Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w21 Oktoba kur. 14-17
  • Kujenga Upya Urafiki Wako Pamoja na Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujenga Upya Urafiki Wako Pamoja na Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • UTAKABILI CHANGAMOTO GANI?
  • JIWEKEE MALENGO UNAYOWEZA KUYAFIKIA
  • USIFE MOYO!
  • Uangalizi Wenye Upendo Hujenga
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Iga Rehema Ya Mungu Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Yehova Anakuthamini!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Enyi Wazee wa Kutaniko—Endeleeni Kumwiga Mtume Paulo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
w21 Oktoba kur. 14-17
Ndugu anaonekana akiwa amelemewa anapofikiria muda na jitihada inayohitajika ili kujenga upya nyumba yake iliyoharibika.

Kujenga Upya Urafiki Wako Pamoja na Yehova

KILA mwaka, kondoo wengi wenye thamani wanarudishwa katika kutaniko la Kikristo. Wazia ‘shangwe kubwa inayokuwa mbinguni’ wakati kila mmoja anaporudi! (Luka 15:7, 10) Ikiwa umerudishwa kutanikoni, uwe na hakika kwamba Yesu, malaika, na Yehova mwenyewe wanafurahi kuona ukichukua tena msimamo upande wa kweli. Hata hivyo, unapojenga upya urafiki wako pamoja na Yehova, huenda ukakabili changamoto. Baadhi ya changamoto hizo ni zipi, na ni nini kinachoweza kukusaidia?

UTAKABILI CHANGAMOTO GANI?

Baada ya kurudi kutanikoni, ndugu na dada wengi wanapambana na hisia zisizofaa. Huenda unaelewa jinsi Mfalme Daudi alivyohisi. Hata baada ya kusamehewa dhambi zake, alisema hivi: “Makosa yangu . . .  yananilemea.” (Zab. 40:12; 65:3) Baada ya mtu kumrudia Yehova, huenda akahisi hatia au kuaibika kwa miaka mingi. Isabelle, alitengwa na ushirika kwa zaidi ya miaka 20.a Alisema hivi: “Ilikuwa vigumu sana kwangu kuamini kwamba Yehova anaweza kunisamehe.” Ikiwa utavunjika moyo, unaweza kudhoofika kiroho tena. (Met. 24:10) Jitahidi kutoruhusu jambo hilo litukie.

Wengine wanahofu kwamba hawatafaulu kufanya yote yanayohusika katika kurudisha uhusiano wao pamoja na Yehova. Antoine, alisema hivi baada ya kurudishwa: “Nilihisi kwamba nimesahau kila kitu kuhusu maisha yangu ya awali nikiwa Mkristo.” Kwa sababu ya hisia kama hizo, huenda baadhi ya watu wakasita kujihusisha kikamili katika utendaji wa kiroho.

Kwa mfano, mtu ambaye nyumba yake anayoipenda inapoharibiwa sana na kimbunga, huenda akahisi kulemewa anapofikiria nguvu na jitihada zinazohitajika ili kuijenga upya. Vivyo hivyo, ikiwa uhusiano wako pamoja na Yehova uliharibika kwa sababu ya dhambi nzito, huenda ukahisi kwamba jitihada kubwa sana inahitajika ili uwe tena na hali nzuri ya kiroho. Hata hivyo, msaada unapatikana.

Yehova anatoa mwaliko huu: “Sasa, njooni, na tunyooshe mambo kati yetu.” (Isa. 1:18) Tayari umefanya jitihada kubwa ili ‘kunyoosha mambo.’ Yehova anakupenda kwa kufanya jitihada hizo. Hebu wazia: Umempa Yehova msingi wa kujibu kwa uthabiti shutuma za Shetani!​—Met. 27:11.

Kwa kufanya hivyo, tayari umemkaribia zaidi Yehova, naye anaahidi kufanya vivyo hivyo. (Yak. 4:8) Hata hivyo, mengi zaidi yanahusika kuliko kutambuliwa tu na wengine kuwa wewe ni sehemu ya kutaniko tena. Unahitaji kuendelea kuimarisha upendo wako kwa Baba na Rafiki yako, Yehova. Unaweza kufanyaje hivyo?

JIWEKEE MALENGO UNAYOWEZA KUYAFIKIA

Jitahidi kujiwekea malengo unayoweza kufikia. Kumbuka kwamba msingi wako wa kiroho, yaani, ujuzi wako kumhusu Yehova na ahadi zake za wakati ujao, ulibaki kama ulivyo. Lakini jengo, yaani, maisha yako ya Kikristo, linahitaji kujengwa upya, na hilo linatia ndani kuhubiri habari njema na kushirikiana kwa ukawaida na ndugu na dada zako. Fikiria malengo yafuatayo.

