Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Julai kur. 20-25
  • Je, ‘Umejifunza Siri’ ya Kuridhika?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je, ‘Umejifunza Siri’ ya Kuridhika?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • SITAWISHA MTAZAMO WENYE SHUKRANI
  • KAZIA FIKIRA MAMBO MUHIMU NA ENDELEA KUWA MNYENYEKEVU
  • TAFAKARI KUHUSU TUMAINI LAKO
  • “WALE WANAOMWOGOPA HAWAKOSI CHOCHOTE”
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Kumbuka Kwamba Yehova Ndiye “Mungu Aliye Hai”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Maamuzi Yanayoonyesha Unamtegemea Yehova
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
  • Je, Unaweza Kuitambua Kweli?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Julai kur. 20-25

MAKALA YA 31

WIMBO 111 Sababu za Kuwa na Shangwe

Je, ‘Umejifunza Siri’ ya Kuridhika?

“Hata hali zangu ziweje nimejifunza kuridhika.”—FLP. 4:11.

JAMBO KUU

Kujifunza kuridhika kwa kusitawisha mtazamo wenye shukrani, kukazia fikira mambo muhimu, kuwa mnyenyekevu, na kutafakari kuhusu tumaini letu la wakati ujao.

1. Kuwa mwenye kuridhika kunamaanisha nini, na hakumaanishi nini?

JE, WEWE una mtazamo wa kuridhika? Mtu aliyeridhika anapata shangwe na amani kwa kukazia fikira baraka alizo nazo sasa. Hahisi uchungu au hasira kwa sababu ya vitu ambavyo hana. Hata hivyo, kuwa mwenye kuridhika hakumaanishi kwamba tuna mtazamo wa kutojali. Kwa mfano, Mkristo hutafuta pia nafasi za kupanua utumishi wake. (Rom. 12:1; 1 Tim. 3:1) Hata hivyo, hapotezi shangwe yake ikiwa mapendeleo ya utumishi hayaji haraka kama alivyotarajia.

2. Kwa nini kutoridhika ni hatari sana?

2 Kutoridhika kunaweza kuwa na matokeo mabaya sana. Wale ambao hawaridhiki na vitu walivyo navyo, huenda wakafanya kazi kwa saa nyingi sana ili kupata vitu vya kimwili ambavyo kwa kweli hawavihitaji. Kwa kusikitisha, Wakristo wachache hata wameiba pesa na vitu vingine walivyotamani. Huenda walijiambia hivi: ‘Ninastahili vitu hivi,’ ‘Nimechoka kusubiri,’ au ‘Nitalipa pesa hizo baadaye.’ Hata hivyo, wizi wa aina yoyote unamchukiza na kumwaibisha Yehova. (Met. 30:9) Wengine wamevunjika moyo sana kwa sababu ya kutopata pendeleo fulani la utumishi hivi kwamba wameamua kuacha kumtumikia Yehova. (Gal. 6:9) Inawezekanaje kwa mwabudu wa Yehova kufikia uamuzi kama huo? Huenda tatizo ni kwamba mtu huyo ameacha kusitawisha sifa ya kuridhika.

3. Tunajifunza kweli gani inayotutia moyo kwenye Wafilipi 4:​11, 12?

3 Sisi sote tunaweza kusitawisha mtazamo wa kuridhika. Mtume Paulo aliandika kwamba ‘hata hali zake ziweje alijifunza kuridhika.’ (Soma Wafilipi 4:​11, 12.) Aliandika maneno hayo alipokuwa kifungoni. Hata hivyo, hakuwa amepoteza shangwe yake. Alikuwa ‘amejifunza siri’ ya kuridhika. Ikiwa ni vigumu kwetu kuwa wenye kuridhika, maneno ya Paulo na mambo aliyopitia maishani yanaweza kutuhakikishia kwamba tunaweza kusitawisha sifa ya kuridhika. Hatupaswi kutarajia kwamba kiasili tutaridhika na hali zetu kwa urahisi. Badala yake, ni lazima tujifunze kuridhika. Jinsi gani? Acheni tuchunguze sifa zitakazotusaidia kujifunza siri ya kuridhika.

