Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • lfs makala 3
  • Kwa Nguvu za Mungu Haturudi Nyuma

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kwa Nguvu za Mungu Haturudi Nyuma
  • Masimulizi ya Maisha ya Mashahidi wa Yehova
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Si Muda wa Kurudi Nyuma
  • Tulihitaji Uvumilivu
  • Kuendelea Kumtumikia Yehova
  • Baraka za Yehova Zilipita Matarajio Yangu Yote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2019
  • 1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    1988 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Yehova Ni Ngome na Nguvu Yangu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
  • Mashahidi wa Yehova—Ripoti ya Kitabu-Mwaka 1994
    1994 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
Pata Habari Zaidi
Masimulizi ya Maisha ya Mashahidi wa Yehova
lfs makala 3
Dayrell Sharp.

DAYRELL SHARP | SIMULIZI LA MAISHA

Kwa Nguvu za Mungu Haturudi Nyuma

“Hatamaliza mwezi mmoja!” Maneno hayo yalisemwa na akina ndugu katika kutaniko letu nilipotuma ombi la kuwa painia wa likizo katika mwaka wa 1956. Nilikuwa na umri wa miaka 16. Ilikuwa miaka minne tangu nilipobatizwa, na nilibatizwa kwa sababu ndugu fulani ninayempenda alipendekeza nibatizwe. Wakati huo hakukuwa na mpango wa wazee kuhakikisha ikiwa mtu anastahili kubatizwa.

Akina ndugu walikuwa na sababu nzuri ya kushuku ikiwa kweli ningefaulu kupainia. Sikuchukua mambo ya kiroho kwa uzito. Sikupenda utumishi wa shambani, na nilisali mvua inyeshe Jumapili ili nisishiriki huduma. Na nilipoenda katika huduma niligawa magazeti tu; sikuwahi kuanzisha mazungumzo kwa kutumia Biblia. Mama yangu mpendwa alinihonga nisome Biblia katika kutaniko. Sikupenda kujifunza na sikuwa na miradi ya kiroho.

Katika msimu wa kiangazi wa mwaka huo kulikuwa na kusanyiko la wilaya (ambalo sasa linaitwa kusanyiko la eneo) huko Cardiff, Wales. Hapo ndipo maisha yangu yalipobadilika kabisa. Msemaji mmoja alituuliza maswali ambayo yalinisaidia kufikiri. Aliuliza hivi: “Je, umejiweka wakfu na kubatizwa?” Nikajiaambia ‘ndiyo.’ “Je, umeahidi kumtumikia Yehova kwa moyo, nafsi, akili, na nguvu zako zote?” Nikajiaambia ‘ndiyo.’ “Je, una matatizo yoyote ya afya au majukumu ya familia yanayokuzuia kuwa painia?” Nikajiaambia ‘Hapana.’ “Je, una kitu chochote kinachokuzuia kuwa painia?” Nikajiaambia ‘Hapana.’ “Ikiwa umejibu hapana kwa swali la mwisho, basi kwa nini wewe si painia?”

Ghafla, nikaanza kuona mambo kwa njia tofauti. Nikajiaambia: ‘Ninapoteza maisha yangu bure. Sitimizi ahadi niliyomwahidi Yehova nilipojiweka wakfu kwake. Simtumikii Yehova kwa nafsi yangu yote.’ Niliwaza kwamba kama mimi ninatarajia Yehova atimize ahadi alizoniahidi, mimi pia ninapaswa kufanya vivyo hivyo. Kwa hiyo, mwezi Oktoba 1956, nilianza upainia wa likizo. Leo unajulikana kuwa upainia msaidizi.

Dayrell akiwa kijana.

Mwaka wa 1959, nilipewa mgawo wa kwenda Aberdeen nikiwa painia wa pekee

Mwaka uliofuata, nikawa painia wa kawaida na kuhamia kutaniko lililokuwa na wahubiri 19. Tangu nilipofika, nilipewa hotuba kila juma. Kwa subira akina ndugu walinisaidia kuboresha hotuba zangu. Miaka miwili baadaye, katika mwaka wa 1959, niliwekwa rasmi kuwa painia wa pekee na kuhamia kwenye mgawo wangu huko Aberdeen, eneo lililokuwa kaskazini kabisa mwa Scotland. Kisha baada ya miezi michache, nilialikwa nitumikie katika Betheli ya London. Kwa miaka saba niliyokuwa Betheli, nilipewa pendeleo la kufanya kazi katika kiwanda cha uchapishaji.

Nilipenda maisha ya Betheli lakini nilitamani kufanya utumishi wa pekee shambani. Nilikuwa kijana mwenye afya, na nilikuwa tayari kutumiwa na Yehova popote. Kwa hiyo, Aprili 1965, nilijaza ombi la kwenda shule ya Gileadi ili kuzoezwa kuwa mmishonari.

Mwaka huo, mimi na ndugu niliyeishi naye Betheli, tuliamua kwenda Berlin, nchini Ujerumani, ili kuhudhuria kusanyiko na kuona Ukuta wa Berlin ambao ulikuwa umejengwa miaka kadhaa mapema.

Siku moja wakati wa kusanyiko, tulipata nafasi ya kushiriki huduma, na nikapangwa pamoja na Susanne Bandrock. Tulifunga ndoa mwaka 1966, na baada ya miaka miwili tulialikwa kuhudhuria darasa la 47 la Gileadi. Hiyo ilikuwa baraka kubwa! Tulihisi hiyo miezi mitano ilipita haraka sana. Tulipewa mgawo wa kwenda Zaire, ambayo sasa inaitwa Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo. Tulishtuka sana! Hatukujua mengi kuhusu nchi hiyo. Tulikuwa na wasiwasi lakini tulikubali mgawo huo na kujiacha mikononi mwa Yehova.

Dayrell na Susanne Sharp wakiwa pamoja na wahitimu wenzao wa darasa la 47 la Gileadi.

Mimi na Susanne tulihitimu Shule ya Gileadi mwaka wa 1969

Baada ya kutumia saa nyingi kwenye uwanja mbalimbali wa ndege na pia kwenye ndege kadhaa, hatimaye tulifika kwenye mji mdogo wa Kolwezi wenye migodi. Tulishangaa kwa nini akina ndugu hawakuja kutupokea. Baadaye tuligundua kwamba telegram ambayo ilipaswa kuwajulisha akina ndugu kwamba tunakuja, ilifika siku mbili baada ya sisi kufika. Kwenye uwanja wa ndege, ofisa mmoja alikuja kuzungumza nasi kwa Kifaransa. Wakati huo, hatukuelewa lugha hiyo. Mwanamke aliyekuwa mbele yetu akageuka na kututafsiria, akasema “Anawakamata.”

Ofisa aliyetukamata alimlazimisha mwanamume mmoja atubebe katika gari lake dogo lenye vitu viwili. Tulishangaa jinsi ofisa huyo, Susanne, mimi, na pia mwenye gari tulivyotoshea kwenye gari hilo. Lazima iwe lilikuwa jambo lenye kuchekesha kutuona tukirushwa-rushwa huku na kule katika barabara hiyo iliyojaa mashimo, huku buti ya gari ikionekana kama mdomo wa samaki uliokuwa ukitafuna mizigo yetu.

Tulipelekwa kwenye makao ya wamishonari. Ingawa hatukujua yako wapi, ofisa huyo alijua. Hakukuwa na mtu nyumbani na malango yalikuwa yamefungwa. Wamishonari wote walikuwa wameenda kwenye makusanyiko ya kimataifa na kwenye likizo. Tulikuwa tumesimama kwenye jua kali na hatukujua la kufanya. Hatimaye ndugu fulani mwenyeji wa eneo hilo alifika. Alipotuona tu, alitabasamu kwa shangwe, nasi tukafarijika. Alimjua ofisa huyo ambaye inaelekea alitarajia kupata pesa kutoka kwetu. Ndugu yetu alizungumza naye na baada ya muda ofisa huyo aliondoka, nasi tukaenda kupumzika.

Dayrell na Susanne wakiwa pamoja na Ndugu Nathan H. Knorr na ndugu na dada wengine.

Tukiwa nje ya makao ya wamishonari nchini Zaire pamoja na ndugu Nathan H. Knorr alipotutembelea mwaka wa 1971

Si Muda wa Kurudi Nyuma

Punde si punde tulitambua kwamba tulikuwa miongoni mwa watu ambao ni wachangamfu, wenye upendo na ambao wamevumilia mambo mengi. Inasikitisha kwamba vurugu na uasi wa kisiasa ulikuwa umesababisha ukatili mwingi nchini kwa miaka kumi iliyotangulia. Kisha mwaka 1971, Mashahidi wa Yehova walipigwa marufuku nchini. Tulijiuliza hali ingekuwaje sasa.

