Maoni ya Biblia
Sala Katika Michezo—Je! Mungu Husikiliza?
HEWA ina kelele za msisimuko huku maelfu ya mashabiki wakimiminika kuingia stediamu, wakipiga mayowe kuunga mkono timu yao waipendayo. Ndipo tu wachezaji wamemaliza mazoezi yao ya kupasha mwili joto, na karibu kipenga cha kuanzisha mchezo kipulizwe. Kwenye upande mmoja wa uwanja, wachezaji wamejikunyata pamoja, na katikati kapteni amepiga magoti, naye asali hivi: “Mungu, tafadhali bariki timu yetu, utupe ushindi juu ya mpinzani wetu, na utulinde na majeraha. Amina.” Songamano hilo latawanyika kwa kupaaza sauti, nao wachezaji wachukua nafasi zao uwanjani, kipenga chapulizwa, kisha yaanza patashika ya mpira wa miguu wa Kiamerika.
Sala ya watu mmoja mmoja na ya timu kwa ujumla kabla ya, na wakati wa, na baada ya kushiriki katika michezo mbalimbali imekuwa tamasha ya kawaida. Lakini je! Mungu husikiliza? Au kama vile wengine hukazania, je! huko ni kudhihaki sala?
‘Mponde-ponde Jirani Yako’
Kotekote ulimwenguni, karibu kila mchezo huharibiwa na jeuri—katika uwanja na katika mabanda ya utazamaji. Mchezaji mmoja wa mpira wa miguu aliyekuwa wa kulipwa hapo zamani katika United States aliandika hivi: “Ni jambo liwezalo kufanyiwa ubishi juu ya kama lengo hasa la mpira wa miguu ni kuvunja-vunja mwili, kama vile kuua na kulemaza mwili kulivyo lengo la vita.” Yeye azidi kueleza hivi: “Majeraha yafanywayo kwa kushindana na kwa njia iliyopangwa ni sehemu kuu ya njia yetu ya maisha, na mpira wa miguu ni kimoja cha vielelezo vyenye kufahamika zaidi . . . vinavyotuonyesha jinsi lilivyo jambo la kusisimua na kuthawabisha Kumponda-ponda Jirani Yako.”
Eti kuponda-ponda jirani yako? Yesu alisema upende jirani yako. (Mathayo 22:39) Haiwezekani kuwazia Mungu wa upendo akiwapo na kubariki mmoja wa michezo ya leo, wenye kukazia kupata ushindi kwa njia yoyote ile.—1 Yohana 4:16.
Je! Mungu Huhudhuria Michezo?
Jambo moja linalotia moyo kusali katika michezo ni lile fundisho la kidini kwamba Mungu yuko kila mahali na katika vitu vyote nyakati zote. Kwa kielelezo, katika kitabu God Goes to Football Games (Mungu Huenda Kwenye Michezo ya Mpira wa Miguu), kasisi ambaye alikuwa chapleni wa michezoni hapo zamani, L. H. Hollingsworth, asema hivi: “Kila imani rasmi tushikiliayo juu ya Mungu hutia ndani wazo la kuwapo Kwake kila mahali; ikiwa yakupendeza, lile wazo la kwamba kwa uhakika Yeye yupo katika kile tukiitacho matukio yetu ya kilimwengu . . . Ndiyo kusema, Mungu huenda kanisani, na Mungu huenda kwenye michezo ya mpira wa miguu.”
Hata hivyo, Biblia haifundishi kwamba Mungu yuko kila mahali. Mtume Mkristo Paulo aliandika hivi: “Kristo . . . aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni pa Mungu kwa ajili yetu.” (Waebrania 9:24) Kuna mambo muhimu mawili ambayo andiko hilo latusaidia kuthamini: kwamba Mungu ni mtu-roho na kwamba ana mahali thabiti pa kukaa, mbinguni. (1 Wafalme 8:49; Yohana 4:24) Kwa hiyo hangeweza kuwa mahali pengine popote wakati ule ule mmoja.
Mungu Huwasikia Rafiki Zake
Basi, ikiwa Mungu hahudhurii michezo, je! angalau yeye husikiliza zile sala? Ili sala zifikie masikio yanayosikia ya Mungu huyu wa mbinguni, ambaye Yesu alitokea mbele zake, ni lazima anayesali awe na maarifa, maarifa juu ya makusudi ya Mungu, utu wake, sifa zake, njia zake, na jina lake. (Yakobo 4:3) Akikazia uhitaji wa kumjua Mungu, Yesu alisali hivi: “Uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3.
Kupata kumjua mtu hutaka mawasiliano. Mungu huwasiliana na binadamu kupitia Biblia, na Biblia ndiyo njia ambayo kwayo sisi hupata kumjua Mungu wa mbinguni. Hutuambia jina lake, Yehova. (Zaburi 83:18) Pia Biblia husema kwamba Mungu aliupenda sana ulimwengu hata akatuma Mwana wake mzaliwa wa pekee, Yesu, hapa duniani ili binadamu awe na fursa ya kupata uhai wa milele. (Yohana 3:16) Tusomapo na kujifunza Biblia, Yehova huwa halisi kwetu, nasi huvutwa kwake kupitia Yesu. (Yohana 6:44, 65; Yakobo 4:8) Kwa sababu Yehova ni halisi, sisi twaweza kusitawisha uhusiano wa kibinafsi wenye ukaribu pamoja naye.
Hata hivyo, urafiki pamoja na Mungu wahusisha ndani mawasiliano ya pande mbili. Hiyo hutaka kuongea na Yehova kupitia sala. Biblia husema kwamba Mungu ni “Msikiaji wa sala” na kwamba “hawi mbali na kila mmoja wetu.” (Zaburi 65:2, NW; Matendo 17:27) Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba Mungu husikiliza sala zote. (Isaya 1:15-17) Mungu ana nia ya kusikiliza sala za nani?
Mtunga zaburi Daudi alisema hivi: “Uhusiano wa kindani pamoja na Yehova ni wa wale wenye kuhofu yeye.” (Zaburi 25:14, NW) Katika Kiebrania cha awali, mzizi wa “uhusiano wa kindani” (sohd) humaanisha “kukazilia.” Hivyo basi, mstari huu una wazo la kupewa ruhusa ya kuingia katika mzingo wa kindani wa Yehova au katika agano la urafiki pamoja naye. Ni waabudu wale tu waonyeshao staha ambao hukubaliwa waingie. Hivyo, urafiki wetu wa kindani pamoja na Mungu husababisha tuhofu kuvunja uhusiano huo kwa kufanya jambo lolote ambalo halingempendeza, kama vile kuchukua sala kama hirizi ya bahati nzuri ya kuhakikishia ushindi michezoni.
Yehova husikiliza sala za watu wenye mioyo ya ufuataji haki wanaotafuta urafiki pamoja naye, naye hana upendeleo. Yeye haonyeshi upendeleo wala haheshimu kikundi kimoja cha kitaifa, rangi, au hata timu ya michezo, kupita nyingineyo. (Zaburi 65:2; Matendo 10:34, 35) Kama Mungu angesikia sala za washindani wa michezo na timu zote mbili zisali kwake ili zipate ushindi, angepaswa kubariki ipi? Au kama mchezaji angejeruhiwa vibaya wakati wa mchezo, je! Mungu ndiye angelaumika?
Kwa hiyo, ni lazima sisi tusali kwa ajili ya mambo yafaayo. Mtume Yohana hueleza jambo hilo hivi: “Tukimwomba chochote kadiri ya mapenzi yake, yeye hutusikiliza.” (1 Yohana 5:14, HNWW) Yehova husikiliza sala ambazo zapatana na mapenzi yake. Sisi twahitaji kujua mapenzi na makusudi yake ili sala zetu zipatane na mambo hayo.
Mapenzi na makusudi ya Mungu na jina lake tukufu hayashirikiani na michezo ya leo iliyo na ushindani na jeuri. Mungu hana upendeleo. Hivyo, sala zitolewapo kwenye michezo hiyo, je! Mungu anasikiliza? Sivyo hata kidogo!