Maoni ya Biblia
“Kwa Nini Mungu Alichukua Mtoto Wangu?”
KIFO cha mtoto huwa ni kumbo kubwa kwa mzazi yeyote. Huwa ni ono kali sana ambalo maneno tu hayawezi kulifuta. Lakini ikiwa ulipoteza mtoto na unashangaa ni kwa sababu gani Mungu alichukua mtoto wako, basi unajitaabisha chini ya uelewevu mbaya ambao waweza kukuongezea tu uguo lako. Unahitaji kujua ukweli huu: Mungu hakuchukua mtoto wako.
Na bado, wengi wanaamini kinyume cha jambo hilo. Kwa mfano, mwanamke mmoja ambaye hangeweza kutulizwa alikodolea macho jeneza lililofunguliwa; mle ndani mlikuwa na mvulana wake mwenye umri wa miaka 17, nywele zake zilikuwa nyembamba kwa sababu ya matibabu yaliyoshindwa kutibu ugonjwa wake wa kansa. Alimgeukia mgeni mmoja na kusema kwa sauti yenye hofu hivi: “Mungu alimtaka Tommy awe pamoja Naye mbinguni.” Akiwa Mkatoliki wa Roma, hilo ndilo jambo alilojifunza kwa kuenda kwake kanisani kwa miaka mingi. Waprotestanti pia wamemlaumu Mungu kwa muda mrefu kwa ajili ya vifo vya watoto. Mrekebishaji Mprotestanti anayejulikana sana John Calvin aliomboleza hivi baada ya mtoto wake mwanamume mwenye umri wa majuma mawaili kufa: “Bwana ametujeruhi kwa jeraha kali katika kifo cha mwana wetu mchanga.”
Kulingana na hekaya moja ya kikale ya Wayahudi, wana mapacha wa rabi mmoja walikufa alipokuwa hayupo. Aliporudi na kuuliza juu ya wana wake, mke wake alisema: “Ikiwa uliazimwa vito viwili vya thamani na kuambiwa kwamba ungevifurahia muda ule ambao ungekuwa navyo, je! ungeweza kubishana ikiwa aliyekuazima vito hivyo auliza virudishwe?” Yeye akajibu: “La hasha!” Basi akamwonyesha wana wawili wake waliokufa na kusema kwa usahili hivi: “Mungu alivitaka vito vyake vimrudie.”
Halifariji Wala si la Kimaandiko
Je! Muumba kweli kweli ni mkatili hivi kwamba angepangia kuua watoto, huku akijua wazi kwamba kitendo hicho huvunja moyo wa wazazi? La, si Mungu wa Biblia; kulingana na 1 Yohana 4:8, “Mungu ni upendo.” Ona kwamba haisemi ya kuwa Mungu ana upendo au kwamba Mungu anapenda bali kwamba Mungu ni upendo. Upendo wa Mungu wenye kina kirefu sana, wenye utakato kweli kweli, wenye ukamilifu kabisa, unaonyeshwa kweli kweli na utu wake na matendo, hivi kwamba kwa kufaa angeweza kusemwa kuwa wonyesho wa upendo. Huyo si Mungu auaye watoto eti ‘kwa sababu anataka vito vyake virudishwe.’
Kinyume cha jambo hilo, Mungu hupenda watoto sana na tena bila ubinafsi. Yesu Kristo, ambaye kila neno lake na tendo lilionyesha utu wa Babake wa kimbingu, alikuwa na upendezi wenye uchangamfu kwa watoto. Pindi moja alimzungushia mtoto mdogo mkono wake na kufundisha wafuasi wake kwamba iliwapasa kuwa na unyofu na unyenyekevu kama wa watoto. (Mathayo 18:1-4; Marko 9:36) Karne kadhaa zilizotangulia, Yehova alikuwa amefundisha watu wake kuwaona watoto wao kuwa wa thamani na kuwazoeza, kuwafundisha, na kuwatunza kwa njia iliyofaa. (Kumbukumbu 6:6, 7; Zaburi 127:3-5) Yeye ataka familia ziungane katika uhai, siyo katika kifo.
“Basi kwa Nini Mtoto Wangu Alikufa?”
Wengi wanahisi kwamba kwa sababu Mungu ni mweza yote, ni lazima iwe ni yeye anayeongoza chochote kinachotendeka ulimwengu, kutia ndani vifo vya watoto. Lakini si lazima iwe hivyo. Wakati Ayubu alipopoteza watoto wake wote kumi katika msiba mmoja, alifikiria kwamba Yehova ndiye aliyeleta msiba huo mbaya sana kwake. Hakujua yale Biblia inatufunulia, kwamba mwenye uwezo zaidi ya binadamu apingaye Mungu ambaye anaitwa Shetani, ndiye kwa kweli aliyekuwa akiongoza mambo yaliyokuwa yakimpata, akijaribu kumtesa Ayubu akane imani yake kwa Muumba. Ayubu 1:6-12.
Kwa njia iyo hiyo, watu wengi leo hawana habari juu ya mweneo wa uvutano wa Shetani juu ya ulimwengu. Biblia yafunua kwamba Shetani, wala si Yehova, ndiye mtawala wa mfumo huu mbovu wa mambo. Ni kama vile 1 Yohana 5:19 inavyosema: ‘Dunia yote hukaa katika yule mwovu.’ Yehova hapaswi kulaumiwa kwa matukio yenye misiba ya ulimwengu huu. Yeye hakuchukua mtoto wako.
Basi je, jambo hilo linamaanisha kwamba ni Shetani aliyechukua mtoto wako? Si moja kwa moja, la. Kule nyuma katika Edeni, binadamu alijiweka chini ya utawala wa Shetani wakati mtu huyo alipoasi dhidi ya Mungu. Hivyo alipoteza zawadi ya uhai wa milele yenye afya nzuri kwake mwenyewe na kwa watoto wake wote. (Warumi 5:12) Matokeo yakawa kwamba, twaishi katika mfumo wa ulimwengu uliotenganishwa na Mungu, ulimwengu ambao ni lazima tukabiliane na kile Biblia inachokiita “wakati na tukio lisilotazamiwa,” matukio ya ghafula ya maisha yasiyotazamiwa na ambayo mara nyingi ni yenye msiba. (Mhubiri 9:11, NW) Shetani ‘anadanganya ulimwengu wote.’ (Ufunuo 12:9) Pendezi lake kuu ni kugeuza watu kutoka kwa Mungu. Hivyo anaeneza uwongo mbaya kweli kweli juu ya Mungu. Mojawapo ya uwongo huo ni kwamba Mungu anatumia kifo kunyakua watoto kutoka kwa wazazi wao.
“Kuna Tumaini Gani kwa Mtoto Wangu?”
Badala ya kumlaumu Mungu, wazazi waliofiwa wapaswa kuangalia faraja ambayo Mungu anatoa katika Biblia. Dini bandia imewacha wengi wakihangaika juu ya walikokwenda na hali ya watoto wao walio kufa. Mbinguni, helo, pargaroti, Limbo— sehemu hizo zinazodhaniwa kuwa wanaenda zinaanzia zile ambazo hazieleweki hadi zile za kuogofya. Biblia, kwa upande mwingine inatuambia kwamba wafu wako katika hali ya kutokuwa na ufahamu, hali iwezayo kulinganishwa bora zaidi na usingizi. (Mhubiri 9:5, 10; Yohana 11:11-14) Hivyo, wazazi hawahitaji kuhangaikia kile watoto wao watapitia baada ya kifo, kama ilivyo na wakimwona akiwa amelala usingizi mzito. Yesu alizungumzia wakati ambapo ‘watu wote waliomo makaburini wangetoka’ kwa uhai mpya tena katika paradiso duniani.—Yohana 5:28, 29; Luka 23:43
Ni kweli, tumaini hilo jangavu halitoi msiba wote wa kifo. Yesu mwenyewe alilia kwa kifo cha rafiki yake Lazaro—na hilo lilikuwa tu dakika chache kabla ya yeye kumfufua! Angalau basi, kifo huwa si ndio mwisho. Yesu na Baba yake, Yehova, wote wanachukia kifo. Biblia inakiita kuwa “adui wa mwisho” na inasema kwamba ‘kitabatilishwa.’ (1 Wakorintho 15:26) Katika paradiso inayokuja, wakati ambapo utawala wa Shetani utakuwa jambo lililopita, kifo kitatoweka milele. Wadhulumiwa wacho wasio na hatia watarudishwa kwa kufufuliwa. Basi, wakati wazazi watakapoungana tena na watoto waliopoteza katika kifo, ndipo tutakapoweza kusema, “ewe mauti, ya wapi mapigo yako?”—Hosea 13:14.