Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • mwbr16 Desemba kur. 1-2
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha
  • Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2016
  • Vichwa vidogo
  • DESEMBA 5-11
  • DESEMBA 12-18
Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha—2016
mwbr16 Desemba kur. 1-2

Marejeo ya Daftari la Huduma na Maisha

DESEMBA 5-11

Kutafuta Hazina za Kiroho

it-2 761 ¶3

Upatanisho

Hatua muhimu za kufanya upatanisho. Wanadamu ndio wanaopaswa kujipatanisha na Mungu kwa kuwa Mungu ndiye aliyekosewa na sikuzote amri zake zimekuwa zikikiukwa. (Zb 51:​1-4) Mwanadamu halingani na Mungu, na viwango vya Mungu vya yaliyo sawa haviwezi kubadilishwa, kurekebishwa, au kuboreshwa. (Isa 55:​6-11; Mal 3:6; linganisha na Yak 1:17.) Kwa hiyo, matakwa yake kwa ajili ya upatanisho hayapaswi kujadiliwa, kutiliwa shaka, au kubadilishwa. (Linganisha na Ayu 40:​1, 2, 6-8; Isa 40:​13, 14.) Watafsiri mbalimbali wametafsiri Isaya 1:18 hivi, “Haya, njoni, tusemezane, asema BWANA” (UV), lakini tafsiri inayofaa na inayotegemeka inasema hivi: “‘Sasa, njooni, nasi tunyooshe mambo kati yetu,’ asema Yehova.” Kosa lililotokeza uhitaji wa upatanisho ni la wanadamu wala si la Mungu.​—Linganisha na Eze 18:​25, 29-32.

DESEMBA 12-18

Kutafuta Hazina za Kiroh

it-1 1219

Isaya

Isaya alipokuwa akitumikia akiwa nabii, hasa katika kipindi cha Mfalme Ahazi, ufalme wa Yuda ulikuwa katika hali mbaya kiadili. Uasi ulikuwa umeenea kati ya wakuu na watu, na machoni pa Yehova, taifa lilikuwa na ugonjwa moyoni na akilini. Watawala walikuwa wakiitwa “madikteta wa Sodoma” na watu walikuwa kama “watu wa Gomora.” (Isa 1:​2-10) Isaya aliambiwa mapema kwamba masikio yao yangekuwa magumu. Yehova alisema kwamba hali hiyo ingeendelea mpaka taifa lingepatwa na uharibifu na kwamba “sehemu ya kumi,” “uzao mtakatifu,” ndio tu ungebaki kama kisiki cha mti mkubwa. Lazima kazi ya Isaya ya kutoa unabii iwe iliwafariji na kuimarisha imani ya watu hao wachache, hata ingawa watu wengi katika taifa hilo walipuuza onyo alilotoa.​—Isa 6:​1-13.

Licha ya kutoa unabii kuhusu Yuda, Isaya pia alitoa unabii kuhusu Israeli na mataifa yaliyozunguka taifa hilo, kwa kuwa yaliathiri hali na historia ya Yuda. Isaya alifanya kazi ya kutoa unabii kwa muda mrefu, kuanzia mwaka wa 778 K.W.K., wakati Mfalme Uzia alipokufa, au huenda mapema zaidi, na aliendelea mpaka wakati fulani baada ya mwaka wa 14 wa utawala wa Hezekia (732 K.W.K.).​—Isa 36:​1, 2; 37:​37, 38.

Familia ya Isaya. Isaya alikuwa amefunga ndoa. Mke wake aliitwa “nabii wa kike” (Isa 8:3), jina ambalo inaonekana halikumaanisha tu kwamba alikuwa mke wa nabii. Inaonekana, alikuwa na mgawo wa kutoa unabii kutoka kwa Yehova kama vile Debora aliyeishi wakati wa Waamuzi na Hulda aliyeishi wakati wa utawala wa Yosia.​—Amu 4:4; 2Fa 22:14.

Biblia inaeleza majina ya wana wawili wa Isaya, aliopewa kama “ishara na kama miujiza katika Israeli.” (Isa 8:18) Shear-yashubu alikuwa na umri wa kutosha kuandamana na baba yake wakati wa siku za Ahazi ili kwenda kupeleka ujumbe kwa mfalme huyo. Jina Shear-yashubu linamaanisha “Mabaki Wachache (Wale Watakaobaki) Tu Ndio Watakaorudi.” Jina hilo lilikuwa la kinabii katika maana ya kwamba kama ilivyo hakika kwamba mwana wa Isaya alipewa jina hilo, vivyo hivyo, baada ya muda, ufalme wa Yuda ungeangushwa na mabaki wachache tu wangerudi baada ya kipindi cha uhamisho. (Isa 7:3; 10:​20-23) Kurudi kwa mabaki hao wachache kulitukia mwaka wa 537 K.W.K. wakati Mfalme Koreshi wa Uajemi alipotoa agizo la kuwaachilia huru mabaki hao kutoka Babiloni baada ya kukaa uhamishoni kwa miaka 70.​—2Nya 36:​22, 23; Ezr 1:1; 2:​1, 2.

