Kushika Ukamilifu-Maadili Katika Ujerumani ya Nazi
KATIKA siku yenye baridi ya Aprili katika 1939, nilipelekwa kwenye kambi ya mateso ya Sachsenhausen katika Ujerumani. Nikiwa pamoja na wafungwa wengine wapya, nilipelekwa mbele ya kamanda wa kambi, mwanamume mkatili aliyebandikwa jina Miraba-minne kwa sababu ya mwili wake mnene. Katika “hotuba [yake] ya ukaribishaji,” alitukemea, akielezea mateso yenye ukatili ambayo tungetarajia.
“Mwaweza kupata kutoka kwangu chochote mtakacho,” akapaaza sauti, “risasi ya kichwa, risasi ya kifua, risasi ya tumbo!” Na akaonya: “watu wangu wajua sana kulenga bunduki. Watawapeleka moja kwa moja mpaka mbinguni! Njia pekee ambayo mtatoka humu ni mkiwa maiti.”
Baadaye nilipelekwa mahali pa Kutengwa. Kisehemu kilichozungushiwa ua ndani ya kambi. Hapo ndipo Mashahidi wa Yehova walipowekwa, pamoja na wafungwa wengine walioonwa kuwa hatari. Nilipoletwa hapo, kijana mmoja wa SS (Kikosi Maalumu cha Hitler) alinipiga kofi la uso kwa kurudia-rudia kwa sababu nilikuwa nimekataa kutia sahihi taarifa ya kukana imani yangu.
Otto Kamien kutoka Herne alinionyesha urafiki, akinisaidia kushonelea juu ya yunifomu yangu namba yangu ya mfungwa na pembetatu ya zambarau, iliyotumikia kuwatambulisha Mashahidi wa Yehova kambini. Pia alinionyesha jinsi ya kutandika kitanda changu—wafungwa walipigwa au hata kuuawa kwa kutotandika vitanda vyao ifaavyo.
Otto alinitahadharisha hivi: “Pindi kwa pindi, watakuuliza kama wewe ungali mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Uwe imara, usiondoleke, na useme kwa sauti kubwa na waziwazi: ‘Mimi ningali mmoja wa Mashahidi wa Yehova.’” Aliongeza: “Ukiwa imara na usiondoleke, Ibilisi atakuacha.” (Yakobo 4:7) Kitiamoyo cha Otto kilinisaidia kushika ukamilifu-maadili kwa Mungu katika miaka sita iliyofuata ambayo nilitumia katika kambi tatu za mateso.
Ninapofikiri nyuma kwenye miaka hiyo yenye kujaribu, mimi natambua leo, zaidi ya wakati mwingine wowote, kwamba ilikuwa kwa msaada wa Mungu tu kwamba nilishika ukamilifu-maadili. Ilitukiaje kwamba katika Januari 20, 1938, nilikamatwa?
Miaka Yangu ya Mapema
Miaka kadhaa kabla ya mimi kuzaliwa katika 1911, wazazi wangu, walioishi katika Königsberg, Prussia Mashariki, walipata kuwa Bibelförscher (Wanafunzi wa Biblia), kama Mashahidi wa Yehova walivyojulikana wakati huo. Nilikuwa na ndugu watatu na dada wawili, na mara nyingi Mama alitupeleka mikutanoni. Kwa huzuni, baada ya wakati Baba hakujiunga tena na familia katika ibada ya kweli. Ijapokuwa ndugu zangu na mmoja wa dada zangu walipata kuwa wapiga mbiu ya Ufalme wenye bidii, baada ya wakati dada yangu Lisbeth nami tuliacha kutoa uangalifu mwingi kwa kweli za Biblia tulizokuwa tumejifunza.
Nilipokuwa katika miaka yangu ya mapema ya 20, Hitler alishika mamlaka katika Ujerumani, nao watu walitiwa chini ya msongo mkali. Nilifanya kazi nikiwa mekanika wa magari kwenye kiwanda kikubwa cha kurekebishia magari kati-ka Königsberg. Wakati Führer alipotoa hotuba katika pindi za pekee, wote katika kiwanda walilazimika kukusanyika. Ikawa pia kawaida kutumia salamu ya “Heil Hitler!” Hatimaye niliamriwa nishiriki katika mazoezi ya kabla ya kuingia jeshini, hivyo nikalazimika kukabili swali, Niko upande wa nani?
Kutokana na Matendo 4:12, nilijua kwamba heil, au wokovu haukuja kutoka kwa Hitler bali kupitia Yesu Kristo tu. Hivyo singeweza kusema “Heil Hitler,” nami sikusema hivyo kamwe. Pia, nilipuuza ile amri ya kushiriki katika mazoezi ya kabla ya kuingia jeshini.
Wakati wa 1936 na 1937, mama yangu, dada yangu mdogo Helene, na ndugu zangu, Hans na Ernst, wote walikamatwa. Tokea hapo na kuendelea mimi pia nilitaka kuchukua msimamo wangu kwa ajili ya Mungu wa kweli. Nilianza kusoma Biblia jioni, na nikasali kwa Yehova anisaidie. Lisbeth pia alianza kuonyesha kupendezwa zaidi.
Kuchukua Msimamo Wangu
Wakati ulipofika, nilichukua msimamo dhahiri kwa ajili ya Yehova, nikakataa kutumikia katika jeshi la Hitler, hata ingawa nilikuwa bado sijabatizwa. Nilikamatwa na kukabidhiwa jeshi. Majuma matano baadaye mahakama ya kijeshi katika jiji la Rastenburg ilinihikumia mwaka mmoja katika gereza.
Niliwekwa katika kifungo cha upweke katika Gereza Kuu katika Stuhm, Prussia Magharibi. Wakati wa mazoezi yangu katika ua wa gereza, nilipata faraja kwa kubadilishana mitazamano na Mashahidi waaminifu kutoka Königsberg niliokuwa ninawajua tokea utoto. Halafu ndugu zangu—Paul, Hans, na Ernst—wote wakatiwa katika gereza hilihili kwa sababu ya imani yao katika Mungu. Nilipokuwa katika kifungo cha upweke, nyakati nyingine Hans alifaulu kuniletea kisirisiri kipande cha mkate.
Nilipomaliza muda wa kifungo changu, nilihojiwa mara nyingi na Gestapo katika Königsberg. Kwa kuwa nilikataa kubadili nia yangu, nilipelekwa kwenye kambi ya mateso katika Sachsenhausen. Humo nilipewa mgawo kufanya kazi ya kujenga gereji, nikifanya kazi ngumu tokea saa kumi na mbili asubuhi mpaka saa kumi na mbili jioni. Kwa sababu ya kutendewa kikatili, baadhi ya wafungwa walijaribu kutoroka, hali wakijua kwamba ikiwa wangekamatwa, wangepigwa risasi. Wakati mmoja nilimuona mfungwa akijiua kwa kujitupa kwenye ua wa umeme.
Msongo Wazidi
Katika Septemba 1939, Vita ya Ulimwengu 2 ilifyatuka, nao msongo uliokuwa juu yetu katika Sachsenhausen ukazidi. Kazi yetu iliongezeka, nasi tulinyang’anywa mavazi yetu ya sufu yenye moto. Katika Septemba 15 Wanazi wangemtumia ndugu yetu Mkristo August Dickmann, aliyekuwa amekataa utumishi wa kijeshi, kuwa kielelezo. Hivyo kusanyiko la pekee lilipangwa kwa ajili ya kuuawa kwake.
Mamia kadhaa yetu sisi Mashahidi wenzi tulikuwa mashahidi waliojionea wenyewe wakati kikosi cha kupiga risasi kilipompiga risasi August naye akaanguka akafa. Baadaye wafungwa wote waliruhusiwa waende isipokuwa Mashahidi wa Yehova. Miraba-minne akauliza ni nani aliyekuwa tayari kutia sahihi taarifa ya kukataa imani yake na kuonyesha nia yake ya kuwa askari. Hakuna hata mmoja aliyetia sahihi, naye Miraba-minne alikasirika sana.
Majira ya baridi ya 1939 yalikuwa makali sana. Nasi hatukuwa na mavazi mazuri na hatukulishwa vizuri, hivyo vifo vikaanza. Wengi wa ndugu zetu wenye umri mkubwa walikufa, lakini asilimia ya ujumla ya vifo miongoni mwetu sisi Mashahidi ilikuwa ndogo kwa kulinganisha na vile vikundi vingine vya wafungwa. Hata Miraba-minne mwenye nguvu aliugua na akafa katika Februari 1940.
Kwenye Kambi Nyingine
Siku chache baada ya kifo cha Miraba-minne, 70 kati yetu tulihamishiwa kambi ndogo ya Wewelsburg karibu na jiji la Paderborn. Tulikuwa tumetumaini kwamba hali zingekuwa afadhali humo, lakini ikawa kinyume. Tulikuwa na chakula kidogo zaidi na kazi ilikuwa ngumu zaidi katika mgodi wa mawe. Baadhi ya siku tuliloweshwa kabisa na theluji na mvua. Katika pindi ya wakati huo uliokuwa mgumu hasa nilikuwa nikijifunika kichwa kwa blanketi yangu usiku na kumwaga mbele ya Yehova yaliyokuwamo moyoni mwangu huku nikitoa machozi. Kila wakati nilipofanya hivyo, nilihisi utulivu kindani na amani ya akili, hivyo nikipokea kutoka kwa Mungu ‘msaada wakati wa uhitaji.’—Waebrania 4:16.
Yehova alitunza afya yetu ya kiroho. Mashahidi kutoka kambi ya mateso ya Buchenwald walipelekwa Wewelsburg, wakaja na chakula cha kiroho kwa namna ya fasihi ya Biblia. Tuliingia mabweni tukiwa vikundi vidogo, ambamo tulijiunga nao katika funzo la siri la Mnara wa Mlinzi. Hata chakula cha kimwili katika kambi kilikuwa afadhali kidogo.
Nilimshukuru Yehova kwa fadhili zake wakati Shahidi mwenzi alipopanga nifanye kazi pamoja naye katika kiwanda cha kufua vyuma. Viwandani, ambamo sana-sana Mashahidi walifanya kazi, wafungwa walipokea vipimo vya chakula vilivyo afadhali. Zaidi ya hilo, mlikuwa joto, na wafanyakazi hawakusukumizwa kazini kwa uonevu. Nilinufaika sana kimwili hivi kwamba katika muda wa miezi sita nilikuwa na nguvu tena, ijapokuwa mapema nilikuwa nimepungua nikakonda sana.
Napata Habari Juu ya Ndugu Zangu
Nilipokuwa katika Wewelsburg, nilipokea habari kutoka kwa dada yangu Lisbeth kwamba ndugu yetu Ernst alikuwa ameshika ukamilifu-maadili kwa Yehova hadi kifo. Alikuwa amekatwa kichwa katika Berlin Juni 6, 1941, baada ya kifungo cha miaka minne. Mashahidi wengine waliposikia habari hiyo walikuja kunipongeza. Mtazamo wao ufaao ulinigusa sana moyo. Kuendelea tukiwa washikamanifu kulimaanisha zaidi kwetu kuliko kuokoka.
Miaka miwili baadaye, katika Februari 1, 1943, ndugu yangu mkubwa Hans alipigwa risasi katika Quednau karibu na Königsberg. Hans alikuwa na miaka 34 naye alikuwa amefungwa kwa miaka mitano. Baadaye, mtu aliyejionea kwa macho yake mwenyewe akiuawa aliniambia kwamba ofisa alimuuliza Hans kama alikuwa na ombi la mwisho. Hans aliomba ruhusa atoe sala, naye akapewa. Sala hiyo iliwagusa sana moyo askari hivi kwamba wakati hatimaye ofisa huyo alipotoa amri ya kupiga risasi, hakuna hata mmoja wao aliyetii. Alirudia amri, ndipo risasi moja ikapigwa, ilimpiga Hans mwilini. Kisha ofisa akachomoza bastola yake mwenyewe na yeye binafsi akamuua.
Vielelezo Zaidi vya Ukamilifu-maadili
Kati ya wale Mashahidi waliohamishiwa Wewelsburg kutoka Buchenwald, 27 walichaguliwa kwa ajili ya utumishi wa jeshi na kupelekwa kwenye vikosi mbalimbali. Kila mmoja wao alikataa kuingizwa jeshini; ni mmoja tu aliyekubali utumishi usio wa mapigano. Wale 26 walitishwa kuuawa, lakini wapi. Baada ya wao kurudi kwenye kambi ya Wewelsburg, kamanda alitisha hivi: “Mtakuwa mmekufa na kuzikwa katika muda wa majuma manne.”
Ndugu hao washikamanifu walitendewa vikali sana. Nao askari wa SS walifikiria kila namna ya njia ya kuwakandamiza, kuwachosha, na kuwatesa mpaka kifo. Hata hivyo, wote 26 waliokoka! Baadaye, baadhi ya wasio Mashahidi walitendewa hivyohivyo, na miongoni mwao kiwango cha kifo kilikuwa juu hata baada ya kipindi kifupi cha wakati.
Dada Zangu Washika Ukamilifu-Maadili
Katika Aprili 1943, nilihamishiwa kambi ya Ravensbrück. Ilikuwa sana-sana kambi ya wanawake lakini ilikuwa na sehemu ndogo ya wanaume. Niliwekwa nifanye kazi katika kiwanda cha kurekebishia magari, kukabili moja kwa moja kambi ya wanawake. Akina dada Wakristo waliokuwa wakipitia hapo na upesi wakaona ishara yangu ya pembetatu ya zambarau. Ilikuwa sha-ngwe kama nini kubadilishana salamu ya siri au tabasamu changamfu! Upesi habari ikaenea kwamba nilikuwa mwana wa Nyanya Rehwald. Ndiyo, mama yangu alikuwa miongoni mwa hao waliokuwa katika kambi ya wanawake, pamoja na dada yangu Helene na dada mkwe wangu, mke wa Hans aliyeuawa!
Dada zetu Wakristo waliweza kuniandalia mavazi ya ndani na kipande cha mkate mara kwa mara. Wakati mmoja waliongoza mambo hivi kwamba niliweza kusema na mama yangu mpendwa. Kama kukutana kwetu kungaligunduliwa, kungalimaanisha taabu kubwa kwetu. Kulikuwa kukutana tena kwenye shangwe kama nini! Miezi kadhaa baadaye, muda mfupi kabla ya kambi kukombolewa, mama yangu akafa. Alikuwa ameshika ukamilifu-maadili hadi kifo.
Kukombolewa Hatimaye!
Katika Aprili 1945 Warusi na Waamerika walikuwa wakikaribia Ravensbrück. Niliaminishwa trekta na trela ili kusaidia kuondoa watu kambini. Baada ya safari yenye hatari nyingi, ofisa wa SS alituambia kwamba Waamerika walikuwa karibu na kwamba tulikuwa huru kufanya kama tupendavyo.
Hatimaye tulifika Schwerin, mkoa wa Mecklenburg, ambapo tulikutana na idadi fulani ya Mashahidi waliokuwa katika kambi ya Sachsenhausen, miongoni mwao ndugu yangu Paul. Alikuwa ameokoka safari ya kifo kutoka Sachsenhausen, pamoja na magumu mengine. Siku kadhaa baadaye tulipanda garimoshi kwenda Berlin nasi tulipata familia moja ya Mashahidi iliyotupokea kwa ukaribishaji-wageni.
Familia hiyo ilisaidia sana akina ndugu na dada waliokombolewa kutoka kambini na gerezani. Katika 1946, nilimwoa Elli, binti ya familia hiyo. Hatimaye, mipango ilifanywa ili nibatizwe, jambo ambalo halikuwa limewezekana katika kambi za mateso.
Umekuwa msisimuko kama nini kwa muda wa miaka iliyopita kwenye mkusanyiko kukutana na akina ndugu niliokuwa pamoja nao katika kambi za mateso! Baadhi yao walikuwa wamehatirisha maisha zao kwa ajili ya ndugu zao, na hao hasa ninawapenda sana. Wale washiriki sita wa familia yangu waliokamatwa—mama yangu, dada yangu Helene, nami, kutia na ndugu zangu, Paul, Hans, na Ernst—walitumia jumla ya miaka 43 kifungoni. Na dada yangu Lisbeth pia alishika ukamilifu-maadili kwa Mungu mpaka kifo chake katika 1945.
Kutegemea Nguvu za Yehova
Baada ya kufunga ndoa, Elli nami tulipendelewa kutumikia kwa miaka kadhaa katika Betheli ya Magdeburg na katika kazi ya painia mpaka tulipoanza kulea wana wetu wawili. Sisi ni wenye shukrani sana kwamba mmoja wao, Hans-Joachim, anatumikia akiwa mzee na mke wake akiwa painia. Kwa kusikitisha, yule mwana wetu mwingine hakushikamana na mwendo wa Kikristo tuliomwelekeza.
Zaidi ya miaka 45 imepita haraka tangu mambo yaliyonipata katika kambi za mateso. Lakini hata sasa, Mungu wa fadhili zote zisizostahiliwa mwenyewe hajamaliza mazoezi yangu. (1 Petro 5:10) Nimekumbushwa mara nyingi maneno ya mtume Paulo kwenye 1 Wakorintho 10:12: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.”
Leo, nikiwa na miaka 81, mimi ni mwenye shukrani kwamba ningali naweza kushiriki katika kazi ya kutoa ushahidi na kutumikia nikiwa mzee wa kundi. Na nina shukrani kwamba nimeweza kusaidia idadi fulani ya watu kufikia hatua ya wakfu na ubatizo. Hilo pia naliona kuwa wonyesho wa fadhili zisizostahiliwa za Yehova.—Kama ilivyosimuliwa na Josef Rehwald.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 18]
Josef Rehwald katika 1945
Labor strike, Leslie’s
[Picha katika ukurasa wa 21]
Familia ya Rehwald, yapata 1914. Mama akiwa na mtoto Josef pajani mwake
[Picha katika ukurasa wa 23]
Josef na Elli Rehwald kwenye mkusanyiko wa
1991 wa Berlin, pamoja na mwana Hans-Joachim na mke wake, Ursula