Kukunjua Moyo ili Kusaidia Wengine
KATIKA 1973, yote hayo yalipotukia, nilikuwa wa miaka 22 na mwenye afya. Maisha yangu yalikuwa yamejawa na anasa. Nilishiriki katika michezo na nilipenda kazi ya kutumia nguvu. Wakati wa likizo ningeenda kuelea juu ya mawimbi. Nilifurahia kuendesha motokaa. Lakini mfoko wa kijinga wa hasira kali ulikomesha hayo yote kwa ghafula.
Nikiwa na mke wangu, Gemma, nilikuwa nazuru watu wa ukoo wakati wavulana wachanga walipovuta fikira zangu. Tuliwatazama wakivunja visehemu-sehemu vya ukigo wa bustani walipokuwa wakitembea barabarani. Walipotuona, wakaanza kutupa vipande vya mbao kwenye bustani na kisha kwenye varanda ya orofani ya nyumba, ambapo tulikuwa tumesimama. Kipande kimoja kilimgonga Pippa, binti yangu wa miaka minne. Kwa mfoko wa ghadhabu, nikageuka na kuwatupia watundu hao bilauri ya gilasi niliyokuwa nimeshika. Varanda hiyo ilikuwa meta 3.6 kutoka ardhini, na ilitukia nikateleza. Nilipinduka huyo-o chini, nikaangukia kichwa changu, na mifupa kadhaa ya uti wa mgongo shingoni ikatoka mahali payo na kuvunjika.
Nikiwa nimelala katika kitanda cha hospitali kwa karibu mwaka mmoja, nilikuwa na wakati wa kufikiria juu ya hali yangu. Mwanamume aliyekuwa kando yangu alijiua, na wengine niliojua wamefanya vivyo hivyo tangu wakati huo. Kukosa tumaini na kuvurugika fikira hakuelezeki. Mzigo niliokuwa nawekelea wengine na kujua kwamba hakungeweza kuwa na maendeleo yoyote vilinihuzunisha sana. Ndiyo, nyakati nyingi mimi pia nilifikiria kukomesha maisha yangu. Kwa kweli, nilimwuliza mke wangu anisaidie kufanya hivyo kwa kuniletea tembe fulani. Lakini akaniambia nilikuwa na kichaa na kukataa. Jinsi sote wawili tunavyoshukuru sasa kwamba alikataa!
Mambo yalianza kubadilika wakati shangazi yake Gemma, aliyekuwa amekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwa miaka mingi, alipoanza kujifunza Biblia pamoja naye. Gemma akaanza kuelewa, lakini mimi sikuwa nimepata kamwe kupendezwa na dini. Mambo niliyosikia makasisi wakisema kwenye televisheni hayakunivutia. Ingawaje mimi sikuwa mtu wa kupenda kujifunza sana. Lakini Gemma alipoanza kuongea nami juu ya imani yake mpya, nikaona mambo mawili yenye kuvutia mara moja.
Kwanza, nikajifunza kwamba Biblia ina uhusiano na mojawapo ya masomo niliyokuwa nimeona yakivutia shuleni, historia. Hilo lilinistaajabisha. Sikuwa nimepata kujua kamwe kwamba kuna ukamatano huo. Pili, haki ya Mungu ilinivuta kwake. Sikuzote nilikuwa nimefikiri kwamba ukosefu wa haki maishani haungeweza kuondolewa kamwe. Lakini kadiri nilivyojifunza juu ya kusudi la Yehova na Ufalme wake, ndivyo nilivyoanza kuona kwamba haki itadumu.—Kumbukumbu la Torati 32:4; Luka 18:7, 8.
Kusudi Katika Maisha
Baada ya hilo nilifanya maendeleo ya haraka katika funzo langu la Biblia. Nilikuwa nimepata kusudi la kuishi, nikiwa katika hali ile ile ya kutojiweza kimwili ambayo ningeendelea kuwa nayo. Nilikuwa na kila sababu ya kushukuru. Lakini maoni yangu upesi yakapanuka nilipotambua ningeweza kufanya mengi ili kuwasaidia wengine na maarifa niliyokuwa nikiyapata.
Ningeweza kufanyaje maendeleo? Hilo ndilo swali lililosumbua. Gemma na mimi tulibatizwa pamoja, nami nilikuwa nikijifunza kwa bidii, kwa msaada wa walimu wengi wazuri, ili nikue kiroho. Hata hivyo, badiliko kubwa lilitukia wakati niliposoma juu ya Shahidi mmoja katika Lebanon.a Alikuwa na miaka 46 na alikuwa amelazwa kitandani kwa miaka 18. Hata hivyo, lijapoonekana kuwa jambo lisilowezekana, yeye alikuwa mzee katika kundi la Kikristo! Kufikia wakati huo, yeye alikuwa amewasaidia watu 16 wakawa watumishi walio wakfu wa Yehova na alikuwa akiongoza mafunzo ya Biblia saba kila mwezi. Ono lake lilinitia moyo sana.
Mamlaka ya utoaji nyumba ya mahali hapo iliipa familia yangu nyumba ya orofa moja, yenye vyombo kamili vya kujiendesha ambavyo hunisaidia kwenda hapa na pale. Mimi nimebarikiwa na msaada wote wa kimwili ninaohitaji. Familia zetu zilichukua hatua ya pamoja na kununua kilori kidogo ili kiti changu chenye magurudumu kiweze kuingia kwa urahisi. Hilo hutuwezesha sisi tukiwa familia tufike mikutanoni kwenye Jumba la Ufalme. Kwa upendo, kundi la mahali hapo lilipanga upesi Funzo la Kitabu la Kundi liongozwe nyumbani mwangu.
Tamaa yangu ya kutoa ushahidi nyumba kwa nyumba ilitoshelezwa wakati akina ndugu na dada katika kundi walipojitolea kusukuma kiti changu cha magurudumu. Naweza kuongea na wenye nyumba lakini, nikiwa siwezi kutumia mikono na viganja vyangu, siwezi kutumia Biblia. Kwa hiyo mimi hurejezea maandiko, na kisha mwenzangu huonyesha mistari hiyo katika Biblia yake na kutoa vifaa vya funzo la Biblia ninavyorejezea.
Bila shaka, watu wengi huja kunitembelea nyumbani, na kwa njia hiyo naweza kuongoza mafunzo ya Biblia. Pia nimekuwa mtaalamu wa kuandika barua kwa kushika kalamu kinywani mwangu, kwa hiyo naweza kuwa mtendaji katika kuhubiri wakati wowote wa siku. Nami nimeweza kufanya upainia msaidizi kwa ukawaida kwa miaka mitatu.
Kustahili Kuwa Mwalimu
Baada ya muda nikastahili kuwa mtumishi wa huduma, lakini ningewezaje kufundisha kutoka jukwaani? Wakati wa mojawapo ya majifunzo yangu, nilikuwa nimejifunza kugeuza kurasa za Biblia kwa kutumia kijiti kati ya meno yangu. Ijapokuwa zoea hilo ni lenye msaada, kwa asili yamaanisha ni lazima niache kunena ninapochukua kijiti na kisha kukiweka chini. Upesi nikang’amua kwamba suluhisho lilikuwa ni kutumia ulimi wangu—katika kugeuza kurasa za Biblia! Na hivyo ndivyo mimi hufanya sasa.
Njia hiyo isiyo ya kawaida iliniwezesha kusitawisha uwezo wangu wa kunena, nami nikajifunza mengi zaidi kutokana na migawo ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Wazia mawazo yangu wakati katika 1984 nilipowekwa nitumikie nikiwa mzee wa kundi!
Hatua iliyofuata ilikuwa ni kutoa hotuba ya watu wote, ya muda wa dakika 45. Hiyo hutaka matayarisho ya uangalifu mkubwa, na ingawa sikuzote mimi huiona kuwa yenye kuchosha kimwili, mimi huendelea bila kuacha. Sasa nina pendeleo la ziada la kuzuru makundi ya karibu pindi kwa pindi ili kuyatolea hotuba. Watoto hustaajabu sana kuniona nikigeuza kurasa za Biblia kwa ulimi wangu, na nyakati nyingine wao hujaribu kuniiga. Lakini upesi wanaacha. Inataka mazoezi mengi ili kuweza kufanya hivyo kwa ufundi.
Ninapotazama nyuma, ningali nakumbuka waziwazi uchungu niliokuwa nao nilipoondoka hospitalini hapo kwanza. Nilijua kwamba wake wa wengine wengi ambao hawajiwezi kama mimi walikuwa wameacha waume wao. Kama Gemma angeniacha ningeelewa. Badala yake, akiwa mwenzi mwenye upendo, hakuniacha, akiungwa mkono na Pippa, binti yetu. Kwa msaada wao na kwa msaada wa kundi, nimeweza ‘kukunjua moyo’ na kuwasaidia wengine. (2 Wakorintho 6:13)—Kama ilivyosimuliwa na Tony Wood.
[Maelezo ya Chini]
a Ona makala iliyotangazwa katika Mnara wa Mlinzi wa Februari 1, 1982, “Kutoka Hali ya Kukosa Tumaini Mpaka Kuwa na Furaha,” kama inavyosimuliwa na Estefan Kalajian.
[Picha katika ukurasa wa 19]
Nikiwa na Gemma na Pippa, mke wangu na binti yangu
Nikigeuza kurasa kwa ulimi wangu