Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
DESEMBA 2-8
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | UFUNUO 7-9
“Umati Mkubwa Usioweza Kuhesabiwa Utabarikiwa na Yehova”
it-1 997 ¶1
Umati Mkubwa
Hilo linatokeza swali: Ikiwa “umati mkubwa” ni watu wanaopata wokovu na kubaki duniani, inawezaje kusemwa kwamba “wamesimama mbele ya kiti cha ufalme na mbele ya Mwanakondoo”? (Ufu 7:9) Neno ‘kusimama’ mara nyingine linatumiwa katika Biblia kuonyesha kibali machoni pa yule ambaye mtu au kikundi fulani kinasimama. (Zb 1:5; 5:5; Met 22:29, AT; Lu 1:19) Kwa kweli, sura iliyotangulia ya Ufunuo inasema kwamba “wafalme wa dunia, maofisa wa cheo cha juu, viongozi wa kijeshi, matajiri, wenye nguvu, kila mtumwa, na kila mtu aliye huru” wanaonyeshwa kuwa wanataka kujificha “kutoka kwenye uso wa Yule anayeketi kwenye kile kiti cha ufalme na kutoka kwenye ghadhabu ya Mwanakondoo, kwa sababu siku kuu ya ghadhabu yao imekuja, na ni nani anayeweza kusimama?” (Ufu 6:15-17; linganisha Lu 21:36.) Hivyo, inaonekana kwamba “umati mkubwa” inafanyizwa na watu waliohifadhiwa katika kipindi hicho cha ghadhabu na ambao wamefaulu ‘kusimama’ wakiwa na kibali cha Mungu na Mwanakondoo.
it-2 1127 ¶4
Dhiki
Miaka 30 hivi baada ya Yerusalemu kuharibiwa, mtume Yohana aliambiwa hivi kuhusu umati mkubwa wa watu kutoka mataifa yote, makabila, na watu: “Hawa ndio wale wanaotoka katika ile dhiki kuu.” (Ufu 7:13, 14) Ukweli wa kwamba umati mkubwa ‘unatoka katika ile dhiki kuu’ unaonyesha kwamba wataokoka dhiki hiyo. Hilo linathibitishwa na maneno yanayolingana na hayo katika Matendo 7:9, 10: “Mungu alikuwa pamoja [na Yosefu], akamkomboa kutoka katika dhiki zake zote.” Kukombolewa kwa Yosefu hakumaanishi tu kwamba aliwezeshwa kuvumilia dhiki hizo, bali pia alifanikiwa kukabiliana nazo hadi zilipokwisha.
it-1 996-997
Umati Mkubwa
Utambulisho. Jambo moja la msingi linaloweza kutusaidia kutambulisha “umati mkubwa” ni ufafanuzi unaopatikana katika Ufunuo sura ya 7 na katika maandiko mengine yanayozungumzia habari zinazofanana na hizo. Ufunuo 7:15-17 inasema kwamba Mungu “atatandaza hema lake juu yao,” kwamba wanaongozwa kwenye “chemchemi za maji ya uzima,” na kuwa Mungu atafuta “kila chozi katika macho yao.” Katika Ufunuo 21:2-4 tunapata maneno kama hayo: “Hema la Mungu [litakuwa] pamoja na wanadamu,” kwamba “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao,” na kuwa “kifo hakitakuwapo tena.” Maono yanayotajwa hayahusu watu walio mbinguni, ambako ‘Yerusalemu Jipya linashuka,’ bali duniani, kati ya wanadamu.
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-1 12
Abadoni
Abadoni, malaika wa abiso—ni nani? Hata hivyo, katika Ufunuo 9:11, neno “Abadoni” linatajwa kuwa jina la “malaika wa shimo refu lisilo na mwisho.” Neno linalolingana na hilo la Kigiriki Apollyon linamaanisha “Mwangamizaji.” Katika karne ya 19 kulikuwa na jitihada za kuonyesha kwamba andiko hilo lilizungumzia mfano wa kinabii ambao ulihusianishwa na watu kama Maliki Vespasian, Muhammad, na hata Napoleon, na kwa kawaida malaika huyo alionwa kuwa wa “kishetani.” Hata hivyo, katika Ufunuo 20:1-3 malaika anayetajwa kuwa na “ufunguo wa shimo refu lisilo na mwisho” anaonyeshwa kuwa mwakilishi wa Mungu kutoka mbinguni, na badala ya kuwa wa “kishetani,” anamfunga Shetani ndani ya shimo refu lisilo na mwisho. Kitabu kimoja cha marejeo (The Interpreter’s Bible) kinasema hivi kuhusu Ufunuo 9:11: “Hata hivyo, Abadoni si malaika wa Shetani bali wa Mungu, akifanya kazi ya kuangamiza kwa amri ya Mungu.”
Katika maandiko ya Kiebrania yaliyozungumziwa hapo juu, ni wazi kwamba neno ʼavad·dohnʹ lina maana sawa na neno Sheoli na kifo. Katika Ufunuo 1:18 tunamwona Kristo Yesu akisema hivi: “Ninaishi milele na milele, nami nina funguo za kifo na za Kaburi.” Nguvu zake kuhusiana na abiso zinaonyeshwa katika Luka 8:31. Andiko la Waebrania 2:14 linaonyesha kwamba ana uwezo wa kuangamiza, kutia ndani kumwangamiza Shetani. Andiko hilo linasema kwamba Yesu alishiriki damu na mwili ili “kupitia kifo chake amwangamize yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi.” Katika Ufunuo 19:11-16 anaelezwa waziwazi kuwa Mwangamizaji au Mtekelezaji wa Hukumu wa Mungu aliyemweka rasmi.—Ona APOLLYON.
DESEMBA 9-15
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 880-881
Kitabu cha kukunjwa
Matumizi ya mfano. Kwa mara kadhaa neno “kitabu cha kukunjwa” kimetajwa kwa njia ya mfano katika Biblia. Ezekieli na Zekaria waliona kitabu cha kukunjwa chenye maandishi pande zote mbili. Kwa kuwa ni upande mmoja tu wa kitabu cha kukunjwa ulioandikwa, huenda kuandika pande zote mbili kulirejelea uzito, ukubwa, na umuhimu wa hukumu zilizokuwa katika vitabu hivyo. (Eze 2:9–3:3; Zek 5:1-4) Katika maono ya Ufunuo, yule aliyeketi kwenye kile kiti cha ufalme alikuwa na kitabu cha kukunjwa alichoshika kwenye mkono wa kuume, kitabu hicho kilikuwa na mihuri saba, ambayo ilizuia mtu kuona maandishi yaliyomo hadi Mwanakondoo wa Mungu aifungue. (Ufu 5:1, 12; 6:1, 12-14) Baadaye katika maono, Yohana mwenyewe alipewa kitabu cha kukunjwa na kuamriwa ale kitabu hicho. Kilikuwa kitamu kwa Yohana lakini kilifanya tumbo lake liwe chungu. Kwa kuwa kitabu cha kukunjwa kilikuwa kimefunguliwa na hakikuwa na mihuri, ujumbe wake ulipaswa kueleweka. Ujumbe ambao Yohana aliupata ulikuwa ‘mtamu’ lakini inaonekana ulikuwa unabii wa mambo machungu kuyatangaza, kama alivyoambiwa afanye. (Ufu 10:1-11) Ezekieli alipitia hali kama hiyo alipopewa kitabu cha kukunjwa kilichokuwa na “huzuni na maombolezo na vilio.”—Eze 2:10.
it-2 187 ¶7-9
Maumivu ya Kuzaa
Katika maono ya mtume Yohana ya Ufunuo alimwona mwanamke wa kimbingu akilia “akiwa katika maumivu na uchungu wa kuzaa.” Mtoto aliyezaliwa alikuwa “mwana, wa kiume, atakayechunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma.” Licha ya jitihada za joka za kutaka kummeza “mtoto wake akanyakuliwa mpaka kwa Mungu na kwenye kiti chake cha ufalme.” (Ufu 12:1, 2, 4-6) Kunyakuliwa kwa mtoto huyo mpaka kwa Mungu kunaonyesha kwamba Mungu anamkubali mwana huyo kuwa wake, kama ilivyokuwa desturi katika nyakati za kale baba alikuwa akipewa mwana aliyezaliwa ili amkubali. (Ona KUZAA.) Inamaanisha kwamba “mwanamke” huyo ni “mke” wa Mungu, yaani, “Yerusalemu la juu,” ambalo ni “mama” ya Kristo na ndugu zake wa kiroho.—Gal 4:26; Ebr 2:11, 12, 17.
Bila shaka, “mwanamke” wa Mungu wa kimbingu angekuwa mkamilifu, na angezaa bila maumivu halisi. Hivyo, maumivu ya kuzaa yangeonyesha kwamba “mwanamke” huyo angegundua kuwa wakati wa kuzaa umefika; angetarajia jambo hilo upesi.—Ufu 12:2.
Huyu “Mwana wa kiume” angekuwa nani? Mwana huyo “[angechunga] mataifa yote kwa fimbo ya chuma.” Hilo lilitabiriwa kumhusu Mfalme wa Mungu wa Kimasihi katika Zaburi 2:6-9. Lakini Yohana aliona maono hayo muda mrefu baada ya Kristo kuzaliwa duniani, kufa, na kufufuliwa. Hivyo, maono hayo yanaonekana yanarejelea kuzaliwa kwa Ufalme wa Kimasihi mikononi mwa Mwana wa Mungu Yesu Kristo, ambaye alipofufuliwa kutoka kwa wafu, “[aliketi] kwenye mkono wa kuume wa Mungu, tangu wakati huo akisubiri mpaka adui zake wawekwe kuwa kiti cha miguu yake.”—Ebr 10:12, 13; Zb 110:1; Ufu 12:10.
DESEMBA 23-29
HAZINA ZA NENO LA MUNGU | UFUNUO 17-19
it-1 1146 ¶1
Farasi
Katika maono aliyoona mtume Yohana, Yesu Kristo aliyetukuzwa anaonyeshwa akiendesha farasi mweupe na kuandamana na jeshi, ambalo washiriki wake wote wameketi juu ya farasi weupe. Maono hayo yalifunuliwa kwa Yohana yakiwakilisha uadilifu na haki ya vita ambavyo Kristo atapigana dhidi ya maadui wote kwa ajili ya Mungu na Baba yake, Yehova. (Ufu 19:11, 14) Kabla ya hilo, tendo la Kristo kuchukua ufalme na majanga yaliyofuata yaliwakilishwa na wapanda farasi mbalimbali na farasi wao.—Ufu 6:2-8.
DESEMBA 30–JANUARI 5
Kutafuta Hazina za Kiroho
it-2 249 ¶2
Uhai
Katika amri aliyompa Adamu, Mungu alidokeza kwamba ikiwa Adamu angetii, hangekufa. (Mwa 2:17) Hivyo, adui wa mwisho, kifo atakapoondolewa, miili ya wanadamu watiifu haitakuwa na dhambi inayosababisha kifo. Hawatakufa mpaka wakati usio na kipimo. (1Ko 15:26) Kuangamizwa kwa kifo kunatukia mwishoni mwa utawala wa Kristo, utawala ambao kitabu cha Ufunuo kinaonyesha utakuwa wa miaka 1,000. Wale watakaokuwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo wanasemwa kwamba “wakawa hai na kutawala wakiwa wafalme pamoja na Kristo kwa miaka 1,000.” Inaonekana kwamba “wale wafu wengine” ambao hawakuwa hai “mpaka ile miaka 1,000 ilipokwisha” ni wale watakaokuwa hai mwishoni mwa ile miaka elfu, lakini wanafanywa kuwa hai kabla ya Shetani kuachiliwa kutoka katika shimo refu lisilo na mwisho na kuleta jaribu la mwisho juu ya wanadamu. Kufikia mwishoni mwa miaka elfu moja, watu duniani watakuwa wamefikia ukamilifu wa kibinadamu, hali ambayo Adamu na Hawa walikuwa nayo kabla ya kufanya dhambi. Sasa watakuwa na maisha makamilifu. Wale ambao baada ya hapo watapita jaribu la Shetani atakapoachiliwa kwa muda mfupi kutoka shimo refu lisilo na mwisho, wataweza kufurahia maisha milele.—Ufu 20:4-10.
it-2 189-190
Ziwa la Moto
Msemo huo unapatikana tu katika kitabu cha Ufunuo na ni wazi kwamba ni wa mfano. Biblia inatupa ufafanuzi wa msemo huo ikisema hivi: “Hilo linamaanisha kifo cha pili, lile ziwa la moto.”—Ufu 20:14; 21:8.
Inaonekana wazi kwamba ziwa la moto ni la mfano unapochunguza muktadha wa marejeo yake katika kitabu cha Ufunuo. Kifo kinasemekana kwamba kinatupwa ndani ya ziwa hilo la moto. (Ufu 19:20; 20:14) Bila shaka kifo hakiwezi kuteketezwa kihalisi. Pia, Ibilisi, kiumbe wa roho, anatupwa ndani ya ziwa hilo. Kwa kuwa yeye ni roho, hawezi kuumizwa na moto halisi.—Ufu 20:10; linganisha Kut 3:2 na Amu 13:20.
Kwa kuwa ziwa la moto linafananisha “kifo cha pili” na kwa kuwa Ufunuo 20:14 inasema kwamba “kifo na Kaburi” vinatupwa ndani yake, inaonekana kwamba ziwa hilo haliwezi kuwakilisha kifo ambacho mwanadamu amerithi kutoka kwa Adamu (Ro 5:12), wala haliwezi kuwakilisha Kaburi (Sheoli). Hivyo basi, ziwa hilo linawakilisha aina tofauti ya kifo, kifo ambacho hakiwezi kutenguliwa, kwa sababu rekodi haizungumzii popote kwamba “ziwa” likitoa wafu waliomo, kama inavyosema kuhusu wale waliokufa kutokana na kifo kilichotokana na Adamu na Hadesi (Sheoli). (Ufu 20:13) Kwa hiyo, wale ambao hawapatikani wakiwa wameandikwa katika “kitabu cha uzima,” wapinzani wasiotubu wa enzi kuu ya Mungu, wanatupwa ndani ya ziwa la moto, yaani, kuangamizwa milele, au kupatwa na kifo cha pili.—Ufu 20:15.