Matumizi ya Internet—Uwe Chonjo Kuhusu Hatari Zake!
1 Watu wa Yehova hufurahia ushirika mzuri unaowajenga. Wao hufurahia kushiriki mambo yaliyoonwa kutoka katika huduma ya shambani na huthamini kusikia juu ya matukio yanayotokea kuhusiana na Mashahidi wa Yehova na kazi ya Ufalme tufeni pote. Wao hupenda kujulishwa habari ya jambo lolote lenye kutokeza ambalo huenda likawapata ndugu zetu, kama vile taabu au msiba wa asili, nao hutaka kujua kama kuna jambo lolote wawezalo kufanya ili kusaidia. Kupendezwa huko huonyesha muungano wa udugu, hiyo ikithibitisha kwamba kwa kweli sisi hupendana.—Yn. 13:34, 35.
2 Leo, sisi husikia juu ya matukio ya ulimwengu haraka. Matangazo ya redio na televisheni huonyesha matukio yanayotokea wakati huohuo kinaganaga kwa watazamaji tufeni pote. Pia simu hufanya iwezekane kuwasiliana mara moja na watu ulimwenguni pote. Internet imekuwa njia ya kuwasiliana ya hivi karibuni inayozidi kupendwa na wengi.—Ona Amkeni!, Julai 22, 1997.
3 Kubuniwa kwa simu kulifungua njia ya mawasiliano ya kibinafsi ya haraka ulimwenguni pote. Ijapokuwa simu ni yenye mafaa sana, tahadhari yahitajiwa katika njia inayotumiwa, kwa kuwa inaweza kutuhusisha na ushirika au utendaji usiofaa, na matumizi ya simu ya kupita kiasi yanaweza kuwa ghali sana. Televisheni na redio zinaweza kutumiwa kuelimisha. Ingawa hivyo, kwa kusikitisha programu nyingi zina ukosefu wa adili, na kuzikazia fikira sana ni kupoteza wakati. Hekima hutushurutisha tuwe wateuzi katika matumizi ya televisheni na redio.
4 Internet humwezesha mtu kuwasiliana na mamilioni ya watu wengine ulimwenguni pote kwa gharama ndogo, nayo hufungua njia ya kupata habari nyingi mno. (Amkeni!, Januari 8, 1998) Hata hivyo, matumizi ya Internet yasiyo na mpango, yanaweza kumweka mtu katika hatari kubwa za kiroho na za kiadili. Jinsi gani?
5 Wengi wanahangaika juu ya habari inayopatikana kwa utayari ambayo huonyesha jinsi ya kutengeneza silaha, kutia ndani makombora. Viwanda hulalamika juu ya kiwango cha wakati ambacho wafanyakazi hupoteza wakitumia Internet. Mengi yamesemwa katika vichapo vyetu juu ya hatari za kiroho za waziwazi zinazopatikana kwenye Internet. Mahali mbalimbali katika Internet hutoa habari zenye jeuri na za kiponografia ambazo haziwafai Wakristo kabisa. (Zab. 119:37) Mbali na hatari hizo, kuna hatari yenye kudhuru isiyotambulikana kwa urahisi ambayo Mashahidi wa Yehova hasa wanahitaji kujilinda dhidi yake. Hatari hiyo ni nini?
6 Je, ungemwalika mtu usiyemjua nyumbani mwako bila kwanza kujua yeye ni nani? Vipi kama hakungekuwa na njia ya kujua? Je, ungemruhusu mtu huyo asiyejulikana awe pamoja na watoto wako akiwa peke yake? Uwezekano huo hauwezi kubishaniwa katika Internet.
7 Barua zaweza kupelekwa na kupokewa kupitia kompyuta kutoka kwa watu usiowajua. Ndivyo ilivyo unapoongea kwa njia ya kompyuta au katika mahali pa kupigia gumzo. Huenda nyakati fulani washiriki wakadai kuwa Mashahidi wa Yehova, lakini mara nyingi huwa sio. Huenda mtu fulani akadai kuwa kijana ilhali siye. Au huenda hata mtu akadai isivyo kweli kuwa wa jinsia fulani.
8 Huenda habari unayopitishiwa iwe ni mambo yaliyoonwa au maelezo juu ya itikadi zetu. Habari hiyo hupitishiwa wengine ambao huipitishia wengine pia. Habari hiyo kwa ujumla huwa haijathibitishwa na huenda isiwe ya kweli. Maelezo hayo yaweza kuwa kisingizio cha kueneza maoni ya uasi-imani.—2 The. 2:1-3.
9 Unapokumbuka hatari hiyo, ukitumia Internet jiulize hivi: ‘Mimi huitumia kwa kusudi gani? Je, kuna uwezekano kwamba huenda nikaumizwa kiroho na jinsi ninavyoitumia? Je, labda nachangia madhara ya kiroho kwa wengine?’
10 Mahali Mbalimbali Katika Internet pa “Mashahidi wa Yehova”: Kwa mfano, fikiria baadhi ya mahali mbalimbali katika Internet pa watu wanaodai kuwa Mashahidi wa Yehova. Wanakualika utembelee mahali pao pa Internet usome mambo yaliyoonwa yaliyowekwa hapo na wengine wanaodai kuwa Mashahidi. Unatiwa moyo kuwaambia wengine mawazo yako na maoni yako kuhusu fasihi za Sosaiti. Wengine hutoa mapendekezo juu ya utoaji mbalimbali unaoweza kutumiwa katika huduma ya shambani. Mahali hapo mbalimbali huandalia watu mmoja-mmoja mahali pa kupigia gumzo, kukiruhusu mawasiliano ya moja kwa moja pamoja na wengine, sawa tu na kuongea kwa simu. Mara nyingi wao hukuelekeza kwenye mahali kwingine mbalimbali unakoweza kuwasiliana na Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Lakini je, waweza kujua kwa hakika kwamba njia hizo za mawasiliano hazijawekwa na waasi-imani?
11 Kuwa na ushirika kupitia Internet huenda kusipatane na pendekezo lipatikanalo kwenye Waefeso 5:15-17. Mtume Paulo aliandika hivi: “Fulizeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia kabisa wakati unaofaa, kwa sababu siku ni za uovu. Kwa ajili ya hili acheni kuwa wenye kukosa akili, bali endeleeni kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini.”
12 Kutaniko la Kikristo ni njia ya kitheokrasi ambayo kupitia kwake tunalishwa kiroho na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45-47) Katika tengenezo la Mungu, twapata mwelekezo na ulinzi wa kututenganisha na ulimwengu na vilevile kutuchochea twendelee kuwa na shughuli nyingi katika kazi ya Bwana. (1 Kor. 15:58) Mtunga-zaburi alionyesha kwamba aliona shangwe na kuhisi akiwa salama miongoni mwa kutaniko la watu wa Mungu. (Zab. 27:4, 5; 55:14; 122:1) Pia kutaniko huandaa tegemezo la kiroho na usaidizi kwa wote wanaoshirikiana nalo. Humohumo, unaweza kupata kikundi cha marafiki wenye upendo, wanaohangaika na kujali—watu ambao unawajua kibinafsi ambao wako tayari kusaidia na kufariji wengine nyakati za taabu. (2 Kor. 7:5-7) Washiriki wa kutaniko wanalindwa na uandalizi wa Kimaandiko wa kutenga na ushirika wale ambao wanafanya dhambi bila kutubu au wanaoendeleza mawazo ya uasi-imani. (1 Kor. 5:9-13; Tito 3:10, 11) Je, twaweza kutazamia kupata mipango hiihii yenye upendo tunaposhirikiana na wengine kupitia Internet?
13 Imeonekana wazi kwamba inakuwa kinyume cha hilo. Mahali pengine katika Internet ni njia zilizo wazi za propaganda ya uasi-imani. Mahali hapo mbalimbali huenda pakakana dai hilo, na wale wanaotegemeza mahali hapo huenda wakatoa ufafanuzi wa kindani kuhakikisha kwamba kwa kweli wao ni Mashahidi wa Yehova. Hata huenda wakakuomba habari fulani ili kuthibitisha kama wewe ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.
14 Yehova anataka utumie utambuzi. Kwa nini? Kwa sababu anajua kwamba utambuzi utakulinda dhidi ya hatari mbalimbali. Mithali 2:10-19 husema hivi: “Maana hekima itaingia moyoni mwako, na maarifa yatakupendeza nafsi yako; busara itakulinda; ufahamu utakuhifadhi.” Utakuhifadhi na nini? Na mambo kama vile “njia ya uovu,” wale wanaoziacha njia za unyoofu, na watu ambao hawana adili na wenye hila katika mwenendo wao kwa ujumla.
15 Tunapokwenda kwenye Jumba la Ufalme, hakuna shaka kwamba tuko na ndugu zetu. Twawajua. Hakuna mtu aliye na haja ya kuhakikishiwa hilo kwa sababu upendo wa kidugu unaonyeshwa waziwazi. Hatuhitaji kuandaa hati za utambulishi ili kuthibitisha kwamba kwa kweli sisi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Ni hapo ndipo tunapopata badilishano la kweli la kitia-moyo ambalo Paulo alisema juu yake kwenye Waebrania 10:24, 25. Mahali mbalimbali katika Internet ambapo huendeleza mawasiliano hapawezi kutegemeka ili kuandaa mambo hayo. Kukumbuka maneno ya Zaburi 26:4, 5, kwaweza kutufanya tuwe macho kuona hatari ambazo zaweza kupatikana kwa urahisi tunapotumia mahali mbalimbali katika Internet.
16 Hakuna mipaka wala vizuizi kuhusu habari zinazodumishwa na kupatikana na watumiaji wa Internet. Mara nyingi watoto na matineja huwa mitego rahisi ya uhalifu na kutumiwa vibaya katika mazingira hayo. Watoto huitibari, huwa wadadisi, na wenye hamu ya kuvumbua mambo mapya katika ulimwengu wa kompyuta. Kwa hiyo, wazazi wanahitaji kusimamia watoto wao na kuwapa mwongozo ufaao wa Kimaandiko juu ya kutumia Internet, kama tu vile ambavyo wangewaongoza katika uchaguzi wao wa muziki au sinema.—1 Kor. 15:33.
17 Kwa kusikitisha, watu fulani ambao hapo awali walikuwa ndugu na dada zetu wamelazimika kutengwa na ushirika kwa sababu ya ushirika ambao ulianza kwa kukutana na watu wa kilimwengu mahali pa kupigia gumzo kwenye Internet na hatimaye wakaongozwa kwenye ukosefu wa adili. Amini usiamini, wazee wameandika kwamba wengine wameacha waume au wake zao ili kufuatia uhusiano ambao ulianzia kwenye Internet. (2 Tim. 3:6) Watu wengine wameikana kweli kwa sababu ya kuamini habari iliyoandaliwa na waasi-imani. (1 Tim. 4:1, 2) Kwa kufikiria hatari hizi mbaya sana, je, halionekani kuwa jambo linalofaa kujihadhari kuhusu kujiingiza katika vipindi hivyo vya kupiga gumzo kwenye Internet? Hakika, kutumia hekima, ujuzi, uwezo wa kufikiri, na ufahamu uliosemwa kwenye Mithali 2:10-19 kwapaswa kutulinda na hayo.
18 Kwa kutokeza, kuna idadi ya watu mmoja-mmoja ambao wamefanyiza mahali wazi katika Internet ili wahubiri habari njema. Mahali pengi katika Internet panategemezwa na akina ndugu wasio na busara. Mahali mbalimbali pengine huenda pakategemezwa na waasi-imani ambao wanataka kushawishi wasioshuku. (2 Yoh. 9-11) Ikieleza kama kuna uhitaji wa ndugu zetu kufanyiza mahali kama hapo katika Internet, Huduma ya Ufalme Yetu ya Novemba 1997, ukurasa wa 3, ilisema: “Hakuna haja kwa mtu yeyote kutayarisha habari za Internet juu ya Mashahidi wa Yehova, utendaji wetu, au itikadi zetu. Mahali petu rasmi [www.watchtower.org] hutoa habari sahihi kwa yeyote mwenye kuitaka.”
19 Je, Ni Misaada ya Funzo Kupitia Internet? Watu fulani wamehisi kwamba wanawatumikia akina ndugu kwa kuweka habari iliyofanyiwa utafiti kuhusiana na utendaji mwingine mbalimbali wa kitheokrasi. Kwa mfano, mtu anaweza kufanya utafiti unaotegemea muhtasari wa hotuba ya watu wote kisha aiweke, akifikiria kwamba habari hiyo itanufaisha wale wanaohitaji kutayarisha muhtasari huohuo. Wengine wataweka maandiko yote ya Funzo la Mnara wa Mlinzi linalofuata au kuandaa chanzo cha habari kwa ajili ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi au Funzo la Kitabu la Kutaniko. Huenda wengine wakatoa madokezo ya utoaji mbalimbali wa huduma ya shambani. Je, kwa kweli hayo husaidia?
20 Vichapo vilivyoandaliwa na tengenezo la Yehova huchochea akili zetu kwa mawazo yenye kujenga na kutuzoeza “kutofautisha lililo sahihi na lililo kosa.” (Ebr. 5:14) Je, twaweza kusema kwamba hilo hutimizwa ikiwa wengine wanatufanyia utafiti?
21 Waberoya walisemwa kuwa “wenye akili ya uelekevu bora zaidi kuliko wale katika Thesalonike.” Kwa nini? Kwa sababu “walilipokea neno kwa hamu ya akili iliyo kubwa zaidi sana, wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku juu ya kama mambo hayo yalikuwa hivyo.” (Mdo. 17:11) Ijapokuwa Paulo na Sila waliwahubiria, hawangeweza kuifanya kweli iwe yao bila wao kujichunguzia wenyewe.
22 Kutumia utafiti wa mtu mwingine kwa ajili ya hotuba au utayarishaji mwingine wa mkutano kwa kweli hubatilisha kusudi la funzo la kibinafsi. Je, si tamaa yako kujenga imani yako mwenyewe katika Neno la Mungu? Ikitegemea kusadikishwa kibinafsi, basi unaweza kueleza hadharani imani yako—katika hotuba zako, maelezo yako mikutanoni, na katika huduma ya shambani. (Rom. 10:10) Kutumia utafiti wa mtu mwingine hakupatani na ufafanuzi ulio kwenye Mithali 2:4, 5 wa ‘kutafuta na kuutafutia kama hazina iliyositirika.’
23 Kwa mfano, unapochunguza maandiko katika nakala yako ya Biblia, unaweza kupitia kifupi muktadha wa kila andiko. Unaweza ‘kufuatisha kwa uangalifu mambo yote,’ kama alivyofanya Luka alipoandika Gospeli yake. (Luka 1:3) Pia jitihada hiyo ya ziada itakusaidia uwe ustadi katika kuchunguza maandiko katika huduma na unapotoa hotuba. Watu wengi wamesema kwamba wanavutiwa na Mashahidi wa Yehova kwa sababu wanajua kutumia Biblia zao. Njia pekee ambayo jambo hilo laweza kutuhusu ni kama tunazoea kibinafsi kuchunguza maandiko katika Biblia zetu wenyewe.
24 Kutumia Wakati Wetu kwa Hekima: Jambo jingine la kufikiria kwa habari hii, ni wakati unaotumiwa kufanyiza, kusoma, na kujibu habari iliyowekwa kwenye Internet. Zaburi 90:12 hututia moyo tusali hivi: “Utujulishe kuzihesabu siku zetu, tujipatie moyo wa hekima.” Paulo alisema: “Wakati ubakio umepunguzwa.” (1 Kor. 7:29) Na zaidi ya hilo: “Kwa kweli maadamu tuna wakati wenye kufaa kwa ajili ya hilo, acheni sisi tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.”—Gal. 6:10.
25 Shauri hilo lakazia uhitaji wa sisi kuwa wenye busara tunapotumia wakati wetu. Itatufaidi zaidi kama nini kusoma Neno la Mungu! (Zab. 1:1, 2) Hayo ndiyo mashirika bora zaidi tuwezayo kuwa nayo. (2 Tim. 3:16, 17) Wazazi, je, mwafundisha watoto wenu thamani ya kutumia wakati wao kwa hekima ili kufuatia mambo ya Ufalme? (Mhu. 12:1) Wakati unaotumiwa katika funzo la Biblia la kibinafsi na la familia, kuhudhuria mikutano, na huduma ya shambani ni wenye thamani zaidi ya wakati unaotumiwa kupitia-pitia Internet, ukitazamia kupata faida.
26 Kwa habari hii, ni mwendo wa hekima kukazia fikira zetu mambo ya kiroho na mambo muhimu na yanayohusu maisha yetu tukiwa Wakristo. Hilo lahitaji kufanya uchaguzi uliofikiriwa vizuri kuhusu habari ambazo zastahili wakati wetu na mawazo yetu. Tukiwa Wakristo, mambo yanayohusu maisha yetu yanajumlishwa na Kristo, aliyesema hivi: “Basi, fulizeni kutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, na vitu vingine vyote hivi mtaongezewa.” (Mt. 6:33) Je, wewe huwi mwenye furaha zaidi maisha yako yanapojaa mambo ya Ufalme badala ya shughuli nyingine zozote?
27 Barua za Kompyuta Kupitia Internet: Ijapokuwa kushiriki mambo yaliyoonwa au mawazo ya kibinafsi miongoni mwa familia na marafiki wanaoishi mbali ni jambo linalofaa, je, kwa kweli ni jambo lenye upendo kupitisha mambo hayo kwa watu wengine wasiojua familia yako au marafiki wako? Au je, hayo yapasa kuwekwa kwenye ukurasa wa Internet ili mtu yeyote tu ayasome? Je, ujumbe huo mbalimbali wa kibinafsi utolewe nakala bila busara na kupelekewa watu ambao huenda unawajua au huwajui? Vivyo hivyo, ukipokea ujumbe mbalimbali kutoka kwa wengine ambao si wewe uliyekusudiwa kuupata, je, ni jambo lenye upendo kuwapitishia wengine pia?
28 Vipi ukipitisha jambo lililoonwa lisilo sahihi? Je, hiyo haitakuwa kushiriki kuendeleza jambo lisilo la kweli? (Mit. 12:19; 21:28; 30:8; Kol. 3:9) Kwa hakika, kuendelea “kuangalia sana kwamba jinsi [tu]navyotembea si kama wasio na hekima bali kama watu wenye hekima” kutatuchochea tufikirie jambo hilo. (Efe. 5:15) Tuna furaha kama nini kwamba Yearbook, Mnara wa Mlinzi, na Amkeni! vimejaa mambo yaliyoonwa yaliyothibitishwa ambayo hututia moyo na kutuchochea twendelee kutembea katika “njia!”—Isa. 30:20, 21.
29 Pia kuna hatari nyingine. Mtume Paulo alisema hivi kuhusu wengine: “Wao hujifunza pia kuwa wasio na shughuli, wakizurura huku na huku kwenye nyumba; ndiyo, si wakiwa wasio na shughuli tu, bali pia wapiga-porojo na wajiingizaji katika mambo ya watu wengine, wakiongea juu ya mambo yasiyowapasa.” (1 Tim. 5:13) Hilo hupinga kutumia wakati na jitihada kupitishia ndugu zetu habari ya kipuuzi.
30 Hebu wazia pia, wakati unaotumiwa kusoma barua nyingi za kompyuta. Kwa kupendeza, kitabu Data Smog kilisema: “Mtu anapotumia wakati mwingi zaidi kwenye Internet barua za kompyuta hubadilika upesi kutoka kuwa jambo jipya lenye kusisimua hadi kuwa mzigo unaopoteza wakati, kukiwa na ujumbe mbalimbali wa kusoma na kujibu kila siku kutoka kwa wafanyakazi wenzako, marafiki, familia, . . . na matangazo ya biashara yaliyofanywa bila kuombwa.” Zaidi ya hilo, kitabu hicho chasema hivi: “Watumiaji wenye pupa wa elektroni wamekuwa na tabia mbaya sana ya kupeleka habari yoyote yenye kutumbuiza wanayopokea—vichekesho, hadithi za jijini, barua za kompyuta za mfuatano, na nyingi zaidi—kwa kila mtu aliye katika kitabu chao cha anwani za elektroni.”
31 Imekuwa hivyo na barua za kompyuta zinazoenezwa kwa ndugu wengi—habari kama vile vichekesho au hadithi zenye kuchekesha juu ya huduma; shairi linalodhaniwa kuwa lategemea itikadi zetu; vielelezo kutoka kwenye hotuba mbalimbali zilizosikiwa kwenye makusanyiko, mikusanyiko, au kwenye Jumba la Ufalme; mambo yaliyoonwa katika huduma ya shambani; na kadhalika—mambo yanayoonekana kuwa yasiyo na kosa. Wengi hupeleka barua za kompyuta kama hizo bila kuchunguza kiini, ikifanya iwe vigumu kujua kikweli ni nani aliyekuwa mwanzilishi, jambo ambalo humfanya mtu ajiulize kama habari hiyo ni ya kweli.—Mit. 22:20, 21.
32 Ujumbe mbalimbali wa kipuuzi kama huo mara nyingi si wenye maneno yenye afya ambayo Paulo alikuwa nayo akilini alipomwandikia Timotheo, akisema: “Fuliza kushika kiolezo cha maneno yenye afya ulichosikia kutoka kwangu pamoja na imani na upendo vinavyohusiana na Kristo Yesu.” (2 Tim. 1:13) “Lugha iliyo safi” ya kweli ya Kimaandiko ina “kiolezo cha maneno yenye afya” yanayotegemea hasa kichwa cha Biblia cha kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova kupitia Ufalme wake. (Sef. 3:9) Twapaswa kujitahidi sana kutumia wakati wetu wote na nishati iliyopo kuunga mkono kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova.
33 Kwa kuwa tumo kabisa katika wakati wa mwisho wa huu mfumo wa mambo, huu si wakati wa kuacha kuwa macho. Biblia hutuonya hivi: “Tunzeni akili zenu, iweni wenye kulinda. Mpinzani wenu, Ibilisi, hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.” (1 Pet. 5:8) Yaendelea kusema: “Vaeni suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mpate kuweza kusimama imara dhidi ya mbinu za Ibilisi.”—Efe. 6:11.
34 Internet ikitumiwa vibaya, inaweza kuwa njia ya Shetani ya kushinda wale wanaoshawishwa na uwezo wake. Ijapokuwa inaweza kuwa na manufaa ya kadiri, kuna hatari mtu asipojihadhari. Hasa wazazi wanahitaji kujali jinsi watoto wao wanavyotumia Internet.
35 Kudumisha maoni yaliyosawazika kuhusu Internet ni ulinzi. Twathamini kikumbusha cha wakati ufaao cha Paulo: “Acheni wale . . . wanaoutumia ulimwengu [wawe] kama wale wasioutumia kwa ukamili; kwa maana mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Kor. 7:29-31) Kukumbuka mambo hayo kutatusaidia sisi na familia zetu kutokengeushwa na mambo yote ambayo ulimwengu waweza kutoa, kutia ndani mambo yapatikanayo kwenye Internet.
36 Ni muhimu kwetu kuwa karibu na ndugu zetu katika kutaniko na kutumia wakati unaobaki kwa hekima, hivyo tukijitoa kwa ajili ya kuendeleza masilahi ya Ufalme. Mfumo huu ukaribiapo kukoma, acheni “[tu]siendelee tena kutembea kama vile mataifa watembeavyo pia katika ukosefu wa faida wa akili zao,” bali acheni “[twendelee] kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini.”—Efe. 4:17; 5:17.