Zungumza na Yehova kwa ukawaida. Baba yako anaelewa kwamba unapoendelea kuhisi hatia inaweza kuwa vigumu kwako kusali kwake. (Rom. 8:26) Hata hivyo, ‘dumu katika sala,’ ukimweleza Yehova ni kwa kadiri gani unataka kuwa rafiki yake. (Rom. 12:12) Andrej anakumbuka hivi: “Nilihisi hatia sana na kuaibika. Lakini baada ya kila sala niliyotoa, hisia hizo zilipungua. Nilipata utulivu mwingi zaidi wa akili.” Ikiwa hujui usali kuhusu nini, fikiria sala za Mfalme Daudi aliyetubu, zinazopatikana kwenye Zaburi ya 51 na 65.

Jifunze Biblia kwa ukawaida. Kufanya hivyo kutakuimarisha kiroho na kusaidia upendo wako kwa Yehova uongezeke. (Zab. 19:7-11) Felipe anasema hivi: “Kutokuwa na ratiba nzuri ya kiroho, ndiyo sababu iliyofanya nidhoofike na kumuumiza Yehova mara ya kwanza. Sikutaka kurudia kosa hilohilo mara ya pili, hivyo niliamua kulifanya funzo langu la kibinafsi liwe ulinzi wangu.” Wewe pia unaweza kufanya hivyo. Ikiwa unahitaji msaada ili uweze kupata habari zinazofaa kwa ajili ya funzo lako la kibinafsi, unaweza kumwomba rafiki yako aliye mkomavu kiroho akusaidie.

Jenga upya urafiki wako pamoja na ndugu na dada zako. Baadhi ya ndugu na dada wanaorudi kutanikoni wanahofu kwamba wengine watawaona kwa njia isiyofaa. Larissa anakiri hivi: “Niliaibika sana. Nilihisi kwamba nilikuwa nimelisaliti kutaniko. Na nilihisi hivyo kwa muda mrefu.” Uwe na hakika kwamba wazee wa kutaniko na ndugu na dada wengine wakomavu kiroho, wako tayari kukusaidia unapojenga upya hali yako ya kiroho. (Tazama sanduku “Wazee wa Kutaniko Wanaweza Kufanya Nini?”) Wanafurahi kwamba umerudi kutanikoni, na wanataka ufanye vizuri!​—Met. 17:17.

Ni nini kitakachokusaidia kulikaribia zaidi kutaniko? Shiriki kikamili katika mambo ambayo ndugu na dada wanafanya—hudhuria mikutano na kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani. Kufanya hivyo kutakusaidiaje? Felix alisema hivi: “Kutaniko lilikuwa linatazamia kwa hamu nirudi. Nilihisi ninathaminiwa. Wote walinisaidia kuwa sehemu ya familia tena, nihisi nimesamehewa, na kusonga mbele.”—Tazama sanduku “Wewe Unaweza Kufanya Nini?”

Wewe Unaweza Kufanya Nini?

Jenga upya hali yako ya kiroho kwa kuwa na ratiba nzuri ya kusali, kujifunza Biblia, na kushirikiana na ndugu na dada zako

Mzee wa kutaniko akisali pamoja na ndugu ambaye amemrudia Yehova.

ZUNGUMZA NA YEHOVA KWA UKAWAIDA

Mweleze Yehova ni kwa kadiri gani unataka kuwa rafiki yake. Wazee wa kutaniko watasali kwa ajili yako, na pamoja nawe

Mzee huyo akitumia kitabu “Mkaribie Yehova” kuongoza funzo la Biblia pamoja na ndugu huyo.

JIFUNZE BIBLIA KWA UKAWAIDA

Jilishe kiroho, kufanya hivyo kutakusaidia kukuza upendo wako kwa Yehova

Ndugu akizungumza pamoja na wengine kutoka kutanikoni wakiwa kwenye tafrija.

JENGA UPYA URAFIKI WAKO PAMOJA NA NDUGU NA DADA ZAKO

Shirikiana kikamili pamoja na kutaniko lako, mikutanoni na katika huduma

USIFE MOYO!

Shetani ataendelea kukuletea “vimbunga” ili kujaribu kukudhoofisha unapokuwa ukijenga upya urafiki wako pamoja na Yehova. (Luka 4:13) Jitayarishe kwa kuimarisha nyumba yako ya kiroho sasa.

Kuhusu kondoo wake, Yehova anaahidi hivi: “Aliyepotea nitamtafuta, anayetangatanga nitamrudisha, aliyejeruhiwa nitamfunga, na aliye dhaifu nitamtia nguvu.” (Eze. 34:16) Yehova amewasaidia wengine wengi warudishe tena uhusiano wao mzuri pamoja naye. Uwe na hakika kwamba anataka kukusaidia wewe pia uendelee kuimarisha hata zaidi uhusiano wako pamoja naye.

Wazee wa Kutaniko Wanaweza Kufanya Nini?

Mzee wa kutaniko akimsaidia ndugu kujenga upya nyumba yake iliyoharibika.

Wazee wa kutaniko wanatimiza jukumu muhimu la kuwasaidia wahubiri waliorudishwa wajenge upya uhusiano wao pamoja na Yehova. Ona mambo wanayoweza kufanya kwa ajili ya wale waliorudishwa.

Kuwahakikishia wanapendwa. Mtume Paulo alijua kwamba mtenda dhambi aliyetubu anaweza ‘kulemewa na huzuni inayopita kiasi.’ (2 Kor. 2:7) Huenda mara nyingi akahisi hatia na kuvunjika moyo. Paulo alilipa kutaniko shauri hili: ‘Wamsamehe kwa fadhili na kumfariji.’ Waliorudishwa wanahitaji kuhakikishiwa kwamba Yehova na waamini wenzao wanawapenda sana. Pongezi za kuendelea na msaada hususa huenda ukawasaidia wasivunjike moyo.

Kusali pamoja nao. “Dua ya mtu mwadilifu ina nguvu nyingi.” (Yak. 5:16) Larissa, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Niliwaambia wazee wa kutaniko kuhusu shaka na hofu zangu. Walisali kwa ajili yangu. Kisha, nikaelewa kwamba wazee hawakuwa wamenikasirikia. Walitaka kunisaidia nirudishe uhusiano wangu pamoja na Yehova.” Theo anasema hivi: “Sala za wazee zilinipa uhakika kwamba kwa kweli Yehova ananipenda na anaona mambo mazuri ndani yangu, na si tu mabaya.”

Kuwa rafiki zao. Wale waliorudishwa wanahitaji marafiki kutanikoni. Mzee wa kutaniko anayeitwa Justin, anasema hivi: “Tumia kila fursa kuwaalika ili ushirikiane nao katika huduma, na jambo muhimu zaidi, watembelee nyumbani kwao. Ni muhimu sana kuwa rafiki yao!” Henry, mzee mwingine wa kutaniko, anasema hivi: “Ikiwa wengine kutanikoni wanaona wazee wakifanya urafiki na watu waliorudishwa, wao pia watajitahidi kufanya hivyo.”

Kuwasaidia wajifunze kibinafsi. Rafiki mkomavu anaweza kumsaidia mtu aliyerudishwa awe na ratiba nzuri ya kujifunza. Mzee anayeitwa Darko, anasema hivi: “Ninapenda kushiriki nao hazina za kiroho ambazo nimepata katika funzo langu la kibinafsi, na kuwaonyesha jinsi ninavyofurahia kujifunza Biblia. Pia, ninafanya nao mipango ili tujifunze pamoja habari fulani.” Mzee mwingine wa kutaniko anayeitwa Clayton, anasema hivi: “Ninawatia moyo watafute masimulizi ya Biblia yanayofanana na hali walizopitia.”

Kuwachunga. Wale waliorudishwa wamewaona wazee katika jukumu lao la kuhukumu. Sasa, kuliko wakati mwingine wowote, wanahitaji kuwaona wakiwa wachungaji. (Yer. 23:4) Iweni wepesi kuwasikiliza na tayari kuwapongeza. Wasilianeni nao kwa ukawaida. Ona kile ambacho mzee wa kutaniko anayeitwa Marcus, anafanya anapokuwa kwenye ziara za uchungaji: “Tunazungumzia wazo la Kimaandiko, kuwapongeza, na kuwahakikishia kwamba tunawaonea fahari kwa kujitahidi sana ili kurudi kutanikoni na kwamba Yehova anahisi hivyo pia. Mwishoni mwa kila ziara, tunapanga siku ya ziara inayofuata.”

a Majina katika makala hii yamebadilishwa.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki