Fungu la Dini Katika Vita vya Binadamu
“HAKUJAPATA kuwa na watu ambao hawakuwa na namna fulani ya dini,” yasema The World Book Encyclopedia (chapa ya 1970). Na bado, wanahistoria Will na Ariel Durant waliandika hivi: “Vita ni mojayapo vitu vinavyodumu vya historia.” Je! vitu hivi viwili vinavyodumu, vita na dini, vina uhusiano wowote?
Kwa kweli, katika historia yote, vita na dini vimekuwa havitenganiki. Kuhusu Misri, mojayapo mamlaka za kwanza za ulimwengu katika historia, Lionel Casson alieleza hivi katika kitabu Ancient Egypt: “Miungu ilipewa shukrani kwa kila ushindi wa kijeshi; na wakitaka mali nyingi zaidi, makuhani walikuwa na hamu nyingi ya ushindi zaidi wa kigeni kama ilivyokuwa na mafarao.”
Vivyo hivyo, kasisi W. B. Wright alisema hivi juu ya Ashuru, iliyokuwa mamlaka nyingine ya awali ya ulimwengu: “Vita vilikuwa shughuli za taifa, na makuhani walikuwa wachocheaji wasiokoma wa vita. Kwa sehemu kubwa walitegemezwa na nyara za vita.”
Kuhusu kile alichokiita “Ulaya yenye ukatili,” Gerald Simons aliandika hivi: “Jamii yao ilikuwa sahili, iliyopangwa tu kwa kusudi moja, kupigana vita.” Na dini ilihusika. “Hekaya nyingi zaeleza juu ya panga zenye mashetani, au zinazotenda kwa niaba ya miungu,” akaandika Simons.
Na bado, hali ya Milki ya Roma, iliyoonwa kuwa imestaarabika sana, ilifanana na zile nyingine. “Warumi walizoea vita,” aeleza Moses Hadas katika kitabu Imperial Rome. Majeshi ya Roma yalichukua vitani bendera zenye ishara za miungu yao. Na ensaiklopedia moja ilionelea: “Ilikuwa kawaida kwa mkuu wa jeshi kuamuru bendera irushwe miongoni mwa adui, ili kuongezea bidii ya shambulio la majeshi yake kwa kuwachochea wapate tena kile ambacho kwao kilikuwa kitu kitakatifu zaidi duniani.”
Vita na Wanaojiita Wakristo
Kuibuka kwa Jumuiya ya Wakristo ulimwenguni hakukubadilisha mambo. Kwa kweli, Anne Fremantle aliandika katika kitabu Age of Faith: “Kati ya vita vyote vilivyopiganwa na wanadamu, hakuna ile iliyopiganwa kwa bidii sana kuliko vile vita vya kupigania imani. Na kuhusu hivyo ‘vita vitakatifu,’ hakuna ile iliyokuwa na umwagikaji damu mwingi na wenye kudumu zaidi ya zile Krusedi za Kikristo za Enzi za Kati.”
Kwa kushangaza, hata leo kuna mabadiliko madogo sana. “Kupigana na kufa chini ya uongozi wa dini kwaendelea kwa jeuri isiyokoma,” gazeti Time laripoti. “Waprotestanti na Wakatoliki wa Roma katika Ulster waliuana kwa namna ya upuzi usiokoma. Waarabu na Waisraeli wako tayari kwenye mipaka ya ubishi ya kieneo, kitamaduni, na kidini.” Na hivi karibuni zaidi, tofauti za kikabila na kidini zimetokeza mauaji ya kikatili katika zile zilizokuwa jamhuri za Yugoslavia, na vilevile katika nchi za Esia.
Kwa kustaajabisha, wale wanaojiita Wakristo mara nyingi huenda vitani dhidi ya washiriki wa imani yao wenyewe. Hivyo, Wakatoliki huua Wakatoliki vitani. Mwanahistoria Mkatoliki E. I. Watkin alikiri hivi: “Ingawa ni jambo la uchungu kukubali, kwa kupendelea mafundisho bandia au kukosa unyoofu, hatuwezi kukana au kupuuza uhakika wa kihistoria kwamba Maaskofu wameendelea kuunga mkono vita vyote vinavyopiganwa na serikali ya nchi yao. Kwa kweli sijasikia hata tukio moja ambapo makasisi wa taifa walishutumu vita vyovyote kuwa vita visivyofaa . . . Hata iwe ni kwa sababu gani, wakati wa vita Maaskofu wa Kikatoliki wamefuata kihalisi ile kanuni ya ‘nchi yangu ni sawa siku zote.’”
Isitoshe, hiyo si kanuni ya Wakatoliki pekee. Tahariri moja katika gazeti Sun la Vancouver, Canada, lilisema: “Uprotestanti hauwezi kudai kwa njia yoyote kuwa umeepuka uvutano huo mwingi wa utaifa wenye kugawanya. utaifa. Ni udhaifu wa labda dini zote mashuhuri kwamba kanisa hufuata bendera . . . Ni vita gani iliyopata kupiganwa ambayo haikudaiwa kwamba Mungu alikuwa akiunga mkono pande zote?”
Kwa wazi hakuna hata moja! Kasisi Mprotestanti Harry Emerson Fosdick alikiri hivi: “Hata ndani ya makanisa yetu tumeziweka bendera za vita . . . Kwa upande mmoja wa mdomo wetu tumemsifu Mwana-Mfalme wa Amani na kwa upande ule mwingine tukatukuza vita.” Na mwandishi wa gazeti Mike Royko alisema kwamba Wakristo “hawajapata kuona ubaya katika kupigana vita dhidi ya Wakristo wengine.” Alieleza hivi: “Ikiwa wangeuona, vita vingi vikali zaidi havingetokea katika Ulaya.” Vita yenye kutokeza kati ya hivyo ilikuwa ni ile Vita ya Miaka Thelathini katika Ujerumani kati ya Waprotestanti na Wakatoliki.
Kwa kweli, mambo ya hakika ni wazi sana. Dini imeunga mkono, na nyakati nyingine, hata imeendeleza vita. Hivyo, wengi wamejiuliza maswali haya: Je! kweli Mungu huunga mkono taifa moja dhidi ya jingine wakati wa vita? Je! yeye huunga mkono upande wowote mataifa yanapopigana? Je! kutapata kuwa na wakati ambapo vita havitakuwapo tena?
[Blabu katika ukurasa wa 3]
Majeshi ya Roma yalitupa bendera zenye ishara za miungu yao miongoni mwa adui zao