Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Misiba Niliudhiwa sana na makala yenu iliyozungumzia misiba ya tufani na tetemeko la dunia. (Desemba 8, 1990) Mlitaja kisa kimoja cha kuteka vitu kuwa mfano wa tofauti kati ya “walimwengu” na Mashahidi wa Yehova. Nahisi kuwa ni vibaya sana kuonyesha Mashahidi pekee kuwa ndio wenye sifa nzuri mno.
J. K., United States
Makala hiyo ilitumika kuonyesha jinsi Wakristo leo wanavyoonyesha upendo wa kweli kwa mmoja na mwenzake nyakati za majaribu, kama walivyofanya katika karne ya kwanza. (2 Wakorintho 8:1-4) Ingawa matendo yasiyostahili yaliripotiwa, makala hiyo pia ilitaja kwamba “vitendo hivyo vya moyo mkavu vilifunikwa na vitendo vingi vya fadhili na huruma za kibinadamu.”—MHARIRI.
Wazazi Wanaopigana Nilisoma makala “Vijana Wanauliza . . . Nifanye Nini Wazazi Wangu Wakipigana?” (Oktoba 8, 1990) Ingawa mimi si kijana sana tena, naweza kukumbuka jinsi wazazi wangu walivyokuwa wakipigana kila mara. Familia nzima inaweza kuumia wazazi wanapopigana. Lakini sasa naelewa kwamba unazidisha umizo hilo unapounga mkono upande mmoja kama nilivyofanya. Asanteni sana kwa makala hiyo.
G. H., Uholanzi
Ushetani Natoa shukrani za kina kirefu kwa ajili ya ile makala juu ya Ushetani. (Septemba 8, 1990) Mama yangu alijionyesha kuwa mtu mzuri nje-nje, na watu wengi walimwona kuwa mwema. Hata hivyo, alikuwa katika kikundi kilichokuwa na mazoea ya ushetani. Mimi nilitumiwa vibaya kingono na katika utumiaji mbaya wa dawa za kulevya. Baada ya miaka mingi ya kuteseka, nilijaribu hata kujiua. Kwa vyovyote, sikujiunga naye katika matendo ya kishetani, na baadaye nikawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Hilo lilikuwa pigo kubwa kwa mama yangu kwa sababu anatambua kwamba hakuna uwezo mkuu kushinda Yehova Mungu.
A. M., United States
Historia ya Kidini Baada tu ya kumaliza makala ya mwisho ya mfululizo wa “Wakati Ujao wa Dini kwa Kutegemea Wakati Wayo Uliopita” (Desemba 8, 1990), ni lazima niandike nikiwaeleza jinsi nilivyothamini sana mfululizo huo. Nimejifunza mengi kama nini kuhusu Ubudha, Uhindu, Ukonfyushasi, na dini nyingine nyingi! Ukuzi wa Jumuiya ya Wakristo kufikia wakati wa leo hasa ulikuwa ukipendeza. Siyo tu kwamba naweza kuona kadiri Jumuiya ya Wakristo imejiingiza katika vita na umwagaji wa damu bali pia naweza kutambua kwa uwazi zaidi pendeleo la kuwa tayari nimepata dini ya kweli.
G. V., Jamhuri ya Muungano ya Ujeremani
Makala ya kumalizia katika mfululizo wenu ilikuwa moja ya makala bora zaidi ambazo nimepata kusoma katika Amkeni! kwa miaka karibu 40 ambayo nimekuwa nikiisoma. Makala hiyo ilikuwa sawa katika kueleza ‘njia za uwongo, udanganyifu, hila, na chuki ambazo zimeipa dini bandia sura mbaya machoni pa Mungu na binadamu pia.’
M. M., Uhispania
Njia Kumi za Kuacha Kuvuta Sigareti Nimevuta sigareti kwa miaka 40 na nimejaribu kuacha kuvuta kwa njia kadhaa kama kwa utibabu wa kuchomekwa-chomekwa visindano mwilini, kutiwa katika utulizo wa akili ili kudhibitiwa fikira, aina nyingi tofauti-tofauti, kwa hivyo picha yenu iliyokuwa katika ukurasa wa kwanza ya fuvu la kichwa likivuta sigareti iliniathiri sana. (Machi 8, 1990) Kwa msaada wa sala, nitaacha kuvuta.
B. H., United States
Nina umri wa karibu miaka 15. Mwalimu wetu alituomba tufikirie sababu kumi za kutovuta sigareti na tutokeze mawazo kumi juu ya jinsi ya kuacha kuvuta. Makala ya Amkeni! ilinisaidia sana kwa sababu ilikuwa ni mimi tu niliyepata majibu kwa maswali yote. Mwalimu akanipongeza na kunipa alama nzuri.
S. C., Ufaransa