Njia za Kupanua Huduma Yako
1 Zaidi ya miaka 40 iliyopita, makala yenye kichwa “Je, Unafanya Yote Uwezayo?” ilitokea katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 15, 1955, (la Kiingereza). Lilikazia kwa njia ya upendo jinsi inavyowezekana kwa watu wa Yehova kuboresha jitihada yao wenyewe katika huduma ili waweze kuongeza utendaji wao wa Ufalme. Shauri hilo zuri pia latumika leo, tuendeleapo kufanya yote tuwezayo hata vema zaidi.
2 Utumishi wetu wote wapasa kuchochewa na amri iliyo kuu kupita zote: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Mr. 12:30) Twaonyesha upendo wetu kamili kwa Yehova kwa kutumia fursa kamili tulizo nazo kuendeleza kazi yake ya Ufalme. Fikiria njia zifuatazo ambazo waweza kupanua huduma yako.
3 Tekeleza Madaraka Yako: Ndugu waliojiweka wakfu wanaweza kujitahidi kustahili wawe watumishi wa huduma kisha kusonga mbele watumikie wakiwa wazee. Makala zenye kichwa “Je! Wewe Wajitahidi Kufikia?” na “Je! Wewe Wastahili Kutumikia?,” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Septemba 1, 1990, zimechochea ndugu wengi wajitoe kwa ajili ya madaraka ya kutaniko. Uliza wazee wako madokezo hususa ya jinsi ya kufikia na kustahili.
4 Wazee na watumishi wa huduma walio waseja wanaombwa kufikiri kwa uzito juu ya kujiandikisha katika Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Waweza kujifahamisha habari kuhusu shule hii kwa kusoma marejezo yaliyo chini ya “Ministerial Training School” katika Watch Tower Publications Index za 1986-1995, 1996, na 1997. Je, waona ‘mlango huo mkubwa wa utendaji’ ukifunguka mbele yako? (1 Kor. 16:9a) Ndugu wengi ambao waliingia humo, hawakuwa wamewazia kamwe mapendeleo yote ya utumishi baada ya kuhitimu. Leo wanafurahia kutumikia katika Betheli au shambani wakiwa mapainia wa pekee, wamishonari, au waangalizi wasafirio.
5 Jitahidi Kufikia Utumishi wa Wakati Wote: Vijana wanaohitimu shule ya sekondari, wake wa nyumbani, na wowote ambao wamefikia umri wa kustaafu wapaswa kufikiria kwa uzito kupainia. Pitia nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Julai 1998, kisha uzungumze na mapainia ambao hali zao zilikuwa sawa na zile za maisha yako mwenyewe. Huenda ikawa utachochewa kupanua huduma yako kwa kupainia, kama wanavyofanya. (1 Kor. 11:1) Je, ingewezekana kupanua utendaji wako hadi muda wa saa 70 kila mwezi hivyo utumikie ukiwa painia wa kawaida?
6 Zaidi ya ndugu na dada 17,000 sasa wanatumikia katika ofisi za tawi na makao ya Betheli ulimwenguni pote. Kitabu Huduma Yetu kwenye ukurasa wa 116 chazungumzia utumishi wa Betheli. Kwa nini usikisome na kuona yale yanayopendekezwa kama una mradi wa utumishi wa Betheli?
7 Tumikia Palipo na Uhitaji Mkubwa Zaidi: Je, unaishi katika eneo linalohubiriwa mara nyingi au mahali palipo na ndugu wengi wanaoshiriki kazi hiyo? Je, umefikiria kupanua huduma yako kwa kuhamia mahali palipo na uhitaji mkubwa zaidi? Labda waweza kuhamia eneo la karibu la mashambani ambamo kuna uhitaji wa wafanyakazi zaidi. (Mt. 9:37, 38) Hilo halipasi kufanywa bila kufikiria. Jambo hilo huhitaji kufikiriwa kwa sala. (Luka 14:28-30) Zungumza hali yako na wazee na mwangalizi wa mzunguko. Watasababu pamoja nawe kuona kama ni jambo la hekima kuhama sasa au kujitayarisha kufanya hivyo wakati ujao. Ukitaka kuandikia Sosaiti ili upate dokezo la pale unapoweza kuhamia, barua iliyotiwa sahihi na Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko lazima iambatane na barua yako.
8 Zidisha Ubora wa Utumishi Wako: Yaelekea kwamba sote twaweza kushiriki kikamili katika huduma kwa kuzidisha ubora wa utumishi wetu wa shambani. Je, wahusika katika sehemu zote za kazi hii, kutia ndani kutoa ushahidi nyumba hadi nyumba na kivivi hivi na pia kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia? Ikiwa unaongoza funzo, je, unaweza kuzidisha ufundi wako wa kufundisha? Ingefaa kupitia nyongeza ya Huduma ya Ufalme Yetu ya Juni 1996 upate madokezo unayoweza kutumia ili uchochee wanafunzi wako kuelekea wakfu na ubatizo.
9 Mazungumzo zaidi ya njia za kupanua na kuboresha huduma yetu yapatikana katika sura ya 9 ya kitabu Tumefanywa Tengenezo Tutimize Huduma Yetu. Hakika, sisi sote twapaswa kutamani kufanya yote tuwezayo katika utumishi wa Mungu. Kwa nini usifikirie kwa uzito miradi yako ya kiroho? Fanya vile 1 Timotheo 4:15 hupendekeza: “Fikiri kwa uzito juu ya mambo haya; vama katika hayo, ili kusonga mbele kwako kupate kuwa dhahiri kwa watu wote.”