Ushuhuda wa Imani!
1. Yesu alitabiri mambo gani mabaya?
1 Mitume walisikiliza kwa makini Yesu alipokuwa akizungumza kuhusu kuwapo kwake na umalizio wa mfumo wa mambo. Mambo mabaya yangewakumba wanadamu—vita, upungufu wa chakula, matatemeko ya nchi, tauni. Kisha, Yesu akasema kwamba wanafunzi wake wangechukiwa, wangeteswa, na kuuawa. Manabii wa uwongo wangetokea na kuwadanganya wengi. Upendo wa walio wengi zaidi ungepoa.
2. Kwa nini inastaajabisha kwamba habari njema inahubiriwa ulimwenguni pote?
2 Baada ya Yesu kuwaambia mambo hayo, hapana shaka kwamba mitume walishangaa aliposema kwamba habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa. (Mt. 24:3-14) Leo tunaona utimizo wa ajabu wa unabii huo wenye kusisimua. Ingawa tunaishi katika nyakati hatari, Mashahidi wa Yehova wanatangaza habari njema kwa bidii. Huku upendo wa ulimwengu ukipoa, upendo wetu unazidi kuwaka. Licha ya kuchukiwa na “mataifa yote,” tunahubiri katika karibu mataifa yote.
3. Unaona takwimu gani zenye kupendeza katika ripoti ya ulimwenguni pote?
3 Inatia moyo kama nini kuchunguza utendaji wa Mashahidi wa Yehova wa mwaka uliopita wa utumishi kama unavyoonyeshwa katika chati iliyo kwenye ukurasa wa 3 hadi wa 6! Kwa miaka 16 mfululizo, saa zaidi ya bilioni moja zimetumiwa kila mwaka katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Huo ni ushuhuda ulioje wa imani! Kulikuwa na ongezeko la asilimia 5.8 katika idadi ya mapainia, asilimia 3.1 katika idadi ya wahubiri, na asilimia 4.4 katika idadi ya mafunzo ya Biblia. Idadi ya waliobatizwa iliongezeka kwa asilimia 20.1 zaidi ya mwaka uliotangulia wa utumishi. Inasisimua kuona kwamba watu karibu milioni saba wanamtumikia Yehova kwa uaminifu—watu wengi zaidi kuliko wakati mwingine wowote katika historia ya wanadamu! Unapochunguza chati hiyo, ni nini kinachokutia moyo wewe hasa?
4. Ni matatizo gani ambayo mtu fulani alishinda ilipokuwa akijitahidi kufikia ubatizo?
4 Ijapokuwa takwimu zenyewe zinapendeza, tusisahau kwamba zinawakilisha watu ambao wamethibitisha imani yao. Fikiria mfano mmoja. Guillermo alilelewa huko Bolivia. Alizaliwa katika 1935, naye alianza kufanya kazi katika shamba la koka akiwa na umri wa miaka tisa. Tangu utoto, alitafuna majani ya koka ili kupunguza mfadhaiko uliotokana na kufanya kazi ngumu. Baadaye alitumia vibaya vileo na kuvuta sigara. Alipoanza kujifunza kuhusu yale ambayo Yehova anataka afanye, Guillermo aliacha kuvuta sigara na kutumia vibaya kileo. Tatizo kubwa alilokabili ni kushinda zoea alilokuwa nalo tangu utotoni la kutafuna majani ya koka. Alisali bila kuacha na akashinda zoea hilo. Baada ya kushinda mazoea hayo mabaya, alibatizwa. “Sasa,” anasema, “ninajihisi kuwa safi nami ni mwenye furaha sana.”
5. Una tamaa gani?
5 Yehova anapendezwa na watu kikweli. Ni mapenzi yake kwamba watu wa namna zote wafikie toba. (2 Pet. 3:9) Hiyo ndiyo tamaa yetu pia. Mioyo yetu na ituchochee kufanya yote tunayoweza ili kuendelea kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu wamjue na kumpenda Yehova kama sisi.