Utamwambia Nini Mwislamu?
1 Je, umewahi kumhubiria Mwislamu? Ikiwa ndivyo, huenda umeona kwamba Waislamu wana imani yenye nguvu katika Mungu. Hata hivyo, wanajua mambo machache kuhusu Paradiso itakayokuwa duniani kama ilivyotabiriwa na manabii wa Yehova, na tungependa kuwajulisha tumaini hilo. (1 Tim. 2:3, 4) Habari ifuatayo itakusaidia kutoa ushahidi mzuri.
2 Waislamu humwamini Allah, au Mungu, na huamini kwamba Muhammad ni mtume wa Mungu. Kitabu chao kitakatifu ni Kurani, na dini yao inaitwa Uislamu, jina linalomaanisha “unyenyekevu.” Kurani inasema kuwa kusema uwongo na kuabudu sanamu ni kosa, na kwamba Mungu ni mmoja na yeye si sehemu ya Utatu. Pia, inafundisha kuhusu kutokufa kwa nafsi, moto wa mateso, na paradiso ya mbinguni. Waislamu wanakubali Biblia kuwa Neno la Mungu lakini wanaamini kwamba imebadilishwa, ilhali Kurani iliyo katika lugha yake ya awali, haijatiwa unajisi.
3 Uwe Mwenye Urafiki, Busara, na Utambuzi: Unapoongea na Mwislamu, uwe mwenye urafiki na busara. (Met. 25:15) Kumbuka kwamba Waislamu huwa na imani zilizotia mizizi na wengi wao wamejifunza imani hizo kwa kukariri. Hivyo, kutumia uwezo wa kufikiri ili kujadili mafundisho ya dini na kujihakikishia wenyewe mapenzi ya Mungu ni nini si sehemu ya ukuzi wao wa kiroho. (Rom. 12:2) Ili kuwasaidia Waislamu ni muhimu tuwaelewe na tuwe wenye subira.—1 Kor. 9:19-23.
4 Epuka kutumia maneno ambayo yatamfanya Mwislamu afikiri kwamba wewe ni mshiriki wa dini zinazodai kuwa za Kikristo. Mweleze wazi kwamba wewe ni tofauti na si Mkatoliki au Mprotestanti. Unaporejelea Biblia tumia jina Kitabu cha Mungu. Kwa kuwa Waislamu huuchukia msemo “Mwana wa Mungu,” kwa kawaida ni vizuri zaidi kutoutumia au kutozungumzia jambo hilo mpaka atakapokuwa amefanya maendeleo ya kiroho. Hata hivyo, unaweza kuzungumza kuhusu Yesu kwa kumtaja kuwa nabii au mjumbe. Epuka mabishano. Ukiona ameanza kukasirika, ondoka mara moja.
5 Ni bora kuongea na mtu mmoja tu badala ya kikundi cha watu. Kwa kawaida, inapendekezwa wanawake waongee na wanawake na wanaume waongee na wanaume. Bila shaka, hali hutofautiana, lakini ni vizuri kutumia utambuzi. Pia, Waislamu wengi huzingatia sana jinsi wanawake wanavyovaa na kujipamba. Akina dada wanahitaji kuzingatia jambo hilo.—1 Kor. 10:31-33.
6 Mambo ya Kuzungumzia: Zungumza waziwazi kuhusu ukuu wa Mungu na upendo wake. Usisite kueleza kuwa wewe ni mwabudu wa kweli, na kwamba Mungu ni mmoja (si Utatu), na haifai kuabudu sanamu. Zungumzia kuhusu uovu ulio ulimwenguni leo—vita, mapigano ya wenyewe kwa wenyewe, chuki ya kijamii, na unafiki unaoonekana wazi miongoni mwa wanadini wengi.
7 Broshua Mwongozo wa Mungu—Njia Yetu ya Kwenda Paradiso ina habari zaidi ambazo unaweza kutumia kuanzisha mazungumzo na Waislamu. Imekusudiwa kuwavutia Waislamu wanaoishi katika maeneo ambayo wanaweza kujihisi huru kujifunza Biblia.
8 Unaweza kusema hivi: “Ninafanya jitihada ya pekee ili kuzungumza na Waislamu. Nimekuwa nikisoma kuhusu dini yenu na ninatumaini kuwa sijakosea nikisema kwamba Waislamu humwamini Mungu mmoja wa kweli na manabii wote. [Mruhusu ajibu.] Ningependa kuongea nawe kuhusu unabii fulani wa zamani ambao ulitabiri jinsi dunia itakavyobadilishwa kuwa paradiso. Je, ninaweza kukusomea mambo ambayo nabii aliandika? [Soma Isaya 11:6-9.] Unabii huu unanifanya nifikirie nukuu fulani ya Kurani inayopatikana katika broshua hii.” Fungua ukurasa wa 9 katika broshua Mwongozo wa Mungu, na usome nukuu yenye maandishi mazito, ambayo inazungumzia kuhusu waadilifu kuirithi dunia. Akionyesha upendezi, endeleza mazungumzo kwa kuzungumzia fungu la 7 hadi 9 katika ukurasa wa 8. Mwachie broshua, na upange kufanya ziara ya kurudia.—Kwa pendekezo lingine, ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Februari 1998, ukurasa wa 6, fungu la 27.
9 Unapomwomba mtu fulani mzungumzie broshua Mwongozo wa Mungu, ni afadhali zaidi kutumia neno mazungumzo, badala ya funzo la Biblia. Mnapomaliza kuzungumzia broshua hiyo, mwanafunzi anapaswa kuwa tayari kujifunza broshua Habari Njema au kitabu Biblia Inafundisha. Machapisho mengine ambayo yamekusudiwa hasa kwa ajili ya Waislamu ni trakti Jinsi ya Kuipata Barabara ya Kwenda Kwenye Paradiso, kijitabu Sasa Ndio Wakati wa Kumtii Mungu Kweli Kweli, na broshua Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha.
10 Kujua imani za Waislamu na mambo wanayozingatia sana, kutatuwezesha kutambua ni machapisho gani tunayoweza kuwaachia na jinsi tutakavyowahubiria. Yehova na aendelee kubariki jitihada zetu za kuwasaidia watu wa namna zote waliitie jina lake na kuokolewa.—Mdo. 2:21.