Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w23 Februari kur. 26-30
  • Nimewaona Waaminifu Wakisitawi

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Nimewaona Waaminifu Wakisitawi
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • IRELAND KASKAZINI—“NCHI YA MABOMU NA RISASI”
  • SIERRA LEONE—IMANI LICHA YA UMASKINI
  • NIGERIA—KUJIFUNZA TAMADUNI MPYA
  • KENYA—AKINA NDUGU WALINIONYESHA SUBIRA
  • MAREKANI—IMANI LICHA YA UFANISI
  • Yehova Amenisaidia
    2014 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehovah
  • Niliinuliwa Kutoka Ardhini Nikakwezwa Kwa Njia Ambayo Sikutazamia
    Masimulizi ya Maisha ya Mashahidi wa Yehova
  • Wapiga Mbiu ya Ufalme Waripoti
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1990
  • “Wale Wanaokusikiliza” Wataokolewa
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
w23 Februari kur. 26-30
Robert Landis.

SIMULIZI LA MAISHA

Nimewaona Waaminifu Wakisitawi

LIMESIMULIWA NA ROBERT LANDIS

HUENDA ukakumbuka mazungumzo uliyofanya na wengine ambayo yalikuwa muhimu sana kwako. Nilikuwa na mazungumzo kama hayo miaka 50 hivi iliyopita nikiwa pamoja na rafiki yangu tukiota moto nchini Kenya. Ngozi zetu zikiwa zimebadilika rangi na kuwa ngumu kwa sababu ya jua na miezi mingi ya kusafiri, tulikuwa tumeketi tukizungumzia sinema ambayo inahusu mambo ya kidini, rafiki yangu aliposema, “Haikuwakilisha Biblia vizuri.”

Nilicheka—kwa sababu sikufikiri kwamba rafiki yangu alikuwa mtu wa kidini. Nilimuuliza, “Unajua nini kuhusu Biblia?” Hakunijibu mara moja. Mwishowe, aliniambia mama yake alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova; alikuwa amejifunza baadhi ya mambo kutoka kwake. Nikiwa na udadisi, nilimwomba anieleze mengi zaidi.

Mazungumzo yetu yaliendelea hadi usiku wa manane. Rafiki yangu aliniambia kwamba Biblia inamtambulisha Shetani kuwa mtawala wa ulimwengu huu. (Yoh. 14:30) Huenda wewe umelijua jambo hilo maisha yako yote, lakini kwangu, jambo hilo lilikuwa jipya na lenye kusisimua. Sikuzote nilikuwa nikisikia kwamba Mungu mwenye fadhili na haki alikuwa akitawala ulimwengu huu. Lakini jambo hilo halikupatana na mambo niliyojionea maishani. Ingawa nilikuwa na umri wa miaka 26 tu, nilikuwa nimejionea mambo mengi yaliyonihangaisha.

Baba yangu alikuwa rubani kwenye Jeshi la Anga la Marekani. Hivyo, nilipokuwa kijana, wazo la kwamba vita vya kinyuklia vingeweza kutokea lilikuwa halisi kwangu; jeshi lilikuwa tayari kuangusha bomu la kinyuklia wakati wowote. Vita nchini Vietnam vilipiganwa nilipokuwa chuo kikuu huko Carlifornia. Nilijiunga kwenye maandamano ya wanafunzi. Polisi walitukimbiza wakiwa na marungu, na tulikimbia tukiwa hatuwezi kuona na kupumua vizuri kwa sababu ya mabomu ya machozi. Kilikuwa kipindi cha misukosuko na uasi. Kulikuwa na mauaji ya kisiasa, maandamano, na vurugu. Kila mtu alikuwa na maoni tofauti kuhusu ni nini kilichopaswa kufanywa. Hayo yote yalinichanganya sana.

Robert akiwa amesimama kando ya pikipiki yake anaonyesha kwenye ramani safari zake.

Kutoka London hadi Afrika ya Kati

Mwaka wa 1970, nilianza kufanya kazi kwenye pwani ya kaskazini ya Alaska na nilipata pesa nyingi sana. Kisha nilipanda ndege na kwenda London, nikanunua pikipiki, na nikaiendesha kuelekea kusini nikiwa sina mahali hususa ninapokwenda. Baada ya miezi kadhaa, nilifika barani Afrika. Nikiwa njiani, nilikutana na watu ambao walitamani ikiwa wangeweza kuondoka—kujiweka huru na kukimbia matatizo yao yote.

Hivyo, kwa sababu ya mambo niliyokuwa nimejionea na kusikia, kwangu, fundisho la Biblia kwamba kuna kiumbe wa roho aliye mwovu ambaye anaongoza mambo duniani lilipatana na akili. Lakini Mungu alihusikaje katika hayo? Nilitaka kujua.

Katika miezi iliyofuata, nilipata jibu. Na baada ya muda, mimi pia nilikuja kuwafahamu na kuwapenda wanaume na wanawake wengi ambao chini ya hali zote, walithibitika kuwa waaminifu kwa Mungu pekee wa kweli.

IRELAND KASKAZINI—“NCHI YA MABOMU NA RISASI”

Wakati niliporudi London, niliwasiliana na mama ya rafiki yangu, na alinipatia Biblia. Baadaye, nilipoenda Amsterdam, nchini Uholanzi, Shahidi mmoja aliniona nikisoma Biblia chini ya taa ya barabarani, naye akanisaidia kujifunza mengi zaidi. Kisha, nikaenda jijini Dublin, Ireland, na nikaipata ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Nikabisha hodi. Hapo ndipo nilipokutana na Arthur Matthews, ndugu mwenye hekima na uzoefu. Nilimwomba anifundishe Biblia, naye akakubali kujifunza nami.

Nilizama katika funzo langu, nikisoma kwa bidii sana vitabu na mabuku yaliyochapishwa na Mashahidi. Na bila shaka, nilisoma pia Biblia. Ilisisimua sana! Katika mikutano ya kutaniko, niliona kwamba hata watoto walijua majibu ya maswali haya ambayo wasomi walikuwa wametafakari kwa karne nyingi: ‘Kwa nini kuna uovu? Mungu ni nani? Ni nini hutendeka mtu anapokufa?’ Nilishirikiana tu na Mashahidi wa Yehova. Hilo lilikuwa rahisi kwa sababu sikumfahamu mtu yeyote mwingine katika nchi nzima. Walinisaidia nimpende Yehova na kutaka kufanya mapenzi yake.

Nigel, Denis, na mimi

Nilibatizwa mwaka wa 1972. Baada ya mwaka mmoja, nikaanza upainia na nikajiunga na kutaniko dogo huko Newry, Ireland Kaskazini. Nilihamia kwenye nyumba ya kupangisha ya mawe iliyo peke yake mlimani. Kulikuwa na ng’ombe kwenye eneo la malisho kando ya nyumba yangu, na nilifanya mazoezi ya kutoa hotuba zangu mbele yao. Walionekana kana kwamba wanasikiliza kwa makini huku wakitafuna nyasi. Hawakunipatia shauri lolote, lakini walinisaidia nijizoeze kuwatazama wasikilizaji. Mwaka wa 1974, niliwekwa rasmi kutumikia nikiwa painia wa pekee, na Nigel Pitt ambaye alikuja kuwa rafiki yangu wa karibu maishani, alijiunga nami.

Kile kipindi cha “Mapigano” cha Ireland Kaskazini kilianza wakati huohuo. Kwa kufaa, baadhi ya watu waliita Ireland Kaskazini, “nchi ya mabomu na risasi.” Mapigano ya barabarani, mashambulizi ya wapiga risasi walio mafichoni, magari kulipuliwa na mabomu, na watu kufyatuliana risasi yalikuwa mambo ya kawaida. Mambo ya kisiasa na kidini yaliingiliana. Hata hivyo, Waprotestanti na Wakatoliki walitambua kwamba Mashahidi hawakuunga mkono upande wowote katika siasa, hivyo tuliweza kuhubiri kwa uhuru na kwa usalama. Mara nyingi wenye nyumba walijua vurugu zingetokea wakati na mahali gani, na wangetuonya ili tuweze kuepuka hatari.

Hata hivyo, bado kulikuwa na hali za hatari. Siku moja, mimi na Denis Carrigan, ambaye pia alikuwa painia, tulikuwa tukihubiri katika mji jirani ambako hakukuwa na Mashahidi na kabla ya hapo tulikuwa tumetembelea mara moja tu mji huo. Mwanamke mmoja alitushutumu kwamba tulikuwa majasusi wa jeshi la Uingereza, huenda kwa sababu tulikuwa hatuzungumzi na lafudhi ya Ireland. Shutuma hiyo ilituogopesha sana. Ikiwa ungeonekana kuwa mwenye urafiki na wanajeshi ungeweza kuuawa au kupigwa risasi kwenye goti. Tukiwa tumesimama nje, peke yetu kwenye baridi, na tukisubiri basi, tuliona gari likisimama kwenye mkahawa ambako yule mwanamke alikuwa ametushutumu. Alitoka nje na akazungumza na wanaume wawili waliokuwa kwenye gari hilo, huku akitunyooshea kidole akiwa amesisimka. Kisha wanaume hao waliendesha gari polepole hadi kufikia mahali tulipokuwa, na wakatuuliza maswali machache kuhusu ratiba ya basi. Basi lilipowasili walizungumza na dereva. Hatukusikia kile walichokuwa wakizungumza. Hakukuwa na abiria wengine, hivyo tulikuwa na uhakika kwamba mipango ilikuwa ikifanywa ili watudhuru tukifika nje ya mji. Lakini hilo halikutokea. Nilipokuwa nikishuka nilimuuliza dereva hivi: “Je, wale wanaume walikuwa wakituulizia?” Alijibu hivi: “Ninawajua nyinyi, na niliwajulisha hilo. Msiwe na wasiwasi. Mko salama.”

Robert na Pauline kwenye siku yao ya harusi.

Siku yetu ya harusi, Machi  1977

Mwaka wa 1976, katika kusanyiko la wilayaa jijini Dublin, nilikutana na Pauline Lomax, painia wa pekee kutoka Uingereza. Alikuwa dada wa kiroho, mnyenyekevu, na mwenye utu mzuri. Yeye na Ray, ndugu yake, walikuwa wamelelewa katika kweli. Mwaka mmoja baadaye, mimi na Pauline tulifunga ndoa na tukaendelea kutumikia tukiwa mapainia wa pekee huko Ballymena, Ireland Kaskazini.

Tulifanya kazi ya mzunguko kwa kipindi fulani, tukiwatumikia ndugu zetu huko Belfast, Londonderry, na sehemu nyingine hatari. Tuliguswa moyo na imani ya ndugu na dada zetu ambao waliacha imani za kidini zilizokita mizizi, ubaguzi, na chuki ili kumtumikia Yehova. Yehova aliwabariki sana na kuwalinda!

Nilikuwa nimeishi Ireland kwa kipindi cha miaka kumi. Kisha mwaka wa 1981, tulialikwa kuhudhuria darasa la 72 la Shule ya Gileadi. Baada ya kuhitimu, tulipewa mgawo nchini Sierra Leone, Afrika Magharibi.

SIERRA LEONE—IMANI LICHA YA UMASKINI

Tuliishi katika nyumba ya wamishonari pamoja na watu 11 wazuri sana. Tulitumia jiko moja, vyoo vitatu, bafu mbili, mashine moja ya kufua nguo, na moja ya kukausha nguo. Umeme ulikatika mara kwa mara na bila kutarajia. Kulikuwa na panya kwenye paa, na nyoka aina ya swila waliingia kwenye chumba cha chini ya ardhi.

Robert na wengine wakiwa na pikipiki zao, wanavuka mto kwenye chelezo cha magogo.

Nikivuka mto ili kuhudhuria kusanyiko kwenye nchi jirani ya Guinea

Ingawa tuliishi katika mazingira ambayo hayakuwa rahisi, tulifurahia sana huduma. Watu waliiheshimu Biblia na walisikiliza kwa makini. Wengi walijifunza na kukubali kweli. Wenyeji waliniita “Bwana Robert.” Pauline walimwita “Bibi Robert.” Hata hivyo, baadaye nilipokuwa nikitumia muda mwingi zaidi katika kazi kwenye ofisi ya tawi na muda mchache zaidi katika utumishi wa shambani, watu walianza kumwita Pauline “Bibi Pauline.” Mimi nikawa “Bwana Pauline.” Jambo hilo lilimfurahisha Pauline!

Robert na Pauline wakiwa na gari lao.

Tukienda kuhubiri kwenye eneo fulani nchini Sierra Leone

Akina ndugu wengi walikuwa maskini, lakini sikuzote Yehova aliwaandalia mahitaji yao, nyakati nyingine hata katika njia zenye kustaajabisha. (Mt. 6:33) Nakumbuka dada mmoja alikuwa na pesa za kutosha kununua chakula cha siku hiyo tu kwa ajili yake na watoto wake, lakini alimpa pesa hizo zote ndugu mgonjwa ambaye hakuwa na pesa za kununua dawa za malaria. Baadaye siku hiyo, mwanamke fulani alienda kwa dada yetu bila kutarajiwa na akamlipa ili amtengeneze nywele. Hali nyingi kama hizo zilitukia.

NIGERIA—KUJIFUNZA TAMADUNI MPYA

Tulikuwa nchini Sierra Leone kwa miaka tisa. Kisha tukahamishiwa kwenye Betheli ya Nigeria. Sasa tulikuwa katika ofisi ya tawi kubwa. Bado nilikuwa ninafanya kazi ileile ya ofisini ambayo nilikuwa nikifanya Sierra Leone, lakini kwa Pauline, lilikuwa badiliko kubwa na gumu. Awali alikuwa anatumia saa 130 kwa mwezi katika huduma, na alikuwa na wanafunzi wa Biblia wenye maendeleo. Sasa alipewa mgawo kwenye chumba cha kushonea, ambako alitumia muda mwingi kurekebisha nguo. Ilichukua muda kuzoea mgawo huo, lakini alikuja kutambua kwamba wengine walithamini sana kazi ambayo alikuwa anafanya, na pia alikazia fikira zaidi kutafuta fursa za kuwatia moyo Wanabetheli wenzake.

Utamaduni wa watu nchini Nigeria ulikuwa mpya kwetu, hivyo tulikuwa na mengi ya kujifunza. Pindi moja, ndugu alikuja kwenye ofisi yangu ili kumtambulisha dada ambaye alikuwa ametoka tu kualikwa Betheli. Niliponyoosha mkono wangu kumsalimu, aliinama miguuni pangu. Nilishtuka! Mara moja nikakumbuka maandiko haya mawili: Matendo 10:25, 26 na Ufunuo 19:10. Nilijiuliza, ‘Je, ninapaswa kumwambia asifanye hivyo?’ Lakini nilitambua kwamba alikuwa amealikwa Betheli; alijua kile ambacho Biblia inafundisha.

Sikujihisi huru mazungumzo hayo yalipokuwa yakiendelea. Kisha baadaye nikafanya utafiti. Nilijifunza kwamba dada huyo alikuwa akitenda kulingana na utamaduni ambao wakati huo bado ulifuatwa katika sehemu fulani za nchi. Wanaume pia walifuata utamaduni huo. Ilikuwa njia ya kuonyesha heshima. Halikuwa tendo la ibada; kuna mifano kama hiyo katika Biblia. (1 Sam. 24:8) Ninashukuru kwamba sikusema lolote ambalo lingeweza kumwaibisha dada yangu.

Tulikutana na watu wengi nchini Nigeria ambao walionyesha imani ya pekee kwa miaka mingi. Mfikirie Isaiah Adagbona.b Alijifunza kweli akiwa kijana, lakini kisha akagunduliwa kuwa ana ugonjwa wa ukoma. Alipelekwa kwenye kambi ya watu wenye ukoma ambako ni yeye peke yake aliyekuwa Shahidi. Licha ya upinzani, aliwasaidia watu zaidi ya 30 wenye ukoma wakubali kweli na alianzisha kutaniko katika kambi hiyo.

KENYA—AKINA NDUGU WALINIONYESHA SUBIRA

Nikiwa na kifaru yatima nchini Kenya

Mwaka wa 1996, tulipewa mgawo mpya kwenye ofisi ya tawi ya Kenya. Hii ilikuwa mara yangu ya kwanza kurudi nchini humo tangu kipindi kile kilichotajwa kwenye utangulizi. Tuliishi Betheli. Na miongoni mwa wale waliotutembelea ni tumbili. “Waliwapora” akina dada matunda waliyobeba. Siku moja, dada hapo Betheli aliacha dirisha lake wazi. Aliporudi chumbani, aliikuta familia ya tumbili wakifurahia chakula kilichokuwa chumbani kwake. Alipiga kelele na kutoka haraka chumbani. Tumbili walishtuka na wakaruka nje ya dirisha.

Mimi na Pauline tulijiunga na kutaniko la Kiswahili. Baada ya muda mfupi, nilipewa mgawo wa kuongoza Funzo la Kitabu la Kutaniko (sasa linaitwa Funzo la Biblia la Kutaniko). Hata hivyo, ujuzi wangu wa lugha hiyo ulikuwa kama wa mtoto mdogo sana. Ningejifunza habari mapema, hivyo niliweza kusoma maswali. Lakini ikiwa maelezo kutoka kwa ndugu na dada yangetofautiana hata kidogo na kilichoandikwa, sikuyaelewa. Hali hiyo haikuwa rahisi! Niliwahurumia akina ndugu na dada. Nilitiwa moyo kwamba kwa subira na unyenyekevu waliniruhusu niongoze mkutano huo.

MAREKANI—IMANI LICHA YA UFANISI

Tulikuwa nchini Kenya chini ya mwaka mmoja. Kisha mwaka wa 1997, tulialikwa kwenye Betheli ya Brooklyn, New York. Sasa, tulikuwa katika nchi ambayo ilikuwa na ufanisi wa kimwili na hilo lingeweza kuleta matatizo. (Met. 30:8, 9) Lakini hata katika nchi kama hiyo kuna ufanisi mkubwa wa kiroho. Ndugu zetu wanatumia muda na mali zao, si kujitajirisha, bali kuunga mkono kazi nzuri inayofanywa na tengenezo la Yehova.

Kwa miaka mingi, tumejionea imani ya Mashahidi wenzetu katika hali mbalimbali. Nchini Ireland, imani licha ya misukosuko ya kijamii. Barani Afrika, imani licha ya umaskini na kuwa mbali na wengine. Nchini Marekani, imani licha ya ufanisi. Kwa hakika, Yehova anafurahi sana anapotazama chini na kuona watu wanaoonyesha kwamba wanampenda katika kila aina ya hali!

Nikiwa na Pauline katika Betheli ya Warwick

Miaka imesonga upesi sana—“kuliko gurudumu la mfumaji.” (Ayu. 7:6) Sasa tunafanya kazi pamoja na wengine katika makao makuu ya ulimwenguni pote huko Warwick, New York, na tuna shangwe ya kuendelea kutumikia pamoja na watu wanaopendana kikweli. Tuna furaha, tumeridhika, na tunahisi shangwe kwa kufanya yale tunayoweza ili kumuunga mkono Mfalme wetu, Kristo Yesu, ambaye hivi karibuni atawathawabisha wote walio waaminifu kwake.​—Mt. 25:34.

a Wakati huo, makusanyiko ya eneo yaliitwa makusanyiko la wilaya.

b Simulizi la maisha ya Isaiah Adagbona linapatikana katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 1998, uku. 22-27. Alikufa mwaka wa 2010.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki