Sanduku la Swali
◼ Ni nini kinachopaswa kubandikwa kwenye ubao wa matangazo wa kutaniko?
Ubao wa matangazo katika Jumba la Ufalme huwa na habari zinazohusu shughuli za kutaniko. Hakuna kitu kinachopaswa kubandikwa kwenye ubao wa matangazo bila idhini ya mwangalizi-msimamizi.
Kwa kawaida, vitu vinavyobandikwa hutia ndani: Ratiba na migawo ya Mkutano wa Utumishi na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, orodha ya hotuba za watu wote ambazo zimepangwa kutolewa, migawo ya wenyekiti wa Mkutano wa Watu Wote na wasomaji wa Mnara wa Mlinzi, orodha ya washiriki wa Mafunzo ya Kitabu ya Kutaniko na mahali yanapofanyiwa, taarifa kuhusu ziara ya mwangalizi wa mzunguko itakayofuata pamoja na habari zinazoihusu, habari kuhusu kusanyiko linalokuja, na ratiba ya usafi wa Jumba la Ufalme. Nyakati nyingine, wazee huagizwa wabandike barua fulani au vitu vingine kwenye ubao wa matangazo. Jambo lisilo la kawaida likitokea, baraza la wazee linaweza kuamua ikiwa itafaa kubandika habari hiyo.
Ingawa tangazo fupi kuhusu arusi iliyopangwa kufanyiwa katika Jumba la Ufalme linaweza kutolewa kwenye mkutano mmoja, tangazo rasmi la arusi halipaswi kubandikwa kwenye ubao wa matangazo. Pia, haifai kubandika matangazo kuhusu tafrija kwa kuwa hazihusiani na shughuli za kutaniko.—Ona Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 1984, ukurasa wa 12 au Aprili 15, 1984, ukurasa wa 15 (Kiingereza); Huduma ya Ufalme, Julai 1975, ukurasa wa 4 au Juni 1975, ukurasa wa 4 (Kiingereza), na Juni 1970, ukurasa wa 3 au Mei 1970, ukurasa wa 8 (Kiingereza).
Ubao wa matangazo unapaswa kuwa nadhifu na wenye kuvutia. Unapaswa kuwa mkubwa vya kutosha ili uweze kubandikwa vitu muhimu vilivyotajwa hapa. Ratiba ambazo hazitumiki tena na habari nyingine ambazo kutaniko limejua zinapaswa kuondolewa haraka. Ikiwa kutaniko zaidi ya moja linatumia jumba lilelile, kila kutaniko linapaswa kuwa na ubao wake wa matangazo au sehemu maalumu katika ubao huo na jina la kutaniko lionyeshwe wazi. Tunapendekeza kwamba mwangalizi-msimamizi, au mtu mwingine aliyeteuliwa naye, achunguze ubao mara kwa mara ili kuhakikisha kwamba habari zilizobandikwa hapo ni za karibuni, zinafaa, na zimepangwa kwa unadhifu.