Maoni ya Biblia
Kuna Kosa Gani Kuwa na Wake Zaidi ya Mmoja?
Matatizo ya Jane yalianza wakati baba yake alipopata kazi katika mji fulani.a Huko, wakiwa mbali na nyumba yao iliyo sehemu ya mashambani ya Afrika, yeye alianza kuishi na mwanamke mwingine. “Maisha hayakuwa rahisi kwetu,” aeleza Jane, “kwa sababu baba yangu hakututegemeza kifedha; yeye alikuwa anategemeza mke wake wa pili pamoja na watoto wake. Katika miaka yangu ya mwisho ya shule, mara nyingi nilienda kulala nikiwa na njaa. Nyumba yetu ilikuwa katika hali mbaya ya ubovu. Katika miisho juma nilijaribu kumsaidia mama yangu kwa kuuza matunda, lakini hatukuweza kulipia gharama za maisha. Nilikuwa ninalia usiku baada ya usiku.”
ONO la Jane laonyesha magumu ambayo ndoa ya wake zaidi ya mmoja mara nyingi hutwisha juu ya wale wasio na hatia. Watu wasemao lugha ya Kivenda kusini mwa Afrika wana jina, muhadzinga, ambalo mke mmoja aweza kumwita mke mwingine katika nyumba yenye wake zaidi ya mmoja. Linatokana na neno linalomaanisha “choma” (kwa moto), ambalo labda linaeleza vizuri magumu ambayo mara nyingi huwa kati ya wake yanayosababishwa na ndoa ya wake zaidi ya mmoja.
‘Lakini,’ huenda ukauliza, ‘je, kuwa na wake zaidi ya mmoja ni kosa? Ikiwa ndivyo, kwa nini watu fulani wanaojulikana sana katika Biblia walikuwa na wake zaidi ya mmoja?’
Kuwa na Wake Zaidi ya Mmoja Katika Biblia
Mungu aliruhusu kuwa na wake zaidi ya mmoja kwa wakati fulani, kwa sababu ilichangia katika kutimizwa kwa ahadi yake kwa Abrahamu: “Nitakufanya wewe kuwa taifa kubwa.” (Mwanzo 12:2; Kutoka 1:7) Kwa wakati huo, mke wa Abrahamu, Sara, alikuwa hana mtoto. Hatimaye, alimwomba Abrahamu azae mtoto kwa mjakazi wake, Hagari. Kwa kupendeza, Biblia inaeleza wazi matatizo ambayo hilo lilileta juu ya nyumba ya Abrahamu.—Mwanzo 16:5, 6; 21:8-10.
Kwa habari ya Yakobo, mjukuu wa Abrahamu, yeye alikusudia kuoa mwanamke mmoja tu, Raheli. (Mwanzo 44:27) Ilikuwa ni mkwe wa Yakobo, Labani, ambaye alimdanganya kuoa binti wawili wa Labani mwenyewe, Raheli na Lea. (Mwanzo 29:21-28) Na ilikuwa ni baada ya Yakobo kuhimizwa na wake hawa kwamba yeye alizaa watoto kwa kulala na vijakazi vyao, Bilha na Zilpa. Tena, Biblia haifichi matatizo mengi yaliyoletwa juu ya nyumba kubwa ya Yakobo kwa kuoa wake zaidi ya mmoja.—Mwanzo 29:30, 31; 30:1-3, 15, 16, 20; 37:2-4; 44:20-29.
Biblia pia inarekodi hadithi ya Elkana, ambaye alikuwa baba ya nabii Samweli, na wake wawili wa Elkana, Hana na Penina. Hana alitendewa bila fadhili na Penina hivi kwamba angelia mara nyingi na kupoteza hamu yake ya kula. Penina, kwa upande wake, inaonekana alikuwa mwenye wivu kwa sababu Elkana alionyesha upendo mwingi zaidi kwa Hana.—1 Samweli 1:4-7.
Kwa hakika, zoea la kuoa wake zaidi ya mmoja limesababisha magumu. Hali likiwa limevumiliwa kati ya watu wa Mungu wa kale, Biblia inaonyesha wazi kama Mungu alikusudia au hakukusudia mwanzoni kwamba mwanadamu aoe wake zaidi ya mmoja.
Kiwango cha Awali cha Mungu
Ili kuelewa kiwango cha Mungu cha ndoa, inatubidi turudi nyuma kwenye mwanzo wenyewe wa historia ya binadamu. Neno la Mungu linaeleza uvutio ambao Adamu alihisi wakati alipojulishwa kwa Hawa, mke wake mmoja aliyekuwa ndipo tu ameumbwa. “Sasa huyu ni mfupa katika mifupa yangu, na nyama katika nyama yangu,” yeye akasema. “Kwa hiyo,” Biblia yaendelea kusema, “mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.”—Mwanzo 2:21-24.
Kwa ndoa za Kikristo, Yesu alirudisha tena kiwango cha awali cha Mungu—kuoa mke mmoja tu. (Mathayo 19:4, 5) Zaidi ya hilo, alionyesha kwamba watu waliooa au kuolewa wapaswa kupatana sasa na takwa hilo la kimungu. Kama vile alivyoeleza: “Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.” (Mathayo 19:6) Hivyo, Mkristo aliyeoa lazima alinde kifungo cha “mwili mmoja” ambacho huwa kati yake na mwenzi wake halali.b Kufanya ngono na mke aliye mtu wa tatu katika ndoa yako kungekuwa ni kuenda kinyume cha mpango huo wa kimungu. Kitendo kama hicho kimekatazwa katika kundi la Kikristo.—1 Wakorintho 5:11; 6:9, 16, 18; Waebrania 13:4.
Huwa si jambo la kushangaza basi, kwamba Maandiko yanataja kwa kupendelea juu ya Wakristo waliooa ambao wana mke mmoja tu. (1 Wakorintho 9:5; 1 Timotheo 3:2) Biblia inaeleza: “Mwanamume na awe na mke wake mwenyewe [si wake], na kila mwanamke na awe na mume wake mwenyewe [si mwanamume ambaye tayari ana mke halali].”—1 Wakorintho 7:2; Mithali 5:18.
Baada ya kujifunza juu ya katazo la Biblia la kuoa wake zaidi ya mmoja, wengine wamechukua hatua za ujasiri kuleta maisha zao kwa upatano na mapenzi ya Mungu. Fikiria John, ambaye anaishi katika mji mmoja katika Afrika ya kati.c Hapo mbeleni alikuwa na wake watatu. Lakini baada ya kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, John alikuja kuwa na uamuzi wa kibinafsi baada ya kuzungumza na wake zake. Baada ya kufanya mipango kwa ajili ya utunzaji wa wakati ujao wa mke wake wa pili na wa tatu pamoja na watoto wao kutokana na ndoa ya kwanza ya wake zaidi ya mmoja, walirudi nyumbani mashambani. Kwa njia hii John alistahili pendeleo la kumtumikia Mungu kwa kushirikiana na kundi lililokuwa karibu. Yeye aliona mibaraka mingine pia.
“Kila usiku,” yeye aeleza, “Nilikuwa nikija nyumbani katika nyumba iliyojaa matatizo. Kwa mfano, mke mmoja angepata kosa katika watoto wa mwingine, na watoto wangechagua upande huu au ule kati yao wenyewe. Jambo la kwanza nililopaswa kufanya ni kunyorosha tatizo hilo. Kwa kuwa sasa nimejifunza kuishi na mke mmoja, nyumba yangu imekuwa mahali pa pumziko na amani.”
Naam, amani na baraka ya Mungu inastahili jitihada zozote.—Warumi 12:1, 2.
[Maelezo ya Chini]
a Jina halisi halikutumiwa.
b The New International Dictionary of New Testament Theology yasema kwamba neno la Kigiriki lililotafsiriwa “mwili mmoja” katika Mathayo 19:5b lina maana ya kipekee kama ile tafsiri ya maneno ya Kiebrania ya Mwanzo 2:24 na humaanisha “ushirikiano kamili wa mwanamume na mwanamke ambao hauwezi kuvunjwa bila ya kuwaumiza washirika wenyewe.”
c Jina halisi halikutumiwa.
[Blabu katika ukurasa wa 23]
“Wivu wa kingono na mabishano ni matatizo ya kawaida kwa familia ya [wake zaidi ya mmoja]; na inambidi mume awe mwenye hekima, mwenye nguvu, msuluhishi, na mwerevu ili adumishe upatano.”—The New Encyclopædia Britannica
[Picha katika ukurasa wa 22]
Mfinyango-udogo wa kikundi cha familia ya Kiafrika; Mume na wake wa Kiigbo
[Hisani]
Courtesy of The British Museum