SITAWISHA MTAZAMO WENYE SHUKRANI

4. Kuwa na mtazamo wenye shukrani kunatusaidiaje kuridhika? (1 Wathesalonike 5:18)

4 Kuwa wenye shukrani kunatusaidia kuwa na mtazamo wa kuridhika. (Soma 1 Wathesalonike 5:18.) Kwa mfano, ikiwa kwa kweli tunashukuru kwamba tuna mahitaji yetu ya lazima, kuna uwezekano mkubwa kwamba hatutafikiria kupita kiasi kuhusu vitu ambavyo tunavitaka lakini hatuna. Tunapotafakari kwa uthamini kuhusu mapendeleo ya utumishi tunayofurahia sasa, tutakazia fikira kufanya yote tuwezayo katika migawo hiyo, badala ya kufikiria kupita kiasi jinsi ya kupata pendeleo tofauti tunalotaka. Haishangazi kwamba Maandiko yanatusihi tutie ndani maneno ya shukrani katika sala zetu kwa Yehova! Kuwa na mtazamo wenye shukrani kunatusaidia kuhisi “amani ya Mungu inayozidi uelewaji wote.”—Flp. 4:​6, 7.

5. Kwa nini Waisraeli walipaswa kuwa wenye shukrani? (Tazama pia picha.)

5 Fikiria kilichowapata Waisraeli. Katika pindi kadhaa, walimlalamikia Yehova kwamba walikosa chakula walichokuwa wakifurahia walipokuwa Misri. (Hes. 11:​4-6) Ni kweli kwamba haikuwa rahisi kuishi nyikani. Ni jambo gani ambalo lingeweza kuwasaidia kuwa na mtazamo wa kuridhika? Walipaswa kutafakari kuhusu mambo yote ambayo tayari Yehova alikuwa amewafanyia na kuonyesha shukrani. Walipaswa kukumbuka kwamba walipokuwa watumwa Misri na kutendewa kwa ukatili, Yehova alileta yale mapigo kumi na kuwakomboa. Baada ya Waisraeli kuwekwa huru, ‘walichukua mali za Wamisri’ zilizotia ndani fedha, dhahabu, na mavazi. (Kut. 12:​35, 36) Waisraeli walipojikuta kati ya jeshi la Farao na Bahari Nyekundu, Yehova aliyagawanya maji kimuujiza. Na walipokuwa wakisafiri nyikani, aliwalisha mana kila siku. Basi, tatizo lilikuwa nini? Waisraeli hawakuridhika, si kwa sababu walikosa chakula walichohitaji, bali kwa sababu hawakuwa na shukrani kuelekea vitu ambavyo tayari walikuwa navyo.

Baadhi ya Waisraeli wakimlalamikia Musa kuhusu mana waliyokusanya huku wengine walio karibu wakiwatazama na kuendelea kukusanya mana.

Kwa nini Waisraeli walikosa kuridhika? (Tazama fungu la 5)


6. Taja baadhi ya njia tunazoweza kusitawisha mtazamo wa kuonyesha shukrani.

6 Hivyo, unawezaje kusitawisha mtazamo wa kuonyesha shukrani? Kwanza, tenga wakati kila siku na utafakari kuhusu mambo mazuri unayofurahia maishani. Hata unaweza kuandika mambo mawili au matatu ambayo unashukuru kuwa nayo. (Omb. 3:​22, 23) Pili, waeleze wengine kwamba unashukuru. Chukua hatua ya kwanza kuwashukuru wengine kwa mambo wanayokufanyia. Zaidi ya yote, mshukuru Yehova kwa ukawaida. (Zab. 75:1) Tatu, chagua marafiki wa karibu ambao wana mtazamo wa kuonyesha shukrani. Marafiki wetu wanaweza kutuambukiza mtazamo wa kuonyesha shukrani au mtazamo wa kutoridhika. (Kum. 1:​26-28; 2 Tim. 3:​1, 2, 5) Tunapokazia fikira kuonyesha shukrani, tutakuwa na uwezekano mdogo zaidi wa kulemewa na hisia za kutoridhika.

7. Aci alisitawishaje mtazamo wa kuonyesha shukrani, na matokeo yalikuwaje?

7 Fikiria kisa cha Aci, anayeishi nchini Indonesia. Anakiri hivi: “Wakati wa janga la COVID-19 nilianza kulinganisha hali zangu na za waamini wenzangu. Kufanya hivyo kulisababisha nikose kuridhika.” (Gal. 6:4) Ni jambo gani lililomsaidia abadili mtazamo wake? Aci anasema hivi: “Nilianza kuhesabu baraka nilizopokea kila siku na kutafakari kuhusu mambo mengi mazuri niliyopata kwa sababu ya kuwa na sehemu katika tengenezo la Mungu. Kisha nikamshukuru Yehova kwa mambo yote aliyonipatia. Kufanya hivyo kulinisaidia kuridhika kikweli.” Ikiwa unalemewa na maoni yasiyofaa kuhusu hali yako, je, unaweza kuchukua hatua hizo ili kuwa mwenye shukrani tena?

KAZIA FIKIRA MAMBO MUHIMU NA ENDELEA KUWA MNYENYEKEVU

8. Baruku alinaswa na mtego gani?

8 Baruku, mwandishi wa nabii Yeremia, alinaswa na mtego fulani kwa muda mfupi. Baruku alikuwa na mgawo mgumu wa kumsaidia Yeremia alipokuwa akitangaza ujumbe mzito kwa taifa lililokosa shukrani. Pindi moja, Baruku alikosa kukazia fikira mambo muhimu. Badala ya kukazia fikira mambo ambayo Yehova alitaka afanye, inaonekana kwamba alianza kukazia fikira kupita kiasi mambo ambayo yeye alitaka kufanya. Kupitia Yeremia, Yehova alimwambia hivi Baruku: “Unajitafutia mambo makuu. Acha kuyatafuta mambo hayo.” (Yer. 45:​3-5) Kwa maneno mengine alikuwa akisema hivi: “Ridhika na hali ulizo nazo sasa.” Baruku alikubali shauri hilo na akaendelea kufurahia kibali cha Yehova.

9. Kulingana na 1 Wakorintho 4:​6, 7, sifa ya unyenyekevu inatusaidia kutambua nini? (Tazama pia picha.)

9 Pindi fulani, huenda Mkristo akahisi kwamba anastahili pendeleo fulani la utumishi. Labda ana kipawa fulani, anafanya kazi kwa bidii, au ana uzoefu fulani—au huenda ana sifa hizo zote tatu. Hata hivyo, huenda wengine wakapewa pendeleo lilelile ambalo yeye angependa kupata. Ni jambo gani linaloweza kumsaidia katika hali hiyo? Anaweza kutafakari maneno ya mtume Paulo yanayopatikana katika 1 Wakorintho 4:​6, 7. (Soma.) Kila pendeleo tunalopata na kila kipawa tulicho nacho kinatoka kwa Yehova. Hatupatii zawadi hizo kwa sababu sisi ni wa pekee zaidi kuliko watu wengine. Zawadi hizo zote ni wonyesho wa fadhili zisizostahiliwa za Yehova.—Rom. 12:​3, 6; Efe. 2:​8, 9.

Mkusanyo wa picha: Ndugu na dada walio na mapendeleo ya utumishi. 1. Ndugu akipima mabomba yaliyo kwenye jengo la kitheokrasi. 2. Dada akihojiwa na ndugu katika kusanyiko la mzunguko la lugha ya ishara. 3. Ndugu akitoa hotuba katika mkutano wa kutaniko.

Zawadi yoyote tuliyo nayo ni wonyesho wa fadhili zisizostahiliwa za Yehova (Tazama fungu la 9)b


10. Tunawezaje kusitawisha unyenyekevu?

10 Tunaweza kusitawisha unyenyekevu kwa kufikiria kwa makini kuhusu mfano ambao Yesu alituwekea. Fikiria kile kilichotokea usiku ambao Yesu aliwaosha miguu mitume wake. Mtume Yohana aliandika hivi: “Yesu akijua [1] kwamba Baba alikuwa ameviweka vitu vyote mikononi mwake na [2] kwamba alikuja kutoka kwa Mungu na [3] alikuwa akienda kwa Mungu, . . . akaanza kuiosha miguu ya wanafunzi.” (Yoh. 13:​3-5) Yesu angeweza kuhisi kwamba mitume wake walipaswa kuosha miguu yake. Lakini alipokuwa duniani, hakuhisi kamwe kwamba anastahili maisha yenye ufanisi na yenye kustarehesha. (Luka 9:58) Yesu alikuwa mnyenyekevu na mwenye kuridhika. Alituwekea kielelezo kikamilifu.—Yoh. 13:15.

11. Sifa ya unyenyekevu imemsaidiaje Dennis kuridhika?

11 Dennis, kutoka nchini Uholanzi, amejitahidi kufuata kielelezo cha Yesu cha unyenyekevu, lakini haijawa rahisi kwake kufanya hivyo. Anasema hivi: “Nyakati nyingine ninagundua kwamba ninaanza kuwa na hisia za kiburi au kutoridhika, wakati mtu mwingine anapopewa pendeleo la utumishi. Hali hiyo inapotokea, mimi hujifunza kuhusu sifa ya unyenyekevu. Katika programu ya JW Library®, nimehifadhi maandiko yanayozungumzia sifa ya unyenyekevu ili niweze kuyapata kwa urahisi na kuyasoma tena. Pia, nimepakua kwenye simu yangu hotuba kadhaa kuhusu unyenyekevu, na ninazisikiliza mara kwa mara.a Nimejifunza kwamba kazi zote tunazofanya ni ili tumtukuze Yehova, si kujitukuza wenyewe. Kila mmoja wetu anatimiza sehemu ndogo katika kazi ambayo Yehova anafanikisha.” Ukianza kuwa na hisia za kutoridhika na hali yako, chukua hatua ili kusitawisha sifa ya unyenyekevu. Hilo litaimarisha urafiki wako na Yehova na kukusaidia uridhike.—Yak. 4:​6, 8.

TAFAKARI KUHUSU TUMAINI LAKO

12. Ni tumaini gani la wakati ujao linalotusaidia kuridhika? (Isaya 65:​21-25)

12 Tunaridhika zaidi tunapotafakari kuhusu tumaini letu zuri la wakati ujao. Maneno ya Yehova yaliyoandikwa na nabii Isaya yanaonyesha wazi jinsi maisha yanavyoweza kuwa magumu na yanatuhakikishia kwamba Yehova ataondoa matatizo hayo. (Soma Isaya 65:​21-25.) Tutaishi katika nyumba nzuri na zenye usalama. Tutakuwa na kazi zenye kuridhisha, na tutakula chakula kitamu na chenye lishe. Hatutakuwa na wasiwasi kamwe kwamba sisi au watoto wetu watapatwa na mambo mabaya. (Isa. 32:​17, 18; Eze. 34:25) Wakati wetu ujao ni mzuri ajabu na hakika.

13. Ni katika njia gani hasa huenda tukahitaji kukazia fikira tumaini letu?

13 Sasa kuliko wakati mwingine wowote, tunahitaji kukazia fikira tumaini letu. Kwa nini? Kwa sababu tunaishi katika “siku za mwisho” na sisi sote tunakabili hali zilizo “ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Kila siku Yehova anatusaidia kuvumilia kwa kutupatia mwongozo, kutuimarisha, na kutupatia msaada tunaohitaji. (Zab. 145:14) Kwa kuongezea, tumaini letu la Kikristo linaweza kututegemeza katika nyakati ngumu. Huenda unapambana ili kuiandalia familia yako mahitaji ya kimwili. Je, hilo linamaanisha kwamba sikuzote utahitaji kupambana? Hapana! Yehova ameahidi kukupatia mambo unayohitaji—na mengi hata zaidi—katika Paradiso. (Zab. 9:18; 72:​12-14) Huenda unakabiliana na maumivu ya kudumu, kushuka moyo, au tatizo kubwa lingine la afya. Je, utakuwa hivyo maisha yako yote, bila tumaini la kupona kamwe? Hapana. Katika ulimwengu mpya wa Mungu hakutakuwa na magonjwa na kifo. (Ufu. 21:​3, 4) Tumaini hilo linatusaidia kuwa wenye kuridhika sasa, na kutokuwa na hasira na uchungu. Tunaweza kuwa wenye kuridhika tunapokabili ukosefu wa haki au kufiwa, tunapokuwa wagonjwa, au tunapokabili jaribu lingine lolote. Kwa nini? Kwa sababu haidhuru changamoto tunazokabili leo ni ngumu kadiri gani, tunajua kwamba “dhiki ni ya muda mfupi” na hivi karibuni ulimwengu huo mpya utatupatia kitulizo cha kudumu.—2 Kor. 4:​17, 18.

14. Tunawezaje kuimarisha tumaini letu?

14 Kwa kuwa tumaini ni muhimu ili tuwe wenye kuridhika, tunawezaje kuimarisha tumaini letu? Kama tu ambavyo huenda mtu akahitaji kuvaa miwani ili aone vizuri zaidi vitu vilivyo mbali, ndivyo ambavyo huenda tukahitaji kuchukua hatua zinazofaa kuimarisha tumaini letu ili tuone vizuri zaidi maisha yetu katika Paradiso ya wakati ujao. Tunapolemewa na wasiwasi kwa sababu ya matatizo ya kifedha, tunaweza kuwazia jinsi maisha yatakavyokuwa wakati pesa, madeni, na umaskini hautakuwepo tena. Ikiwa tuna mahangaiko kuhusu mapendeleo ya utumishi ambayo bado hatujapewa, tunaweza kutafakari jinsi ambavyo mahangaiko hayo hayatakuwa na umuhimu kwa kulinganisha na jinsi maisha yatakavyokuwa bora tutakapokuwa wakamilifu na kumtumikia Yehova kwa maelfu ya miaka. (1 Tim. 6:19) Huenda mwanzoni ikawa rahisi zaidi kuwa na wasiwasi kuhusu matatizo yetu ya sasa, kuliko kutafakari kuhusu wakati wetu ujao. Hata hivyo, baada ya muda, itaanza kuwa rahisi zaidi kwetu kutafakari kuhusu wakati ujao mzuri ambao Yehova ameahidi.

15. Unajifunza nini kutokana na maelezo ya Christa?

15 Fikiria jinsi ambavyo kuwa na tumaini kulimsaidia Christa, mke wa Dennis, aliyetajwa awali. Christa anasema hivi: “Nina ugonjwa wa misuli ambao unaendelea kuwa mbaya zaidi, unaonilazimu kutumia kiti cha magurudumu na kutumia muda mwingi kitandani. Ninahisi maumivu kila siku. Hivi karibuni daktari aliniambia kwamba hali yangu itazidi kuwa mbaya. Lakini mara moja nikajiambia, ‘Maoni yake kuhusu wakati ujao ni tofauti na yangu.’ Ninakazia fikira tumaini langu, jambo ambalo linanipa amani ya akili. Leo, huenda nikahitaji kuvumilia hali yangu katika ulimwengu huu, lakini nitafurahia maisha kikamili katika ulimwengu mpya!”

“WALE WANAOMWOGOPA HAWAKOSI CHOCHOTE”

16. Kwa nini Mfalme Daudi aliweza kuandika kwamba wale wanaomwogopa Yehova “hawakosi chochote”?

16 Mtumishi wa Yehova aliyeridhika bado atakabili changamoto. Mfalme Daudi alifiwa na watoto wake watatu. Alishtakiwa kwa uwongo, alisalitiwa, na kuwindwa akiwa mkimbizi kwa miaka mingi. Licha ya hayo, alipokuwa akivumilia jaribu kali, alisema hivi kumhusu Yehova: “Wale wanaomwogopa hawakosi chochote.” (Zab. 34:​9, 10) Kwa nini aliweza kusema hivyo? Kwa sababu ingawa tukiwa watu wa Yehova hatutarajii kuishi maisha yasiyokuwa na matatizo, tuna uhakika kwamba kamwe hatutakosa chochote tunachohitaji kikweli. (Zab. 145:16) Na tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatutegemeza katika majaribu yetu yote. Tunaweza kuwa wenye kuridhika.

17. Kwa nini umeazimia kujifunza siri ya kuridhika?

17 Yehova anataka uwe mwenye kuridhika. (Zab. 131:​1, 2) Hivyo, jitahidi kujifunza siri ya kuridhika. Ikiwa utajitahidi kusitawisha mtazamo wenye shukrani, kukazia fikira mambo muhimu na kuwa mnyenyekevu, na kuimarisha tumaini lako, utaweza kusema hivi: “Naam, nimeridhika.”—Zab. 16:​5, 6.

MAMBO YAFUATAYO YANAKUSAIDIAJE KURIDHIKA?

  • Kusitawisha mtazamo wenye shukrani

  • Kuendelea kukazia fikira mambo muhimu na kuwa mnyenyekevu

  • Kutafakari kuhusu tumaini lako

WIMBO 118 “Tusaidie Tuwe na Imani Zaidi”

a Kwa mfano, tazama video ya programu ya Ibada ya Asubuhi yenye kichwa, Yehova Anawajali Wanyenyekevu na pia Kiburi Hutangulia Kuanguka kwa Kishindo kwenye jw.org.

b MAELEZO YA PICHA : Ndugu akifanya kazi za udumishaji katika jengo la kitheokrasi, dada ambaye amejifunza lugha ya ishara akihojiwa katika kusanyiko la mzunguko, na ndugu akitoa hotuba ya watu wote.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki