Endelea Kufanya Maendeleo Ukiwa Mhudumu
1. Ni mifano gani ya karne ya kwanza inayoonyesha kwamba tunapaswa kufanya maendeleo tukiwa wahudumu?
1 Wakristo wanapaswa kufanya maendeleo wakiwa wahudumu. Hiyo ndiyo sababu Yesu aliwazoeza wafuasi wake hatua kwa hatua katika kazi ya kuhubiri. (Luka 9:1-5; 10:1-11) Hiyo pia ndiyo sababu Akila na Prisila walimchukua Apolo na “kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.” (Mdo. 18:24-26) Kwa sababu hiyohiyo, Paulo alimtia moyo Timotheo, mweneza-injili mwenye uzoefu, aendelee kufanya bidii katika kufundisha ili maendeleo yake “yawe wazi kwa watu wote.” (1 Tim. 4:13-15) Hata ikiwa tumemtumikia Bwana kwa muda mrefu kadiri gani tukiwa wahubiri wa habari njema, tunahitaji kuendelea kuboresha ustadi wetu wa kuhubiri.
2. Tunawezaje kujifunza kutoka kwa wengine?
2 Jifunze Kutoka kwa Wengine: Njia moja ya kuboresha ustadi wetu ni kujifunza kutoka kwa wengine. (Met. 27:17) Kwa hiyo, sikiliza kwa makini wahubiri wenzako wanapohubiri. Omba mashauri kutoka kwa wahubiri wenye uzoefu, na usikilize kwa makini wanayosema. (Met. 1:5) Je, una wasiwasi kuhusu kufanya ziara za kurudia, kuanzisha funzo la Biblia, au kushiriki katika aina fulani ya utumishi? Chukua hatua ya kwanza, na umwombe msaada mwangalizi wako wa kikundi au mhubiri mwenye uzoefu. Pia, kumbuka kwamba roho takatifu inaweza kuboresha uwezo wetu, hivyo sali kwa ukawaida ili upate roho hiyo.—Luka 11:13.
3. Tunapaswa kutendaje tunapopewa mapendekezo, ambayo huenda hatukuomba?
3 Usikasirike unapopewa mapendekezo ya kukusaidia kufanya maendeleo, hata kama hukuomba ushauri. (Mhu. 7:9) Kama Apolo, kubali msaada kwa unyenyekevu na uwe mwenye shukrani. Ukifanya hivyo, utaonyesha hekima.—Met. 12:15.
4. Yesu alitoa sababu gani yenye nguvu inayotuchochea kufanya maendeleo tukiwa waeneza-injili?
4 Maendeleo Humtukuza Mungu: Akitumia mfano, Yesu aliwatia moyo wafuasi wake wafanye maendeleo wakiwa wahudumu. Alijifananisha na mzabibu na kuwafananisha wafuasi wake watiwa mafuta na matawi. Alisema kwamba Baba yake hulisafisha kila tawi linalozaa matunda ili “lipate kuzaa matunda zaidi.” (Yoh. 15:2) Kama vile mmiliki wa shamba la mizabibu anavyotaka mizabibu yake izae vizuri zaidi, Yehova anataka tuendelee kuboresha uwezo wetu wa kutoa “tunda la midomo.” (Ebr. 13:15) Tunapata matokeo gani tunapofanya maendeleo tukiwa waeneza-injili? Yesu alitoa jibu aliposema: “Baba yangu hutukuzwa katika hili, kwamba mwendelee kuzaa matunda mengi.”—Yoh. 15:8.