Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g92 10/8 kur. 14-15
  • Misiba—Adhabu Kutoka kwa Mungu?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Misiba—Adhabu Kutoka kwa Mungu?
  • Amkeni!—1992
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Je! Mungu Mweza Yote Huhukumu Watu Leo?
  • Je! Kuna Masomo Tunayoweza Kujifunza?
  • Je! Kutakuwa na Hukumu ya Mwisho kwa Ainabinadamu?
  • Biblia Inasema Nini Kuhusu Misiba ya Asili?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Misiba ya Asili​—Kwa Nini Imeongezeka Sana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Misiba ya Asili-Je! Mungu Ndiye Huisababisha?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Je, Misiba ya Asili Ni Adhabu Kutoka Kwa Mungu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2008
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1992
g92 10/8 kur. 14-15

Maoni ya Biblia

Misiba—Adhabu Kutoka kwa Mungu?

KATIKA Ufilipino, nchi inayokumbwa mara nyingi na misiba ya asili, watu wengi wamejiuliza, ‘Je! Mungu hujaribu mwanadamu kwa misiba kama hiyo?’ Katika 1991, baada ya mlipuko wa volkeno wenye uharibifu mkubwa zaidi katika karne hii, kichwa kikuu katika gazeti moja la Ufilipino kilikuwa: “Mlipuko: Adhabu kutoka kwa Mungu?”

Mwandikaji safu za magazeti Nelly Favis-Villafuerte alionyesha maoni hayo alipoandika: “Kwa Wakristo wanaoiamini Biblia hata hivyo—kuna elezo moja tu: mlipuko wa volkeno wa Mlima Pinatubo ni tendo la kimungu la kutukumbusha kwa mara nyingine tena kwamba kuna Mungu mwenye enzi kuu mwenye kutia hofu aliye na uwezo wa kupita mwingine wote katika mambo na wakati ujao wa wanadamu na mataifa.” Tukiwa na wazo hilo akilini, sisi tunauliza:

Je! Mungu Mweza Yote Huhukumu Watu Leo?

Uhakika wa kwamba Mungu alifanya hivyo wakati uliopita hauwezi kukanwa. Mifano iliyoandikwa katika Maandiko yaani Furiko la siku ya Nuhu, uharibifu wa Sodoma na Gomora, na visa viwili vya kuchomwa kwa Yerusalemu, jiji lililoshirikishwa na jina lake kuu, yaonyesha kwamba Mungu Mweza Yote aweza kuleta hukumu ya makusudi juu ya wale ambao kwa kurudia-rudia hushindwa kushika viwango vyake.—Mwanzo 7:11, 17-24; 19:24, 25; 2 Mambo ya Nyakati 36:17-21; Mathayo 24:1, 2.

Lakini namna gani leo? Kwamba kungekuwako wakati wa uharibifu wa duniani pote kulitabiriwa na Yesu Kristo katika Mathayo sura ya 24, Marko sura ya 13, na Luka sura ya 21. Katika sura hizo, yeye alitoa maonyo ya kiunabii ya matukio na hali ambazo zingeshirikishwa na mwisho wa mfumo huu wa mambo ili kwamba watu wenye kutumia akili waweze kung’amua kwamba yeye alikuwa anatawala bila kuonekana akiwa mbinguni. Unabii huo mbalimbali unatimizwa leo. Hata hivyo, inapaswa ifahamike kwamba katika kila hukumu iliyotajwa juu, Yehova Mungu alitoa maonyo ya wazi, na ya kurudia-rudia kabla ya uharibifu kuja. (Amosi 3:7) Hata hivyo, kwa habari ya misiba ya asili inayotokea katika wakati wetu, maonyo mara nyingi hutolewa na wenye mamlaka wa kilimwengu, yakitegemea uchunguzi wa kisayansi.

Zaidi ya hilo, mwanafunzi Yakobo anatujulisha katika sura ya kwanza ya barua yake, mstari 13: “Mungu hawezi kujaribiwa na maovu, wala yeye mwenyewe hamjaribu mtu.” Kukiwa na idadi kubwa ya watu ulimwenguni pote inayozidi kuongezeka, mwanadamu amekuja kuishi karibu na mambo mengi yanayoweza kuwa hatari. Uhitaji wa nafasi ya kuishi na ya kukuza vyakula hutokeza kukatwa kwa miti katika sehemu zilizokuwa na misitu, nyakati nyingine hata ikizidisha uharibifu mkubwa wa misiba ya kiasili kutokana na mvua nyingi na mtiririko wa kasi wa maji.

Kwa hiyo, haingekuwa sawa kusema kwamba misiba ya kiasili huletwa moja kwa moja na Mungu Mweza Yote kuwa adhabu kwa watu wanaoishi katika sehemu zilizoathiriwa. Kwa kweli, ni rahisi kuona kwamba wengi wasio na hatia, kama vile watoto wadogo, ndio huteseka zaidi wakati wa shida. Hata hivyo, hata ikiwa Mungu Mweza Yote hasababishi maafa kama hayo, bado huenda tukauliza:

Je! Kuna Masomo Tunayoweza Kujifunza?

Ndiyo. Kwa wale wanaoishi katika sehemu zilizoathiriwa, kuna jaribu la kwamba, wao huchukua mali zao za kimwili kuwa za thamani kadiri gani kwa kulinganisha na uhai wenyewe. Ili kuokoa mali chache, watu wamefanya mambo ya kuhatarisha uhai wao katika misiba kama hiyo. Tunahitaji kukumbuka kwamba Yesu alisema: “Uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.” (Luka 12:15) Mtu aweza kupata vitu vingine vya kimwili, lakini hakuna mwanadamu anayeweza kupata uhai wake tena baada ya kuupoteza.—Mathayo 6:19, 20, 25-34.

Misiba ya kiasili pia hufanya watu mmoja mmoja wafikirie jinsi wanavyoishi. Mtume Paulo aliwahimiza Wakristo wawe waangalifu kwa namna wanavyojiendesha: “Kwa hiyo chunguzeni kwa makini jinsi mnavyotembea, si kama wasio na hekima bali kama wenye hekima, mkiwezana na mkasa kadiri mwezavyo, kwa sababu siku ni zenye uovu.” (Waefeso 5:15, 16, Byington) Kila jaribu ambalo mtu hukabiliana nalo maishani ni kikumbusha cha jinsi lilivyo jambo la maana kuwa na imani yenye nguvu.

Somo la tatu tunalojifunza kutokana na misiba ya asili ni kwamba tunahitaji kukuza zaidi hisia-mwenzi, au huruma, kwa wengine. Katika sehemu ya msiba, mtu anahitaji kuonyesha hangaiko la upendo kwa wenzake wanaoteseka badala ya kuwa na mwelekeo kwamba kila mtu na ajisaidie. Hasa hilo ni kweli kwa wale wenye madaraka ya kuwatunza wengine. Nabii Isaya alieleza watu aliowaita “wakuu” kuwa “kama mahali pa kujificha na upepo, na mahali pa kujisitiri na dhoruba; kama mito ya maji mahali pakavu, kama kivuli cha mwamba mkubwa katika nchi yenye uchovu.”—Isaya 32:1, 2.

Katika kuonyesha huruma wakati wa misiba, kuna pindi nyingi za kushiriki na wengine yale ambayo mtu anayo, kwa maneno na matendo pia. Kwa mfano, mlipuko wa volkeno wa Mlima Pinatubo na misiba iliyofuata ilitoa fursa zisizohesabika za kushiriki katika kusaidia wale waliolazimika kukimbia msiba huo. Wengi hata hawakuwa na chakula cha kila siku. Hivyo, watu mmoja mmoja waliweza kuonyesha kuwa si wenye ubinafsi kwa kutoa msaada kwa wengine. Hata hivyo, wengi bado wamejiuliza:

Je! Kutakuwa na Hukumu ya Mwisho kwa Ainabinadamu?

Ndiyo, kutakuwako, kama inavyoonyeshwa wazi katika Neno la Mungu. (Mathayo 24:37-42; 2 Petro 3:5-7) Kabla ya hukumu hiyo kuja, kazi ya kuonya ya ulimwenguni pote ni lazima ifanywe, kama vile Yesu alivyotoa unabii zaidi: “Na sharti Injili [habari njema, NW] ihubiriwe kwanza katika mataifa yote.”—Marko 13:10.

Hivyo, kila mmoja wetu anahitaji kujiuliza, ‘Mimi nitafanya nini?’ Tunakuhimiza utumie wakati kuchunguza yale ambayo Biblia hututia moyo kila mmoja wetu kufanya ili tuokoke msiba huo wa tufeni pote.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki