Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g90 6/8 kur. 6-9
  • Wenye Ujitoaji kwa Mungu-mwanadamu kwa Nini?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wenye Ujitoaji kwa Mungu-mwanadamu kwa Nini?
  • Amkeni!—1990
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mungu Lakini Mtawala Mara Chache
  • Suala Juu ya Daraka
  • Jambo la Kuhangaisha
  • Maziko ya Aliyekuwa Mungu
    Amkeni!—1990
  • Kanisa na Serikali Huko Byzantium
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2002
  • Kutoka kwa Wasomaji Wetu
    Amkeni!—1991
  • Ukristo wa Mapema na Serikali
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1990
g90 6/8 kur. 6-9

Wenye Ujitoaji kwa Mungu-mwanadamu kwa Nini?

KINA cha ujitoaji kwa maliki wakati na kabla ya Vita ya Ulimwengu ya 2 chaweza kuwa vigumu kwa wengi kuelewa leo. “Picha ya Hirohito iliwekwa kwenye kihekalu maalum shuleni,” akumbuka Mitsuko Takahashi, “na kila asubuhi wanafunzi walipaswa kusimama na kufanya kitendo cha ibada kuelekea kihekalu hicho.”

“Maliki alipopita,” akumbuka Masato Sakamoto, “tulipaswa kuinamisha vichwa vyetu chini sana. Tuliaminishwa kwamba maliki alikuwa mwenye kutisha mno kwa binadamu wa kawaida kumtazama ana kwa ana.” Kwa kweli, watoto waliambiwa kwamba wangepofushwa kama wangetazama uso wake.

Viongozi wa kijeshi na wa kisiasa wa Japani walitumia mfumo huo wa kielimu kuingiza fundisho la ujitoaji kwa maliki. “Nilifunza wachanga, ‘Mwe na nia ya kufa,’” asema Kazuo Matsumoto, ambaye miaka yake 50 ya kufundisha ilitia ndani kipindi cha vita. “Niliwapeleka vijana wengi kwenye uwanja wa pigano. Siwezi kusahau lawama hiyo ya wakati wangu uliopita.”

Vijana wa Japani waliambiwa kwamba raia za maliki walikuwa aohitogusa, au “magugu ya kibinadamu yenye kukua,” na kwamba walipaswa kumhami kwa kutumika kuwa ngao yake. Toshio Mashiko, aliyeshiriki katika mashambulizi ya ujiuaji katika Ufilipino na akayaokoka, alieleza: “Tulifunzwa kwamba kufa kwa ajili ya maliki kulikuwa ndiyo heshima kubwa zaidi kwa raia zake.”

Kwa kweli wengi waliamini uwezo wenye kuokoa wa maliki, kwa hiyo walijibwaga kwenye pigano bila hofu yoyote. Kwa kielelezi, Shunichi Ishiguro, alidhani kwamba risasi zingebanduka kwenye mwili wake kwa sababu yeye alikuwa askari-jeshi wa ambacho watu walifunzwa kuwa ni “Taifa la Kimungu.”

Japani ilipokuwa inaelekea kabisa kushindwa vita, mvulana mchanga, Isamu, alimweleza mamake hisia zake za wasiwasi. “Usiwe na wasiwasi,” mamake Mshinto akamhakikishia, akirudia maoni yaliyoshikiliwa na wengi: “Hatutashindwa kamwe kwa sababu kamikazea (upepo wa kimungu) utapeperusha maadui wetu.”

Mungu Lakini Mtawala Mara Chache

Ibada ya maliki ina historia ndefu katika Japani, ikiwa ni sehemu ya maisha za watu kwa zaidi ya maelfu ya miaka. Na utamaduni wa kidini ni mgumu kuondoa. Kwa kielelezo, hata katika Jumuiya ya Wakristo watu husema: ‘Kama dini yangu ilifaa wazazi wangu, yanifaa mimi.’ Na, ‘Kila mtu anaamini hilo, na wote hawawezi kuwa wanakosea.’ Lakini katika karne nyingi zilizopita, mamia ya mamilioni ya watu wamekosea kuamini kwamba viongozi walikuwa wa kimungu! Chunguza, kwa ufupi historia ya maliki Mjapani.

Fungu lake katika muda wa karne nyingi limetofautiana sana. “Maliki alidhaniwa kuwa na nguvu za kimwujiza za kutuliza au kufanya maombezi kwa miungu,” chaeleza Kodansha Encylopedia of Japan. “Lakini kwa sababu ya hofu kubwa iliyohusianishwa na utu wake, pia ilionwa kuwa haifai maliki ajishughulishe na mambo ya kilimwengu ya serikali. Shughuli hiyo, kutia ndani kufanyiza sera na kuzitekeleza, ilikuwa juu ya mawaziri waliotumikia maliki.”

Kwa hiyo maliki hasa alitumika katika kazi ya kikuhani, si ya kisiasa. “Kipindi kikubwa cha pekee cha historia ya Japani ambacho maliki aliunganisha kazi zote mbili kwa maana halisi,” yasema ensaiklopedia iliyotajwa juu, “kilikuwa kuanzia utawala wa TENJI katika nusu ya baadaye ya karne ya 7 hadi utawala wa KAMMU kwenye mwisho wa karne ya 8 na mwanzo wa karne ya 9.”

Isipokuwa kwa wakati huo hasa, wamaliki Wajapani kwa kweli hawakutawala. Baada ya karne ya tisa, uwezo wa maliki ulipungua, na, baada ya muda, shogun, jina linalomaanisha “kamanda wa jeshi,” akaja kuwa mwenye mamlaka ya kisiasa. Ingawa kinadharia maliki alimteua shogun, shogun ndiye aliyekuwa mtawala halisi. Lakini ndipo, baada ya karne nyingi za kutawala Japani, serikali ya shogun ilimrudishia maliki mamlaka mnamo 1867.

Katika mwaka huo Maliki Meiji, babu yake Hirohito, alifanywa mtawala wa Japani. Baadaye aliwapa raia zake katiba iliyosema kwamba maliki alikuwa “mtakatifu na asiye wa kushambuliwa.” Lakini ajabu ni kwamba maliki ajapopewa mamlaka ya kisiasa, hakupewa uwezo wa kisiasa. Yeye alitawala lakini kikweli hakutawala.

Katiba ilisema: “Mawaziri wahusika wa Serikali watatoa shauri lao [na msaada] kwa Maliki na daraka litakuwa lao.” Kulingana na Kodansha Encyclopedia, “kwa ukamili hilo lilimaanisha kwamba daraka la kisiasa halikuwa la maliki bali la mawaziri wake.”

Kwa hiyo mawaziri wa serikali ndio waliokuwa hasa na mamlaka ya kisiasa. Hata hivyo, maliki, alionyeshwa kwa akina yahe kuwa mungu mwenye mamlaka kamili juu ya taifa. Kwa hiyo, jamii yenye kutawala ilitumia uungu wa maliki wa kitamaduni na wa kirasmi kutiisha akina yahe. Vita ambavyo Japani ilipigana katika karne hii ya 20 vilipigwa katika jina la maliki. Na kwa ujumla watu waliamini kwamba yeye alikuwa mungu mwenye nguvu za kimwujiza.

Hata hivyo, kwa kushangaza wengi, Hirohito kwa wazi hakuamini uungu wake mwenyewe. “Sijapata kamwe kujifikiria kuwa mungu,” aliambia maamiri-jeshi Waamerika baada ya vita ya ulimwengu ya pili. Baada ya kukanusha “wazo bandia kwamba Maliki ni mungu na kwamba watu Wajapani ni bora zaidi ya wale wa rangi nyinginezo,” anaripotiwa kuwa alimwuliza mkeye hivi: “Je! unaona tofauti yoyote? Je! mimi naonekana kuwa binadamu zaidi kwako sasa?”

Bila shaka, Wajapani wengine pia waliona hicho kilikuwa kibandiko cha uungu na wakatambua ukweli. Walisababu kwa msingi wa kizibiti. Kwa kielelezo, Minoru Yamanaka, aliyetumikia kwa miaka minne katika jeshi la maliki, alieleza: “Babake maliki alikufa mwenye umri wa 47 na babu yake mwenye umri wa 59, mapema zaidi ya wengine wengi. Kwa hiyo mimi sikudhani kamwe kwamba maliki alikuwa Mungu›”

Suala Juu ya Daraka

Ugonjwa na kifo cha Hirohito vilizusha tena lile suala lenye kuleta ubishi: Maliki alikuwa na daraka gani kwa ajili ya uchokozi wa kijeshi wa Japani? Kwa wazi maoni ya walio wengi ni kwamba Hirohito, akiwa mtu binafsi, alipinga vita hiyo lakini kwamba alikuwa na wajibu wa kuunga mkono maamuzi ya mawaziri wake. Kwa hiyo, kuhusu mipango ya mawaziri wake ya kushambulia United States mnamo 1941, yeye alidai: “Singeliweza kutangua maamuzi yao. Mimi naamini kwamba hilo lilikuwa linapatana na maandalizi ya Katiba ya Kijapani.”

Kwa upande mwingine, Hirohito alichukua hatua ya kwanza na akafanya uamuzi amri isalimiwe mawaziri wake walipokuwa wamegawanyika juu ya suala hilo. Halafu, siku chache baada ya uamuzi huo kufanywa, mnamo Agosti 15, 1945, raia wake walishtuka kusikia sauti yake kwa mara ya kwanza alipotangaza kusalimu amri kwenye radio ya kitaifa. Alitoa wito kwao “wachukuliane na yasiyochukulika na kuvumilia yasiyovumilika.”

Miezi mingi baadaye, serikali ya Uingereza ilitangaza: “Kombora la kiatomi silo lililofanya Wajapani wasalimu amri, ilikuwa ni amri iliyoandikwa ya Maliki ya kuwaamuru wafanye hivyo. Pasipo hilo tungefanya uvamizi wenye kugharimu.”

Kwa hiyo, kulipokuwapo vilio vya baada ya vita kuwa Hirohito ashtakiwe kama mhalifu wa vita, Jenerali Douglas MacArthur, kamanda wa U.S. wa Mwungano wa uvamizi wa Japani, alikinza kwa uimara. Baadaye yeye alieleza: “Niliamini kwamba kama Maliki huyo angeshtakiwa jinai, na labda anyongwe, serikali ya kijeshi ingeanzishwa katika Japani yote, na vita vya waasi vingeanza.”

MacArthur alikutana na Hirohito katika Septemba 26, 1945, akaguswa moyo. Badala ya kujaribu kuepa daraka la vita, maliki alikubali “kuwa jukumu lote la kila uamuzi wa kisiasa na kijeshi uliofanywa na kutekelezwa na watu [wake] katika mwenendo wa vita lilimkalia.”

Lakini, labda walio wengi katika Japani leo hawamlaumu Hirohito kwa ajili ya vita ambayo kwa wazi ilihimizwa na mawaziri wake. Kwa hiyo, wakati maliki huyo alipokuwa amelala penye kitanda chake akifa mwaka juzi, Hitoshi Motoshima, meya wa Nagasaki, alichokora wengi wakaudhika kwa kuthubutu kusema hadharani: “Kutokana na niliyojionea mwenyewe pamoja na elimu ya kijeshi, nafikiri maliki ana daraka kwa ajili ya vita.”

Motoshima alisema kwamba akiwa ofisa wa jeshi ambaye alifundisha askari wapya wakati wa vita, yeye “alilazimishwa kuwaambia watu wafe katika jina la Maliki.” Kwa wazi Motoshima anahisi, kama vile wengine, kwamba sauti ya maliki aliyekuwa anaabudiwa na raia wake ingelikuwa na uzito mkubwa kama ingeliinuliwa kupinga vita hiyo.

Jambo la Kuhangaisha

“Lakini,” wengine wanasema, “yote hayo yamepita.” Yaweza kuwa hivyo, lakini imani za kitamaduni hazitoweki rahisi. Kwenye kihekalu cha Shinto maarufu kule Ise katika Japani ya kati, hivi karibuni kuhani wa Shinto alisema: “Watu wengi hapa wamekuja kuabudu mungu-mke jua kuwa mzazi wa kale wa Maliki wetu na mbari yetu ya Kijapani.”

Kiasi cha kumcha maliki kinaelezwa na vitisho vya kumwua Motoshima kwa ajili ya maneno yake juu ya daraka la maliki huyo kwa ajili ya vita. Mwanamume mmoja alikamatwa akijaribu kuvunja aingie katika ofisi ya Motoshima akiwa na kopo la petroli, na karibu malori mia moja yenye vipaaza sauti yalifunga barabara za Nagasaki yakitangaza, “Kifo kwa Motoshima.” Kicho kwa maliki kimeonyeshwa pia kwa njia nyinginezo.

Kwa kielelezo, wakati Hirohito alipokuwa mahututi, nchi yote ilijiepusha kufanya mambo mengi. Sherehe na karamu zilifutwa, hilo likaathiri biashara inayoshughulikia pindi za furaha. Watoto wa shule walilazimishwa wavunjilie mbali mashindano yao ya riadha. Hata Yakuza, au majambazi, waliacha kupigana na kutupa risasi. Maisha katika Japani yaliathiriwa sana, na kusababisha The Daily Yomiuri liseme kwamba “nchi imehuzunikia kupita kiasi maradhi ya Maliki.”

Wengine walishtuliwa na ujitoaji huo wa kupita kiasi. Lakini hata kama hawakukubaliana na hilo, kwa ujumla waliuachilia na kuuendekeza, labda wakifikiria matokeo mabaya kama wasingefanya hivyo. “Kufuata mambo kama yalivyo kufikia hatua hii ndilo jambo salama zaidi,” akasema msaikolojia mmoja. Lakini mmoja aliyekuwa askari-jeshi wakati mmoja aliomboleza hivi: “Watu wanatazama huku na huku tu na kufuata yale ambayo wengine wanafanya. Mtazamo huo huo ndio uliotuchokora sisi kuingia vitani.”

Lakini je! jinsi tunavyojiendesha, na hasa tunayeabudu, vyapasa kuongozwa tu na tabia na ibada ya wale wanaotuzunguka? Fikiria mamilioni ambao imani zao za kidini zisizo na msingi zimewafanya wapoteze maisha zao katika vita visivyo na sababu! Kwa wazi kufuata kiupofu umati kwaweza kuleta msiba. Kufikiria matukio hayo yaliyopita kwapasa kutufundishe kwamba kuabudu ‘tusichojua’ kweli kweli kwaweza kuleta msiba. (Yohana 4:22) Basi, jinsi lilivyo jambo la maana tuchunguze kama tunaabudu tunachojua kweli kweli!

[Maelezo ya Chini]

a Washiriki wa jeshi la hewani la Kijapani waliofanya mashambulizi ya kujiua kwenye lengo (kama merikebu) pia waliitwa kamikaze.

[Picha katika ukurasa wa 8, 9]

Maelfu walikufa katika jina la maliki

[Picha] Hirohito alikiri kwake Jenerali Douglas MacArthur daraka lake kwa ajili ya vita

[Hisani]

Juu: Foto rasmi ya Jeshi la Wana-maji wa U.S. Kulia: Jeshi la Nchi Kavu la U.S.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki