Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi za Kidini—Hiyo ni Nini?
HARAKATI ya kufuata kanuni za msingi ilianza wapi? Mwishoni mwa karne iliyopita, wanatheolojia wasioshikamana na desturi za zamani walikuwa wakibadili itikadi zao ili zilingane na uhakiki wa Biblia na nadharia za kisayansi, kama vile mageuzi. Tokeo ni kwamba, uhakika wa watu katika Biblia ulidhoofishwa. Viongozi wa kidini wenye kushikamana na desturi za zamani katika Marekani waliitikia kwa kuanzisha zile walizoita kanuni za msingi za imani.a Mapema katika karne ya 20, walichapisha mazungumzo juu ya kanuni hizo za msingi katika mfululizo wa mabuku wenye kichwa The Fundamentals: A Testimony to the Truth (Kanuni za Msingi: Ushuhuda wa Kweli). Usemi “harakati ya kufuata kanuni za msingi” watokana na kichwa hicho.
Katika nusu ya kwanza ya karne ya 20, harakati ya kufuata kanuni za msingi ilizungumziwa mara kwa mara. Kwa kielelezo, mwaka wa 1925, washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi katika dini walipeleka mahakamani mwalimu wa shule aitwaye John Scopes wa Tennessee, Marekani, katika ile iliyokuja kuitwa kesi ya Scopes. Uhalifu wake ulikuwa nini? Alikuwa akifundisha mageuzi, na hilo lilipingana na sheria ya jimbo. Siku hizo, watu fulani waliamini kwamba harakati ya kufuata kanuni za msingi isingedumu. Mwaka wa 1926, Christian Century, gazeti la Kiprotestanti, lilisema kwamba harakati hiyo ilikuwa “ya kijuujuu tu na si halisi” na “yenye kukosa kabisa sifa za utimizo wenye kujenga au wenye kudumu.” Kadirio hilo lilikosea kama nini!
Tangu miaka ya 1970, harakati ya kufuata kanuni za msingi imekuwa katika habari daima. Profesa Miroslav Volf, wa chuo cha Fuller Theological Seminary, California, Marekani, asema hivi: “Harakati ya kufuata kanuni za msingi za kidini haijadumu tu, bali imesitawi pia.” Leo, maneno “harakati ya kufuata kanuni za msingi za kidini” hutumiwa si kuhusu harakati za Kiprotestanti tu, bali pia kuhusu wale katika dini nyingine, kama vile Ukatoliki, Uislamu, Dini ya Kiyahudi, na Dini ya Hindu.
Itikio kwa Nyakati Zetu
Kwa nini harakati ya kufuata kanuni za msingi yaenea? Wale wanaochunguza harakati hiyo husema kwamba inasababishwa, angalau kwa sehemu, na ugeugeu wa kiadili na wa kidini wa nyakati zetu. Katika miaka ya mapema jamii zilizo nyingi ziliishi katika mazingira yenye uthabiti wa kiadili uliotegemea itikadi za kidesturi. Sasa itikadi hizo zinapingwa au kukataliwa mbali. Watu wengi wenye akili hudai kwamba hakuna Mungu na kwamba mwanadamu yuko peke yake katika ulimwengu wote mzima usiojali. Wanasayansi wengi hufundisha kwamba wanadamu wametokana na mageuzi ya kinasibu, si kutokana na matendo ya Muumba mwenye upendo. Maoni yenye uendekevu yaenea. Ulimwengu unakumbwa na hali ya kupoteza kanuni za kiadili katika sehemu zote za jamii.—2 Timotheo 3:4, 5, 13.
Washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi hutamani sana ule uthabiti mbalimbali wa zamani, na baadhi yao hujitahidi kurudisha jumuiya zao na mataifa yao kwenye ile waonayo kuwa misingi ifaayo ya kiadili na ya kimafundisho. Wao hufanya vyovyote wawezavyo kuwalazimisha wengine waishi kulingana na sheria ya kiadili na utaratibu wa itikadi za kimafundisho ulio “sahihi.” Mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi husadiki kwa uthabiti kwamba yeye yuko sahihi na wengine wamekosea. Profesa James Barr, katika kitabu chake Fundamentalism, asema kwamba harakati ya kufuata kanuni za msingi “mara nyingi huonwa kuwa usemi wenye uhasama na wa kudharau, unaodokeza hali ya kushika sana maoni ya kibinafsi, ushupavu, unyimivu wa ujuzi na ugumu.”
Kwa kuwa hakuna yeyote apendaye kuitwa mwenye kushika sana maoni ya kibinafsi, mshupavu, au mgumu, si wote wanaokubaliana juu ya ni nani aliye mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi na ni nani asiye mshiriki wa harakati hiyo. Hata hivyo, kuna mambo fulani yanayoonyesha tabia za harakati ya kufuata kanuni za msingi katika dini.
Kumtambulisha Mshiriki wa Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi
Kwa kawaida harakati ya kufuata kanuni za msingi kidini ni jaribio la kuhifadhi zile zionwazo kuwa desturi au itikadi za kidini za awali za utamaduni fulani na kupinga ile ionwayo kuwa roho ya kilimwengu ya ulimwengu. Hilo si kusema kwamba washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi hupinga mambo yote yaliyo ya kisasa. Baadhi yao hutumia njia za uwasiliano za kisasa kwa matokeo sana ili kuendeleza maoni yao. Lakini wanapiga vita dhidi ya kufanywa kilimwengu kwa jamii.b
Baadhi ya washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi wanaazimia si kujihifadhia wenyewe tu muundo wa kidesturi wa mafundisho au wa njia ya maisha bali pia kulazimisha wengine waufuate, wapate kubadili miundo ya kijamii ili ipatane na itikadi za washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi. Kwa hiyo, Mkatoliki aliye mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi, hatakazia tu upingaji wa utoaji-mimba. Yamkini atawasonga wanasheria wa nchi yake waendeleze sheria zinazokataza utoaji-mimba. Katika Poland, kulingana na gazeti la habari La Repubblica, ili sheria inayopinga utoaji-mimba ikubaliwe, Kanisa Katoliki liliongoza “‘vita’ ambayo katika hiyo lilitumia mamlaka na nguvu zalo zote.” Katika kufanya hivyo, wenye mamlaka wa kanisa walikuwa wakitenda sawa sana na washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi. Ule Muungano wa Kikristo wa Kiprotestanti katika Marekani hupiga “vita” vya aina hiyohiyo.
Washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi hutambulika hasa kwa masadikisho yao ya kidini yenye msingi imara. Hivyo, Mprotestanti aliye mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi atakuwa muungaji-mkono mwenye kusadikishwa wa ufafanuzi wa halisi wa Biblia, yamkini kutia ndani itikadi ya kwamba dunia iliumbwa katika siku sita halisi. Mkatoliki aliye mshiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi hana shaka zozote juu ya ukamilifu wa papa.
Basi, yaeleweka ni kwa nini usemi “harakati ya kufuata kanuni za msingi” hutokeza maoni ya ushupavu usio wenye kukubali sababu na kwa nini wale wasio washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi huhangaika waonapo harakati ya kufuata kanuni za msingi ikienea. Tukiwa mtu mmoja-mmoja, huenda tusikubaliane na washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi na huenda tukafadhaishwa na werevu wao mbalimbali wa kisiasa na matendo yao yenye jeuri ya mara kwa mara. Kwa kweli, washiriki wa harakati ya kufuata kanuni za msingi wa dini moja huenda wakashtuliwa na matendo ya wale wa dini nyingine! Bado, watu wengi wenye kufikiri wanahangaikia mambo yanayosababisha kuenea huko kwa harakati ya kufuata kanuni za msingi—kule kuongezeka kwa ulegevu wa kiadili, hali ya kupoteza imani, na kule kukatalia mbali hali ya kiroho katika jamii ya kisasa.
Je, harakati ya kufuata kanuni za msingi ndiyo njia pekee ya kuitikia mielekeo hiyo? Ikiwa sivyo, njia nyingine ni ipi?
[Maelezo ya Chini]
a Zile ziitwazo kwa kawaida Hoja Tano za Harakati ya Kufuata Kanuni za Msingi, zilizofasiliwa mwaka wa 1895, zilikuwa “(1) upulizio wa kamili na ukamilifu wa Andiko; (2) uungu wa Yesu Kristo; (3) kuzaliwa kwa Kristo na bikira; (4) ufuniko wa badala wa Kristo juu ya msalaba; (5) ufufuo wa kimwili wa Kristo na kuja kwake kwa pili duniani, kibinafsi na kimwili.”—Studi di teologia (Masomo ya Kitheolojia).
b “Kufanywa kilimwengu kwa kitu” kwamaanisha kukazia mambo ya kilimwengu, badala ya mambo ya kiroho au mambo matakatifu. Mambo ya kilimwengu hayahusiani na dini wala na itikadi za kidini.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Mwaka wa 1926, gazeti la Kiprotestanti, lilifafanua harakati ya kufuata kanuni za msingi za kidini kuwa “ya kijuujuu tu na si halisi” na “yenye kukosa kabisa sifa za utimizo wenye kujenga au wenye kudumu”