Kutoka kwa Wasomaji Wetu
Kadi za Mkopo Nilifurahia hasa makala “Kadi za Mkopo—Je! Uzitumie?” (Desemba 8, 1993) Miaka kadhaa iliyopita, mke wangu nami tulijipata katika deni lenye kushusha moyo la kadi za mkopo lililochukua muda mrefu kulipa, hata baada ya sisi kuharibu kadi zetu. Hata hivyo, kwa ajili tu ya kuwa msaada kwetu, hivi karibuni tumepata kadi mpya. Makumbusho yenu ya wakati ufaao juu ya kadi za mkopo na hatari zazo yametusaidia kuazimia tusiitumie vibaya wakati huu.
M. B. na D. B., Marekani
Hadithi za Wanyama Asanteni kwa makala juu ya dubu-barafu yenye kichwa “Madubwana Wenye Kuvutia wa Kaskazini mwa Kanada.” (Desemba 8, 1993) Makala hiyo iliandikwa vizuri sana. Mambo hakika yaliyoelezwa yalinifanya nithamini kwelikweli jinsi Yehova alivyofanya jambo la upendo kuumba wanyama ili tuwafurahie.
D. C., Marekani
Makala yenu “Tandala Afanya Simba Waaibike” (Novemba 22, 1993) ilichekesha. Ningeweza kuwazia tandala-dume mwenye ghadhabu na aibu akijaribu kupiga kwa nguvu tandala huyo wa shaba nyeusi asiyesogea. Na jinsi alivyofanya kikundi cha simba kitoroke—ilichekesha sana! Yaonyesha kwamba Yehova apenda ucheshi.
A. L., Marekani
Nilisisimuliwa na jinsi mlivyochanganua mada “Kutafuta Siri za Mkunga.” (Oktoba 22, 1993) Viumbe hao waonyesha ukweli wa masimulizi ya Biblia juu ya uumbaji na kukataa majaribio yote ya kuthibitisha nadharia ya mageuzi.
C. S. S., Brazili
Nina miaka 11, na nilipenda sana lile dondoo katika “Kuutazama Ulimwengu” lililoitwa “Ibada ya Panya.” (Novemba 8, 1993) Makala hiyo ilieleza kwamba makasisi kwenye hekalu nchini India huamini kwamba wanapokufa, wao hupata wokovu kwa kuzaliwa tena wakiwa panya! Wao husema kwamba wao si panya hasa, bali ni wajumbe kutoka kwa Mungu. Inashtua!
E. L., Marekani
Sikukuu Nataka kuwashukuru sana kwa mfululizo, “Sikukuu—Sababu Inayofanya Watoto Fulani Wasizisherehekee.” (Novemba 22, 1993) Ile sehemu “Sisi Hatunyimwi!” ilinifanya nitoe machozi. Nyakati nyingi mimi huhisi niko peke yangu ninapoeleza itikadi zangu kwa wanashule wenzangu, na makala hii ilinisaidia ning’amue kwamba kamwe sijakuwa peke yangu na daima sitakuwa peke yangu.
B. P., Marekani
Kwa kadiri niwezavyo kukumbuka, sijasherehekea Krismasi. Kuna nyakati ambapo nimewaonea wivu watoto wengine. Na kabla tu makala hii haijatoka, nilialikwa kwenye karamu ya Krismasi. Nilikataa na nikajaribu kueleza sababu kutokana na yale niliyojua tayari. Lakini kwa kuona jinsi Krismasi, ambayo imekuwa sherehe ya kila mwaka hata nchini Japani, ilivyo sherehe ya kipagani yenye ushirika wa kimashetani, nahisi mwenye uhakika kwamba nilifanya yale yaliyofaa.
K. I., Japani
Maisha Maradufu Asanteni kwa kuchapisha makala “Vijana Huuliza . . . Kuishi Maisha Maradufu—Kwa Nini Nisifanye Hivyo?” (Desemba 22, 1993) Nina miaka 15 na nimelelewa kuwa Mkristo. Lakini sijakuwa nikiendelea vizuri, na kila wakati naona kwamba naelea mbali na kweli hatua kwa hatua. Mojawapo sababu zangu ni kwamba wazazi wangu ni wakali kupita kiasi, na mara nyingi mimi huwa na hamu ya kufanya jambo fulani ambalo wamekataza, hata ikiwa najua halifai. Niliposoma makala hiyo, niling’amua kwamba Yehova Mungu alikuwa akiniletea msaada. Nilijua kwamba si mimi pekee niliyefanya mambo bila wazazi wangu kujua. Lakini nilipoendelea kusoma, nilishangaa kuona jinsi wengine walivyohisi kama mimi. Najua haitakuwa rahisi, lakini natumaini kubadili mtindo-maisha wangu kwa msaada wa Yehova.
K. J., Marekani