Sanduku La Swali
◼ Je, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anaunga mkono vikundi vya Mashahidi wa Yehova vinavyokutana kwa lengo la kufanya utafiti wa Maandiko au majadiliano?—Mt. 24:45. 47.
Jibu ni hapana, mtumwa haungi mkono jambo hilo. Hata hivyo, katika sehemu mbalimbali ulimwenguni, washiriki wachache wa tengenezo letu wameunda vikundi vinavyojitegemea vya kufanya utafiti kuhusu masuala mbalimbali ya Biblia. Watu fulani wameanzisha vikundi vyao vya kuchunguza lugha ya Kiebrania na Kigiriki iliyotumiwa kuandika Biblia ili wachanganue usahihi wa Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Wengine hufanya utafiti wa mambo ya kisayansi yanayohusiana na Biblia. Wamefungua vituo vya Intaneti na vya maongezi kwa kusudi la kubadilishana na kujadiliana maoni yao. Pia, wamefanya mikutano na kuchapisha vichapo vyao vinavyoonyesha matokeo ya utafiti wao ili kuongezea habari tunazopata kwenye mikutano yetu ya Kikristo na katika vichapo vyetu.
Ulimwenguni pote, watu wa Yehova wanapata mafundisho na vitia moyo vingi vya kiroho kwenye mikutano, mikusanyiko na makusanyiko na pia kupitia vichapo vya tengenezo la Yehova. Chini ya mwelekezo wa roho na Neno lake la kweli, Yehova anaandaa kile kinachohitajiwa ili watu wa Mungu ‘waunganishwe vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri’ wakibaki ‘imara katika imani.’ (1 Kor. 1:10; Kol. 2:6, 7) Kwa kweli tunathamini sana maandalizi ya kiroho ambayo Yehova anatuandalia katika siku hizi za mwisho. Hivyo “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” haungi mkono vichapo vyovyote, mikutano, au vituo vya Intaneti ambavyo haviko chini ya usimamizi wake.—Mt. 24:45-47.
Ni jambo la kupongezwa ikiwa watu wanatumia uwezo wao wa kufikiri kuendeleza habari njema. Hata hivyo, malengo binafsi hayapaswi kupotosha kile ambacho Yesu Kristo amekuwa akikitimiza kupitia kutaniko lake hapa duniani leo. Katika karne ya kwanza, mtume Paulo alionya kuhusu kujiingiza katika mambo yanayochosha na kupoteza wakati kama vile “kutafuta-tafuta ukoo, ambayo mwisho wake si kitu, lakini ambayo hutokeza maswali ya utafiti badala ya kugawa kitu chochote kutoka kwa Mungu kuhusiana na imani.” (1 Tim. 1:3-7) Wakristo wote wanapaswa kujitahidi ‘kuepuka maswali ya upumbavu na kutafuta-tafuta ukoo na mizozo na mapigano juu ya Sheria, kwa maana hayo hayana faida na ni ya ubatili.’—Tito 3:9.
Kwa wale wanaopenda kujifunza na kufanya utafiti wa ziada wa Biblia, tunapendekeza wafanye utafiti kwenye mabuku ya Insight on the Scriptures, “Kila Andiko Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa” na vichapo vyetu vingine kama vile vinavyoelezea unabii unaopatikana kwenye Biblia katika kitabu cha Danieli, Isaya, na Ufunuo. Vitabu hivyo vina habari nyingi kwa ajili ya utafiti wa Biblia na kutafakari, ili ‘tujazwe ujuzi sahihi wa mapenzi [yake] katika hekima yote na utambuzi wa kiroho, ili tutembee kwa kumstahili Yehova kwa kusudi la kumpendeza yeye kikamili tunapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema na kuongezeka katika ujuzi sahihi wa Mungu.’—Kol. 1:9, 10.