Marejeo ya Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha
MEI 6-12
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 36-37
Hazina za Kiroho
it-2 445
Mlima
Uimara, udumifu, au kukwezwa. Milima huonwa kuwa imara na ya kudumu. (Isa 54:10; Hab 3:6; linganisha Zb 46:2) Hivyo, mtunga-zaburi alipozungumza kuhusu uadilifu wa Yehova kuwa kama “milima ya Mungu” (Zb 36:6, maelezo ya chini) huenda alimaanisha kwamba uadilifu wa Mungu hauwezi kutikisika. Au, kwa kuwa milima imeinuka sana, huenda hilo likarejelea ukweli wa kwamba uadilifu wa Mungu unazidi kwa mbali ule wa mwanadamu. (Linganisha Isa 55:8, 9.) Kuhusiana na kumwagwa kwa bakuli la saba la hasira ya Mungu, Ufunuo 16:20 inasema hivi: “Milima haikupatikana tena.” Hilo linadokeza kwamba hata vitu vilivyokwezwa kama milima havitaokoka kutekelezwa kwa hasira ya Mungu.—Linganisha Yer 4:23-26.
MEI 27–JUNI 2
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 42-44
Hazina za Kiroho
it-1 1242
Mbwamwitu
Katika maandiko mbwamwitu anatajwa mara nyingi katika njia ya mfano. Ayubu alipofafanua hali yake yenye kusikitisha, alisema kwamba amekuwa “ndugu ya mbwamwitu.” (Ayu 30:29) Mtunga-zaburi alisema hivi akiomboleza kuhusiana na kushindwa kwa aibu kwa watu wa Mungu, labda akirejelea uwanja wa vita ambako mbwamwitu hukusanyika ili kula maiti za waliouawa (linganisha Zb 68:23): “Umetuponda mahali ambapo mbwamwitu wanakaa.” (Zb 44:19) Wababiloni walipozingira Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. kulikuwa na hali ngumu sana na pia kulikuwa na njaa kali, hivi kwamba akina mama waliwatendea watoto wao wenyewe kwa ukatili. Kwa sababu hiyo, Yeremia alitofautisha ukatili wa “watu wangu” na jinsi ambavyo mbwamwitu huwatunza watoto wao.—Omb 4:3, 10.
JUNI 3-9
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 45-47
it-2 1169
Vita
Vita hivyo vitakapokwisha, kutakuwa na amani duniani kwa miaka elfu moja. Zaburi inayosema “[Yehova] anakomesha vita katika dunia yote. Anauvunja upinde na kuuvunja mkuki vipandevipande; anayateketeza magari ya vita motoni,” ilitimia kwa mara ya kwanza Mungu alipoleta amani katika nchi ya Israeli kwa kuharibu vifaa vya vita vya maadui wao. Baada ya Kristo kuwashinda wanaoendeleza vita kwenye Har–Magedoni, kila sehemu ya dunia itafurahia amani ya kudumu na inayoridhisha. (Zb 46:8-10) Watu ambao watastahili kupata uzima wa milele watakuwa wale ambao wamefua “panga zao ziwe majembe ya plau na mikuki yao iwe miundu” na ambao “hawatajifunza vita tena kamwe.” “Kwa maana kinywa cha Yehova wa majeshi kimesema hayo.”—Isa 2:4; Mik 4:3, 4.
JUNI 10-16
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 48-50
Hazina za Kiroho
it-2 805
Utajiri
Kwa kuwa taifa la Israeli lilikuwa na ufanisi, Waisraeli walifurahia kula na kunywa (1Fa 4:20; Mhu 5:18, 19), na utajiri wao uliwalinda dhidi ya matatizo yanayotokana na umaskini. (Met 10:15; Mhu 7:12) Hata hivyo, ingawa ilipatana na kusudi la Yehova kwamba Waisraeli wafurahie ufanisi kutokana na kazi yao ngumu (linganisha Met 6:6-11; 20:13; 24:33, 34), Yehova aliona pia kwamba inafaa waonywe kuhusu hatari ya kumsahau yeye akiwa ndiye Chanzo cha utajiri wao na badala yake waanze kuutegemea utajiri huo. (Kum 8:7-17; Zb 49:6-9; Met 11:4; 18:10, 11; Yer 9:23, 24) Walikumbushwa kwamba utajiri ni wa muda tu (Met 23:4, 5), usingeweza kutolewa kwa Mungu kuwa fidia ya kumkomboa yeyote kutokana na kifo (Zb 49:6, 7), na usingeweza kumnufaisha aliyekufa (Zb 49:16, 17; Mhu 5:15). Walionyeshwa kwamba kuupatia utajiri umuhimu kungeongoza kwenye matendo ya ulaghai na kuwafanya wakose kibali cha Yehova. (Met 28:20; linganisha Yer 5:26-28; 17:9-11.) Pia, walitiwa moyo “[wamheshimu] Yehova kwa vitu [vyao] vyenye thamani.”—Met 3:9.
JUNI 17-23
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 51-53
Hazina za Kiroho
it-1 644
Doegi
Mwedomu aliyetumikia akiwa mkuu wa wachungaji wa Mfalme Sauli, cheo muhimu cha usimamizi. (1Sa 21:7; 22:9) Inaonekana wazi kwamba Doegi alikuwa mgeuzwa-imani. Kwa kuwa alikuwa “amezuiliwa mbele za Yehova” huko Nobu, labda kwa sababu ya kiapo, ukosefu fulani wa usafi, au huenda alishukiwa ana ukoma fulani, Doegi alimwona Kuhani Mkuu Ahimeleki akimpa Daudi mikate ya wonyesho na upanga wa Goliathi. Baadaye, Sauli alipokuwa akizungumza na watumishi wake na kusema kwamba walikuwa wakipanga njama dhidi yake, Doegi alifunua mambo aliyokuwa amejionea huko Nobu. Baada ya kumwita kuhani mkuu pamoja na makuhani wengine wa Nobu na kumhoji Ahimeleki, Sauli aliagiza wakimbiaji wawaue makuhani wote. Wakimbiaji hao walipokataa kufanya hivyo, kwa agizo la Sauli, Doegi aliwaua makuhani 85 bila kusita. Baada ya tendo hilo la kikatili, Doegi alishambulia jiji lote la Nobu, akawaua wakaaji wake wote, vijana kwa wazee, pamoja na mifugo.—1Sa 22:6-20.
Kama inavyoonyeshwa katika maelezo ya utangulizi ya Zaburi ya 52, Daudi aliandika hivi kumhusu Doegi: “Ulimi wako, wenye makali kama wembe, hupanga madhara na kutunga mambo ya udanganyifu. Unapenda uovu kuliko mema, kusema uwongo kuliko kusema ukweli. Unapenda kila neno linalodhuru, ewe ulimi mdanganyifu!”—Zb 52:2-4.
JUNI 24-30
HAZINA ZA NENO LA MUNGU ZABURI 54-56
Hazina za Kiroho
it-1 857-858
Kujua Kimbele, Kuamua Kimbele
Mwendo wa usaliti wa Yuda Iskariote ulitimiza unabii uliotolewa na Mungu na kuonyesha kwamba Yehova na Mwana wake wana uwezo wa kujua mambo kimbele. (Zb 41:9; 55:12, 13; 109:8; Mdo 1:16-20) Hata hivyo, haiwezi kusemwa kwamba Mungu aliamua kimbele au kupanga mapema kwamba Yuda mwenyewe ndiye angetenda jambo hilo. Unabii ulitabiri kwamba Yesu angesalitiwa na mtu wake wa karibu, lakini haukutaja kihususa ni nani kati ya rafiki zake wa karibu ambaye angefanya hivyo. Kwa mara nyingine tena, kanuni za Biblia zinapinga kwamba Mungu aliamua kimbele matendo ya Yuda. Mtume anataja kiwango kilichowekwa na Mungu: “Usiharakishe kamwe kuweka mikono yako juu ya mwanamume yeyote; wala usishiriki dhambi za wengine; endelea kuwa safi.” (1Ti 5:22; linganisha 3:6.) Alipokuwa akichagua mitume wake 12, Yesu alitumia usiku mzima akisali na kumwomba Baba yake kabla ya kutangaza uamuzi wake. Jambo hilo linaloonyesha kwamba alihangaikia uchaguzi huo ufanywe kwa hekima na kwa njia inayofaa. (Lu 6:12-16) Ikiwa tayari Mungu alikuwa ameamua mapema kwamba Yuda atakuwa msaliti, hilo lingepingana na mwongozo na maagizo ya Mungu, na kupatana na sheria, hilo lingemfanya Mungu awe mshiriki katika dhambi za yule aliyetenda dhambi.
Hivyo, inaonekana wazi kwamba Yuda alipokuwa akichaguliwa kuwa mtume, moyo wake haukuonyesha kwamba alikuwa na mtazamo wa kuwa msaliti. Aliruhusu ‘mzizi wenye sumu uchipuke’ ambao ulimtia unajisi, na hilo likamfanya apotoke naye akakubali, si kuelekezwa na Mungu, bali akakubali kuongozwa na Ibilisi kuwa mwizi na msaliti. (Ebr 12:14, 15; Yoh 13:2; Mdo 1:24, 25; Yak 1:14, 15; ona YUDA Na. 4.) Yuda alipokuwa amepotoka kwa kiasi fulani, Yesu mwenyewe angeweza kusoma moyo wa Yuda na kutabiri kwamba angemsaliti.—Yoh 13:10, 11.