Mradi Mzuri kwa Ajili ya Mwaka Mpya wa Utumishi
1 Ili tufanye maendeleo ya kiroho, lazima tuwe na miradi. Umejiwekea miradi gani kwa ajili ya mwaka mpya wa utumishi? Mradi mmoja bora ni kufanya upainia msaidizi kwa mwezi mmoja au zaidi. Kwa kuwa utendaji huo wenye kufurahisha unahitaji kupangiwa mapema, sasa ndio wakati mzuri wa kuanza kufanya mipango. Kwa nini tufikirie kujiwekea mradi wa kufanya upainia msaidizi?
2 Sababu za Kufanya Upainia Msaidizi: Upainia msaidizi hutuwezesha kumpendeza Baba yetu wa mbinguni “kwa ukamili zaidi” kwa kuongeza muda tunaotumia katika huduma. (1 The. 4:1) Tunapofikiria yote ambayo Yehova ametufanyia, mioyo yetu hutuchochea kuwaeleza wengine kumhusu. (Zab. 34:1, 2) Yehova huona na kuthamini jinsi tunavyojidhabihu ili kufanya mengi zaidi katika huduma. (Ebr. 6:10) Tunapata shangwe kubwa tunapojua kwamba bidii yetu inampendeza Yehova.—1 Nya. 29:9.
3 Kwa kawaida, kadiri unavyoendelea kufanya jambo fulani, ndivyo linavyokuwa rahisi zaidi na lenye kufurahisha zaidi. Kutumia wakati mwingi katika huduma kutafanya uwe na uhakika zaidi unapohubiri nyumba kwa nyumba. Utakuwa stadi zaidi katika kuanzisha mazungumzo na katika kutumia Biblia. Kadiri unavyozungumza kuhusu imani yako, ndivyo itakavyokuwa yenye nguvu zaidi. Wengi ambao hawakuwa wakiongoza funzo la Biblia waliweza kuanzisha funzo walipokuwa wakifanya upainia msaidizi.
4 Kufanya upainia msaidizi kunaweza pia kukuchochea uache kuzembea kiroho. Ndugu mmoja ambaye hapo zamani alikuwa painia wa kawaida aliamua kufanya upainia msaidizi kwa mwezi mmoja kwa sababu alitambua kwamba anatumia wakati mwingi kupita kiasi katika kazi yake ya kimwili. Alisema hivi: “Sikuamini jinsi nilivyotiwa nguvu kiroho katika mwezi huo mmoja! Nilifanya mipango ili nifanye upainia msaidizi kwa kuendelea, na hilo lilinisaidia kurudia upainia wa kawaida.”
5 Shinda Vizuizi: Wengine wanaweza kusita kuwa mapainia-wasaidizi kwa sababu wanahisi hawana ustadi wa kuhubiri. Ikiwa hilo linakuzuia, Yehova anaweza kukusaidia kama alivyomsaidia Yeremia. (Yer. 1:6-10) Ingawa Musa alikuwa na ‘kinywa kizito na ulimi mzito,’ Yehova alimtumia kutimiza mapenzi Yake. (Kut. 4:10-12) Ukihisi huna ustadi wa kutosha, mwombe Yehova akupe ujasiri.
6 Je, wewe husita kuwa painia-msaidizi kwa sababu ya matatizo ya afya au shughuli nyingi? Ikiwa wewe ni dhaifu kimwili, unaweza kufanya upainia msaidizi ukipanga ratiba kulingana na hali yako. Ikiwa una shughuli nyingi, huenda unaweza kupanga kufanya mambo yasiyo ya lazima mwezi mwingine. Wengine wanaofanya kazi kwa muda wote wamefaulu kununua wakati wa kufanya upainia msaidizi kwa kuchukua likizo ya siku moja au mbili.—Kol. 4:5.
7 Jinsi ya Kufaulu: Sali kuhusu tamaa yako ya kufanya upainia msaidizi. Mwombe Yehova abariki jitihada zako za kuongeza huduma yako. (Rom. 12:11, 12) Anaweza kukusaidia kufanya maamuzi ya hekima kuhusu jinsi ya kurekebisha ratiba yako. (Yak. 1:5) Ikiwa huna tamaa hiyo, mwombe Yehova akusaidie kupata shangwe katika kazi ya kuhubiri.—Luka 10:1, 17.
8 Zungumzeni mkiwa familia kuhusu mradi wa upainia msaidizi. (Met. 15:22) Labda mshiriki mmoja wa familia anaweza kufanya upainia msaidizi akisaidiwa na wengine katika familia. Zungumza pamoja na wengine kutanikoni kuhusu tamaa yako ya kufanya upainia, hasa wale walio na hali kama zako. Hilo linaweza kukuchochea zaidi kufanya upainia msaidizi.
9 Unapochunguza ratiba yako ya huduma kwa ajili ya mwaka mpya wa utumishi, unafikiri unaweza kufanya upainia msaidizi wakati gani? Ikiwa unafanya kazi ya muda wote au ungali shuleni, unaweza kufikiria miezi yenye sikukuu au yenye Jumamosi tano au Jumapili tano. Kwa mfano, miezi ya Septemba, Desemba, Machi, na Agosti ina Jumamosi tano na Jumapili tano. Mwezi wa Mei una Jumamosi tano, na wa Juni una Jumapili tano. Ikiwa una matatizo ya afya, fikiria miezi ambayo hali ya hewa huwa shwari. Unaweza pia kufikiria kufanya upainia mwezi ambao mwangalizi wa mzunguko atatembelea kutaniko lenu. Wakati wa ziara yake, utakuwa na pendeleo la kuhudhuria sehemu ya kwanza ya mkutano anaofanya pamoja na mapainia wa kawaida. Kwa kuwa Ukumbusho wa mwaka ujao utakuwa Machi 22, miezi ya Machi, Aprili, na Mei ni miezi bora ya kupainia. Ukiisha chagua mwezi au miezi ambayo unataka kufanya upainia msaidizi, anza kuandika ratiba itakayokuwezesha kutimiza takwa la saa.
10 Hata ukihisi kwamba huwezi kufanya upainia msaidizi katika mwaka wa utumishi unaokuja, bado unaweza kudumisha roho ya upainia. Endelea kufanya yote uwezayo katika huduma, huku ukiwa na hakika kwamba Yehova anapendezwa na jitihada zako za nafsi yote za kumtolea utumishi bora. (Gal. 6:4) Waunge mkono na uwatie moyo wale wanaoweza kufanya upainia msaidizi. Labda unaweza kurekebisha ratiba yako ili ushiriki katika huduma kwa siku moja ya ziada pamoja na wale wanaofanya upainia.
11 Watu wa Yehova wanajua kwamba kuna jambo linalohitaji kufanywa haraka. Kuna kazi ambayo inahitaji kufanywa, kazi ya kuhubiri habari njema. Maisha ya watu yako hatarini, na wakati uliobaki umepungua. (1 Kor. 7:29-31) Kumpenda Mungu na jirani kutatuchochea kufanya yote tuwezayo katika huduma. Tukitia bidii na kufanya mipango mizuri, huenda tukaweza kufanya upainia msaidizi angalau mwezi mmoja katika mwaka mpya wa utumishi. Huo ni mradi mzuri kwelikweli!
[Maswali ya Funzo]
1. Tunaweza kufikiria kujiwekea mradi gani kwa ajili ya mwaka mpya wa utumishi?
2. Kwa nini tufikirie kujiwekea mradi wa kufanya upainia msaidizi?
3, 4. Tunafaidikaje kwa kufanya upainia msaidizi?
5. Tunaweza kufanya nini tukihisi kwamba hatuna ustadi wa kutosha?
6. Huenda ikawezekanaje kufanya upainia msaidizi licha ya matatizo ya afya au ratiba yenye shughuli nyingi?
7. Kwa nini inafaa kusali kuhusu mradi wa kuwa painia-msaidizi?
8. Kufuata kanuni iliyo kwenye Methali 15:22 kunaweza kukusaidiaje kufanya upainia msaidizi?
9. Huenda ukachagua kufanya upainia msaidizi miezi gani?
10. Unaweza kufanya nini ikiwa huwezi kufanya upainia msaidizi?
11. Kwa nini tutambue kwamba kuna kazi inayohitaji kufanywa haraka?