Wakati Ujao wa Dini kwa Kutegemea Wakati Wayo Uliopita
Sehemu ya 19: Karne ya 17 hadi ya 19 Jumuiya ya Wakristo Yamenyana na Badiliko la Ulimwengu
“Falsafa na dini haziwezi kupatanishwa.” Georg Herwegh, mshairi Mjeremani wa karne ya 19
“FALSAFA,” neno lililotolewa katika mizizi ya Kigiriki inayomaanisha “kupenda hekima,” ni gumu kulifasili. Huku ikitia shaka kama “fasili yenye kutumika kila mahali na kuhusisha mambo yote” yaweza kufanywa, The New Encyclopædia Britannica huthubutu kusema kwamba “jaribio la kwanza katika jambo hili lingeweza kuwa ni kufasili falsafa kama ‘kufikiria namna mbalimbali za ujuzi wa kibinadamu’ au kama ‘ufikirio wa akili ya kiasi, wa kufuata mpangilio mzuri, na utaratibu, wa habari zile ambazo humpendeza binadamu kwa kadiri kubwa zaidi.’”
Fasili hizi zaonyesha wazi kwa nini dini ya kweli na falsafa haziwezi kupatanishwa. Dini ya kweli hutegemea msingi wa ufunuo wa kimungu, wala haitegemei “namna mbalimbali za ujuzi wa kibinadamu.” Kwanza na mbele kabisa, hiyo huzungukia mapendezi ya Muumba, si “habari zile ambazo humpendeza binadamu kwa kadiri kubwa zaidi.” Kwa upande mwingine, dini bandia, kama vile falsafa, hutegemea msingi wa ujuzi wa kibinadamu na huweka mapendezi ya kibinadamu juu kabisa. Uhakika huu ulionekana wazi hasa kuanzia karne ya 17 na kuendelea wakati Jumuiya ya Wakristo ilipokuwa ikimenyana na badiliko la ulimwengu.
Tisho Mara Tatu
Mara tu sayansi ya ki-siku-hizi ilipozaliwa katika karne ya 17, ilionekana kwamba mgongano kati yayo na dini haungeepukika. Mafanikio makubwa ajabu ya kisayansi yaliipa sayansi heshima nyingi mno ya kutoweza kukosea na ya mamlaka, hiyo ikitokeza ibada ya sayansi, ambayo yenyewe ni dini, ng’ombe mtakatifu. Kulingana na “mambo hakika” ya kisayansi, madai ya kidini yakaonekana ghafula kana kwamba yalikuwa hoi kwa kukosa uthibitisho. Sayansi ilikuwa mpya na yenye kusisimua; dini ilionekana kuwa ya kizamani na isiyo na upendezi.
Mtazamo huo kuelekea dini uliongezewa nguvu na ule Mwangazio (Mwerevuko), harakati ya wenye akili iliyokumba Ulaya katika karne za 17 na 18. Ikikazia maendeleo ya kiakili na ya kimwili, ilikataa mamlaka ya siasa na dini na mapokeo kwa kupendelea kuhakiki mambo kwa kutoa sababu. Ilidhaniwa kwamba hicho kilikuwa ndicho chanzo cha maarifa na furaha. “Mizizi yayo ya kikale,” yasema The New Encyclopædia Britannica, ilipatikana katika “falsafa ya Kigiriki.”
Harakati hiyo ya Mwangazio ilikuwa sana-sana ni tukio la Ufaransa. Viongozi mashuhuri katika Ufaransa walihusisha Voltaire na Denis Diderot. Katika Uingereza ilipata wasemaji katika John Locke na David Hume. Wenye kuitetea walipatikana pia miongoni mwa mababa waanzilishi wa United States, kutia na Thomas Paine, Benjamin Franklin, na Thomas Jefferson. Kwa uhakika, mtenganisho wa Kanisa na Serikali ambao Katiba ya United States ilidai ufanywe huonyesha jinsi mawazo ya Mwangazio yalivyokuwa. Washiriki wenye kutokeza katika Ujeremani walikuwa Christian Wolff, Immanuel Kant, na Moses Mendelssohn, babu ya mtungaji Felix Mendelssohn.
Kant, kwa kutia shuku juu ya dini, husemwa kuwa alifasili “mwangazio” kuwa “kufunguliwa kwa binadamu kutoka kwenye hali ya kujifundisha.” Allen W. Wood wa Cornell aeleza kwamba, kwa kusema hivyo Kant alimaanisha “utaratibu ule ambao kupitia huo wanadamu mmoja mmoja hupokea moyo mkuu wa kujifanyia fikira zao wenyewe juu ya maadili, dini, na siasa, badala ya kuamrishiwa maoni yao na mamlaka za kisiasa, za kidini, au za kimaandiko.”
Wakati wa nusu ya pili ya karne ya 18, ule Mvuvumko wa Viwanda ulianza, kwanza katika Uingereza. Mkazo uliacha kutiwa juu ya ukulima ukawa juu ya kutengeneza bidhaa na kuzifanyiza kwa msaada wa mashine na taratibu za kutumia kemikali. Hiyo ilivuruga jamii yenye kufuata sana ukulima na mashamba, ikapeleka maelfu ya watu wakasongamane ndani ya majiji ili kufanya kazi. Kulitokea visa vingi sana vya kukosa kazi, upungufu wa makao, umaskini, na maovu mbalimbali yenye kuhusiana na kazi.
Je! Jumuiya ya Wakristo ingeweza kukabiliana na tisho mara tatu la sayansi, Mwangazio, na shughuli za viwandani?
Kusukuma-sukuma Mungu Kando, Japo kwa Uanana Sana
Watu wenye kuvutwa na fikira za Mwangazio walilaumu dini kwa mengi ya maovu ya jamii. Wazo la kwamba “jamii yapasa kuundwa kulingana na ramani zilizotangulia kuandikwa za sheria ya kimungu na ya asili,” yasema The Encyclopedia of Religion, “liliondolewa na mahali palo pakachukuliwa na ‘ubuni’ au ‘utunzi’ wa binadamu mwenyewe. Hivyo, kulitokea ufuataji wa mawazo ya kibinadamu katika jamii ambao, nao, ungetokeza nyingi za nadharia zilizo za kifalsafa na kisosholojia za ulimwengu wa ki-siku-hizi.”
Nadharia hizi zilihusisha “dini ya umma” iliyotetewa na mwanafalsafa Mfaransa mwenye uvutano mwingi Jean-Jacques Rousseau. Ilitegemea hasa jamii na kujishughulisha kwa binadamu katika mahangaikio yao badala ya kutegemea Mhai wa kimungu na ibada yake. Mwandikaji Mfaransa wa nyasifu, Claude-Henri de Rouvroy, alitetea “Ukristo Mpya,” hali kibaraka wake Auguste Comte aliongea juu ya “dini ya jamii ya kibinadamu.”
Mwishoni mwa karne ya 19, harakati ya Kiamerika ijulikanayo kuwa gospeli ya kijamii ilisitawi miongoni mwa Waprotestanti; ilihusiana kwa ukaribu na nadharia za Ulaya. Wazo hilo lenye msingi wa kitheolojia lilikazania kwamba wajibu mkuu wa Mkristo ni kujihusisha katika mambo ya kijamii. Hilo huungwa mkono sana miongoni mwa Waprotestanti hadi leo. Namna za Kikatoliki za wazo hilo hupatikana katika mapadri-wafanya-kazi wa Ufaransa na miongoni mwa makasisi wa Amerika ya Kilatini ambao hufundisha theolojia ya ukombozi.
Wamisionari wa Jumuiya ya Wakristo pia huiga elekeo hilo, kama vile ionyeshwavyo na ripoti moja ya gazeti Time la 1982: “Miongoni mwa Waprotestanti, kumekuwa na badiliko la kujihusisha kwa kadiri kubwa zaidi na matatizo ya msingi ya watu ya kiuchumi na ya kijamii . . . Kwa hesabu inayoongezeka ya wamisionari Wakatoliki, kujihusisha na hali ya walio maskini humaanisha kutetea mabadiliko makubwa sana katika mifumo ya kisiasa na ya kiuchumi—hata ikiwa mabadiliko hayo yanaongozwa na harakati za kimapinduzi za wenye kufuata mawazo ya Marx. . . . Kwa kweli, kuna wamisionari ambao huamini kwamba uongofu haufaani kabisa na furushi halisi wapaswalo kutimiza.” Yaonekana wazi kwamba wamisionari hao huafikiana na mwanasosholojia Mfaransa Émile Durkheim, aliyedokeza hivi wakati mmoja: ‘Lengo halisi la ibada ya kidini ni jamii, si Mungu.’
Kwa wazi, Jumuiya ya Wakristo ilikuwa ikisukuma-sukuma Mungu atoke katika dini, japo kwa uanana sana. Kwa wakati huo, kani nyingine pia zilikuwa zikifanya kazi.
Mahali pa Mungu Pachukuliwa na Dini za Bandia
Makanisa hayakuwa na matatuzi kwa matatizo yaliyofanyizwa na ule Mvuvumko wa Viwanda. Lakini dini za bandia, zikiwa mazao ya falsafa za kibinadamu, zilidai kuwa nayo, nazo zilifyatuka mbio zikajazie pengo hilo.
Kwa kielelezo, watu fulani walipata kusudi lao maishani kwa kufuatia utajiri na mali, elekeo la kujifaidi binafsi lililochochewa na ule Mvuvumko wa Viwanda. Ufuatiaji wa vitu vya kimwili ukawa dini. Mahali pa Mungu Mweza Yote palichukuliwa na ile ‘Dola Yenye Kuweza Yote.’ Katika mchezo wa kuigiza uliotungwa na Bernard Shaw, wazo hilo liligusiwa na mhusika aliyepaaza sauti hivi: “Mimi ni Milionea. Hiyo ndiyo dini yangu.”
Watu wengine waligeukia harakati za kisiasa. Mwanafalsafa msosholojia Friedrich Engels, mshirikiani pamoja na Karl Marx, alitoa unabii wa kwamba hatimaye usosholojia ungechukua mahali pa dini, na huo wenyewe utwae sifa za kidini. Hivyo, usosholojia ulipoimarika pande zote za Ulaya, asema Profesa Robert Nisbet aliyestaafu, “kitu maarufu kilikuwa uasi-imani wa wanasosholojia kwa kuacha Dini ya Kiyahudi au Ukristo na kugeukia kitu hafifu.”
Kushindwa kwa Jumuiya ya Wakristo kukabiliana na badiliko la ulimwengu kuliruhusu usitawi wa kani ambazo World Christian Encyclopedia huzirejezea kuwa “uulimwengu, ufuatiaji wa sayansi wa vitu vya kimwili, ukomunisti usioamini kuwako kwa Mungu, utukuzo wa taifa, unazi, ufashisti, Umao, ufuataji wa mawazo ya kibinadamu kuhusu ukombozi na dini za bandia nyingine nyingi sana za kuundwa au kutungwa tu.”
Kwa sababu ya matunda ambayo hizi dini bandia za kifalsafa zimetokeza, maneno ya mshairi Mwingereza John Milton yangeonekana kuwa yenye kufaa sana: “Yote ni hekima bure, na falsafa bandia.”
Kutafuta Uridhiano
Wakiwa wamenaswa kati ya mifumo ya kidini isiyo na matokeo kwa upande mmoja na dini za bandia zenye udanganyifu kwa upande ule mwingine, mamilioni ya watu walikuwa wakitafuta kitu bora. Baadhi yao walifikiri wamekipata kwa namna ya Udei (“Deism”), ambao pia hujulikana kuwa “dini ya kiasili.” Ukiwa wenye kupata umaarufu hasa katika Uingereza katika karne ya 17, Udei umeelezwa kuwa ni uridhiano ulioikubali sayansi kwa moyo bila kumwacha Mungu. Kwa hiyo waabudu wa Udei walikuwa watu wenye kufuata mawazo ya hiari kwa kufuata maoni ya katikati.
Mtungaji Wood huelewesha wazi hivi: “Katika maana yalo kuu, udei humaanisha imani katika Mungu mmoja na katika zoea moja la kidini lenye kutegemea kusababu mambo kiasili badala ya kutegemea ufunuo wa nguvu zipitazo zile za kiasili.” Lakini kwa kukataa “ufunuo wa nguvu zipitazo zile za kiasili,” waabudu fulani wa Udei walifikia hatua ya kuikataa Biblia kwa ujumla. Siku hizi mtajo huo hautumiwi sana, ingawa watu wajidaio kuwa Wakristo ambao hukataa mamlaka ya kidini au ya Kimaandiko kwa kupendelea maoni ya kibinafsi au falsafa nyinginezo kuhusu maisha huwa kwa kweli wanafuata kanuni zao.
Nadharia Linganifu za Mageuzi
Mkabiliano ulio wa kutazamisha zaidi kati ya dini na sayansi ulitukia baada ya kuchapishwa katika 1859 kwa Origin of Species cha Darwin, ambamo yeye alitokeza nadharia yake ya mageuzi. Viongozi wa kidini, hasa katika Uingereza na United States, walishutumu nadharia hiyo kwa maneno makali hapo kwanza. Lakini muda si muda upinzani ukafifia. Kufikia wakati wa kufa kwa Darwin, yasema The Encyclopedia of Religion, “makasisi wenye kufikiri zaidi na wafasaha wakawa wamefikia kauli ya kwamba mageuzi yalipatana kabisa na uelewevu uliopata mwangazio mzuri kuhusu andiko.”
Huenda hiyo ikaeleza ni kwa nini Vatikani haikuweka vitabu vya Darwin katika faharasi yao ya Index of Forbidden Books (Faharasi ya Vitabu Vilivyokatazwa). Huenda pia ikaeleza ni kwa nini wasikilizaji waliitikia kama walivyofanya kwenye mkutano wa Chicago mwaka 1893 wa Bunge la Dini za Ulimwengu. Huku Wabuddha na Wahindu wakisikiliza, msemaji “Mkristo” alisema hivi: “Nadharia ya mageuzi yajazia pengo lililo kwenye mwanzo wenyewe wa dini yetu, na ikiwa sayansi imeridhishwa kijumla na nadharia yayo ya mageuzi kuwa ndiyo njia ya uumbaji, wale ambao kazi yao ni kuzijua na kuzipenda njia za Mungu hawapaswi kuikubali kwa ulegevu.” Yaripotiwa kwamba taarifa hiyo ilipokewa kwa makofi ya nderemo.
Maoni hayo hayashangazi inapofikiriwa kwamba ile iliyokuja kujulikana kuwa dini ya ulinganisho ilifuatwa kwa umaarufu mwishoni mwa karne ya 19. Huo ulikuwa ni uchunguzi wa kisayansi wa dini za ulimwengu wenye kusudi la kupambanua jinsi dini tofauti zinavyohusiana na jinsi zilivyotokea. Kwa kielelezo, John Lubbock aliye mwandikaji wa asili na imani za kibinadamu alitamka nadharia ya kwamba wanadamu walianza wakiwa hawaamini kuwako kwa Mungu halafu pole kwa pole wakageuka na kuamini ibada ya hirizi (“fetishism”), ibada ya asili (maumbile), na ushamani (ibada ya mazingaombwe) kabla ya kufikia ibada ya Mungu mmoja.
Hata hivyo, kama vile kielezavyo The Encyclopedia of Religion: “Ikionwa kwa njia hiyo, dini haikuwa ukweli kamili uliofunuliwa na mungu, bali ilikuwa kumbukumbu la dhana za kibinadamu zenye kusitawi kuhusu Mungu na maadili.” Kwa hiyo wale waliokubali nadharia hii hawakuona ikiwa vigumu kukubali Udei, “dini ya umma,” au “dini ya jamii ya kibinadamu” kuwa vidato vya kupanda ngazi ya mageuzi ya dini.
Mwisho basi, maoni ya jinsi hiyo huongoza wapi? Tayari katika karne ya 19, mwanafalsafa Mwingereza Herbert Spencer alisema kwamba jamii ilikuwa ikisonga mbele ikafikie hatua ambayo haingepatana tena na dini. Na juu ya karne ya 20, Profesa Nisbet alionelea kwamba wanasosholojia kwa ujumla huamini kwamba dini “hutimiza mahitaji fulani ya kisaikolojia katika wanadamu, na iwapo au isipokuwa mahitaji haya yamalizike kwa sababu ya mgeuko-geuko wa kibayolojia wa aina ya kibinadamu, dini kwa namna yoyote ile itaendelea kuwa uhalisi wenye kuwapo daima katika utamaduni wa kibinadamu.” (Italiki ni zetu.) Kwa hiyo, wanasosholojia hawakanushi kabisa uwezekano wa kwamba “maendeleo ya kimageuzi” huenda siku moja yakafanya kusiwe kamwe na dini!
Utafutaji wa Ibada ya Kweli Waongeza Mwendo
Kufikia katikati ya karne ya 19, ilikuwa wazi kwamba kwa miaka kama 200, Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imekuwa ikijitahidi bure dhidi ya badiliko la ulimwengu. Dini yayo ilikuwa imezorota ikawa falsafa ya kilimwengu tu. Mamilioni ya watu wafuataji haki walihangaishwa na jambo hilo. Utafutaji wa ibada ya kweli ukaongeza mwendo. Ingeweza kusemwa kikweli kwamba ilikuwa haiwezekani kufanya mrekebisho katika Jumuiya ya Wakristo. Kilichohitajiwa kilikuwa mrudisho wa ibada ya kweli. Jifunze mengi zaidi katika makala inayokuja.
[Sanduku katika ukurasa wa 23]
Kwa Kubanwa na Badiliko la Ulimwengu Jumuiya ya Wakristo Yaridhiana
KUIBUKA KWA SAYANSI YA KI-SIKU-HIZI kulidhoofisha imani katika visivyoonekana na kufanyiza shaka juu ya mambo ambayo sayansi haikuweza “kuthibitisha.” Jumuiya ya Wakristo iliridhiana kwa kuuacha ukweli wa Biblia kwa kuchagua kufuata nadharia zisizothibitishwa zilizodhaniwa eti kuwa za kisayansi kama vile mageuzi, na kwa kutazamia kwamba ujuzi wa kisayansi, kuliko Ufalme wa Mungu, ndio dawa ya matatizo yote ya ulimwengu.
KUTOKEA KWA MAWAZO YA KISIASA (ubepari, demokrasi, usoshalisti [ujamaa], Ukomunisti, na kadhalika) kulifanyiza mapambano ya kitaifa na mzozano wa kimawazo, hivyo kukificha ukweli wa Biblia kwamba Mungu ndiye Mtawala wa dunia aliye na haki, wala si mwanadamu. Jumuiya ya Wakristo iliridhiana kwa kuacha kanuni za Biblia kwa kuvunja kutokuwamo kwa Kikristo na kuhusika katika vita vilivyogonganisha washiriki wa dini ile ile. Jumuiya ya Wakristo iliunga mkono dini bandia za kisiasa kwa kufanya utendaji au kwa kujikalia tu.
KIWANGO CHA JUU ZAIDI CHA MAISHA kilichofanywa kiwezekane na Mvuvumko wa Viwanda na Sayansi kiliendeleza hali ya kutanguliza faida za kibinafsi na kutanguliza mbele ukosefu wa haki ya kijamii na ukosefu wa usawa. Jumuiya ya Wakristo iliridhiana kwa kupendelea kuhusika katika mapendezi ya kibinadamu ya hali ya kijamii, kiuchumi, kimazingira, au kisiasa.
[Sanduku katika ukurasa wa 25]
Juu au Chini?
Biblia husema: Wanadamu waliumbwa wakiwa wakamilifu na wakafundishwa jinsi ya kuabudu Muumba wao kwa njia yenye kukubalika; lakini wao waliasi dhidi ya Mungu, na kwa miaka kama 6,000, wamekuwa wakizorota kimwili na kiadili pia, wakisonga mbali hata zaidi kutoka kwenye ile dini ya kweli waliyoizoea hapo kwanza.
Mageuzi ya kibayolojia na ya kidini husema hivi: Wanadamu waligeuka-geuka kutoka mwanzo wa kizamani usiositawi sana na walikuwa hawaamini kuwako kwa Mungu wakiwa bila dini; kwa mamilioni yasiyoelezeka ya miaka, wamefanya maendeleo ya uzuri unaowaziwa kuwa kamili kimwili na kiadili pia, wakisogea karibu hata zaidi kwenye usitawi wa kidini, wa kijamii, na wa kiadili.
Kwa kutegemea maarifa yako juu ya mwenendo wa kibinadamu, hali iliyopo ya ainabinadamu, na msimamo wa dini katika ulimwengu wa leo, ni yapi ya maoni hayo yaelekea zaidi kupatana na mambo ya hakika?
[Picha katika ukurasa wa 24]
Makisio yasiyothibitishwa ya Darwin katika Origin of Species yalikuja kuwa kisingizio cha wengi cha kuacha kuamini katika Mungu wa ufunuo
Harper’s
[Hisani]
Harper’s