Tovuti Yetu Rasmi—Imetengenezwa ili Itunufaishe Sisi na Wengine
Yesu alituamuru tuhubiri habari njema za Ufalme “katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Tovuti ya watchtower.org, jw-media.org, na jw.org zimeunganishwa katika Tovuti iliyofanyiwa marekebisho ya jw.org ili kutusaidia ‘tutimize kwa ukamili huduma yetu.’—2 Tim. 4:5.
“Dunia Yote Inayokaliwa”: Karibu theluthi moja ya watu duniani hutumia Intaneti. Imekuwa chanzo kikuu cha habari kwa watu wengi, hasa vijana. Tovuti yetu huwapa watumiaji wa Intaneti majibu sahihi ya maswali ya Biblia. Huwajulisha watu kuhusu tengenezo la Yehova na wanaweza kuomba kwa urahisi kujifunza Biblia nyumbani bila malipo. Hivyo, habari njema zinaweza kufika katika maeneo ya dunia ambayo watu wana nafasi chache za kusikia ujumbe wa Ufalme.
“Mataifa Yote”: Ili kutoa ushahidi kwa “mataifa yote,” tunapaswa kutangaza kweli ya Biblia katika lugha tofauti. Wale wanaotembelea Tovuti ya jw.org wanaweza kupata habari katika lugha karibu 400 kwa urahisi zaidi kuliko Tovuti nyingine yoyote.
Itumie Vizuri: Tovuti iliyofanyiwa marekebisho ya jw.org haijakusudiwa tu kwa ajili ya kuwatolea ushahidi watu ambao si mashahidi. Imetengenezwa ili pia itumiwe na Mashahidi wa Yehova. Ikiwa unatumia Intaneti, tunakutia moyo uitumie Tovuti ya jw.org. Yafuatayo ni baadhi ya mapendekezo ya jinsi ya kutumia Tovuti hiyo.
[Picha katika ukurasa wa 3]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Jaribu Kuitumia
1 Andika www.jw.org kwenye sehemu ya anwani iliyo katika programu ya kutafutia ya Intaneti kwenye kompyuta yako.
2 Chunguza yaliyomo katika Tovuti hiyo kwa kubonyeza vichwa vya sehemu za Tovuti, orodha ya mambo unayoweza kuchagua, na viunganishi.
3 Jaribu kutumia Tovuti ya jw.org kwenye kifaa chako kinachobebeka kilichounganishwa na Intaneti kama vile simu ya mkononi. Muundo au mpangilio wa kurasa unaweza kutoshea kwenye vifaa hivyo vidogo, na habari ni zile zile.