Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g90 8/8 kur. 26-29
  • Sehemu ya 20: Karne ya 19 na kuendelea—Mrudisho Uko Karibu!

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sehemu ya 20: Karne ya 19 na kuendelea—Mrudisho Uko Karibu!
  • Amkeni!—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuwasha Mishumaa Yao Wenyewe
  • Dini Yajiharibia Hali
  • Wakati Ndio Uliohitajiwa
  • Mfalme wa Mungu Atawazwa!
  • Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi za Kidini—Hiyo ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Sehemu ya 17: 1530 na kuendelea —Uprotestanti—Je! Ni Marekebisho?
    Amkeni!—1990
  • Kuenea kwa Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi za Kidini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1997
  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1990
g90 8/8 kur. 26-29

Wakati Ujao wa Dini kwa Kutegemea Wakati Wayo Uliopita

Sehemu ya 20: Karne ya 19 na kuendelea—Mrudisho Uko Karibu!

“Njia bora kabisa ya kuona nuru ya kimungu ni kuzima mshumaa wako mwenyewe.” Thomas Fuller, tabibu na mwandikaji Mwingereza (1654-1734)

KARNE ya 19 imeitwa kimoja cha vipindi vya kujikaza sana kisulubu vya historia ya Kikristo, ikilingana na karne za mapema na miaka ile ya Mrekebisho. Sababu za ongezeko hilo katika ujuaji na utendaji wa kidini ni nyingi na za namna mbalimbali.

Mtungaji Kenneth S. Latourette aorodhesha visababishi 13 vinavyohusiana na jambo hili, baadhi yavyo vikiwa vimezungumzwa katika toleo lililotangulia la gazeti hili. Yeye asema kwamba “jamii ya kibinadamu haijapata kamwe kubadilishwa kwa kadiri kubwa na kwa njia mbalimbali jinsi hiyo.”

Katika United States, kutokea upya kwa dini kulionekana wazi. Kwa kielelezo, uanashirika wa kanisa uliongezeka kutoka chini ya asilimia 10 ya idadi ya watu mwanzoni mwa karne ukawa karibu asilimia 40 mwishoni mwayo. Shule za Jumapili—zilizoanzishwa katika Uingereza katika 1780—ziliongezeka umaarufu. Sababu ni kwamba, tofauti na Ulaya, kutenganisha Kanisa na Serikali katika United States kulizuia maagizo ya kidini katika shule za umma. Zaidi ya hilo, koleji nyingi za kidhehebu na sosaiti za Biblia za mchanganyiko wa kimadhehebu zilianzishwa, na wakati wa nusu ya kwanza ya karne hiyo, angalau seminari 25 za kitheolojia zilianzishwa katika United States.

Kwa sasa, katika tufe lote, Uprotestanti ukawa ukifikiria umisionari. Fundi-viatu na mwalimu Mwingereza William Carey alikuwa amechukua uongozi katika 1792 kwa kuchapisha kitabu An Enquiry Into the Obligations of Christians to Use Means for the Conversion of the Heathens. Wakiwa wanatumikia wakiwa wamisionari katika India, Carey na washirika wake walitafsiri Biblia kwa ukamili au kwa sehemu katika lugha na lahaja zaidi ya 40 za Kihindi na nyinginezo za Kiesia. Kazi ambayo baadhi ya wamisionari hawa wa mapema walifanya katika kugawanya Biblia yastahili pongezi.

Pia sayansi mpya ya akiolojia (uchimbuzi wa vitu vya kale) ya Kibiblia ilipata hadhi nyingi zaidi wakati wa karne iliyopita. Katika 1799 askari Wafaransa katika Misri waligundua bamba la jiwe-basalti jeusi ambalo sasa huitwa jiwe la Rosetta. Lilikuwa na mwandiko ule ule ukiwa umeandikwa mara tatu, mara mbili kwa namna mbili za mwandiko-maumbo wa Kimisri na mara moja katika Kigiriki. Hivyo lilithibitika kuwa lenye thamani kubwa sana katika jitihada ya kuelewa miandiko-maumbo ya Kimisri. Upesi baada ya hapo miandiko-kabari ya Kiasiria (Kiashuri) ilieleweka pia. Kwa hiyo machimbuo yalipoanza katika Asiria na Misri upesi baada ya hapo, vitu vya sanaa vilivyofukuliwa ardhini vilichukua maana mpya. Masimulizi mengi ya Biblia yalihakikishwa kuwa kweli hadi kwenye vijambo vidogo kabisa.

Kuwasha Mishumaa Yao Wenyewe

Kadiri upendezi wa kidini ulivyoongezeka, ndivyo pia na hesabu ya waliotaka kuwa warekebishi. Hata hivyo, ilikuwa wazi kwamba si wote waliokuwa na weupe wa moyo. Mtungaji aliyetangulia kutajwa, Kenneth S. Latourette, hukiri kwa wazi kabisa kwamba baadhi ya madhehebu mpya za kidini “zilitokana na husuda, magomvi, na makuu ya kibinafsi.” Lakini warekebishi wenye kuwasha mishumaa yao wenyewe ya kujitafutia makuu ya kibinafsi hawangeweza kutarajiwa wawe ndio chaguo la Mungu la kurudisha ibada ya kweli.

Katikati ya shelabela hii ya kila mtu kuwasha-washa mshumaa wake mwenyewe (kujitafutia sifa), fikira za kitheolojia zilikanganyika. Uchambuzi wa juu zaidi, ambao sana-sana ulikuwa tokeo la vyuo vikuu vya Kijeremani, ulifasiri upya Maandiko kulingana na wazo “la juu” la kisayansi. Wachambuzi wa juu zaidi waliiona Biblia kuwa ni maandishi ya dini ya Kiyahudi tu. Umamlaka wa Biblia wa kuwa na umaana wa kuamua njia ya wokovu ulitiliwa shaka, hali moja na hekima ya viwango vya kiadili ambavyo hiyo huvitetea.

Uchambuzi wa juu zaidi uliungwa mkono kwa utayari, hasa miongoni mwa makasisi Waprotestanti. Kulingana na ripoti moja, kufikia 1897 hakuna hata mshiriki mmoja wa kitivo cha vyuo vikuu 20 vya theolojia ya Kiprotestanti katika Ujeremani aliyekuwa angali akishikilia maoni yale ya jadi juu ya uandikaji wa Pentateuko (vile vitabu vitano) au kitabu cha Isaya.

Miaka michache baadaye, katika 1902, ubishano juu ya uchambuzi wa juu zaidi ulitokea kwenye mkutano mmoja wa Makusanyiko Makuu ya Makanisa ya Kipresbiteri katika Uskochi. Edinburgh Evening News liliripoti hivi: “Kulingana na wachambuzi wa juu zaidi, . . . Biblia ni mkusanyo wa hadithi za ubuni, ambazo mhubiri aweza kutoa chembe chache za fundisho la kimaadili sawasawa na vile mfunza-maadili stadi aweza kutoa chembe chache za fundisho la kimaadili kutoka kwenye ‘Hekaya za Æsop.’” Hata hivyo, gazeti hilo lilitoa maoni haya halafu: “Tabaka za wafanya kazi si za wapumbavu. Wao hawatahudhuria kanisa kusikiliza wanaume ambao wanaishi katika ukungu wa kiakili wao wenyewe.”

Makala ya pili ya siku chache baadaye ilitoboa mambo kwa uwazi hata zaidi, ikieleza hivi: “Hakuna sababu ya kutotoboa maneno. Kanisa la Kiprotestanti ni unafiki uliopangwa kitengenezo, na viongozi walo ndio walaghai wa mwisho. Mambo yamefikia kilele hivi kwamba kama mtungaji wa ‘Kipindi cha Kusababu Mambo’ angalikuwa hai leo hangalitajwa kimadharau kuwa Tom Paine, yule kafiri, bali kuwa Reverendi Thomas Paine, mwenye Shahada ya Uanamungu, Profesa wa Kiebrania na Fasili ya Agano la Kale, Koleji ya U[nited] F[ree], Glasgow. Hangekuwa na ugumu wowote kuhubiri kutoka mimbari ya Kiprotestanti . . . [na] kuchuma mshahara mnono akiwa profesa wa theolojia.”

Dini Yajiharibia Hali

Tangu mwanzo wao, Uprotestanti ulikazia uongofu wa kibinafsi na ujuzi wa Kikristo, ukategemea Andiko sana-sana, na kushusha hadhi ya sakramenti na mapokeo.

Katika miaka ya 1830 na 1840, Waevanjeliko wengi Waprotestanti walianza kupiga mbiu kwamba kuja kwa pili kwa Kristo kulikuwa kunakaribia pamoja na mwanzo wa ile Mileani. William Miller, mkulima wa New York, alithubutu kusema kwamba kuja kwa pili kungeweza kutokea karibu 1843. Harakati hii ya kimileani ilisaidia kuweka msingi wa namna maarufu na yenye ukinzani zaidi ambayo ilijulikana kuwa Ufandamentali.

Kwa kadiri kubwa Ufandamentali ulikuwa ni kujiharibia ile hali ya kutia shaka, fikira za kujitegemea, kupunguza uzito wa mambo, na ya ulegevu wa kiadili iliyokuwa imetokezwa na Uprotestanti wenye kuleta uhuru mwingi wa mambo. Baadaye huo ulikubali jina lao kutokana na mfululizo wa vichapo 12 vyenye kichwa The Fundamentals, kilichochapishwa kuanzia 1909 hadi 1912 na Moody Bible Institute.

Ufandamentali, hasa katika United States, umejulikana vema kupitia huduma zao zenye matokeo za redio na televisheni, taasisi zao za Biblia, na mikutano yenye hisia nyingi za moyoni ambayo hutangazwa sana kuhuisha imani ya watu. Hata hivyo, hivi majuzi sifa zao zimeharibiwa na matendo mabaya ya kifedha na kingono yaliyotendwa na baadhi ya viongozi wao walio mashuhuri zaidi. Pia imechambuliwa kwa utendaji wao unaoongezeka kuwa wa kisiasa, hasa tangu kuanzishwa kwa kikundi cha “Moral Majority” katika 1979, kilichovunjwa hivi majuzi.

Ingawa Ufandamentali hudai kuitetea Biblia, kwa kweli umebomoa mamlaka yao pia. Njia moja ambavyo umefanya hivyo ni kwa fasiri ya kufuata maana halisi juu ya maandiko ambayo kwa wazi hayakusudiwi yachukuliwe kwa maana halisi. Kielelezo cha jambo hilo ni lile dai la kwamba, kulingana na usimulizi wa Mwanzo, dunia iliumbwa kwa siku 6 halisi za saa 24. Kwa wazi, hizo zilikuwa siku za ufananisho za muda mrefu zaidi. (Linganisha Mwanzo 2:3, 4; 2 Petro 3:8.) Njia nyinginezo ambazo Ufandamentali huibomoa Biblia ni kwa kufundisha mafundisho yasiyo ya kimaandiko, kama mateso ya milele katika moto wa mateso, na nyakati fulani kwa kutetea viwango vya mwenendo ambavyo ni tofauti na vile vinavyotakwa na Andiko, kama vile kukataza kunywa vileo au utumizi wa wanawake wa marembo. Katika njizi hizi Ufandamentali umesababisha watu waukatae ujumbe wa Biblia kuwa wa akili haba, usio na usababu mzuri, na usiopatana na sayansi.

Wakati Ndio Uliohitajiwa

Kwa wazi, kilichohitajiwa kilikuwa mrudisho, mrudisho wa ibada ya kweli! Lakini kama vile Mhubiri 3:1, NW, isemavyo: “Kwa kila jambo kuna wakati uliowekwa.”

Huko nyuma katika karne ya kwanza, Yesu alitendesha upya ibada ya kweli ikiwa kwa namna ya Ukristo. Hata hivyo, alitoa unabii kwamba kungekuwa na uasi-imani. Alisema kwamba Wakristo wa kweli, kama ngano, na Wakristo bandia, kama magugu, ‘wangekua wote pamoja mpaka mavuno.’ Wakati huo, malaika ‘wangekusanya magugu na kuyateketeza,’ hali Wakristo wa kweli wangekusanywa ndani ya upendeleo wa Mungu. (Mathayo 13:24-30, 37-43, NW) Katika sehemu ya mwishoni mwa karne ya 19, wakati uliowekewa mrudisho huu wa ibada ya kweli ulikuwa karibu sana.

Charles Taze Russell alizaliwa katika Pittsburgh, Pennsylvania, katika 1852, na hata akiwa mtoto, alidhihirisha upendezi mkubwa katika Biblia. Katika miaka yake ya mapema ya 20, aligeuza uangalifu wake kutoka biashara ya familia ukawa kwenye kutoa wakati wake wote kwenye kuhubiri. Kufikia 1916, alipokufa akiwa na umri wa 64, yaripotiwa kuwa alikuwa amehubiri mahubiri zaidi ya 30,000 na kuandika vitabu vyenye kurasa zaidi ya 50,000.

Ingawa aliitambua kazi ya kupongezeka iliyokuwa imefanywa na wengine katika kutetea Biblia, Russell aling’amua kwamba kutafsiri, kuchapa, na kugawanya tu Biblia hakutoshi. Kwa hiyo katika 1879 alianza kuchapisha gazeti ambalo leo hujulikana kuwa Mnara wa Mlinzi. Toleo lalo la kwanza lilisema hivi: “Sisi tuna mbetuko mwingi mno wa kuuliza, Kanisa langu husema nini juu ya swali lolote, badala ya Maandiko husema nini? Hujifunza theolojia nyingi mno, lakini Biblia si kwa kadiri ya kutosha. Basi, kwa wazo la kwamba ‘Maandiko yaweza kutufanya wenye hekima,’ kwamba ‘shuhuda za Bwana ni hakika zikiwahekimisha wajinga,’ acheni tuchunguze.”

Leo, Mnara wa Mlinzi (ambao sasa huchapishwa katika lugha 107 ukiwa na mwenezo wa nakala zaidi ya milioni 13 kwa toleo), ukiwa umemaliza miaka 110 ya kuchapishwa bila kukatizwa, huendelea kuchunguza Neno la Mungu. Mamilioni ya watu wamejifunza kuthamini msaada ambao huandaliwa nao katika funzo, uelewevu, na utumizi wa mambo ambayo Biblia hufundisha.

Russell alikuwa tofauti na wengi wa marika wake wenye akili ya kufanya mrekebisho katika maana ya kwamba hakuhubiri juu ya njia maalumu ya kumfikia Mungu, hakujisifu juu ya kuwa na njozi au mafunuo ya kimungu, hakuvumbua jumbe zenye kuhusu wachache fulani tu zikiwa kwa namna ya vitabu vilivyofichika au kwa namna yoyote ile, na hakudai kamwe kwamba angeweza kuponya wagonjwa kimwili. Zaidi ya hilo, hakukazania kwamba angeweza kuifasiri Biblia. Akiwa chombo chenye nia ya kutumiwa katika mikono ya kimungu, yeye alikinza vishawishi vyote vya kuruhusu ‘mshumaa wake mwenyewe’ ung’ae kupita nuru ya kimungu.

“Ukweli wala si mwenye kuutumikia ndio upasao kuheshimiwa na kupigiwa mbiu,” Russell akaandika katika 1900, akiongeza hivi: “Kuna elekeo jingi mno la kumsifu mhubiri kwa ajili ya ukweli, kwa kusahau kwamba ukweli wote ni wa Mungu, ambaye hutumia mtumishi mmoja au mwingine katika kuupigia mbiu kama impendezavyo.” Hii ndiyo sababu kuu ambayo hufanya waandikaji na watafsiri wa vichapo vya Watch Tower, na pia washiriki wa New World Bible Translation Committee, wachague kubaki bila kutajwa majina.

Mfalme wa Mungu Atawazwa!

Katika karne ya kwanza, Yohana Mbatizaji alitangaza mtokeo wenye kukaribia wa Yesu akiwa Mfalme mkusudiwa wa Mungu. Katika karne ya 19, wakati ukawa umefika wa kutangaza mtokeo wenye kukaribia wa Mfalme huyo akiwa katika mamlaka ya kimbingu. Kwa hiyo, katika toleo lalo la Machi 1880, Zion’s Watch Tower lilijulisha rasmi hivi: “‘Nyakati za Wasio Wayahudi’ zafika 1914, na ufalme wa kimbingu hautadhibiti mambo kikamili mpaka wakati huo.”

Hivyo, kikundi ambacho leo hujulikana kuwa Mashahidi wa Yehova kilitambulikana peupe zaidi ya miaka mia moja iliyopita juu ya kujulisha kwamba mwaka 1914 ungetia alama mwanzo wa Ufalme wa Mungu. Kutawazwa kwa Mfalme wa Mungu ilikuwa hatua moja ya kwanza kuelekea kuzimwa hatimaye kwa mshumaa wenye kusinzia-sinzia wa dini bandia, ili isiweze tena kuficha nuru ya kimungu.

Karne ya 19 ilipokuwa ikikaribia kumalizika, dini ya Jumuiya ya Wakristo haikuwa na mavazi ya kujitambulisha kuwa mtumishi wa Mungu. Ilistahili kuachiliwa mbali na Mungu. Wakati wayo wa hukumu ulikuwa ukikaribia. Jifunze mengi zaidi juu ya hilo katika toleo letu linalokuja.

[Sanduku katika ukurasa wa 27]

Baadhi ya Watoto “wa Baadaye”

Kanisa la Kristo, Mwanasayansi: Harakati hii ya kidini hujulikana kwa kawaida kuwa Sayansi ya Kikristo. Ilianzishwa katika 1879 na Mary Baker Eddy, aliyekuwa akijali sana afya. Yaripotiwa kwamba nafuu aliyopata akiisha kuwa na aksidenti mbaya sana katika 1866 ilimsadikisha kwamba alikuwa amevumbua kanuni zilizowezesha Yesu kuponya wagonjwa na kuinua wafu. Kitabu chake cha 1875 Science and Health With Key to the Scriptures hufundisha kwamba mambo ya kiroho yapita ya kimwili, kwamba dhambi, magonjwa, kifo, na mambo hasi mengineyo ni maoni ya kuwaziwa tu ambayo yaweza kushindwa kwa kuwa na maarifa ya ukweli na fikira chanya kupatana na Akili, akimaanisha Mungu.

Wanafunzi wa Kristo: Kanisa hili lilifanyizwa katika 1832 na Wapresbiteri Waamerika wenye akili za mrudisho. Shime yao ilikuwa: “Pale maandiko yasemapo, ndipo sisi tusemapo; pale Maandiko yakimyapo, ndipo sisi tukimyapo.” Kichapo kimoja cha marejezo chaeleza watu hao kuwa “wenye uvumilio mwingi wa maoni ya wengine katika mambo ya kimafundisho na ya kidini.” Washiriki waliruhusu siasa ziwagawanye vibaya sana wakati wa ile Vita ya United States ya Wenyewe kwa Wenyewe. Katika 1970 zilikuwako madhehebu 118, kutia na Makanisa ya Kristo yaliyofanyizwa katika 1906.

Jeshi la Wokofu: William Booth alianzisha hiki kikundi cha kidini ambacho kimepangwa kitengenezo kwa kufuata taratibu za kijeshi. Booth aliingia huduma ya Kimethodisti katika miaka yake ya mapema ya 20 na akawa mwevanjeli mwenye kujitegemea katika 1861. Yeye na mke wake walianzisha utume wa kuhubiri miongoni mwa maskini katika East End ya London. Jina la kikundi hicho lilibadilishwa katika 1878 likaacha kuwa Utume wa Kikristo (“Christian Mission”) na kuwa Jeshi la Wokofu. Jeshi la Wokofu hutafuta ‘kuokoa nafsi za watu’ kwa kutoa msaada wa kijamii kwa wasio na makao, wenye njaa, wenye kutendwa vibaya, wenye shida.

Waadventisti wa Siku ya Saba (“Seventh-Day Adventists”): Hii ndiyo kubwa kabisa kati ya madhehebu za Kiadventisti zipatazo 200. Msingi wa jina lazo ni imani katika kule kuja kwa pili au adventi ya Kristo. Shina la Waadventisti ni harakati ya miaka ya mapema ya 1840 ya William Miller mhudumu Mbaptisti wa cheo cha kawaida. Wakifundisha kwamba Amri Kumi zingali zinafanya kazi, Waadventisti wa Siku ya Saba hushika sabato halisi ya Jumamosi. Washiriki fulani hukaribia kuiona kuwa yenye uvuvio wa Kibiblia miandiko ya Ellen Gould White, mmoja wa viongozi wenye uvutano mwingi zaidi wa kikundi hicho, aliyedai kuwa alimulikiwa nuru na mfululizo wa njozi za kimungu.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Jiwe la Rosetta limesaidia kuhakikisha ukweli wa Biblia

[Hisani]

Kwa hisani ya Wadhamini wa British Museum

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki