Watayarishe Wapya Wakabili Upinzani
1 Watu wanapoanza kujifunza Biblia na ‘kutamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu,’ Shetani hujitahidi sana kuwapinga. (2 Tim. 3:12) Mtu anaweza kupingwa na wafanyakazi wenzake, wanafunzi shuleni, au majirani. Linaweza kuwa jambo gumu sana kwa mwanafunzi mpya anapopingwa na watu wa ukoo, hata kama wanafanya hivyo kwa nia nzuri.—Mt. 10:21; Marko 3:21.
2 Upinzani Ulitabiriwa: Wapya wanahitaji kujua kwamba watapatwa na mateso na kwamba mateso yanaonyesha wao ni wanafunzi wa kweli wa Kristo. (Yoh. 15:20) Nyakati nyingine, huenda upinzani ukatokea kwa sababu watu hawajui ukweli kuwahusu Mashahidi wa Yehova. Kumbuka kwamba mtu anapata shangwe kubwa anapovunjiwa heshima kwa sababu ya kuwa mfuasi wa Yesu na kwa sababu ya kumtii Mungu. (Mdo. 5:27-29, 40, 41) Wahakikishie wapya kuwa Yehova atawategemeza kwa upendo. (Zab. 27:10; Marko 10:29, 30) Kwa kudumisha utimilifu, wanachukua msimamo upande wa Yehova kuhusiana na suala la enzi kuu ya ulimwengu wote mzima.—Met. 27:11.
3 Ujuzi Sahihi Unavyohusika: Wasaidie wanafunzi wa Biblia waone umuhimu wa kuendelea kupata ujuzi sahihi licha ya matatizo ambayo huenda wakakabili. Kwa kutumia upinzani, Shetani hujaribu kuzuia mambo wanayojifunza yasitie mizizi katika mioyo yao ya mfano. (Met. 4:23; Luka 8:13) Kwa hiyo, ni lazima waendelee kupata ujuzi sahihi wa Neno la Mungu ili wawe thabiti kabisa katika imani.—Zab. 1:2, 3; Kol. 2:6, 7.
4 Uhitaji wa Kuvumilia: Katika hali yoyote ngumu, uvumilivu ni muhimu na unaweza kuwa na matokeo mazuri. (Luka 21:16-19) Wapya wanapovumilia upinzani, wanajifaidi wenyewe na wengine pia. Wanajionea kwamba Yehova anaweza kuwabariki sana wale wanaovumilia kwa uaminifu.—Yak. 1:12.
5 Mtume Paulo alifurahia sana maendeleo ya kiroho ya ndugu zake huko Thesalonike. Paulo alimshukuru Mungu kwa ajili ya ndugu hao, ambao wengi wao alikuwa amewasaidia kuijua kweli. (2 The. 1:3-5) Sisi pia tunaweza kupata furaha na uradhi kama huo ikiwa tutawasaidia wanafunzi wetu wa Biblia kukabili upinzani na kuuvumilia.