Huo hakuwa muda wa kurudi nyuma kwa woga, na ni ndugu na dada wachache tu waliorudi nyuma, licha ya kushinikizwa vikali ili walegeze msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote wa kisiasa kwa kubeba kadi ya chama na kuvaa alama ya chama. Iwapo wangekataa kuvaa alama hiyo, hawangepata huduma za serikali na wangesumbuliwa na wanajeshi na polisi. Ndugu zetu walipoteza kazi na watoto walifukuzwa shuleni. Mamia ya akina ndugu walifungwa gerezani. Ulikuwa wakati mgumu. Hata hivyo, kwa ujasiri, Mashahidi waliendelea kuwahubiria watu habari njema.

Tulihitaji Uvumilivu

Katika miaka hiyo, nilikuwa mwangalizi wa mzunguko na wa wilaya, hivyo mimi na Susanne tulitumia muda wetu mwingi kusafiri vijijini. Tulipokuwa vijijini tulikabili changamoto kubwa na zisizo za kawaida. Nyumba ndogo zilizoezekwa paa za nyasi hazikuwa na nafasi ya kutosha hata kulala chini. Mara nyingi niligongwa kichwa nilipokuwa nikipita kwenye milango yake midogo. Tulioga kwa maji yaliyochotwa mtoni. Usiku ulipofika, tulitumia mishumaa kusoma. Tulipika kwa makaa. Kwa kweli, tulihisi hayo yalikuwa maisha halisi ya kimishonari. Tulikuja kwa sababu hii​—nasi tulisisimka sana kuwa kwenye mstari wa mbele katika kazi ya Yehova.

Tulipoishi pamoja na Mashahidi wa eneo hilo, tulianza kuthamini mambo ambayo hapo mwanzoni hatukuyathamini sana: chakula, maji, mavazi, na makao. (1 Timotheo 6:8) Mambo mengine yote ni ya ziada. Bado tunakumbuka jambo hilo la msingi.

Ingawa hatukukabili majaribu kama yale ambayo mtume Paulo alikabili, nyakati nyingine safari zetu zilifanya tuhisi imani yetu na nia yetu ilikuwa ikijaribiwa. Tulilazimika kusafiri kwenye barabara zenye hali mbaya na wakati mwingine hata hakukuwa na barabara. Tuliposafiri kwenye barabara zenye mawemawe, gari letu lilitikiswa sana. Wakati mwingine, gari letu lilikwama kwenye mchanga. Wakati wa msimu wa mvua, tulikwama kwenye matope ambayo yalinasa kama gundi. Siku fulani tulisafiri kwa kilomita 70 tu, na gari letu lilikwama mara 12.

Dayrell na ndugu wengine wakichimba ili kukwamua gari lililobeba mizigo kutoka kwenye matope.

Tulipokuwa katika mgawo wetu, mara nyingi tulikwama barabarani

Lakini hatujawahi kujihisi tukiwa karibu na Yehova kama tulivyohisi tulipokuwa tukitumikia huko vijijini chini ya hali hizo ngumu. Tulijifunza kwamba kwa msaada wa Yehova tunaweza kuvumilia kwa shangwe, hata ikiwa hatuwezi kubadili hali ngumu tunayokabiliana nayo. Kwa kawaida, Susanne anapenda zaidi kukaa ndani na si mtu wa kujaribu kufanya mambo yenye kusisimua sana, lakini hata tulipopitia majaribu na hali ngumu hakulalamika kamwe. Kweli, nyakati hizo zilikuwa zenye furaha, zenye kuridhisha, na tulijifunza mambo mengi.

Tukiwa huko Zaire, nilikamatwa mara kadhaa. Wakati fulani nilishtakiwa kwa uwongo kwamba ninanunua na kuuza almasi kwa magendo. Bila shaka, hilo lilitupatia mkazo sana lakini tulijiambia ikiwa Yehova alitaka tutimize mgawo wetu, angetusaidia. Naye alitusaidia!

Kuendelea Kumtumikia Yehova

Mwaka wa 1981, tulialikwa kutumikia katika ofisi ya tawi iliyoko Kinshasa. Mwaka uliotangulia, kazi yetu ilitambuliwa tena kisheria. Kwa hiyo, akina ndugu wakanunua uwanja ambapo ofisi kubwa zaidi ya tawi ingejengwa. Ghafla, Machi 1986, rais alitia sahihi agizo la kupiga marufuku kazi ya Mashahidi wa Yehova. Ujenzi ulisimamishwa na muda si muda, wamishonari wengi waliondoka nchini.

Dayrell akirekodi sauti kwenye kifaa cha kurekodi ndani ya ofisi yake.

Tulitumikia kwa miaka michache katika ofisi ya tawi ya Zaire

Sisi tulifaulu kubaki kwa muda fulani. Tuliendelea kuhubiri kwa kadiri tulivyoweza, ingawa tulijua kwamba maofisa walikuwa wakitutazama kwa makini. Licha ya kuwa waangalifu, nilikamatwa nilipokuwa nikiongoza funzo la Biblia. Niliwekwa kwenye chumba kikubwa, chenye giza, pamoja na wafungwa wengine wengi. Kulikuwa na joto, harufu mbaya, giza, na hewa nzito; hewa na mwangaza uliingia kupitia tundu dogo lililokuwa juu kwenye ukuta mmoja. Wafungwa fulani walinivuta na kunipeleka kwa kiongozi wao. Aliniamuru na kusema “Imba wimbo wetu wa taifa!” Nikamjibu “Siujui.” Kisha wakaniambia, “Basi, imba wimbo wa taifa wa nchi yako!” Nikawajibu “Hata huo siujui.” Akaniamuru nisimame wima ukutani kwa dakika 45. Hatimaye, ndugu ambao ni wenyeji walifanya mipango na nikaachiliwa huru.

Dayrell na Susanne wakiwa wamesimama mbele ya ofisi ya tawi ya Zambia.

Mwaka wa 1987, muda mfupi baada ya kuwasili kwenye ofisi ya tawi ya Zambia

Tuliona kwamba mambo yalizidi tu kuzorota nchini, na baada ya muda mfupi, tukapata mgawo mpya wa kwenda Zambia. Tulipokuwa tukivuka mpaka, tulihisi huzuni na wakati huohuo tulifarijika. Tulikumbuka miaka 18 tuliyotumika pamoja na wamishonari wengine waaminifu na ndugu na dada wenyeji. Ingawa maisha yetu yalikuwa magumu wakati mwingine, tulihisi kwamba Yehova alitubariki. Tulijua kwamba Yehova alikuwa nasi muda wote. Tulikuwa tumejifunza Kiswahili na Kifaransa, na hata Susanne, alijifunza Kilingala kidogo. Tulipata matokeo katika huduma, na tuliwasaidia watu zaidi ya 130 kufanya maendeleo na kubatizwa. Tulihisi tumeridhika sana kujua kwamba tulikuwa tumeshiriki kazi ya kuweka msingi kwa ajili ya ukuzi wa baadaye. Na ukuzi ulikuwa mkubwa kwelikweli! Mwaka 1993, Mahakama Kuu iliondoa marufuku iliyokuwa imewekwa mwaka 1986. Sasa, kuna zaidi ya wahubiri 240,000 wa Ufalme nchini Kongo.

Kwa muda ambao tumekuwa Zambia, tumeona ujenzi wa ofisi mpya na baadaye upanuzi wa majengo hayo. Idadi ya wahubiri wanaotenda imeongezeka mara tatu zaidi ya idadi tuliyokuta tulipofika mwaka wa 1987.

Picha ya ofisi ya tawi ya Zambia

Yule ndugu kijana ambaye alionekana hangeweza kumaliza mwezi mmoja katika utumishi wa wakati wote, anaendeleaje? Kwa baraka za Yehova na utegemezo wa mke wangu mpendwa, Susanne, sasa nimemaliza miaka 65 katika utumishi wa wakati wote, na nimeonja na kuona kwamba Yehova ni mwema!—Zaburi 34:8.

Tunajua kwamba sisi ni watu wa kawaida tu; hata hivyo, tumejitahidi kufanya yote tuwezayo ili kuwa waaminifu na kutimiza ahadi tuliyotoa tulipojiweka wakfu. Tunaamini kwamba Yehova ataendelea kutusaidia ‘tusirudi nyuma’ kamwe bali tuendelee kukua katika imani ili “kuhifadhi uhai wetu.”​—Waebrania 10:39.

Dayrell na Susanne.

Mimi na Susanne bado tunatumikia kwenye ofisi ya tawi ya Zambia

Tazama video Dayrell and Susanne Sharp: We Promised to Serve Jehovah Whole-Souled.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki