Thamani Zinazobadilika Wakati Historia Inapopita
“MFUMO wa sheria ambazo binadamu hufuata (au apaswa kufuata) katika maisha yake ya kibinafsi na maisha yake ya kijamii.” Hivyo ndivyo Encyclopædia Universalis ya Kifaransa ifasilivyo neno “maadili.”
Kwa kweli fasili hii yatumika kwa kila mtu. Yahusisha ndani mwamini afuataye kanuni za dini yake na pia mtu asiyeshikamana na mfumo wowote wa tabia au dini lakini aliye na kanuni fulani ziongozazo maisha yake. Hata mtu asiyekubali utawala wowote, mwenye kudai kwamba hana “Mungu wala bwana-mkubwa,” amechagua thamani zake za kiadili, hata kama ni haki tu ya kufanya maamuzi yake mwenyewe.
Lakini ni nini msingi wa thamani hizi? Machaguo hayo ya maadili yana msingi gani? Je! hayo hubadilika muda upitapo?
Thamani Mbalimbali Katika Wakati Uliopita
“Kisparta” ni neno litumiwalo katika lugha nyingi kueleza ukosefu wa starehe. Neno hilo hurejezea hali ngumu ambazo raia wachanga wa kutoka jiji la Sparta la Ugiriki ya kale walielimishwa chini yazo. Kwa kutenganishwa na wazazi wao kuanzia utoto wa mapema, ilikuwa lazima wajifunze utii kamili. Kusudi la elimu hii lilikuwa kuwafanya askari walio violezo.
Vikundi vingine vya watu vilifuata thamani tofauti za kiadili. Mathalani, Israeli ya kale ilikuwa na fungu la sheria ambazo Musa alipewa na Mungu. Sheria hizo zilihusisha ndani vizuizi vya ulaji, vya kimwili, vya kiadili, na vya kiroho. Waisraeli walipaswa kumwabudu Yehova Mungu, tena yeye peke yake.
Kuhusu maadili ya ngono, Sheria ya Kimusa ililaani vikali uasherati, uzinzi, ugoni-jinsia-moja, na kufanya ngono na mnyama. Kusudi la jambo hili lilikuwa kutenganisha Waisraeli na jirani zao, si kidini tu bali pia kiadili. Hii ilikuwa kwa sababu vikundi vingi vya watu waliozunguka Israeli vilizoea ibada ya ngono yenye kushusha tabia na kudhuru, kutia na umalaya wa kiume na kike hekaluni. Baadhi yao hata walitoa watoto wao wenyewe kuwa dhabihu kwa miungu yao bandia.
Katika karne ya kwanza W.K., amri moja iliyotolewa na baraza la mitume na wazee Wakristo katika Yerusalemu iliagiza Wakristo wafuate maadili ya ngono ambayo kwa msingi yalikuwa yale yale ya Wayahudi, ikiwaambia ‘wajiepushe na uasherati.’ Kulingana na Dictionnaire de la Bible ya Vigouroux, agizo hili lilikuwa lenye thamani kabisa, kwa kuwa uasherati ulikuwa zoea la kawaida miongoni mwa wapagani wakati huo.—Matendo 15:29.
Unamna-namna wa viwango vya maadili uliendelea muda wote wa historia, kukiwa na vipindi mbalimbali vya mara kuvumilia viwango tofauti na mara kufuata sheria kali zaidi za tabia. Ugoni-jinsia-moja, uliolaaniwa vikali katika Enzi za Kati, ni kama ulivumiliwa wakati wa kile kipindi cha Uzaliwa Upya wa Maarifa katika Ulaya. Katika Uswisi, Calvin alipokaa katika Geneva wakati wa ule Mrekebisho wa Kidini, alianzisha kipindi cha kufuatilia sana adili bila kuridhiana na maoni mengineyo. Kwa upande mwingine, yapata miaka 200 baadaye, yale Mapinduzi ya Ufaransa yalihalalisha thamani zilizokuwa zimekataliwa hapo kwanza. Yalikuja kuunga mkono “uhuru wa maadili” ulio mpya na yakafanya iwe rahisi zaidi kupata talaka.
Thamani za Kiadili Zinazotofautiana Leo
Leo, hata ndani ya jamii ile ile moja, watu wana viwango tofauti vya maadili. Kuna wale ambao hutetea kufuatilia sana kanuni za kiadili, hali wengine hutetea kuwa na “uhuru” wa kiadili.
Kanuni za maadili zimebadilika upesi. “Kwa Wafaransa walio wengi, uzinzi husemwa wazi kabisa kuwa jambo baya. Ni jambo hasi na ni kinyume cha maadili,” chasema kitabu cha Kifaransa Francoscopie. Hata hivyo, chanzo hicho hicho chataarifu kwamba kwa wengine wengi “ukosefu wa uaminifu katika ndoa hauonwi tena kuwa njia ya kuepukia matatizo bali kuwa haki, haki isiyopaswa kutilia shaka shauku ambayo mume na mke waweza kuwa nayo kwa mmoja na mwenzake, bali yapasa hata kufanya iwe bora zaidi na kuiimarisha.”
Utoaji-mimba ni eneo jingine ambamo thamani za tabia zimebadilika upesi sana. Ingawa utoaji mimba ungali ni uhalifu katika nchi fulani-fulani, huo huvumiliwa—hata kudaiwa—katika nyinginezo. Inapendeza kuona kwamba Shirika la Tiba la Ufaransa liliuona utoaji-mimba kuwa uhalifu mpaka ulipohalalishwa katika 1974. Leo, Wafaransa wengi huuona kuwa wenye kukubalika kiadili.
Hata hivyo, maadili hayo yategemea nini? Je! thamani zetu za kiadili zapasa kuwa zenye kuhusu hali za namna fulani tu na kubadilika kulingana nazo?
Binadamu Ameanzisha Thamani Zake Mwenyewe za Maadili
Muda wa karne zote, wanafalsafa wamependekeza mawazo mengi kujaribu kujibu maswali ya jinsi hiyo. Baadhi yao wamependekeza ‘kanuni za maadili za ulimwenguni pote’ lakini wao washindwa kuafikiana ni fasili ya nani juu ya maadili ipasayo kuwa kiwango.
Wengine wamehisi kwamba hangaiko la mtu kwa binadamu mwenzake ndilo lapasa kuongoza mwenendo wake. Lakini jambo ambalo huenda mtu mmoja akaliona kuwa hangaiko lifaalo kwa wengine huendwa lisionwe hivyo na mtu mwingine. Kwa kielelezo, kwa karne nyingi wenyeji wengi wa watumwa waliliona kuwa hangaiko lifaalo kulisha na kuwapa makao watumwa wao, lakini watumwa walihisi kwamba hangaiko lifaalo lingepasa kuwa na tokeo la kuwaweka huru kutoka utumwani.
Hakuna shaka kwamba maoni ya namna nyingi zenye kuhitilafiana ambayo wanafalsafa wamekuwa nayo kuhusu thamani za kiadili yamevuruga watu wengi. Mawazo yao hayajatokeza kiwango chochote cha maadili yenye kufuatwa na wote, wala falsafa zao hazijaongoza familia ya kibinadamu kwenye amani na mwungamano. Kile tu ambacho mawazo yao mengi yenye kuhitilafiana yamefanya ni kuongoza idadi ya watu wenye kuongezeka wakate shauri kwamba kiwango cha mtu binafsi ni chema tu sawasawa na kile cha “wastadi.”
Ndiyo sababu wengi leo wamechagua kufuata maoni ya mwanafalsafa Mfaransa Jean-Paul Sartre, aliyehisi kwamba binadamu apaswa kujiamulia mwenyewe masuala ya kiadili. Njia hii ya kufikiri hata imefuatwa na waenda-kanisa wengi. Kwa kielelezo, wenye mamlaka wengi Wakatoliki wana wasiwasi kwa sababu sasa Wakatoliki wengi hawafuati mafundisho ya kanisa juu ya mambo ya ngono na hutumia vizuia-mimba ambavyo hulaaniwa vikali na kanisa.
Somo la historia ni kwamba kanuni mbalimbali za kiadili zimeanzishwa na wanadamu, lakini baada ya muda kanuni hizo zimetiliwa shaka, zikabadilishwa, au zikasahauliwa. Hata hivyo, kanuni za Biblia zilizotajwa mapema kidogo katika makala hii si za kuongozwa na misisimuko ya muda ya wanafalsafa au jamii zinazobadilika. Kanuni hizo za Biblia zina thamani gani leo? Je! yawezekana kuzifuata?
[Blabu katika ukurasa wa 7]
“UKOSEFU WA UAMINIFU KATIKA NDOA HAUONWI TENA KUWA NJIA YA KUEPUKIA MATATIZO BALI KUWA HAKI”