Kuenea kwa Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi za Kidini
HARAKATI YA KUFUATA KANUNI ZA MSINGI—miongo michache iliyopita upesi, hiyo ilikuwa harakati ndogo tu katika Uprotestanti. Mambo yamebadilika kama nini! Bruce B. Lawrence, mwelezaji juu ya dini, aliandika kwamba miaka 30 iliyopita, ni wachache ambao wangaliona kwamba mwishoni mwa karne ya 20, harakati ya kufuata kanuni za msingia ingekuwa kichwa cha maana sana na hata cha kupita kiasi cha vyombo vya habari na cha utafiti wa vyuo vikuu.
Hata hivyo, hilo ndilo jambo ambalo limetokea. Ripoti za magazeti ya habari juu ya maandamano ya jeuri mitaani, visa vya uuaji kimakusudi, harakati za kupinga utoaji-mimba, werevu mbalimbali wa kisiasa wa vikundi vya kidini vyenye uvutano juu ya umma, na mioto mikubwa ya hadharani ya kuchomea vitabu vionwavyo kuwa vyenye ukufuru, ni vikumbusha vya daima vya matendo ya washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi. Jarida la kila juma la habari za fedha Mondo Economico la Kiitalia lilitaarifu kwamba karibu kila mahali harakati ya kufuata kanuni za msingi “inashambulia kisiasa kwa kutumia jina la Mungu.”
Washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi mara nyingi huonyeshwa kuwa wenye kupita kiasi na washupavu, wakitunga njama mbalimbali na kufanya mashambulio ya kiharamia. Watu wanatiwa hofu na kule kuongezeka kwa vikundi vya aina hiyo kama vile Comunione e Liberazione katika Ukatoliki wa Kiroma, Gush Emunim katika Dini ya Kiyahudi, na Muungano wa Kikristo katika Uprotestanti wa Amerika Kaskazini. Kwa nini harakati ya kufuata kanuni za msingi inaenea? Inachochewa na nini? Je, labda ni “kisasi cha Mungu,” kama adokezavyo mwanasoshiolojia Mfaransa Gilles Kepel?
[Maelezo ya Chini]
a Mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi ni mtu ashikamanaye sana na kanuni za msingi za kidini zenye kuhifadhi mambo na desturi za kale. Maana ya “harakati ya kufuata kanuni za msingi” itazungumziwa zaidi kikamili zaidi katika makala ifuatayo.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 3]
Nina Berman/Sipa Press