Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Ni Mungu wa Vita? Asanteni kwa makala nzuri katika Amkeni! la Novemba 8, 1993, “Maoni ya Biblia . . . Je! Yehova ni Mungu wa Vita?” Watu wengi wameuliza swali hilo kwa miaka mingi. Mara kwa mara tulikuwa tukilizungumzia tukiwa familia. Makala yenu, pamoja na utafiti mwingine niliofanya, imenisaidia kupata majibu ya maswali yangu.
S. T., United States
Kunyonyesha Matiti Tulifurahia kusoma makala “Uthibitisho wa Mafaa ya Maziwa ya Mama.” (Septemba 22, 1993) Mke wangu ananyonyesha mtoto wetu wakati huu. Hata hivyo, makala hiyo haikutaja kwamba kunyonyesha mtoto humchosha sana mama. Labda si wanawake wote wawezao kunyonyesha watoto wakati wa usiku. Kwa kielelezo, katika hali yetu, mke wangu akipata usingizi mchache sana, hali huwa ngumu sana kwake.
T.K., Ujerumani
Asante kwa maoni yako. Makala za awali zimetaja baadhi ya magumu ambayo wale wanaokuwa mama kwa mara ya kwanza wanaweza kupata kuhusiana na kunyonyesha matiti. Kwa kielelezo, ona “Amkeni!” la Juni 8, 1983, Kiingereza, na Machi 22, 1986, Kiingereza.—Mhariri.
Ni Kupita Kiasi? Ningependa kuwashukuru kwa makala “Vijana Huuliza . . . ‘Kupita Kiasi’ Kwafikia Wapi?” (Oktoba 22, 1993) Nimekuwa Mkristo aliyebatizwa kwa karibu mwaka mmoja sasa, na mara nyingi nimejiuliza juu ya maoni ya Yehova juu ya jambo hilo. Nathamini sana kwamba mlishughulikia habari hiyo. Hata ingawa haitakuwa rahisi, nimeazimia kuishi kulingana na viwango vya Yehova.
C. S., United States
Nimekuwa nikitafuta makala kama hiyo kwa miezi kadhaa. Nimekuwa na urafiki na mvulana mmoja kwa miezi tisa, na makala hiyo ilipowasili, nilimpigia mvulana huyo rafiki yangu simu. Asanteni sana kwa kutufundisha juu ya mambo hayo yasiyotajwa sana na yaliyo magumu.
A. P. G. S., Brazili
Nawashukuru sana kwa moyo wangu wote kwa ajili ya makala hiyo. Ilikuja wakati nilipoihitaji kabisa. Nina miaka 16, na kuna mvulana ninayempenda. Nilifikiria kufanya urafiki naye. Bila shaka, nilijua kwamba ni makosa kufanya uasherati, lakini nilihisi kwamba kupiga busu na kukumbatiana hakukuwa kupita kiasi. Lakini kulingana makala hiyo, naweza kuona kwamba mpaka nifikie umri wa kuweza kuolewa, kufanya mambo hayo ni kupita kiasi!
M. H., Japani
Mimi si kijana, lakini ningali mseja, na nimepata kuuliza swali ilo hilo. Nimekuwa na urafiki na mtu fulani, na nikiwa mhubiri wa wakati wote, napaswa kujua jibu. Lakini unapojihusisha na mtu kihisia-moyo, uwezo wako wa kuamua mambo hudhoofika. Makala hiyo ilikuja kwa wakati ufaao kabisa na imenisaidia sana kuzungumza na yule Mkristo ninayefanya urafiki naye. Tumeisoma tukiwa pamoja na twataka kufanya mambo kwa staha mbele ya wote.
M. R., United States
Nilikuwa nikisali nipate maelezo juu ya suala hilo. Nilipoona kichwa cha makala hiyo, moyo wangu ‘ulishtuka.’ Nilisoma kwa tamaa kubwa makala hiyo, na sasa najua kabisa jinsi nipasavyo kuenenda.
S. G., Italia
Tiba Isiyohusu Damu Nataka kuwashukuru sana kwa makala “Mashahidi wa Yehova na Wastadi wa Tiba Washirikiana.” (Novemba 22, 1993) Nilipokuwa nikiisoma, machozi ya uthamini yalinijaa machoni. Makala hiyo ilielezea baadhi ya kazi ngumu ambazo wengi wetu hawajui kwa sababu hatujapata tatizo kama hilo wakati wowote. Lakini kwa wale baadhi yetu ambao huenda siku moja wakakabili mtihani wa imani yetu kuhusu suala la damu, inafariji sana kujua kwamba ndugu zetu wanafanya kazi kwa bidii kwa niaba yetu.
B. B., United States