Historia ya Kisasa ya Mashahidi wa Yehova—Lebanoni na Syria (Shamu)
SIFA YA MASHAHIDI YAENEA
Katika upande wa kaskazini wa nchi hiyo kuna kijiji cha “Kikristo” ambacho kimezungukwa na vijiji vya Waislamu. Kuna makundi mawili ya Mashahidi wa Yehova katika kijiji hicho. Waislamu waliposhambulia kijiji hicho kisha wakaja katika nyumba ile ambayo Mashahidi walikuwa wamekusanyika, wanaume hao wenye bunduki waliambiwa hivi: “Sisi tu Mashahidi wa Yehova. Hatuna silaha nasi hatumo kabisa. Nyumba zetu ni hizi, zitendeeni kama mtakavyo.” Wanaume hao wenye silaha walishangaa nao wakaahidi hawatawadhuru.
Katika kijiji kingine, hata padri Mkatoliki alikuwa na silaha ya bombom (bunduki). Mashahidi walikazwa sana waachane na msimamo wao wa kutokuwamo na vilevile wajipatie silaha kwa ajili ya shambulio lililokuwa linatazamiwa. Kwa sababu walikataa kufanya hivyo, kiongozi mmoja wa siasa isiyotaka mabadiliko alisema hivi: “Vita hivi viishapo tutageuza fikira zetu juu yenu!” Hata hivyo ni jambo gani lililotokea wakati shambulio hilo lilipoanza katika Januari 20, 1976?
Wenye kulinda kijiji hicho wakati wote walikimbia. Padri huyo akatupa silaha yake naye akajificha. Wanavijiji wengine ambao walikuwa wamejipatia silaha walijaribu kuficha silaha zao; hali wengine walizitupa zao. Kiongozi mmoja wa siasa isiyotaka mabadiliko alimpa Shahidi bunduki yake, akasema hivi: “Inajulikana kwamba Mashahidi wa Yehova hawana silaha.”
Vilevile, watu wengi walikimbilia katika nyumba za Mashahidi. Katika nyumba moja kama hiyo zaidi ya watu 60 walikusanyika! Baada ya mmoja wa Mashahidi wa Yehova kutoa sala yenye kuomba ulinzi wa Yehova, binti ya kiongozi wa kisiasa alisema hivi: “Sasa najisikia kutulia, kwa kuwa Yehova ni Mungu anayeweza kulinda.” Ingawa watu wenye silaha waliingia katika nyumba hiyo na kuiba vitu vyenye thamani hakuna mtu aliyeumizwa.
Katika nyumba nyingine ya Mashahidi karibu watu 50 walikusanyika. Mwangalizi msimamizi wa Mashahidi wa Yehova huko anaripoti hivi: “Nilisikia jirani Mwislamu akiwaambia wanaume hao wenye silaha hivi, ‘Msiguse nyumba hii. Wao ni wanafunzi wa Biblia, tofauti na wengine.’ Hata hivyo baadaye, wanaume wenye bunduki walikuja. Walakini nilikuwa nimefungua milango yote kwa makusudi. Kwa hiyo walipobisha hodi nilijibu mara moja, nikawaalika waingie. Nilizungumza kwa fadhili na bila kusita, nikawaeleza sisi tu Mashahidi wa Yehova. Walipokosa silaha zo zote, walienda zao.” Nyumba zote katika ujirani huo zilivunjwa na mali kuchukuliwa isiokuwa hiyo.
Katika mji wa upande wa kaskazini wa Tripoli mapambano kati ya vikundi vya kisiasa vyenye kupigana yalikuwa makali sana. Mamia ya nyumba na maduka yalivunjwa na mali kuchukuliwa na kuteketezwa. Sana sana lilikuwa jambo la hatari kwa Wakristo kwenda nje, kwa hiyo jirani mmoja Mwislamu alimwambia hivi Shahidi mmoja:”Watu hawa hawajui kwamba ninyi ni Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo tuambie unavyohitaji nasi tutakuletea.”
JAMAA YA MAKAO MAKUU KATIKA HATARI
Mwanzoni mwa vita ya wenyewe kwa wenyewe makao makuu ya afisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova yalikuwa katika sehemu ya Waislamu ya Beirut. Kabla ya kuhama kutoka huko mpaka mahali palipo salama zaidi nje ya mji huo, jamaa ya makao makuu ilipata mambo yenye kutia woga sana. Katika Februari 6, 1976, mshiriki mmoja wa jamaa hiyo alisimulia hali kama hivi:
“Kwa muda wa kama mwezi mmoja hivi hatukujali hata kwenda kwenye vitanda vyetu vyumbani mwetu. Wakati wa kulala ulipofika tuliweka mito ya kulalia katika kijia kidogo cha kuingilia, kwa kuwa ndicho kilichokuwa chumba salama zaidi katika nyumba hiyo. Sote tulijikunja hapo na kulala tukiwa tumevalia nguo zetu, kwa kuwa hatukujua mambo ambayo yangetokea usiku. Sehemu hiyo ya vita ilipomalizika, wasiotaka mabadiliko walijaribu kuchukua usimamizi wa majengo yenye kufaa katika kujikinga wakati wa vita katika upande wetu wa mji.
“Kisha ikawa vita ya barabarani ya kweli, barabara kwa barabara na nyumba kwa nyumba. Ilionekana kama kwamba wanasiasa wasiotaka mabadiliko wangekuja na barabara hata kufika mbele yetu nao wanasiasa wenye kutoka mabadiliko wakiwa nyuma yetu, kwa hiyo tukaamua kuhama. Hata hivyo, hapakuwa na njia ya kutoka kabisa katika eneo hilo, walakini kulikuwako nyumba salama zaidi, kwa hiyo tukaenda kwenye nyumba salama zaidi, kwa hiyo tukaenda kwenye nyumba ya Shahidi mmoja mwendo wa maili moja (kilometres 1.6) upande wa juu wa barabara. Tulikaa kwake kwa juma mbili na kisha tukaweza kurudi nyumbani.”
MIKUTANO YA KIKRISTO NA KUHUBIRI
Wakati wa jeuri yote hiyo faida za Ufalme ziliendelea kuangaliwa. Makundi yalifanya mikutano yao katika vikundi vidogo vidogo au katika vikundi vikubwa, ikitegemea hali katika eneo fulani katika wakati fulani. Hata makusanyiko ya mzunguko na ya wilaya yalifanywa! Lilikuwa jambo la kawaida kusikia katika sehemu ya karibu mshindo wa bunduki zenye kupiga risasi na risasi zenye kulipuka wakati wa mikutano. Pindi fulani ilimlazimu msemaji atue kwa muda fulani mpaka mshindo wa vita upungue vya kutosha ili apate kusikiwa.
Akina ndugu waliendelea kutoa ushuhuda nyumba kwa nyumba mahali po pote ilipowezekana, na kutoa ushuhuda vivi hivi kwa kadiri kubwa kuliendelea kufanywa. Wengi waliitikia vizuri ujumbe huo, hali wengine walikuwa wenye kushughulikia sana kuwa hai na wasiumizwe hata kwamba lilikuwa jambo gumu kufikia mawazo yao kwa tumaini la Ufalme.
HALI YA WAKATI UJAO
Wakati ujao wa kisiasa na wa kijamii wa nchi hii yenye msuko-suko haujulikani kwa hakika. Walakini ni jambo la hakika kwamba Yehova ataendelea kutimiza kuhubiri kwa habari njema katika Lebanoni na Syria (Shamu) mpaka “dhiki kubwa” ilete taratibu yake mpya ya mambo yenye amani. Akina ndugu walioko katika nchi hizi wanaomba kwamba Yehova aendelee kuwatumia katika kazi hiyo mpaka imalizwe.
—Kutoka Kitabu cha Mwaka cha 1980.