Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 1/22 kur. 15-17
  • Naweza Kuachaje Kunywa Kileo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Naweza Kuachaje Kunywa Kileo?
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kushinda Tatizo la Kukana
  • Sitawisha Azimio la Kuacha
  • Pata Msaada
  • Tafuta Marafiki Wapya
  • Unaweza Kuacha Kunywa Kileo!
  • Mtazamo Unaofaa Kuhusu Pombe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2010
  • Fuata Mwongozo wa Mungu Kuhusu Kileo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Je! Unywaji Waweza Kunifanya Niwe Mzoevu Kweli?
    Amkeni!—1993
  • Wakristo Wanapaswa Kuwa na Maoni Gani Kuhusu Kileo?
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 1/22 kur. 15-17

Vijana Wanauliza . . .

Naweza Kuachaje Kunywa Kileo?

“Sikuzote nilihisi vibaya kesho yake, kihisiamoyo na kiroho pia!”—Bob.

“Nilikuwa matatani daima nyumbani, shuleni, pamoja na marafiki na polisi!”—Jerome.

BOB na Jerome wote wawili walilipa bei kwa kunywa kileo kingi mno na kwa mara nyingi mno. Wote wawili wakawa wazoevu wa kileo. Na ingawa Bob hatimaye aliweza kuacha kunywa kabisa, Jerome angali anajaribu kushinda uzoevu wa kileo.

Uzoevu wa kileo ni tatizo linalokua miongoni mwa vijana katika sehemu nyingi za ulimwengu. Baadhi ya watu hukadiria kwamba katika United States pekee, vijana wapatao milioni tano wana tatizo baya sana la kunywa. Ingawa hivyo, ikiwa wewe ni kijana Mkristo, bila shaka umeepuka kujaribu kunywa kileo, hasa ikiwa unywaji wa matineja ni kinyume cha sheria katika jumuiya yenu. Hata hivyo, habari inayofuata yaweza kutumikia kuimarisha azimio lako la kutohusika na kunywa tangu mwanzoni—angalau mpaka unapokuwa na umri mkubwa zaidi na unapokuwa umetayarishwa vizuri zaidi kukishughulikia. Lakini ikiwa wewe ni mmoja ambaye amekuwa mzoevu wa kileo, twatumaini kwamba habari hii itakusaidia kupigana na tatizo hilo. Kwa kufanya jitihada nyingi na kwa msaada wa Yehova Mungu, inawezekana kushinda tatizo hilo.

Kushinda Tatizo la Kukana

Hatua ya kwanza na iliyo ngumu zaidi ambayo lazima uchukue ni kushinda tatizo la kukana. Wazoevu wa kileo hukataa kuamini kwamba wana tatizo la namna yoyote katika kunywa. ‘Nakiweza,’ ndiko kujisifu kwenye kusikitikiwa kwa mzoevu wa kileo. Fikiria, kwa mfano, kijana wa miaka 15 aliyesema: “Mimi sina tatizo la unywaji. Mimi hunywa chupa sita tu kila jioni.” Twakumbushwa lile elezo la Biblia la mtu ambaye “hujipendekeza machoni pake kuwa upotovu wake hautaonekana na kuchukiwa.”—Zaburi 36:2.

Ndiyo, kukana tatizo hilo ni hatari sana. Hivyo ikiwa wewe una tatizo katika kunywa, lazima ukubali ukweli huo mchungu.a Usiwapuuze marafiki, ndugu na dada zako, au wazazi wakuambiao kwamba unakunywa kileo kingi mno. Wao si maadui wako kwa sababu wanakuambia kweli. (Linganisha Wagalatia 4:16.) Bob (aliyetajwa mwanzoni) alizoea kunywa sana kila mwisho-juma. Rafiki yake alipomwendea kuzungumzia jambo hilo, Bob alikataa wazo lolote kwamba alikuwa na tatizo la kunywa, na kumaliza mazungumzo. Lakini kileo kilikuwa kikiathirije maisha ya Bob? “Nilikuwa mwenye wasiwasi na mwenye hangaiko sana nisipokunywa na sikujidhibiti nilipokunywa,” akiri Bob. “Maisha yangu ya familia yaliharibika—na ndivyo uhusiano wangu na Mungu.”

Katika pindi nyingine, hatimaye Bob alikubali na kukiri kwa rafiki yake kwamba alitamani sana kileo. Alipoweza kushinda tatizo lake la kukana, Bob alianza kushinda tatizo la unywaji.

Sitawisha Azimio la Kuacha

Profesa George Vaillant aandika kwamba “uzeovu wa kileo . . . waweza kutibiwa sana, lakini . . . utataka daraka kubwa kutoka kwa mgonjwa.” Hilo latia ndani kuazimia kuacha kunywa kileo. Kukosa azimio kwaweza kumaanisha kuishi—na kufa—ukiwa mzoevu wa kileo. Ni jambo gani linaloweza kusaidia? Kukazia fikira uharibifu wa uzoevu wa kileo kwaweza kukusaidia ‘uchukie uovu’ na kwaweza kuimarisha azimio lako la kuacha kunywa bila kurudia.—Zaburi 97:10.

Kwa mfano, waweza kufikiria yale madhara makubwa yasababishwayo na uzoevu wa kileo kimwili, kihisiamoyo, kiadili. Inakubalika, kinywaji chaweza kuonekana kikiponya kwa muda maumivu yako ya ndani au hisi za kutokuwa na thamani. Lakini mwishowe, kutegemea kileo hutumikia tu kutokeza matatizo zaidi; urafiki huvunjika, mahusiano ya familia huharibika. Zaidi ya hilo, kwa sababu kileo hupunguza hali ya kujidhibiti, kinaweza kwa urahisi ‘kuondoa fahamu’ na kukuongoza kwenye kosa zito.—Hosea 4:11.

Fikiria, pia, yale ambayo kiasi kikubwa cha kileo kiwezacho kufanya kwa mwili wako, kikitia sumu hatua kwa hatua katika viungo vyako vilivyo muhimu sana kwa uhai. Hivyo Biblia husema kwamba kunywa kupita kiasi hutokeza zaidi ya ‘taabu, huzuni, magomvi, mashaka, na machubuko.’ (Mithali 23:29-30, The New English Bible) Je! raha yoyote ya muda upatayo yastahili bei hiyo?

Huenda ikasaidia pia kujikumbusha kwamba huhitaji kileo ili uwe mwenye furaha. Wala huhitaji hisia ya msisimko na furaha isiyo ya asili ili ujistahi, uwe na afya njema, uwe na marafiki waaminifu-washikamanifu, na familia yenye upendo. Fanikio katika maeneo hayo ya maisha huja kupitia kutumia Neno la Mungu. (Zaburi 1:1-3) Neno hilo hukupa tumaini pia kwa ajili ya wakati ujao mwangavu zaidi—uhai wa milele bila maumivu ya kihisiamoyo au ya kimwili! (Ufunuo 21:3, 4) Kuwa na tumaini kama hilo hukupa sababu nyingine bado ya kuepuka kileo.—Linganisha 1 Wakorintho 6:9, 10.

Pata Msaada

Ingawa hivyo, kuwa tu na tamaa ya kupona kwa kawaida hakutoshi. Utahitaji tegemezo na msaada wa wengine. “Afadhali kuwa wawili kuliko mmoja,” akasema Mfalme Sulemani. “Kwa maana wakianguka, mmoja wao atamwinua mwenzake.” (Mhubiri 4:9, 10) Kumtuma-ini mtu fulani akusaidie na tatizo lako haitakuwa rahisi. Lakini mzoevu wa kileo anayepona aitwaye Katy hutoa shauri hili: “Jifunze kutumaini watu, hasa familia yako.” Ndiyo, katika visa vingi familia yako imo katika hali bora zaidi ya kukupatia upendo na tegemezo unalohitaji.

Kweli, huenda hali ya familia yako ikawa ilichangia kuhusika kwako katika kunywa mwanzoni kabisa. Lakini ikiwa wazazi wako walijulishwa hali yako, je, hawawezi kuona uhitaji wa kufanyia maendeleo mambo nyumbani? Hivyo kwa nini usijaribu kuwaendea wazazi wako, ukiwaarifu kwamba una tatizo zito? Badala ya kuweka lawama lote juu yao, omba msaada na tegemezo lao. Kuwaambia wazazi wako mambo waziwazi na kwa unyoofu kutasaidia familia yako ‘iungamanishwe pamoja’ kama vile watu wa nyumba ya Mungu walivyoungamanishwa. (Waefeso 4:16) Kwa njia hiyo nyote mwaweza kufanya kazi pamoja kwa ajili ya kupona kwenye mafanikio.

Ikiwa utegemezo wa familia haupatikani, wengine wanaweza kusaidia.b (Mithali 17:17) Bob alionyeshwa urafiki na mzee Mkristo ambaye alikutana naye kila juma kwa kipindi cha miezi kadhaa ili kukagua maendeleo yake. Bob husema: “Kupendezwa na kujali kwake kulinipatia kule kujistahi nilikohitaji ili kukomesha zoea langu lenye matumizi mabaya.”—Yakobo 5:13, 14.

Zaidi ya yote, ng’amua kwamba wahitaji msaada wa Yehova Mungu. Mwegemee yeye ili upate nguvu. Ndiyo, kwa msaada wa Mungu “waliopondeka moyo” waweza kupata ‘kuponywa na kugangwa jeraha zao’ na Yehova.—Zaburi 147:3; ona pia Zaburi 145:14.

Tafuta Marafiki Wapya

Uchunguzi mmoja katika New Zealand uliripoti kwamba marafiki ndio uvutano mkubwa juu ya vijana ambao hutumia vibaya kileo. Kwa hiyo utaliona kuwa jambo gumu kuacha kunywa ikiwa washirikiana na wanywaji. Kwa sababu hiyo Biblia huhimiza hivi: “Usiwe miongoni mwao wanywao mvinyo.” (Mithali 23:20) Kuza urafiki mpya, wenye kujenga. Kama vile ilivyo kweli kwamba “Mazungumzo [mashirika, NW] mabaya huharibu tabia njema,” waandamani wema ni uvutano mzuri.—1 Wakorintho 15:33.

Kim aligundua ndivyo ilivyo. “Ilikuwa vigumu,” akubali, “lakini ilikuwa lazima nibadili marafiki wangu . . . Mimi sikutaka kuwa karibu na kileo na dawa za kulevya.” Inakubalika, huenda ikawa vigumu kupata marafiki wasiokunywa. Ingawa hivyo, utaona kwamba vijana walio vielelezo vizuri miongoni mwa Mashahidi wa Yehova hawashiriki kunywa ambako ni kinyume cha sheria. Wala hawategemei kileo kuwa chanzo cha tafrija au cha kuepuka matatizo. Kwa hiyo waweza kusaidia—si kuzuia—jitihada zako za ‘kuvua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake.’—Wakolosai 3:9.

Unaweza Kuacha Kunywa Kileo!

Kuishi bila kileo kutakuwa pigano lenye kuendelea kwako. Nyakati nyingine kuepuka kileo kabisa kwaweza kuwa jambo gumu sana. “Ningali nina shurutisho lenye nguvu sana la kunywa,” akiri Ana, “hasa ninapoudhika, kukatishwa tamaa, kushuka moyo au kuumia hisia.” Hivyo si jambo lisilo la kawaida kwa mzoevu wa kileo anayepona kurudia kunywa, kukiongoza kwenye hisia zenye kuumiza sana za hatia. Hili likitukia, kumbuka kwamba “twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi.” (Yakobo 3:2) Kumbuka, pia, kwamba Yehova Mungu ni mwenye rehema afahamuye udhaifu wako mbalimbali.—Zaburi 103:14.

Hata hivyo, uwe mwangalifu usitumie vibaya fadhili ya Mungu. Jifunze kutokana na kosa lako, na kuazimia hata zaidi usirudie kileo tena. Kwa kuonyesha kuazimia kama huko, Bob aliweza kuacha kunywa. Tangu wakati huo, ameweza kufurahia mahusiano yenye amani na familia yake na Mungu pia. Maisha yake yenye furaha sasa hutia ndani utumishi akiwa mhudumu wa wakati wote. Furaha na amani ya akili vitakuwa vyako, pia, ukishinda pigano dhidi ya uzoevu wa kileo.

[Maelezo ya Chini]

a Ile makala “Vijana Wauliza . . . Je! Unywaji Unaweza Kunifanya Niwe Mzoevu Kweli?” (Januari 8, 1993, Amkeni!) yaweza kukusaidia uamue kama una tatizo kuhusu jambo hili.

b Wengi wamenufaishwa na msaada wa matabibu na washauri waliozoezwa kushughulikia uzoevu wa kileo. Wataalam fulani huamini kwamba mpaka tabia yenye uzoevu yenyewe iwe imekomeshwa, kazi ifanywayo juu ya pande nyingine za kupona haiwezi kufanikiwa hata kidogo. Kwa sababu hiyo na nyinginezo, baadhi yao hupendekeza kwamba wazoevu wa kileo waingie katika programu ya kuondoa kileo katika mwili hospitalini au katika kliniki.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Vijana ambao ni wazoevu wa kileo huelekea kukana wana tatizoyyy

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki