Vijana Wanauliza . . .
Kwa Nini Wazazi Wangu Wanajaribu Kuongoza Maisha Yangu?
“Natafuta nafasi ya kutenda yale nitakayo, kuzoeza misuli yangu, kuhisi uwezo wangu. . . . Nataka kujua machungu kutoka kwa mazuri kwa kuonja, si kuambiwa. Nina njaa ya maarifa; [wazazi wangu] wananijaza maelezo.”—Mvulana wa umri wa miaka 16.
“Tunahitilafiana kabisa na mama yangu . . . Anajaribu kunifanya mtoto . . . nataka kuondoka zangu; Siwezi kuvumilia kuwa kama mfungwa. . . . Najaribu kukua na ananizuia.”—Msichana wa umri wa miaka 17.
NI LALAMIKO la kawaida miongoni mwa vijana kwamba wazazi wao wanajaribu kuongoza maisha yao. Na labda wewe mwenyewe una majonzi kama hayo. Unapoendelea kuchelewa nje; wanasema lazima uwe nyumbani mapema. Unasema uko tayari kuanzisha matembezi ya wavulana na wasichana; wanasema ungali mchanga. Yaonekana kila ‘Je, naweza’ inajibiwa na ‘La huwezi.’
Ingawaje, kwa kuwa wenye haki kwa wazazi, angalau vijana wengi wanaruhusiwa kufanya wanavyotaka wakati mwingine. Na huenda ikawa wewe ni mmoja wao. Zaidi ya hilo, wazazi wako labda wanajua kwamba wewe sasa si mtoto tena; upesi au baadaye wataanza kuachilia mwongozo ambao wamekuwa nao tangu uzaliwe. Na kama ilivyo na wazazi wengi, labda wanataka uwe mwenye usawaziko na mtu mzima mwenye kujitegemea.
Huenda ukajiuliza, basi: ‘Ikiwa wazazi wangu wanahisi hivi, kwa nini hawaonyeshi hilo?’ Inaonekana kwako kwamba wamekaba maisha yako na hawaonyeshi dalili ya kukuachilia. Kweli, hata hivyo, labda kuna swali dogo la kama utaweza kuongoza maisha yako. Swali lenyewe ni lini. Unataka hilo sasa. Lakini wazazi wako huenda wakataka uupate polepole.
Tineja mmoja alikuona kama “kutotumainiwa” na wazazi wake, jambo lililoumiza na lililoonyesha kwamba ana “mwelekeo wa kujiangamiza ambao ulikuwa ni lazima udhibitiwe.” Lakini yawezekana kwamba wazazi wako wana sababu nzuri ya kufanya hivyo? Kwa vyovyote, kuelewa maoni yao huenda kukakusaidia ukomeshe hisi zozote za chuki ambazo huenda ukawa nazo kwa sababu ya jinsi wakutendeavyo. Kama vile Mithali 19:11 inavyosema: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake.”
Sababu Wanatoa Uongozi
Kwanza, tambua kwamba ulimwengu umeendelea kuwa hatari zaidi na kufisidika zaidi tangu wazazi wako waupitie katika ujana wao. (2 Timotheo 3:1, 13) Mzazi mmoja alikubali: ‘Ulimwengu ambao mwana au binti yetu anapitia akiwa na miaka 14 au 15 au 16 ni wenye hatari sana kuliko wakati tulipokua sisi. Kutembea ukiwa peke yako ni hatari zaidi. Matineja wengi wanapata mimba kuliko wakati tulipokuwa wachanga.’ Si ajabu wazazi wako wanataka kukulinda!
Ikiwa wazazi wako ni wenye kuhofu Mungu, wanahangaikia kwa uzito hali yako ya kiroho pia. Biblia yaeleza kwamba wazazi wawape watoto wao “agizo na rekebisho, ambalo ni la malezi ya Kikristo.” (Waefeso 6:4, The New English Bible) Na wanajua kwamba hautashikilia thamani na itikadi za Kikristo kwa sababu tu wao wanafanya hivyo. Wanatambua pia kwamba “mwana [au binti] aliyeachiliwa humwaibisha mama yake.” (Mithali 29:15) Ingawa huenda wasikuone kuwa mtoto, huenda bado wakahisi wana daraka la kukuwekea mipaka ya saa za kurudi nyumbani na mipaka mingineyo.
Unaweza kuona vizuizi hivyo kana kwamba vinakushushia heshima, kukufanya mtoto. Lakini kumbuka, si muda mrefu uliopita kwamba ulikuwa mtoto asiyejiweza mikononi mwa wazazi wako. Na sasa wanataka kukulinda kutokana na madhara ya kiadili, kama vile walivyokulinda kutokana na madhara ya kimwili. Kumbuka tena, wazazi wako waliwahi kuwa matineja, na wanajua magumu ambayo kijana anaweza kupitia. Naam, hata mwanamume mwadilifu Ayubu alikiri “maovu ya ujana [wake].” (Ayubu 13:26) Na kama vile vijana, wazazi wengine walifanya makosa mazito ambayo yametatanisha maisha kweli kweli.
Mama mmoja alikiri: “Ilinilazimu niolewe. Ni kwa sababu nilikuwa na rafiki mvulana nikiwa na umri mchanga sana. Nikapata mimba nikiwa na miaka 16. Sasa nina watoto watatu, na wawili ni matineja. Nahisi nikiwa kama mwenye miaka hamsini badala ya thelathini na saba. Nilipoteza ujana wangu.”
Labda wazazi wako hawakuwahi kupatwa kamwe na jambo lenye kutia uchungu kama hilo. Hata hivyo, wanajali sana hatari za mapema za matembezi ya wavulana na wasichana na huenda wakakukataza kufanya hilo. Je! uudhike kwa ajili ya sharti hilo? Ikiwa ndivyo, fikiria maneno ya Mithali 27:12: “Mwenye busara huyaona mabaya na kujificha; bali wajinga huendelea mbele wakaumia.” Kweli, ikiwa utatii shauri la wazazi wako, unaweza kuzuia msiba.
Utu wa Kubadilika
Hata hivyo, waweza kuhisi kama kijana aliyesema: “Najua nifanyalo. Siwezi kuharibu maisha yangu. Kwa nini hawawezi kuniacha niishi maisha yangu mwenyewe?” Lakini shida huenda ikawa kwamba unapatia wazazi wako mchanganyiko wa dalili bila kujua. Wakati mwingine huenda ukatenda kama mtu mzima mwenye akili; wakati mwingine unaonyesha utoto wenye kuhitaji msaada wa mzazi.
Katika kitabu How to Single Parent, Dakt. Fitzhugh Dodson aeleza kisa cha mama mmoja alipokuwa akifanya ununuzi pamoja na binti yake mwenye umri wa miaka 15. Alipochagua marinda matatu, binti huyo akamuuliza lililokuwa zuri kwake. Mama yake alifikiria kidogo halafu akamjibu: “Nafikiri la buluu lapendeza kabisa.” Jibu la ulizo hilo la ushauri lilikuwa nini? “Oh, mama, wewe sikuzote hujaribu kutawala maisha yangu kwa kuniambia la kufanya!”
Miezi kadhaa baadaye walienda kufanya ununuzi tena. Binti huyo alichagua nguo chache na akauliza: “Mama, ni ipi ya hizi inifaayo?” Mama akikumbuka lile jambo la mbeleni, aliamua awe mwangalifu na akajibu: “Nina hakika unaweza kujiamulia mwenyewe,” ambapo binti alisema kwa mshangao: “Oh mama, wewe hunisaidii kamwe ninapokuhitaji!”
Tabia zenye kuyumbayumba kiushupavu na utoto zaweza kutatanisha wazazi. Na kwa kadiri fulani, vijana wote wanasumbuliwa na mwenendo huu; ni sehemu ya asili ya kukua. Lakini hata ikiwa ya asili, inawaambia wazazi wako kwamba bado una “tabia za kitoto” ambazo unapaswa kuziacha na hauko tayari kuwachwa huru.—1 Wakorintho 13:11.
Kupata Uongozi Zaidi
Hata hivyo huenda ukahisi kwamba ingewezekana kwako kutenda bila utegemezo na uangalifu huo. Na ukiwa na matumaini ya kupata uhuru unaotamani, huenda wakati mwingine ukashawishiwa kutumia njia za upotovu. “Najua sipaswi kudanganya,” akaandika msichana tineja, “lakini nilifanya hivyo ili nifanye mambo yawe rahisi. [Mama] ni mkali sana na hawezi kuniacha niende nikisema ukweli.” Hata hivyo, kuwadanganya wazazi wako, hakufanyi kamwe mambo yawe rahisi. Ikiwa uongo utajulikana (na yaelekea itakuwa hivyo), unaweza kuharibu mambo zaidi.
Watungaji wa kitabu Options wanasema kwa hekima: “Kudanganya wazazi wako wakati unataka wakuamini ni kama kuiba na kujaribu kujionyesha jinsi ulivyo mnyofu. Wakati watakapokushika, watakukaba hata zaidi, kwa ajili ya kuwa kwako mdanganyifu.” La maana zaidi, uongo hupatwa na ukosefu wa kibali cha Mungu mwenyewe. Mithali 3:32 husema: “Maana mtu mkaidi ni chukizo kwa BWANA [Yehova, NW].”
Kwa hivyo uwe mnyofu kwa wazazi wako. Wape sababu kamili na sahihi za pale unataka kwenda na ni nani unayeenda naye. Wakiweka masharti, waheshimu. Hilo litawathibitishia kwamba wewe ni mwaminifu. Hawatakuwa na wasiwasi mwingi ukiwa nje. Na kadiri wakati uendeleapo watahisi utumainifu wa kukuongezea uhuru zaidi. Ni kama vile Biblia isemavyo: “Mengi yatatazamiwa yule aliyepewa mengi, naye mtu aliyepewa amana, ndivyo watu watatazamia mengi kutoka kwake.”—Luka 12:48, Phillips.
Wakati wa kuongoza maisha yako mwenyewe utafika upesi. Kwa sasa uwe mwenye subira. Furahia ujana wako. (Mhubiri 11:9) Shirikiana na msimamo ambao wazazi wanachukua kuhusu matembezi ya wavulana na wasichana, sheria, masharti, na kadhalika. Kufanya hivyo sasa kutakuepusha na masikitiko na huzuni ya moyoni baadaye. Ikiwa unahisi kwamba vizuizi vingine havifai kwa umri wako au si vya sababu ya maana, usiasi. Ongea kwa utulivu juu ya mambo hayo pamoja na wazazi wako. Labda utaona kwamba hawaongozi sana maisha yako. Wanataka tu kusalimisha furaha yako ya wakati ujao.
[Picha katika ukurasa wa 14]
Je! unaonaje mipaka ya saa za kurudi nyumbani na mipaka mingineyo?