Sifa Muhimu Zaidi ya Mwalimu Mzuri
1. Ni sifa gani iliyo muhimu zaidi ya mwalimu mzuri?
1 Ni nini kinachomwezesha mtu kuwa mwalimu mzuri wa Biblia? Je, ni elimu ya kilimwengu? Uzoefu? Kipawa? Kwa kweli, kile kinachomfanya mtu kuwa mwalimu mzuri ni sifa ileile ambayo hutimiza Sheria, huwatambulisha wafuasi wa Yesu, na pia, ndio inayojitokeza zaidi na yenye kuvutia zaidi kati ya sifa nne kuu za Yehova. (Yoh. 13:35; Gal. 5:14; 1 Yoh. 4:8) Sifa hiyo ni upendo. Walimu wazuri huonyesha upendo.
2. Kwa nini tunapaswa kuwapenda watu?
2 Wapende Watu: Mwalimu Mkuu, Yesu, aliwapenda watu, na jambo hilo liliwachochea wamsikilize. (Luka 5:12, 13; Yoh. 13:1; 15:13) Ikiwa tunawajali watu, tutatumia kila fursa kuwahubiria. Vizuizi kama kuteswa na kutopendezwa kwa watu havitatuzuia. Tutapendezwa kikweli na watu tunaowahubiria na tutabadili mazungumzo yetu ili yafae hali zao. Tutakuwa tayari kutumia wakati wetu kuwafundisha wanafunzi wa Biblia, na pia kutayarisha kwa ajili ya kila kipindi cha funzo.
3. Kupenda kweli za Biblia kutatusaidiaje katika huduma?
3 Penda Kweli za Biblia: Yesu alipenda pia kweli za Biblia na aliziona kuwa hazina. (Mt. 13:52) Ikiwa tunapenda kweli, tutazizungumzia kwa shauku, na hilo litawafanya wanaotusikiliza wapendezwe na ujumbe wetu. Upendo huo utatusaidia kukazia umuhimu wa ujumbe tulio nao kuliko kukazia udhaifu wetu binafsi, na kwa njia hiyo hatutakuwa na woga sana tunapohubiri.
4. Tunaweza kusitawisha upendo kwa njia gani?
4 Sitawisha Upendo: Tunaweza kusitawishaje upendo kuwaelekea watu? Kwa kutafakari kuhusu upendo ambao Yehova na Yesu wametuonyesha na vilevile kutafakari kuhusu hali mbaya ya kiroho ya watu katika eneo letu. (Marko 6:34; 1 Yoh. 4:10, 11) Upendo wetu kuelekea kweli za Biblia utaimarika kupitia funzo la kibinafsi la kawaida na kutafakari. Upendo ni sehemu ya tunda la roho. (Gal. 5:22) Kwa hiyo, tunaweza kumwomba Yehova atupe roho takatifu na pia atusaidie kukuza upendo. (Luka 11:13; 1 Yoh. 5:14) Hata iwe tuna kiwango gani cha elimu ya kilimwengu, tumemtumikia Yehova kwa miaka mingapi, au tuna vipawa gani, tunaweza kuwa walimu wa Biblia wenye matokeo kwa kuonyesha upendo.