama kwaya. Tukiwa Wakristo wa kweli, kuepuka desturi hizo za kuomboleza zinazopita kiasi huonyesha kwamba tuna imani thabiti huku tukitazamia wakati ambapo wapendwa wetu waliokufa watafufuliwa.—Ayu. 14:14, 15; Yoh. 5:28, 29; Mdo. 24:15.
14. Makesha huathirije familia iliyofiwa?
14 Katika sehemu nyingi ni jambo la kawaida kuwa na makesha kabla ya mazishi. Watu wengi hukesha pamoja usiku kucha, labda wakiimba, kulia, au kunywa kileo. Desturi hizo hutokeza gharama kubwa. Vyakula hununuliwa au wanyama huchinjwa, mahema hukodiwa na usafiri kugharimiwa. Mambo hayo yanaweza kufanya familia iliyofiwa iwe na madeni mengi na pia ijihusishe na mwenendo usio wa Kikristo. Si lazima iwe hivyo! Kuepuka kabisa mapokeo hayo yaliyokita mizizi kunaweza kumfanya mtu ateswe na wanadamu, lakini huleta thawabu kutoka kwa Mungu.—2 Tim. 1:7.
15, 16. Ni mambo gani huamua mahali ambapo mtu atazikwa?
15 Vipi mahali pa kumzika mtu? Fikiria mifano kadhaa ya Biblia. Abrahamu alitumia mali zake kununua shamba la kuzika washiriki wa familia yake. (Mwa. 23:3-20; 25:9; 49:29-32) Yosefu alimheshimu baba yake kwa kusafirisha mwili wake hadi Kanaani ukazikwe. Yaonekana, Farao alimruhusu Yosefu kutumia mali ya Serikali ili kutimiza mapenzi ya baba yake.—Mwa. 47:29, 30; 50:6-13.
16 Siku hizi, washiriki wa familia wa karibu ndio wenye daraka la kupanga mazishi. Kwa kadiri fulani, huenda mahali pa kumzika mtu pakategemea sheria za nchi. Ni jambo la kawaida kwa watu fulani kusafirisha maiti hadi mahali ambapo mtu alizaliwa ili kumzika. Kila familia inapaswa kuamua jambo hilo baada ya kufikiria gharama zinazohusika. (Luka 14:28) Wengine hujisumbua sana na kugharimika sana kwa kusafirisha maiti hadi mahali fulani—kwa kawaida mahali ambapo mtu huyo alizaliwa—ingawa kuna mahali pa kuzika watu karibu na wanapoishi. Kwa nini? Watu wengi huamini kwamba mtu anaweza kuendeleza uhusiano wake na mababu waliokufa anapozikwa kwenye udongo uleule waliozikwa. Tukiwa Wakristo uamuzi wetu hautegemei imani kama hizo.—Mhu. 9:5, 10.
17. Wakristo wanapaswa kuepuka desturi gani za maombolezo zisizopatana na Biblia?
17 Mwanamke Mkristo anapaswa kuwa thabiti kuhusiana na desturi fulani za kitamaduni ambazo humtaka mwanamke aliyefiwa na mume “arithiwe” na jamaa zake wa kiume wakati wa maombolezo. Hilo hukiuka kabisa viwango vya juu vya Yehova vya maadili na vilevile ni hatari kwa afya ya mwanamke. Mwanamke Mkristo hawezi kamwe kukubali jambo hilo.
18. (a) Mkristo akiombwa atoe hotuba ya mazishi, anapaswa kufikiria nini? (b) Wakristo wengine wanawezaje kuiheshimu familia iliyofiwa?
18 Kwa kawaida, Mashahidi wa Yehova hupanga kuwe na hotuba ya mazishi inayotegemea Biblia. Mkristo akiombwa atoe hotuba hiyo, atafuata muhtasari wa hotuba hiyo na kuepuka kushirikiana na wasemaji wengine ambao huenda wakafuata mapokeo yasiyo ya Kikristo au kuzungumzia mafundisho yasiyo ya Biblia. Mazishi yanapaswa kuwa sahili, yenye kufariji, na ya heshima. Hotuba ya mazishi, ambayo kwa kawaida hutolewa wakati wa mazishi inatosha kuwatia moyo kiroho waliofiwa na marafiki wengine. Ingawa ni jambo la upendo kutembelea aliyefiwa pindi kwa pindi, hakuna haja ya kumtembelea nyumbani na kukaa kwa muda mrefu huku akina ndugu na dada wakiimba nyimbo za Ufalme. Kwa kurahisisha mipango ya mazishi, gharama nyingi zisizo za lazima zinaweza kuepukwa na mara nyingi msaada unaotolewa na akina ndugu wakati huo unaweza kushughulikia gharama hizo. Hakuna haja ya kuwa na ‘hazina ya mazishi’ kwenye makutaniko au pesa za kutumiwa hali ya dharura inapotokea.
19. (a) Ni nini kitakachotusaidia kuchukua msimamo unaofaa kuhusu desturi na mapokeo yanayopendwa? (b) Kwa nini umeazimia kujitenga na ulimwengu usiomwogopa Mungu?
19 Tunapomtumikia Yehova katika ulimwengu usiomjua, ni wazi kwamba matatizo yatatokea. Hata hivyo, haiwezekani kutunga sheria kuhusu kila hali. Hata hivyo, ni muhimu kusali kwa Yehova na kumwomba hekima na ufahamu tunapofanya maamuzi na kushughulikia hali mbalimbali. (Yak. 1:5) Wazee wa kutaniko watafurahi kuzungumza nasi kuhusu kanuni za Biblia ili kutuimarisha tufanye maamuzi mazuri. Kwa kumheshimu Yehova katika maisha yetu, tutajitunza “katika upendo wa Mungu . . . kwa kutazamia uzima wa milele.”—Yuda 21; 2 Pet. 3:13.
Bakini Katika Upendo wa Mungu