‘Maneno Yenu na Yawe . . . Sikuzote Yenye Kukolezwa Chumvi’
1. Inamaanisha nini kukoleza maneno yetu chumvi?
1 “Maneno yenu na yawe yenye neema sikuzote, yenye kukolezwa chumvi, ili mjue jinsi mnavyopaswa kumjibu kila mtu.” (Kol. 4:6) Kukoleza maneno yetu chumvi kunamaanisha kuchagua maneno sahihi na kuzungumza kwa njia ambayo itafanya maneno yetu yampendeze msikilizaji. Ni muhimu sana kufanya hivyo tunapohubiri.
2. Ni nini kilichomfanya Yesu afaulu kumhubiria mwanamke Msamaria?
2 Mfano wa Yesu: Alipokuwa akipumzika karibu na kisima fulani, Yesu alitumia nafasi hiyo kuzungumza na mwanamke Msamaria aliyekuja kuteka maji. Mara kadhaa katika mazungumzo yao, mwanamke huyo alitaja mambo ambayo yalionyesha ugomvi wa muda mrefu kati ya Wayahudi na Wasamaria. Pia alisema kwamba aliamini Wasamaria walikuwa wazao wa Yakobo, ingawa Wayahudi waliamini kuwa Wasamaria hawakuwa Wayahudi. Badala ya kubishana naye kuhusu mambo hayo, Yesu alizungumzia mambo yenye kupendeza. Kwa sababu hiyo aliweza kumhubiria na kumsaidia mwanamke huyo na wanaume wa jiji hilo.—Yoh. 4:7-15, 39.
3. Tunawezaje kufuata mfano wa Yesu tunapohubiri?
3 Tunapohubiri tunapaswa kukumbuka kusudi letu, yaani, ‘kutangaza habari njema ya mambo mema.’ (Rom. 10:15) Tungependa kuzungumza na mwenye nyumba kuhusu jambo linalopendeza na linalojenga kutoka kwa Biblia, bila kumfanya afikiri kwamba tunashambulia imani yake. Akitoa maoni yasiyo sawa, si lazima tumkosoe haraka na kwa njia inayoweza kumwaibisha. Je, kuna chochote katika maneno yake ambacho tunakubaliana au ambacho tunaweza kutumia kumpongeza? Labda tunaweza kusema hivi kabla ya kusoma andiko, “Je, umewahi kufikiria mambo kwa njia hii?”
4. Tufanyeje ikiwa mwenye nyumba anatutukana?
4 Tufanyeje ikiwa mwenye nyumba anatutukana au anataka kubishana tu? Tunapaswa kuendelea kuwa watulivu na wapole kwa maneno na matendo. (2 Tim. 2:24, 25) Ikiwa mtu hathamini ujumbe wa Ufalme, ni bora kutumia busara na kuondoka.—Mt. 7:6; 10:11-14.
5. Dada mmoja alipataje matokeo mazuri kwa kujibu kwa upole?
5 Matokeo Mazuri: Dada mmoja alipojaribu kumhubiria jirani wake, mwanamke huyo alikasirika sana na kumtukana. Kwa upole, dada huyo alisema: “Pole sana. Tafadhali uwe na siku njema.” Majuma mawili baadaye, mwanamke huyo alibisha mlango wa dada huyo na kumwomba msamaha kwa yale aliyosema, na akasema yuko tayari kusikiliza. Mara nyingi, jibu la upole huwa na matokeo mazuri!—Met. 15:1; 25:15.
6. Kwa nini ni muhimu kutumia maneno yaliyokolezwa chumvi tunapohubiri?
6 Jaribu kutumia maneno yaliyokolezwa chumvi unapohubiri habari njema. Hata ikiwa mwenye nyumba hapendezwi, huenda akawa tayari zaidi kusikiliza wakati mwingine Mashahidi wa Yehova watakapomtembelea.