Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g91 5/8 kur. 17-21
  • Kutoka Jeshi la Hitler Hadi Kwenye Huduma Katika Hispania

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutoka Jeshi la Hitler Hadi Kwenye Huduma Katika Hispania
  • Amkeni!—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Mageuzi ya Akili na Jeuri ya Nazi
  • Fungu Langu Katika Vita ya Ulimwengu 2
  • Mtazamo Wangu Ulibadilishwa kwa Umilele
  • Utumishi wa Betheli wa Wakati Wote
  • Jiko la Gari-Moshi la Kutumia Mvuke
  • Utumishi wa Misionari Katika Afrika na Hispania
  • Chuki Yangu Iligeuka Kuwa Upendo
    Amkeni!—1995
  • Hatukuunga Mkono Vita ya Hitler
    Amkeni!—1994
  • Ninaweza Kumlipa Yehova Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Kwa Msaada wa Yehova, Tuliokoka Serikali za Kimabavu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1991
g91 5/8 kur. 17-21

Kutoka Jeshi la Hitler Hadi Kwenye Huduma Katika Hispania

Kama ilivyosimuliwa na Georg Reuter

NI NINI maana ya maisha? Kwa wengi wetu, hufika wakati maishani tunapouliza swali hilo la maana. Kifo katika familia, msiba mbaya sana, au kuchakazwa na uzee vyaweza kutulazimisha tufikiri juu ya ni kwa nini na kwa sababu gani tuko hai.

Katika kisa changu ilitukia katika kiangazi cha 1930, nilipokuwa na miaka sita tu. Niliishi na wazazi wangu katika jiji la Essen, Ujerumani. Sitasahau kamwe jinsi ulimwengu wangu wa kutojali ulivyovunjwa-vunjwa siku niliyokuta ndege-chiriku wetu mpendwa amekufa katika kizimba chake. ‘Hili lingewezaje kutukia?’ Nikajiuliza mwenyewe. ‘Sikuzote ameimba vizuri sana.’

Kwa uanana nilimweka ndege huyo aliyekufa ndani ya kopo tupu na kumzika katika shamba letu. Lakini sikuweza kusahau jambo hilo. Ijapokuwa majuma na miezi ilipita, niliendelea kutafakari yaliyompata hata nikawa siwezi kuzuia udadisi wangu tena. Nikapiga hatua kwa kuazimia kwenda shambani na kufukua kopo hilo. Nilipolifungua, nilishangaa! Ndege huyo hakuwapo tena. Kilichobaki tu kilikuwa ni mifupa na manyoya machache. Je! hayo tu ndiyo yaliyokuwa maisha ya ndege? Na vipi sisi? Hutukia nini kwetu tufapo?

Wakati huo maswali yangu yalibaki bila kujibiwa. Lakini bila mimi kujua, kulikuwako matukio ya kuogofya sana yaliyokuwa yakija, matukio ambayo yangenifanya nitafute kwa bidii zaidi majibu ya maswali hayo yenye kusumbua-sumbua ya utoto wangu.

Mageuzi ya Akili na Jeuri ya Nazi

Miaka ilipita haraka, nami nikawa mwanagenzi (mfunzwa kazi) katika kazi ya ujenzi. Wakati uo huo, Hitler alikuwa amekuja mamlakani, na mwenezo wake wa propaganda ulikuwa ukifanywa kwa kasi kabisa ili kugeuza akili ya taifa. Watu wakawa wanasema “Wokovu una Hitler!” badala ya “Habari ya asubuhi.” Kila mahali kulikuwako yunifomu: Jungvolk (Vijana), Hitler-Jugend (Vijana wa Hitler), Bund Deutscher Mädchen (Ushirika wa Wasichana Wajerumani), SA (Sturmabteilungen, au vikosi vya jeshi la kuvamia), na SS (Schutzstaffel, jeshi hodari la Hitler). Nami nakumbuka waziwazi maandamano yasiyohesabika, muziki na vigelegele katika mabarabara—ulikuwa wakati wenye kusisimua kwa kijana mnyumbufu.

Upesi nikajikuta nikishiriki, kwa kuvutwa na msisimuko wa kijumla. Mazingira yalijawa na semi za kizalendo kama vile, “Leo, Ujerumani ni yetu; kesho, ulimwengu wote utakuwa wetu,” na, “Bendera yamaanisha mengi zaidi ya kifo.” Nikiwa kijana mwenye kuamini yote, nilizikubali kama zilivyoonekana kijuu-juu.

Lakini hata katika miaka hiyo ya mapema, kulikuwako upande usiopendeza wa utawala wa Nazi. Asubuhi moja katika Novemba 1938, niliona sinagogi la Kiyahudi likichomeka. Jambo la ajabu ni kwamba, walikuwako wazima-moto waliosimama kulizunguka, lakini hawakufanya lolote kuuzima moto huo. Siku iyo hiyo jumba kuu lenye maduka lilikuwa limejaa vioo vilivyovunjika. Maduka ya Wayahudi yalikuwa yameporwa na kuharibiwa wakati wa kile ambacho baadaye kilikuja kuitwa Kristallnacht (Usiku Mwangavu). Vitendo hivyo vilikuwa vimepangwa na SS viwe “maandamano ya hiari” ya wengi ya kupinga Wayahudi. Chuki kwa Wayahudi ilihubiriwa kila mahali.

Fungu Langu Katika Vita ya Ulimwengu 2

Nilipokuwa na miaka 16, nilisikia tangazo la redio lililotangulia mabaya katika Septemba 1, 1939: Vikosi vya Ujerumani vilikuwa vimevuka mpaka wa Poland. Kuvamia Poland kulikuwa kumeanza, na Vita ya Ulimwengu 2 ilikuwa imelipuka.

Uanagenzi (kujifunza kazi) wangu ulipokamilika, niliingia kwenye jeshi la Ujerumani. Baada ya mazoezi yangu ya kwanza, nilipelekwa Poland ambako nilishuhudia kuteketezwa kwa kijiji chenye vibanda ovyo-ovyo cha Kiyahudi cha Warsaw. Niliona magari-moshi yaliyopakiwa watu wenye hali mbaya, wakielekea kwenye kambi za mateso zenye kuogofya. Jambo fulani lilionekana kuwa baya sana, lakini nikaondolea mbali shaka hizo. Ningali nilitumainia hekima isiyokosea ya Führer.

Upesi baada ya Ujerumani kuvamia Soviet Union, nilipelekwa kwenye mkoa wa Caucasus. Jinsi ilivyosikitisha kuona eneo lenye kupendeza hivyo likilowa na damu ya vita! Kisha kikaja kipupwe chenye kuogofya cha 1942-43, ambacho jeshi la Ujerumani lilikuwa kwa ujumla halijajitayarishia. Hata hatukuweza kuzika wenzetu waliokufa katika mchanga uliogandishwa na barafu. Kipupwe hicho kilisimamisha kusonga kwetu—pigano la Stalingrad halikufua dafu; jeshi zima lilikuwa limepotezwa. Ijapokuwa propaganda ya Hitler ilieleza kurudi nyuma huko kuwa mwimarisho wa “mipaka salama,” sisi askari-jeshi tulitaka tu kurudi nyumbani kwa hali nzuri zaidi ambayo tungeweza. Uhalisi mbalimbali wenye kugutua sana wa vita mwishowe ukanisadikisha kwamba ndoto za makuu za Hitler zilikuwa kisingizio tu.

Wakati wa kurudi nyuma kutoka U.S.S.R., nilipigwa na kipande cha marisau. Kilisababisha jeraha baya la kifuani, nami nikapelekwa kwenye hospitali ya kijeshi. Huko, nilionana kinagaubaga na matokeo yenye kusikitisha sana ya vita: askari-jeshi waliokatwa-katwa, kukosa tumaini, na ubatili mtupu wa yote hayo. Mawazo yangu yalirudi kwenye yule ndege-chiriku aliyekufa. Je! kweli kulikuwako tofauti yoyote kati ya watu na wanyama?

Mimi nilikuwa mmoja wa wale ambao mambo yaliwaendea vizuri. Nilipata nafuu majeraha yangu na pia nikatoka vitani nikiwa hai. Mwishoni mwa vita hiyo, nilipelekwa kwenye kambi ya Kifaransa ya wafungwa wa vita, lakini mwishowe niliweza kurudia familia yangu, wote wakiwa waliiokoka miaka hiyo mibaya sana.

Mtazamo Wangu Ulibadilishwa kwa Umilele

Wakati mrefu ambao sikuwapo, wazazi wangu na ndugu yangu walikuwa wamekuwa Mashahidi wa Yehova, kwa hiyo muda si muda tukawa tumezama katika mazungumzo marefu juu ya dini. Singeweza kuamini katika Mungu ambaye aliruhusu uovu na mteseko mwingi hivyo. Sisi askari-jeshi Wajerumani tulikuwa tumevaa mkanda wenye kishikio kilichoandikwa “Mungu pamoja nasi.” Lakini, Mungu alikuwa amekuwa wapi tulipokuwa tukiteseka na kufa? nikauliza. Makasisi walikuwa wametuhakikishia kwamba Hitler alikuwa ni zawadi kutoka kwa Mungu, lakini kwa sababu yake nchi yetu ilikuwa mabomoko.

Akitumia Biblia kuwa msingi wa maelezo yake, baba yangu alinionyesha kwa subira ni kwa nini tulikuwa tukiishi katika nyakati kama hizo zenye kujaribu. Alinisaidia kuelewa kwamba Mungu haungi mkono upande wowote katika vita vya watu na kwamba karibuni sana Yeye ‘atavikomesha vita hata mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9) Alinionyesha kutoka Maandiko kwamba kwa habari ya kifo chenyewe, “mwanadamu hana kitu cha kumpita mnyama.”—Mhubiri 3:19.

Jumapili iliyofuata, wazazi wangu walinialika niambatane nao kwenye hotuba ya watu wote iliyodhaminiwa na Mashahidi wa Yehova. Sitasahau kamwe siku hiyo. Mkutano huo ulifanywa katika shule ambayo mabenchi madogo yalitumiwa kuwa viti. Sikuwa na tamaa ya kurudi shuleni, lakini mimi huyo, nimeketi miguu yangu mirefu ikiwa imekunjwa chini ya moja ya mabenchi hayo madogo. Lakini hotuba iliyotolewa ilikuwa yenye kupendeza sana hivi kwamba ikanifanya nisahau ukosefu wangu wa starehe. Wakati wa saa ya pili, niliona kwamba wasikilizaji wote walikuwa wakishiriki kwa bidii katika mfikirio wa habari ya Biblia, wakitoa majibu kwa maswali yaliyotokezwa na kiongozi wa mkutano huo.

Mkutano ulipomalizika, wengi wa wale waliokuwapo walikuja kunikaribisha. Urafiki huo wa moyo mweupe ulinivutia mno. Mimi nilikuwa navuta sigareti sana, kwa hiyo uhakika wa kwamba hakuna mtu aliyevuta sigareti ulinitukia mara moja.

Tangu siku hiyo na kuendelea, nilienda kwenye mikutano yote ya Mashahidi na hata nilitoa maelezo yangu mwenyewe. Mwishowe, mambo yalikuwa yakianza kunielea. Nikatambua kwamba Mungu hakuwa wa kulaumiwa kwa ajili ya umwagaji damu wote wa Vita ya Ulimwengu 2. Nilijifunza kwamba lilikuwa ni kusudi lake kusimamisha paradiso ya duniani pote pamoja na baraka za milele kwa ajili ya ainabinadamu watiifu. Na nilikuwa na mahali pangu katika kusudi hilo la kimungu kama ningetamani hivyo.

Hakika huo ulikuwa ujumbe uliostahili kujulishwa watu. Hitler alikuwa amejigamba juu ya “Utawala wa Miaka Elfu Moja” wake lakini alikuwa ametawala kwa 12—na yenye matokeo ya kutisha kama nini! Ni Kristo wala si Hitler, au, si mtawala mwingineye wa kibinadamu yeyote, ndiye anayeweza na ndiye atakayesimamisha utawala wa miaka elfu moja juu ya dunia, aondoe namna zote za uovu zinazotesa ainabinadamu.—Ufunuo 20:4.

Tumaini hilo la ajabu lilinisisimua sana, nami nikawa siwezi kusubiri kuwaambia rafiki zangu juu ya mambo hayo. Hatimaye nilikuwa nimepata maana halisi ya maisha. Bila shaka, nilipaswa kuacha kuvuta sigareti kwanza, jambo ambalo halikuwa rahisi kwangu kamwe. Lakini niliweka tarehe, na tangu siku hiyo na kuendelea, nilikataa kujichafua na tumbako. Nilitambua kwamba nikiwa mhudumu wa Mungu, nilitakwa nijiepushe na “uchafu wote wa mwili na roho.”—2 Wakorintho 7:1.

Utumishi wa Betheli wa Wakati Wote

Baada ya wakfu na ubatizo wangu, upesi nikaanza kufanya kazi nikiwa mhudumu wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova, pamoja na ndugu yangu. Tulimaliza kazi yetu ya kimwili adhuhuri, na kisha tungesafiri kwa baiskeli kwenye eneo ambalo tulikuwa tuhubiri. Ijapokuwa tulikuwa karibu hatuna vitabu vyovyote katika miaka hiyo ya mapema ya baada ya vita, tulitunza vizuri zaidi tulivyoweza upendezi tuliopata, tukiacha magazeti, vitabu, au broshua kwa muda fulani ili kwamba watu wengi iwezekanayvo waweze kufaidika na ujumbe huo. Lakini upesi hali hiyo ingekuja kubadilika.

Ndugu Nathan H. Knorr, ambaye wakati huo alikuwa msimamizi wa Watch Tower Society, alikuwa ametoka tu kutembelea Ujerumani na alikuwa ameona uhitaji wa vitabu zaidi. Upesi upakizi wa kwanza uliwasili kutoka Brooklyn, jambo ambalo lilimaanisha kazi ya ziada kwenye ofisi ya tawi katika Ujerumani yenye kugawanya vitabu hivyo kwa makundi yote. Siku moja ndugu yangu nami tulipokea simu ya barua ikisema: “Njoni bila kukawia kwenye Nyumba ya Biblia [Betheli].”

Nakumbuka nikieleza ndugu yangu kwamba mgawo huo ungetupa sisi nafasi ya kujifunza Biblia karibu siku nzima. Lakini mawazo hayo yenye kosa juu ya Betheli yaliondolewa upesi tulipoambiwa baada ya kuwasili: “Twahitaji mmoja kwa ajili ya matbaa na mwingine kwa ajili ya Idara ya Upakizi! Kwa hiyo tafadhali fikirieni jambo hilo, na kisha mwamue ni nani atakayejitolea kazi ipi.” Ikawa mimi nitafanya kazi katika Idara ya Upakizi, na ndugu yangu katika matbaa.

Katika siku hizo zenye shughuli, wakati wetu wa kusoma Biblia ulikuwa umepunguzwa sana. Nyakati nyingine tulifanya kazi mchana na usiku ili tupeleke vitabu vyote kwenye makundi kwa wakati unaofaa. Hata hivyo, ushirikiano pamoja na ndugu waaminifu, kama vile Erich Frost, Konrad Franke, na August Peters, wote ambao walikuwa wametumia miaka mingi katika kambi za mateso, ulichangia sana ukuzi wetu wa kiroho.

Katika idara ambayo nilifanya kazi, kulikuwako dada mchanga, Magdalena Kusserow. Alikuwa amevumilia miaka minne katika kambi ya mateso kwa ajili ya kukataa kutoa salamu ya “Wokovu una Hitler!” ambapo mimi nilikuwa nimepelekwa kwenye kambi ya wafungwa wa vita kwa ajili ya kupigania wazo hilo kimakosa. Hata hivyo, ukweli wa Neno la Mungu ulikuwa umetuleta pamoja. Tulikuwa na miradi ile ile, nasi tukaamua tulitaka kutumikia Mungu pamoja.a

Jiko la Gari-Moshi la Kutumia Mvuke

Baada ya ndoa yetu, tulikuwa na tamaa ya kuendelea na utumishi wa wakati wote, tukijua kwamba kulikuwako kazi nyingi sana ya kufanya. Nasi tulibarikiwa na migawo mingi yenye kupendeza. Kwa kielelezo, katika 1951, nilipewa mgawo wa kusimamia Idara ya Chakula kwa ajili ya mkusanyiko wa siku tatu katika Frankfurt am Main, ambako tulipanga kulisha wajumbe 35,000.

Mbele yetu kulikuwa na kazi kubwa mno—kutayarisha vyakula moto kwa ajili ya hesabu kubwa hivyo, tukiwa na vyombo vichache sana. Lakini tukapata wazo la kutumia mabirika makubwa ya mvuke 51, ambayo yangeweza kupashwa joto na gari-moshi lenye kutumia mvuke. Tungepata wapi gari-moshi? Mwishowe tulisadikisha kampuni ya reli ituazime moja lao, na shirika moja katika Frankfurt am Main likatuundia vali za msongo wa chini. Hilo lilimaanisha kwamba gari-moshi hilo lingeweza kutoa mvuke wa msongo ule unaofaa kupikia.

Jinsi sote tulivyotulizwa moyo wakati jaribio katika siku iliyotangulia mkusanyiko lilipothibitika kufanikiwa sana! Kulikuwako ripoti nyingi za magazeti zikieleza “uvumbuzi mpya” huo wa kulishia watu wengi, zikiambatana na picha za jiko letu na gari-moshi hilo. Kwa njia hiyo, msambazo wa habari za sifa ulitolewa kwa “Ibada Safi” kusanyiko, ambako mwishowe hudhurio lilifikia zaidi ya 47,000.

Nilipokuwa ningali kwenye mkusanyiko huo, nilipokea mwaliko wa kutumika nikiwa mwakilishi asafiriye wa Watch Tower Society. Nikiandamana na mke wangu, kwanza nilitumikia katika kazi ya mzunguko, nikitembelea kundi tofauti kila juma, na kisha katika kazi ya wilaya, nikitembelea mizunguko mizima-mizima kwenye makusanyiko. Lilikuwa pendeleo kama nini kutumikia pamoja na ndugu kama Martin Poetzinger (ambaye baadaye alikuja kuwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza), H. Dickmann, na R. Kelsey. Tulijifunza mengi mno kutoka kwa ndugu hawa waliokomaa. Mwisho wa kila siku tuliyotumia pamoja nao ulikuwa baraka kwa sababu kila mmoja wao alikuwa na msaada tofauti wa kutoa.

Utumishi wa Misionari Katika Afrika na Hispania

Katika 1961, nilipata pendeleo la kuhudhuria Watchtower Bible School of Gilead katika Brooklyn, Yew York, katika darasa lililokuwa hasa la ndugu na ambalo lilichukua miezi kumi. Wakati huo, mke wangu, ambaye hangeweza kuambatana nami, alibaki Ujerumani. Ijapokuwa tulikuwa tumetengana, tulibadilishana mambo yetu yaliyoonwa katika barua zetu nyingi, kwa hiyo wakati ulipita mbio.

Mgawo wetu wa misionari ulikuwa ni Togo, nchi ndogo katika Afrika Magharibi. Huko tulipaswa kujifunza lugha mpya, Ewe, ili tufikie mioyo ya watu wa bara hilo. Jitihada hiyo ilistahili. Kwa watu walio wakaribishaji-wageni wa Togo, mgeni yeyote ni rafiki, lakini ikiwa anazungumza lugha yao, wao humwona kuwa ndugu yao.

Mara baada ya kuwasili katika Togo, nilianza kuongoza funzo la Biblia pamoja na kijana Mwafrika mmoja anayeitwa Abraham, ambaye alizungumza Kiingereza kidogo. Baada ya muda usio mrefu alikuwa akiambatana nami katika utendaji wa kuhubiri, naye akathibitika kuwa msaada mkubwa katika kunisaidia nieleze watu wasemao Ewe ujumbe wa Biblia.

Pia tulitumia vizuri kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana, ambacho kilikuwa na picha nyingi na kilifaa kwa kuongozea mafunzo ya Biblia. Hata hivyo, mawazo fulani yalikuwa magumu kueleweka na watu wa kawaida wa mashambani. Wangewezaje kuelewa hesabu 144,000 inayotajwa katika Ufunuo sura 7, hali wao walizoeleana na sarafu za faranga 25, 50, au, zikiwa nyingi zaidi, 100? Mwenzangu alikuwa stadi wa kutumia vidole vyake vya mikono, na ikiwa lazima vidole vyake vya miguu pia, ili kushinda tatizo hilo. Na katika pindi nyingi, tulichora katika mchanga.

Tulihuzunika sana wakati, kwa sababu ya matatizo ya afya, tulipolazimika kurejea Ulaya, kwanza Luxembourg na kisha Ujerumani. Lakini roho ya umisionari ilikuwa ingali mioyoni mwetu, na baada ya muda mfupi, tulifikiria kuhamia mahali ambako uhitaji ulikuwa mkubwa zaidi—Hispania.

Baada ya kujifunza lugha nyingine, kwa mara nyingine tulipata pendeleo la kutumikia ndugu zetu wa kiroho katika kazi ya mzunguko na kutumia mwaka mmoja kwenye kituo cha ujenzi wa Makao ya Betheli mapya karibu na Madrid. Imeridhisha sana kwa Magdalena nami kutumikia hapa Hispania. Ijapokuwa hatuna nguvu tulizokuwa nazo hapo mbele, maisha zetu ni zenye maana kwa sababu twaendelea kujifunza, na twaendelea kushiriki pamoja na wengine yale ambayo tumejifunza.

Nikitazama nyuma, naweza kusema kwamba kutafuta kwangu maana ya maisha kulithawabishwa sana. Niliona ujinga wa kutumaini binadamu kama Hitler, na mara tu nilipojua kweli ya Biblia, nilijiweka wakfu kwa Mungu. Lo! hilo limenipa uradhi kama nini! Sasa najua kwamba uhitaji wangu wa wakati ujao si lazima uwe kama wa yule ndege-chiriku aliyekufa. Nina tumaini la uhai wenye maana ambao hautapata kukatishwa kamwe!—Ufunuo 21:1-4.

[Maelezo ya Chini]

a Hadithi ya maisha ya Magdalena Kusserow Reuter ilitokea katika toleo la Septemba 1, 1985 la Mnara wa Mlinzi.

[Picha katika ukurasa wa 18]

Georg na Magdalena Reuter katika Hispania

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki