Maoni ya Biblia
Je! Sayansi Imefanya Biblia Ikawa Bure?
JE! sayansi, imeifanya Biblia kuwa mkusanyo wa hekaya na hadithi za kutungwa kwa sababu ya maarifa yayo yaliyoongezeka juu ya ulimwengu wote mzima? Watu wengi hufikiri hivyo. Je! ndivyo wewe unavyofikiri?
Labda wewe, kama wengi, ulifundishwa kufikiri hivyo kuanzia ujana wako na kuendelea lakini hujapata kamwe kutokeza maswali juu ya hilo. Twakualika utokeze maswali juu ya hilo sasa. Fikiria kielelezo kimoja tu, taarifa iliyomo ndani ya Biblia juu ya ulimwengu wote mzima wa asili. Si kwamba tu taarifa hiyo ilipinga moja kwa moja waliyokuwa wakisema wataalamu wa siku hiyo bali pia ilipinga yale ambayo wanasayansi walikuwa wangali wanasema maelfu mengi ya miaka baadaye.
Habari ya Nguvu ya Uvutano
Dunia inakalia nini? Ni nini kinachoning’iniza mwezi, jua, na nyota juu? Maswali hayo yamekuwa fumbo kwa binadamu kwa maelfu ya miaka. Kwa habari ya dunia, Biblia ina jibu rahisi. Kwenye Ayubu 26:7, NW, yasema kwamba Mungu ‘ananing’iniza dunia pasipo na kitu.’ Katika Kiebrania cha awali, neno la “pasipo na kitu” (beli-mahʹ) linalotumiwa hapa kwa halisi humaanisha “si juu ya kitu chochote,” na hiyo ndiyo pindi pekee linapotokea katika Biblia. Wazo ambalo hilo hutoa juu ya dunia inayozungukwa na anga la juu lililo tupu latambuliwa na wasomi kuwa “njozi yenye kutokeza,” hasa kwa wakati huo.a
Hivyo sivyo watu walio wengi walivyoiona kosmo (ulimwengu) katika siku hizo. Maoni mojawapo ya kale yalikuwa kwamba dunia ilikuwa imeegemezwa na ndovu kadhaa waliosimama juu ya mgongo wa kasa mmoja mkubwa mno.
Aristotle, akiwa mwanafalsafa Mgiriki aliyejulikana na pia mwanasayansi wa karne ya nne K.W.K., alifundisha kwamba dunia haingeweza kamwe kuning’inia kwenye anga la juu lililo tupu. Badala yake, yeye alifundisha kwamba madude ya mbinguni yalikuwa yamekwamilishwa kwenye sakafu ya vizio thabiti vyenye kupenywa na nuru. Kizio kimoja kilikuwa ndani ya kizio kingine. Dunia ndiyo iliyokuwa ndani zaidi; kizio cha nje kabisa kilikuwa chenye nyota. Vizio hivyo vilipozunguka kimoja ndani ya kingine, vitu vilivyokuwa juu yavyo—jua, mwezi, na sayari—vilisonga huku na huku angani.
Taarifa ya Biblia kwamba kwa kweli dunia ‘inaning’inia pasipo na kitu’ ilimwacha nyuma Aristotle na miaka zaidi ya 1,100. Hata hivyo, Aristotle alionwa kuwa mfikiriaji wa kwanza kabisa wa siku yake. Maoni yake yangali yalifundishwa kuwa uhakika karibu miaka 2,000 baada ya kifo chake! Kama The New Encyclopædia Britannica kisemavyo, katika karne za 16 na 17 W.K., mafundisho ya Aristotle “yaliinuliwa kufikia cheo cha kuwa imani ya kidini” machoni pa kanisa.
Mwanafalsafa wa karne ya 16 Giordano Bruno alithubutu kutilia shaka maoni ya kwamba nyota “zilikuwa ndani ya kuba moja.” Aliandika kwamba hilo lilikuwa “wazo la kipumbavu ambalo watoto wangeweza kudhania, labda wakiwazia kwamba ikiwa [nyota] hazikuwa zimeshikilizwa kwenye sakafu ya kimbingu kwa nta nzuri, au kugongomelewa kwa misumari iliyo mikubwa zaidi, zingetuangukia kama mvua ya mawe.” Lakini kutokuafikiana na Aristotle kulikuwa ni mchezo hatari katika siku hizo—kanisa liliagiza Bruno achomwe kwa moto akiwa hai kwa ajili ya kueneza mawazo yasiyokubalika juu ya ulimwengu wote mzima.
Katika Mchuzi wa Kikosmo
Kwa kuvumbuliwa kwa darubini, wataalamu wa nyota wenye kuongezeka walianza kutilia shaka Aristotle. Ikiwa jua, mwezi, na nyota havikuwa vimeshikilizwa kwenye vizio vyenye kuizunguka dunia, basi ni nini kingeweza kuvining’iniza na kuvizungusha? Mwanahisibati wa karne ya 17 René Descartes alifikiri alikuwa na jibu. Alikubaliana na Aristotle kwamba anga lililo baina yetu na madude yale mengine ya kimbingu halingeweza kuwa ni tupu. Kwa hiyo akabuni wazo la kwamba ulimwengu wote mzima ulikuwa umejawa na umaji-maji wenye kupenywa na nuru—namna fulani ya mchuzi wa kikosmo.
Wazo hilo lilionekana limesuluhisha matatizo mawili. Kwanza, lilitokeza kitu fulani cha ‘kuning’inizia’ madude ya kimbingu; yote yalikuwa yamening’inizwa ndani ya mchuzi! Jambo jingine ni kwamba lilisaidia kueleza miendo ya sayari. Descartes alikuwa na maoni ya kwamba sayari zilishikiliwa na mzunguko wa kasi sana ndani ya umaji-maji, ambao ulizifanya zizunguke katika mizunguko yazo. Hiyo “Nadharia ya Mizunguko ya Kasi,” kama ilivyoitwa, yaweza kuonekana kwetu kuwa ya kuchekesha leo. Lakini hiyo ndiyo iliyokuwa nadharia iliyoongoza katika utafiti wa ulimwengu wote mzima kwa zaidi ya karne moja katika nchi fulani fulani.
Wanasayansi wengi waliipendelea kuliko ile iliyojitokeza baadaye: sheria ya Isaac Newton ya nguvu ya uvutano ya ulimwengu wote mzima, iliyotangazwa katika 1687. Newton alitokeza maoni ya kwamba sayari hazikuhitaji vitu vyenye kuziendesha, vyenye kuonekana ili kuzining’iniza. Nguvu ya uvutano ndiyo iliyoongoza miendo yazo na kuzishikilia kwenye mizunguko yazo. Ndiyo kusema, zaning’inia katika anga tupu bila ya kukalia kitu. Wengi wa wenzi wa Newton walidhihaki maoni yake juu ya nguvu ya uvutano. Na hata Newton mwenyewe aliona vigumu kuamini kwamba anga lilikuwa tupu, likiwa bila chochote kwa sehemu iliyo kubwa.
Hata hivyo, maoni ya Newton yalishinda hatimaye. Leo, ni rahisi mno kwetu kusahau swali la kwamba ni nini kinachoning’iniza sayari ambalo lilichochea mjadala uliopamba moto miongoni mwa wanasayansi walioelimika na wenye akili nyingi karne zipatazo 32 baada ya Biblia kutaarifu kwa usahili wa kupendeza kwamba dunia ‘huning’inia pasipo na kitu.’ Ayubu angeliwezaje kujua kuyaeleza mambo kwa njia hiyo? Ni kwa nini angeweza kusema kwamba hakuna kitu chochote kinachoining’iniza dunia, ambapo ilichukua “wataalamu” miaka zaidi ya 3,000 kufikia mkataa uo huo?
Ni kwa Nini Biblia Imeutangulia Sana Wakati Wayo?
Biblia hutoa jibu la akili. Kwenye 2 Timotheo 3:16, NW, twasoma hivi: “Andiko lote limevuviwa na Mungu.” Kwa hiyo Biblia haikutokezwa na hekima ya kibinadamu bali hiyo ni uwasilishaji ulio sahihi wa mawazo ya Muumba kwetu.
Ni jambo la muhimu sana kwamba ujichunguzie kama dai hilo la Biblia ni la kweli. (1 Wathesalonike 2:13) Kwa njia hiyo unaweza kuyapata mawazo ya Yule aliyetubuni na kutuumba. Je! kungeweza kuwa chanzo gani kingine kilicho bora zaidi cha kutuambia mambo ya wakati ujao na jinsi ya kuishi maisha yenye furaha, yenye kuridhisha katika ulimwengu huu wenye mvurugo?
[Maelezo ya Chini]
a Theological Wordbook of the Old Testament chasema: “Ayubu 26:7 kwa kutokeza yaonyesha ulimwengu uliojulikana wakati huo kuwa ulining’inizwa angani, kwa njia hiyo ikatangulia uvumbuzi wa kisayansi wa wakati ujao.”
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]
By permission of the British Library