Wachukueni Manabii Kuwa Kielelezo—Hosea
1. Huenda umewahi kujiuliza swali gani?
1 ‘Niko tayari kudhabihu mambo gani ili kumtumikia Yehova?’ Huenda umejiuliza swali hilo ulipokuwa ukitafakari kuhusu wema na rehema nyingi za Yehova. (Zab. 103:2-4; 116:12) Hosea alikuwa tayari kufanya yote ambayo Yehova alimwamuru, hata ingawa ilimbidi ajinyime mambo fulani. Tunaweza kumwiga Hosea katika njia gani?
2. Tunawezaje kuiga mfano mzuri wa Hosea wa kuendelea kuhubiri bila kuacha?
2 Hubiri Katika Majira Yenye Taabu: Ujumbe wa Hosea ulielekezwa moja kwa moja kwa ufalme wa makabila kumi ya Israeli, ambapo ibada ya kweli ilikuwa karibu kutoweka. Mfalme Yeroboamu wa Pili alifanya yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova na akaendeleza ibada ya ndama iliyoanzishwa na Yeroboamu wa Kwanza. (2 Fal. 14:23, 24) Wafalme waliofuata waliendelea kudhoofisha hali ya kiroho ya ufalme wa makabila kumi mpaka ufalme huo ulipoharibiwa mwaka wa 740 K.W.K. Licha ya kwamba ibada ya uwongo ilikuwa imekita mizizi, Hosea alitumikia kwa uaminifu akiwa nabii kwa miaka isiyopungua 59. Je, sisi pia tumeazimia kuhubiri mwaka baada ya mwaka, licha ya kukabili ubaridi au upinzani?—2 Tim. 4:2.
3. Maisha ya Hosea yanaonyeshaje rehema ya Yehova?
3 Kazia Fikira Rehema za Yehova: Yehova alimwagiza Hosea amchukue “mke wa uasherati.” (Hos. 1:2) Ijapokuwa mke wake, Gomeri, alimzalia mwana, baadaye alizaa watoto wawili nje ya ndoa. Utayari wa Hosea wa kumsamehe mke wake ulionyesha jinsi Yehova alivyokuwa tayari kuwasamehe Waisraeli walipotubu. (Hos. 3:1; Rom. 9:22-26) Je, tuko tayari kuacha mapendezi yetu ya kibinafsi ili tutangaze rehema za Yehova kwa watu wa namna zote?—1 Kor. 9:19-23.
4. Ni mambo gani tunayoweza kudhabihu ili kumtumikia Yehova?
4 Baadhi ya watumishi wa Yehova wamedhabihu fursa za kupata ufanisi wa kimwili ili watumie muda mwingi katika huduma. Wengine wamebaki wakiwa waseja au bila watoto ili watangulize masilahi ya Ufalme. Tunapofikiria kuhusu maisha ya Hosea, huenda tukahisi hivi, ‘Nisingeweza kufanya kama yeye.’ Hata hivyo, tunapoendelea kukuza uthamini wetu kwa fadhili za Yehova zisizostahiliwa na kutegemea roho yake takatifu, anaweza kututumia katika njia ambazo hatungewahi kuwazia, kama vile tu Hosea.—Mt. 19:26; Flp. 2:13.