“Waliniambia Singetembea Tena Kamwe!”
AKIWA na miaka 20, Ed alihusika katika msiba mbaya uliohusu motokaa. Aliporudiwa na fahamu, alishindwa kuinuka. Akatambua kwamba alikuwa amepooza lakini akafikiri ni kwa muda tu. Ed alikumbuka yaliyotokea baadaye hospitalini: “Waliniambia singetembea tena kamwe!” Alikuwa amepooza kuanzia kifua kwenda chini.
“Mafikira yalinilemea sana mwanangu alipoumia,” alikumbuka babae Ed. “Yeye alikuwa kijana mwanamume mwenye afya, lakini sasa hangeweza kutembea tena. Hilo lilikomesha maisha yake kwa ghafula.” Ed alikuwa akifuatia huduma ya wakati wote, iitwayo upainia na Mashahidi wa Yehova.
Mwanamume mwingine kijana katika miaka yake ya 20, Bill, alipiga mbizi kimchezo ndani ya mawimbi ya bahari na kugonga kichwa chake kwenye ukuta wa mchanga. Mara iyo hiyo, akawa hawezi kusonga wala kupumua. Bill hakufa maji kwa sababu alisaidiwa na rafiki waliokuwa karibu. Hata hivyo, akapooza kuanzia shingo kwenda chini. Madaktari walimwambia Bill kwamba yeye pia hangetembea tena kamwe.
Itikio la Kwanza
“Nilitaka kujiua,” akakiri Bill, “lakini singeweza kufanya hivyo katika kitanda cha hospitali.” Bill alikuwa ametumika katika Vita ya Vietnam na alikuwa akipanga kuwa rubani wa ndege. Alipoumizwa katika 1969, ndoto zake zote ziliangamizwa, naye hakuona sababu ya kuishi.
Itikio la kwanza la Ed lilikuwa tofauti alipoambiwa angekuwa amedhoofika daima. “Sikuvunjika moyo, na sababu ilikuwa ni imani yangu katika ahadi za Mungu katika Biblia. Nikatambua kwamba hali yangu huenda ikawa ni ya kudumu sasa lakini haitakuwa ya kudumu milele.” Kwa sababu ya tumaini alilo nalo, kwa kufaulu Ed ameweza kukabiliana na kasoro yake kwa miaka zaidi ya 25 sasa.
Uhitaji wa Kukabili Tatizo
Kwa upande mwingine, Bill hakuwa na maarifa ya ahadi za Mungu. Hata hivyo, jambo fulani lilitukia siku moja ambalo lilimchochea afanye jambo fulani kujihusu.
Baada ya kujilazimisha kuishi tu akiwa hospitalini kwa miezi nane, Bill aliendeshwa kwenye bafu akanyoe ndevu na mwuguzi wa kiume. “Nilipotazama katika kioo,” akasema, “niliona mtu ambaye hakufanana na mimi!”
Hapo awali Bill alikuwa amekuwa mwanamume mwenye nguvu wa kilo 91, mwenye urefu wa meta 1.8, lakini sasa alikuwa gofu tu la kilo 41. Alishindwa kuamini kwamba mfano wa yule mtu katika kioo ulikuwa wake mwenyewe. Jambo hilo liliwasha ndani yake roho ya uhodari ya kukubali tatizo la ulemavu wake. “Mwaka wa kwanza wa ulemavu wako ni wakati wa hatari sana,” asema Bill, “kwa maana huo ndio wakati unaamua unataka kuiendea njia gani.”
Kukabiliana na Magumu
Ed si mtu mwenye wasiwasi, lakini akubali maono yake ya moyoni huwa yenye kubadilika kuwa ya uchangamfu na huzuni. “Nyakati nyingine siwezi kufanya mambo yaliyo rahisi kama kujinyoosha nifikie kitu,” aeleza Ed, “na huenda nikashuka moyo.”
Bill huona ugumu ulio mkubwa ni kuishi na mwili ulio dhaifu na hali sivyo ilivyo kwa ubongo. “Ni kama kuwa na akili yenye kuendeshwa na jeti ikiwa ndani ya mwili ulio kama mkokoteni wa ng’ombe,” asema.
Pia kuna matatizo ya kimwili ambayo hushirikishwa na jeraha la uti wa mgongo, kama vile kushindwa kudhibiti kibofu cha mkojo na utumbo, vidonda vinavyoletwa na kukalia mahali pamoja, na matatizo ya kupumua. Ed amekuwa na matatizo ya figo tangu jeraha lake na ana vipindi vya kuanzia siku sita hadi saba kwa wakati mmoja anapokuwa na halijoto ya nyuzi (digrii) 46 Sentigredi. Pia kushindwa kudhibiti kibofu cha mkojo na utumbo ni jambo lenye kumfadhaisha sana Bill. Ni kama asemavyo: “Hupati kamwe kujirekebisha kwa kuwa na mwili wa kitoto.”
Ed asihi walemavu wote wajitegemee kwa kadiri iwezekanayo. “Jaribu yote uwezayo ujifanyie mambo mwenyewe,” asema, “nawe utafanya mengi zaidi.” Ndiyo sababu, alipokuwa akiondoka hospitalini, jambo la kwanza alilofanya ni kurekebisha motokaa yake iwe na viendesheo vya mkono ili aweze kuendesha. Sasa hata Ed hutumia lori lenye vyombo vya kipekee katika biashara yake ya kusafisha majengo yenye kufanikiwa.
“Jaribu kusahau ulemavu wako,” ashauri Bill, “na utoke ukaishi maisha yako vizuri uwezavyo. Usipotenda kama mtu aliyelemaa, watu hawatakutenda kama mmoja.” Bill hujizoeza yale asemayo. Kwa kufanikiwa amekuwa na biashara na kuiendesha, akienda huku na huku kwenye kigari chake cha gofu, katika kiti chake chenye magurudumu, na kwa vitegemezo.
Ni Nini Liwezalo Kufanywa?
Kizuizi kimoja kwa mtu aliyelemaa chaweza kusemwa kimo katika akili za wale ambao hawakulemaa. Njia bora zaidi ya kuondoa kizuizi hicho ni kupitia uelewevu. Watu waliolemaa hutaka ufikirio na uelewevu ule ule ambao angeonyeshwa mtu asiye na ulemavu wa kimwili.
Baadhi ya watu hujiona hoi au huvurugika wanapokabiliwa na mtu mwenye kilema. Bill asema hivi: “Kwa kweli sisi sote tuna kasoro kwa njia fulani. Ni kwamba tu wengine wana kasoro kubwa zaidi ya wengine.” Kwa kielelezo, wale ambao wana kasoro ni watu kamili, ambao imetukia hawawezi kutembea, kuona, au kusikia kama watu wale wengine. Ni jambo la muhimu kwamba tuone kasoro yoyote kuwa ni tukio na kumwona mtu mwenyewe kwa ujumla.
“Mimi huthamini watu wanaponiona kama vile mtu mwingine yeyote,” akasema Ed. “Nitazame mimi. Usikitazame kiti.” Kisha alisimulia jambo lililotukia kwake na kwa mke wake katika mkahawa: “Mtumikiaji wa kike alichukua ombi la mke wangu kwanza na kisha akamwuliza yeye, badala yangu, mimi nilitaka nini. Mimi si kiziwi! Ni kwamba tu siwezi kutembea.”
“Watu walio wengi hutaka kuonyesha ufikirio kwa watu waliolemaa,” aeleza Ed, “lakini hawajui la kufanya.” Shauri lake ni hili: “Jambo linalofaa zaidi ni kungojea ujue unaloweza kufanya kabla ya kujiingiza ufanye jambo fulani.”
Kwa hiyo hakikisha kuuliza kwanza, “Naweza kusaidia?” Au, “Je! kuna jambo niwezalo kufanya nisaidie?” Usijitangulize kufikiri kwamba mtu aliyelemaa anataka msaada wako; huenda asiwe anataka.
“Pongezi kubwa zaidi kwa mtu aliyelemaa,” ashauri Bill, “ni kumtendea kama kawaida, kushughulika naye kama ambavyo ungeshughulika na mtu mwingine yeyote.” Ni kweli, huenda wengine wakaona ni vigumu kufanya hivyo. Huenda kukawa kizuizi cha kibinafsi cha akili au cha maono ya moyoni kati yao na watu waliolemaa. Hata hivyo, kwa kadiri tuzidivyo kuwajua hao kuwa watu mmoja mmoja, ndivyo tunavyofikiria kidogo zaidi juu ya ulemavu wao.
Ed, ambaye amekuwa na kundi lile lile la Mashahidi wa Yehova kwa miaka mingi, aeleza hivi: “Rafiki walio wengi hawanifikirii mimi kuwa kilema. Kwa kweli, katika utendaji wetu wa kuhubiri peupe, wao hunituma kwenye ziara ya kurudia katika nyumba yenye mfululizo wa ngazi kumi! Kisha mimi hurudi na kuwaambia wamtume mtu mwingine.”
Je! Ed huudhika rafiki zake wanaposahau juu ya vizuizi vyake vya kimwili? Hata kidogo. Ni kama anavyosimulia: “Ni vizuri sana kwamba wao hufikiri mimi sihitaji msaada wowote. Mimi nathamini hilo, kwa maana kwa njia hiyo mimi huona kwamba kwao mimi si kilema, lakini mimi ni mtu mwingineye tu wa kawaida.”
Misaada Yapatikana
Katika miaka ya karibuni maendeleo mengi yamefanywa katika nchi nyingi ili kutoa msaada kwa waliolemaa kimwili. Matengenezo mengi sana, bidhaa, na utumishi mbalimbali hupatikana ili kuwasaidia wafurahie maisha ya kujitegemea. Katika sehemu nyingi, anachohitaji mtu tu ni kufungua kitabu cha simu apate habari juu ya matengenezo na utumishi huo.
Majengo na vifaa vingi vya umma sasa vimetengenezwa vifae watu waliolemaa. Mashirika fulani ya ndege na usafiri hutoa safari za pekee kwa ajili ya waliolemaa. Na walemavu leo waweza kufurahia ujitegemeaji katika motokaa ndogo na kubwa zenye vyombo vya kipekee.
Tekinolojia ya ki-siku-hizi, ambayo katika visa fulani imewezesha kuepuka kazi itimizwayo na neva zilizoumia, imefanya iwezekane kwa watu fulani waliopooza kutembea. Hata hivyo, Dakt. J. Petrofsky, mtafiti mwenye kuongoza katika jambo hilo, akubali kwamba huenda watu wakawa na matumaini bandia kuhusu tekinolojia hiyo. Huenda wakafikia kuamini itamwezesha mtu yeyote aliyelemaa atembee tena. “Jambo la kufanya ni kufuata haki,” Dakt. Petrofsky asema, “na kujaribu kuwaambia kikamili msimamo wa utafiti huo. Ilivyo ni kwamba hatuponyi chochote.”
Ponya la Kweli
Hata hivyo, ponya la kweli na la kudumu la ulemavu wote wa kimwili litapatikana karibuni. Tumaini hilo lililo la hakika la kuweza kutembea tena limempa Ed nguvu na kumsaidia akabiliane na ulemavu wake kwa miaka yote hiyo. Ahadi ya Biblia ni: “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6.
Kuponywa kwa udhaifu wote kutatimizwa papa hapa duniani wakati Ufalme wa Mungu utakapochukua mahali pa serikali zote za kibinadamu. (Danieli 2:44) Kweli kweli, Ufalme wa Mungu, ambao Kristo alifundisha wafuasi wake wasali juu yake, utaleta ulimwengu mpya ambamo ahadi hii ya Biblia itatimizwa: “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24; Mathayo 6:9, 10.
Kufikia wakati wa msiba wake, Bill hakuwa anajua maana ya ahadi hizo za Biblia, ingawa sikuzote alikuwa amekuwa na staha kubwa kwa Biblia. Wakati wa miaka mitano ya kwanza ya kulemaa kwake, yeye alianza kutumia madawa ya kulevya sana. “Nilikuwa nimetumia madawa ya kulevya katika Vietnam ili kuepuka matisho mabaya,” asema, “na baadaye niliyatumia ili kuvumilia maisha katika kiti chenye magurudumu.”
Hata hivyo, katika 1974, kwa msaada wa Mashahidi wa Yehova, Bill akaja kuamini kwamba Biblia ni ya kweli kabisa na kwamba ahadi zayo ni zenye kutegemeka kikamili. “Tangu wakati huo na kuendelea,” akasema, “ni kama kwamba kiwi kilitoka machoni pangu!” Miezi saba baadaye Bill aliweka wakfu maisha yake kwa Yehova Mungu, na baada ya muda mfupi yeye na mke wake wakaanza pamoja maisha katika utumishi wa wakati wote wakiwa mapainia.
Akifikiria juu ya yaliyompata wakati uliopita, Bill akubali kwamba msiba wake na ulemavu ulioletwa nao vilikuwa vyenye kuumiza sana. “Lakini,” yeye akazia, “nimefaidika na mengi kutokana na jeraha hilo.” Kwa nini akasema hivyo?
“N’na shaka kama ningekuwa Mkristo wa kweli leo kama isingalikuwa ni kwa sababu ya ulemavu huu,” ndivyo anavyoeleza. “Hapo mbele, nilikuwa mwenye kiburi sana, mwenye kutafuta makubwa, na yawezekana singeweza kukaa mahali pamoja kwa muda wa kutosha niweze kukubali ujumbe wa Kikristo.”
Kwa hiyo sasa, kama vile Ed, Bill ana imani thabiti ya kwamba karibuni katika ulimwengu mpya wa Mungu, ataweza tena kuwa na matumizi kamili ya mwili wake. Na bila kujali hali inayoelekea kuwa hoi, mtu yeyote aliyelemaa aweza kuwa na uhakika uo huo katika uwezo wa kuponya wa Mungu. Moyo wa mtu kama huyo waweza kuimarishwa kila siku na usadikisho huu: “Najua nitatembea tena!”—Imechangwa.
[Picha katika ukurasa wa 24]
Ijapokuwa ulemavu wake, Ed hushiriki kikamili katika huduma ya Kikristo