Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g93 2/22 kur. 13-17
  • Maisha Yenye Kuthawabisha Nijapokuwa Pekee

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Maisha Yenye Kuthawabisha Nijapokuwa Pekee
  • Amkeni!—1993
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujifunza Juu ya Yehova
  • Hadi Thailandi Kupitia Hispania
  • Kusonga Mbele Hadi Australia
  • Hadi Bougainville
  • Hadi Afrika
  • Katika Amerika Kusini
  • Hadi Papua New Guinea
  • Kufanya Kazi Pamoja na Kutaniko
  • Uamuzi wa Kutumia Maisha Yangu Katika Utumishi wa Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Kitabu-mwaka cha Mashahidi wa Yehova 1990
    1990 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
  • Ni Shangwe Kama Nini Kuketi Kwenye Meza Ya Yehova!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Sehemu ya 4—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1993
g93 2/22 kur. 13-17

Maisha Yenye Kuthawabisha Nijapokuwa Pekee

NILIZALIWA katika Januari 1927, katika Málaga, Hispania, nilikuwa mtoto wa sita katika familia maskini ya Kikatoliki yenye watoto saba. Kutoka 1936 hadi 1939, Vita ya Wenyewe kwa Wenyewe ya Hispania iliharibu nchi yetu, nasi tuliepa-epa mabomu na kuishi kwa chakula cha kipimo. Hata hivyo, nilikuwa mtoto mwenye furaha aliyependa kuimba na kukaa na watu.

Ingawa hivyo, jambo moja lilinitia hofu—tarajio la kuchomeka katika moto wa helo. Ili kuzima hofu hizo, nilihamia makao ya watawa wa kike nikiwa na umri wa miaka 12. Humo, kwa karibu miaka mitatu, nilikuwa nikisafisha ngazi za marimari, nikisali, na kusafisha tena, lakini bado nilihisi kwamba jambo fulani lilikuwa linakosekana. Katika 1941, nilifurahi kuweza kuondoka.

Baada ya miaka kadhaa nilifanya urafiki na mwimbaji aliyefikiri kwamba sauti yangu ingeweza kuchuma pesa, naye mwanamke huyo alinitia moyo nianze masomo ya kuimba na kupiga piano. Vita ya Ulimwengu 2 ilipokwisha katika 1945, nilikwenda Moroko, ambako nilianza kuimba katika vilabu vya usiku katika Kasablanka na Tangier. Hayo yalikuwa maisha yenye kusisimua kwa tineja. Lakini baada ya kila kipindi cha kuimba, nilikwenda kanisani na kumwomba Bikira Maria anisamehe, nikitumaini kwamba naweza kuepuka helo yenye moto.

Baada ya kufanya kazi katika vilabu vya usiku kwa miaka tisa, nilikutana na Mwamerika aliyeitwa Jack Abernathy. Wakati huo alikuwa akifanyia kazi kampuni moja ya ujenzi ya Amerika katika Moroko. Tulifunga ndoa mwaka huo, nami nikaacha kuimba. Upesi baada ya hapo tulihama kwenda Seville, Hispania, ambako tuliishi mpaka 1960. Kisha tukahama kwenda Lodi, Kalifornia, U.S.A.—kuhama ambako kulileta badiliko jingine maishani mwangu.

Kujifunza Juu ya Yehova

Katika 1961 Mashahidi wawili wa Yehova walitembelea nyumbani mwetu na kuacha magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Baadaye walirudi na kujitolea wanifunze Biblia, nami nikakubali toleo hilo. Hivyo, nilijifunza juu ya Mungu wa kweli, Yehova, ambaye ni Baba yetu wa kimbingu mwenye upendo. (Zaburi 83:18) Kilikuwa kitulizo kama nini pia kujifunza kwamba hakuna helo yenye kuwaka moto bali kwamba tuna tarajio la kuishi milele katika paradiso duniani!—Zaburi 37:9-11, 29; Ufunuo 21:3, 4.

Dadangu Paquita, aliyeishi karibu nasi, alianza kujifunza pia. Hapo mbeleni, nilikuwa nikivuta sigareti na nilipenda kufanya karamu. Na hasira yangu acha wee! Lakini nilifanya mabadiliko, na Oktoba 17, 1962, Paquita nami tulibatizwa katika Sakramento, Kalifornia, hivyo tukaweka maisha zetu wakfu ili kumtumikia Yehova.

Hadi Thailandi Kupitia Hispania

Muda mfupi baada ya hapo, kampuni ya ujenzi ambayo mume wangu alifanyia kazi ilimhamisha hadi Thailandi, nami nilijiunga naye. Nikiwa njiani, nilizuru Hispania nami nikaweza kushiriki imani zangu pamoja na washiriki wengine wa familia yangu. Pura dada mkwe wangu aliitikia na akawa Shahidi.

Katika siku hizo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa imepigwa marufuku katika Hispania. Hata hivyo, tulihudhuria mkutano wa siri katika chumba kidogo chenye meza moja na bila viti. Sisi sote 20 tulisimama. Ni tofauti kama nini na mikutano yetu katika Kalifornia! Kuona watu wetu wakihatirisha uhuru wao ili kukutana kulinisadikisha juu ya umaana wa mikutano ya Kikristo, somo la wakati wake kabla tu ya kuwasili Bangkok, Thailandi.

“Nikigundua wakati wowote kwamba unahubiri, nitakuacha,” Jack akaniambia siku tuliyowasili Bangkok. Siku iliyofuata aliondoka akasimamie kazi ya ujenzi katika eneo la mashambani, hivyo nikaachwa peke yangu katika Bangkok yenye shughuli nyingi nikiwa na kijakazi nisiyeweza kuwasiliana naye. Nilijishughulisha kwa kujifunza fasihi yangu ya Biblia tena na tena.

Siku moja katika Septemba 1963, nilipokuwa nikirudi nyumbani, niliona jozi ya viatu vigeni mlangoni pangu. Bibi mwenye nywele ya rangi-shaba-nyeupe yenye kusokota alikuwa ananingojea. “Nikufanyie nini?” Nikauliza.

“Nawakilisha Watch Tower Society,” akasema.

Niliruka kwa kusisimuka, nikimkumbatia na kumbusu. Eva Hiebert alikuwa mishonari kutoka Kanada. Tokea siku hiyo na kuendelea, Eva alikuja kwa ukawaida, akibadili basi mara mbili au tatu ili kunifikia. Niliogopa kupanda mabasi ambamo watu walisongamana sana, lakini hakukuwa na njia nyingine ambayo ningeweza kusafiri. Eva alisema: “Hutaweza kamwe kumtumikia Yehova usipopanda mabasi hayo.” Kwa hiyo tukafanya mazoezi ya jinsi ya kupanda mabasi hayo ili niweze kwenda kwenye mikutano.

Nilisitasita kuhubiri, kwa kuwa sikujua lugha ile. Nilikuwa nikishikilia mkono wa Eva, kikapu chake, na vazi lake. “Huwezi kumtumikia Yehova kwa njia hii,” akasema.

“Lakini mimi sijui hii lugha,” nikanung’unika.

Eva alinipa magazeti kumi akaondoka, akiniacha sokoni katikati. Kiwogawoga, nilimwendea mwanamke Mchina, nikamwonyesha magazeti, naye akayakubali!

“Eva, niliangusha magazeti yote kumi,” nikatabasamu kwa shangwe baadaye. Akasema, “Yehova huwapenda watu kama wewe. Endelea tu.” Nilifanya hivyo, nikajifunza kusalimiana kwa Kithai na, kulingana na desturi ya huko, kuketi sakafuni. Pia nilijifunza jinsi ya kwenda sehemu mbalimbali. Mume wangu aliitikiaje? Siku moja, wakati Jack, aliyekuwa ameniacha nifuate imani zangu, alipokuwa na wageni, aliwaambia: “Safirini na Pepita. Ajua sehemu hii kwa sababu yeye huhubiri.”

Kusonga Mbele Hadi Australia

Mazoezi thabiti lakini yenye upendo ya Eva yalinitayarisha niendelee kuwa mtendaji katika utumishi wa Yehova wakati wa mgawo wa kazi uliofuata wa mume wangu, katika kaskazini-magharibi mwa Australia. Tuliwasili katikati ya 1965, nami nikakaa katika kambi ya wafanyakazi katikati ya jangwa ambapo kampuni ya Jack ilikuwa ikitengeneza njia ya reli. Chakula kililetwa kwa ndege, na halihewa ilikuwa joto sana—zaidi ya digrii 43 Selsio. Mlikuwamo familia 21 za Waamerika wa Kaskazini kambini, hivyo nikaanza kuwaendea nikiwa na ujumbe wa Ufalme. Baadaye, kadiri kazi ilivyoendelea katika njia ya reli, tulisonga ndani zaidi katika jangwa, ambako nilikuwa pekee hata zaidi.

Mapema zaidi nilikuwa nimeandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Australia, nami nilifurahi kama nini kupokea barua iliyosema: “Upendo mchangamfu na salamu . . . Mawazo na sala zetu zitakuwa pamoja nawe katika miezi ijayo”! Wakati wa miaka ambayo nilisafiri na mume wangu katika migawo yake ya kazi kwenye maeneo ya mbali ya dunia, nilitiwa moyo kwa barua kama hizo kutoka tengenezo la Yehova. Kuzisoma kuliniwezesha kupita vipindi hivyo vya upweke na kunitia moyo nitoke na kwenda katika kazi ya kuhubiri hata ingawa mara nyingi nilikuwa pekee, mbali na Mashahidi wengine.

Ofisi ya tawi katika Australia ilipanga mume na mke Mashahidi wanizuru kwa juma moja kambini. Katika huduma yetu tulimpata mwanamke aliyeishi mbali sana, hivyo mara mbili kila juma nilitembea kupitia eneo lenye manyoka na mijusi ili kumzuru. Nilipokuwa nikitembea, nilikuwa nikianza ghafula kuimba wimbo wa Ufalme: “Jipange naye Yah/ Mupende yeye/ Hakuachi kamwe/ Enda nuruni.” Tukajifunza kwa miezi 11.

Kisha, baada ya kukaa mwaka mmoja hivi katika Melbourne, nilihama pamoja na mume wangu kwenda kwenye kambi moja karibu na mji wa migodi wa Port Hedland, pia kaskazini-magharibi mwa Australia. Baada ya siku tano, nikawa na wageni. Ofisi ya tawi ilikuwa imewajulisha Mashahidi mahali nilipo. Baada ya wao kuondoka, niliendeleza mikutano nikiwa peke yangu, nikiongoza Funzo la Kitabu la Kundi, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, Mkutano wa Utumishi, na Funzo la Mnara wa Mlinzi. Baada ya kuimba wimbo na kufungua kwa sala, nilijibu maswali na kumalizia kwa wimbo na sala. Kuhesabu hudhurio hakukuwa tatizo kamwe—sikuzote mmoja. Hata hivyo, mkutano huo wa kila juma ulinidumisha wakati wa miaka hiyo mingi niliyomtumikia Yehova nikiwa pekee.

Hadi Bougainville

Katika 1969, baada ya kuwa katika halihewa yenye joto kwa miaka minne katika Australia, mume wangu alipewa mgawo akatumikie akiwa msimamizi wa mradi wa ujenzi wa barabara ya kwenda kwenye mgodi wa shaba katika milima yenye unyevu ya kisiwa cha Bougainville. Jioni moja mtu fulani alibisha mlango. Jack akafungua. “Ni Shahidi mmoja akiwa na mke wake na watoto wanne,” akasema. Waliishi pwani. Mara moja kwa juma niliwazuru na kuhudhuria Funzo la Mnara wa Mlinzi lililofanywa katika shule ya jumuiya.

Kwenye pindi nyingine Mashahidi watatu kutoka Papua New Guinea walinizuru. Mume wangu aliwaambia wafanyakazi wenzake kwa fahari hivi: “Kokote mke wangu aendako, rafiki zake Mashahidi wanangoja.”

Hadi Afrika

Katika 1972 tuliwasili jangwani katika Algeria, Afrika Kaskazini, ambako kampuni ya Jack ilikuwa ikijenga mfumo wa kunyunyizia maji. Huo ungekuwa mradi wa miaka minne. Niliandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa juu ya kazi ya kuhubiri, nao wakanijibu hivi: ‘Uwe mwenye tahadhari. Kazi yetu imepigwa marufuku humo.’ Sosaiti ilinisaidia kuwasiliana na wanawake wawili Mashahidi wasiotenda, nasi tukafanyiza kikundi cha funzo.

Halafu, mmoja wa majirani katika kambi ya kazi, Cecilia, akawa mgonjwa. Nilimzuru kila siku hospitalini, nikimletea supu na kutandika kitanda chake. Alipokuja nyumbani, niliendelea kumfanyia mambo au kumnunulia vitu, na pia nilishiriki pamoja naye tumaini la Ufalme. Hilo liliongoza kwenye funzo la Biblia, na baada ya miezi minane Cecilia alisema: “Nataka kubatizwa.” Lakini wapi na abatizwe na nani?

Tulipokea barua moja kutoka ofisi ya tawi katika Ufaransa kwamba ndugu Shahidi aitwaye François alikuwa anakuja Algeria kwa likizo fupi. Ikiwa tungeweza kumleta kwenye kijiji chetu cha jangwani na kumrudisha kwenye uwanja wa ndege kwa kuwahi, angeweza kubatiza. Lakini hangeweza kukaa zaidi ya saa 24.

Mara François alipowasili, alichukuliwa mbiombio kwa gari na kupelekwa jangwani. Jioni hiyo, nyumbani mwa Cecilia, alitoa kikaratasi kidogo kutoka mfukoni mwake wa shati na kutoa hotuba nzuri. Mapema asubuhi ya Mei 18, 1974, alimbatiza Cecilia katika bafu yangu na kwenda zake tena.

Vita ilifyatuka katika Algeria mwishoni mwa 1975, na Jack nami tukalazimika kuondoka ghafula. Nilizuru jamaa zangu katika Hispania. Katika 1976, nikaanza kupakia vitu kwa ajili ya mgawo uliofuata wa Jack—kambi ya kazi katika msitu wa mvua wa Suriname, Amerika Kusini.

Katika Amerika Kusini

Kambi katika kusini-magharibi mwa Suriname ilizungukwa na majani mabichi yenye kupendeza. Kasuku wenye kelele na tumbili wenye udadisi walitazama kutoka juu ya miti zile familia 15 zilizowasili karibuni, wengi zaidi kati yao niliwajua kutoka kambi za kazi za hapo zamani. Miezi sita baadaye, familia zaidi za kazi zikawasili, kutia na Cecilia aliyekuwa amebatizwa katika Algeria—mwenzi wangu wa kazi ya kuhubiri!

Machi 23, 1978, ilipokuwa ikikaribia, tulijiuliza tungeadhimishaje Ukumbusho wa kifo cha Kristo. Kwa kukosa usafiri wa kwenda kwenye mji mkuu, Paramaribo, tulipanga kuuadhimisha nyumbani mwangu. Meneja wa kambi alituruhusu kufanya nakala za ukurasa wa mwisho wa Mnara wa Mlinzi uliotangaza Ukumbusho, nasi tukazigawanya nyumba kwa nyumba kambini. Ishirini na mmoja walihudhuria! Cecilia alitoa hotuba nami nikasoma maandiko. Jioni hiyo, tujapokuwa peke yetu, tulihisi tumeunganishwa na tengenezo la Yehova la ulimwenguni pote.

Wakati huohuo, tawi la Suriname la Mashahidi wa Yehova, lilipeleka msaada—mume na mke vijana wamishonari wakiendesha “Land-Rover.” Kabla ya wao kuwasili, nilikuwa nimeanza kuhisi kidogo kuwa nafanya kazi bure kambini, lakini wamishonari hao walinihakikishia: “Pepita, upo hapa kwa kusudi.” Wakati huo sikusadikishwa, lakini upesi nikaelewa.

Siku moja wakati wa ziara ya wamishonari, tulichunguza barabara ya mchanga iliyokuwa imefunguliwa karibuni nasi tukasisimuka kupata vijiji kadhaa vya Wahindi Waamerika ki-lometa zapata 50 kutoka kambi yetu. Siku chache za kuhubiri miongoni mwa Wahindi hao Waarawaki wenye urafiki zilitokeza mafunzo ya Biblia makumi kadhaa. Hivyo wamishonari walipoondoka, Cecilia nami tukaanza kuzuru vijiji hivyo mara mbili kwa juma.

Tuliamka saa kumi za usiku, na kufikia saa moja tulianza funzo letu la Biblia la kwanza. Zapata saa kumi na moja jioni, tulikuwa nyumbani tena. Kwa miaka miwili tuliongoza mafunzo 30 kila juma. Kabla ya muda mrefu watoto katika kijiji walikuwa wakiniita Shangazi Biblia! Hatimaye wengi walibatizwa, na miaka kadhaa baadaye 182 walihudhuria kusanyiko la mzunguko katika kijiji hicho. Kwelikweli, kama vile wale rafiki zangu wapendwa wamishonari walivyokuwa wamesema, tulikuwa katika msitu huo kwa kusudi!

Hadi Papua New Guinea

Tuliondoka Suriname katika 1980, na mwaka uliofuata tulipelekwa Papua New Guinea. Baada ya miezi sita yenye kupendeza ya kuwa pamoja na Mashahidi katika mji mkuu, Port Moresby, helikopta ilinipeleka kwenye makao yangu yaliyofuata—kambi moja juu sana milimani ambako kampuni ya Jack ilikuwa ikisitawisha mgodi wa dhahabu. Hakukuwa na barabara. Watu, vifaa, na chakula viliwasili kwa ndege. Hapa ndipo mahali nilipokuwa pekee zaidi nilipopata kuishi wakati wowote. Kwa mara nyingine tena nilijiuliza, Nipate wapi watu wa kuongea nao?

Watu katika kambi yetu walinijua kutoka kambi za hapo zamani, na hakuna yeyote aliyetaka kusikiliza. Hata hivyo, karibu na wakati huo, kampuni ilifungua duka la kuuza vyakula na bidhaa nyinginezo. Wanawake kutoka sehemu za mbali walinunua bidhaa dukani humo. Upesi nikawa mmoja wa wateja wenye kwenda dukani mara nyingi zaidi. Je! nilifanikiwa?

Siku moja nilizungumza na mwanamke Mpapua. Aliniambia kwamba yeye ni mwalimu. “Oh, mimi ni mwalimu vilevile,” nikasema.

“Kweli?” akauliza.

“Ndiyo, nafundisha Biblia.” Mara hiyo akakubali toleo langu nijifunze pamoja naye. Baadaye, wanunuzi wengine wakakubali kufanya hivyohivyo. Kambi hiyo iliyokuwa karibu na mgodi wa dhahabu ilizaa mafunzo ya Biblia saba—mgodi wa dhahabu ya kiroho kwelikweli!

Baada ya kukaa miaka mitatu katika kisiwa hicho cha Pasifiki, kazi mpya ilitupeleka hadi Grenada kisiwa cha Karibea. Lakini baada ya mwaka mmoja na nusu, mume wangu akawa hana budi kurudi United States kwa sababu za kiafya, hivyo katika 1986 tulifanya makao katika Boise, Idaho.

Kufanya Kazi Pamoja na Kutaniko

Baada ya kuishi miaka hiyo yote nikiwa pekee mbali na ndugu na dada Wakristo, sasa nililazimika kujifunza kufanya kazi pamoja na wengine. Hata hivyo, wazee Wakristo na wengine wamenisaidia kwa subira. Leo, naonea shangwe kuhudhuria mikutano na kuongoza mafunzo ya Biblia katika sehemu hii ya ulimwengu.

Ingawa hivyo, nyakati nyingine ninapoketi kwenye kona fulani yenye utulivu na kujiona tena nikikimbia nyuma ya Eva katika Bangkok wenye shughuli nyingi au nikibubujika kwa wimbo wa Ufalme nitembeapo katika ile barabara ya jangwa katika Australia au nikihubiri miongoni mwa wale Wahindi Waamerika wanyenyekevu katika msitu wa mvua wa Suriname, natabasamu, na macho yangu hujaa machozi ya shukrani kwa ajili ya utunzaji niliopokea wakati wa miaka hiyo mingi niliyomtumikia Yehova nikiwa pekee.—Kama ilivyosimuliwa na Josefa ‘Pepita’ Abernathy.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Nikiimba pamoja na wanafunzi wangu wa Biblia Wahispania katika Melbourne

[Picha katika ukurasa wa 16]

Nilisaidia wengi katika Papua New Guinea wapate kumjua Yehova

Kufundisha Neno la Mungu katika Suriname

[Picha katika ukurasa wa 17]

Sasa natumikia pamoja na kutaniko katika Idaho

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki