Kufanya Mengi Zaidi Katika Huduma Yetu
1 Mtume Paulo aliwasihi Wakristo watembee katika njia ya Mungu na ‘waendelee kufanya hivyo kwa ukamili zaidi.’ (1 The. 4:1) Hilo linamaanisha nini kwetu? Jambo moja ni kwamba tunapaswa kuendelea kutafuta njia za kufanya mengi zaidi katika utendaji wa kiroho, tukijitahidi sikuzote ‘kutimiza kwa ukamili huduma yetu.’—2 Tim. 4:5.
2 Tunachochewa na Nini?: Tunafanya mengi zaidi katika huduma yetu kwa sababu tunatamani kumtumikia Muumba kwa ukamili zaidi. Tungependa kukua kiroho na kutafuta njia za kuboresha huduma yetu. Tunaweza tukafikia miradi ya kiroho ikiwa tutakuwa na mazoea mazuri na ikiwa tunachochewa na jambo linalofaa.—Zab. 1:1, 2; Flp. 4:6; Ebr. 10:24, 25.
3 Tunahitaji kusitawisha roho ya kujidhabihu tunapojitahidi kupanua huduma yetu. Roho kama hiyo husitawishwa kwa kutafakari kupitia sala kuhusu mfano mzuri wa Yesu. (Mt. 20:28) Yesu alipata shangwe kubwa sana kwa kuwatumikia wengine muda wote wa huduma yake. (Mdo. 20:35) Tunaweza kumwiga Yesu kwa kuwaonyesha watu upendezi na kwa kuwa chonjo kutumia nafasi zozote kufanya mengi zaidi katika huduma yetu.—Isa. 6:8.
4 Fungu la Wazazi: Watoto wanaweza kukaziwa tamaa ya kuwatumikia wengine na kupanua huduma yao wanapokuwa bado wadogo. Watoto hutambua bidii ya washiriki wa familia na jitihada wanazofanya za kupanua huduma yao. Ndugu mmoja alichochewa kufanya mengi zaidi alipokuwa mvulana kwa sababu alishirikiana na babu yake katika utendaji mbalimbali wa kutaniko. Kuona bidii na shangwe ya babu yake kulimchochea kutafuta nafasi za kuwatumikia ndugu zake. Sasa yeye ni mtumishi wa huduma.
5 Ndugu Wanahitajiwa: “Ikiwa mwanamume yeyote anajitahidi kufikia . . . , yeye anatamani kazi njema.” (1 Tim. 3:1) Maneno hayo yanawatia moyo akina ndugu wajitahidi kufikia mapendeleo mengine ya utumishi katika tengenezo la Yehova. Mtu hahitaji kuwa na ustadi wa pekee au uwezo fulani wa ajabu. Ndugu anayejitahidi kufikia atatafuta Ufalme kwanza na atakuwa mwenye bidii katika huduma. (Mt. 6:33; 2 Tim. 4:5) Atajitahidi kuwawekea wengine mfano mzuri.
6 Ulimwenguni Pote: Yehova anaharakisha kazi ya kukusanya. (Isa. 60:22) Kuna uhitaji wa haraka kwa wote wanaofuata mfano wa Yesu kufanya mengi zaidi katika huduma yao. Ripoti ya ulimwenguni pote kwa ajili ya mwaka wa utumishi wa 2006 unaonyesha kwamba 248,327 walibatizwa. Huo ni wastani wa zaidi ya watu 680 wapya kila siku! Sisi sote na tuendelee kutafuta njia za kufanya mengi zaidi katika huduma yetu.