Mwana mwingine wa Isaya alipewa jina kabla ya kutungwa kwa mimba yake, na jina lake liliandikwa kwenye bamba na kushuhudiwa na mashahidi waliotegemeka. Inaelekea kwamba jambo hilo lilikuwa siri mpaka mtoto huyo alipozaliwa, wakati ambapo mashahidi wangekuja na kuthibitisha kwamba nabii alikuwa ametabiri kuhusu kuzaliwa kwake, na hivyo kuthibitisha kwamba kuzaliwa huko kulikuwa na umuhimu wa kinabii. Jina alilopewa mvulana huyo kutokana na amri ya Mungu lilikuwa Maher-shalal-hash-bazi, linalomaanisha “Fanya Hima, Ewe Nyara! Amekuja Upesi Kwenye Nyara; au, Fanya Hima Kwenye Nyara, Amekuja Upesi Kwenye Nyara.” Ilisemwa kwamba hata kabla mvulana huyo hajajua kusema “Baba yangu!” na “Mama yangu!” vitisho vilivyoikabili Yuda kutoka kwa taifa la Siria na ufalme wa makabila kumi wa Israeli vingeondolewa.​—Isa 8:​1-4.

Unabii huo ulionyesha kwamba kitulizo cha Yuda kingekuja upesi; kitulizo kilikuja Waashuru walipozuia kampeni ya Mfalme Resini wa Siria pamoja na Mfalme Peka wa Israeli dhidi ya Yuda. Waashuru waliteka Damasko na hatimaye mwaka wa 740 K.W.K. wakauharibu ufalme wa Israeli. Jambo hilo lilitimiza kikamili maana ya kinabii ya jina la mvulana huyo. (2Fa 16:​5-9; 17:​1-6) Hata hivyo, badala ya kumtegemea Yehova, Mfalme Ahazi alijaribu kukabiliana na tisho la Siria na Israeli kwa kumpa rushwa mfalme wa Ashuru ili alindwe. Kwa sababu hiyo, Yehova aliruhusu Waashuru wawe tishio kubwa kwa Yuda na kwa kweli waliingia na kushambulia nchi hiyo mpaka wakafika Yerusalemu, kama Isaya alivyokuwa ameonya.​—Isa 7:​17-20.

Isaya alisema mara nyingi kuhusu “ishara” ambazo Yehova angetoa. Miongoni mwa ishara hizo ni ile ya watoto wake wawili, na katika kisa kimoja, Isaya mwenyewe alikuwa ishara. Yehova alimwamuru atembee akiwa uchi na miguu wazi kwa miaka mitatu kama ishara na utabiri dhidi ya Misri na Ethiopia, ambazo zingechukuliwa mateka na mfalme wa Ashuru.​—Isa 20:​1-6; linganisha na Isa 7:​11, 14; 19:20; 37:30; 38:​7, 22; 55:13; 66:19.

Unabii Kuhusu Kupelekwa Uhamishoni na Kurudishwa. Isaya alikuwa na pendeleo lingine la kutabiri kwamba Waashuru hawangeondoa utawala wa Yuda na kuharibu jiji la Yerusalemu, lakini Wababiloni ndio wangefanya hivyo. (Isa 39:​6, 7) Wakati jeshi la Ashuru lilipofurika kwenye jiji la Yuda “mpaka shingoni,” Isaya alitoa ujumbe wenye kufariji kwa Mfalme Hezekia kwamba jeshi la Waashuru lisingeweza kuingia ndani ya jiji. (Isa 8:​7, 8) Yehova alitimiza neno Lake kwa kumtuma malaika awaue askari-jeshi 185,000 ambao walikuwa wanaume shujaa na wenye nguvu pamoja na viongozi wao, hivyo akaliokoa Yerusalemu.​—2Nya 32:21.

Jambo ambalo bila shaka lilimpatia Isaya shangwe kubwa lilikuwa pendeleo alilopewa na Yehova la kutangaza na kuandika unabii mwingi kuhusu kujengwa upya kwa jiji alilolipenda sana la Yerusalemu. Ingawa Yehova angeruhusu watu wake wapelekwe uhamishoni Babiloni kwa sababu ya uasi na kufanya mambo yaliyomchukiza, kwa wakati wake Mungu angeihukumu Babiloni kwa sababu ilikuwa na nia mbaya ilipowashambulia watu wa Mungu na ilikusudia kuwafanya wakae utekwani milele. Unabii fulani wa Isaya ulihusu hukumu ya Mungu kuelekea jiji la Babiloni, jinsi lingekuwa ukiwa, na kwamba halingejengwa tena.​—Isa 45:​1, 2; sura ya 13, 14, 46-48.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki