Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 2/1 kur. 4-8
  • Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na Mwanzo wa Huzuni Mbalimbali

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na Mwanzo wa Huzuni Mbalimbali
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Taabu Kubwa ya Ulimwengu Inaongezeka
  • Amani Inaondolewa Duniani
  • Vita Ambayo Itavimaliza Vita
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Amani na Usalama Ndio Uhitaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Msababishaji Mkuu wa Vita na Kuteseka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2014
  • Je! Inaweza Kuwa Mwisho wa Ulimwengu Ni Karibu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 2/1 kur. 4-8

Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na Mwanzo wa Huzuni Mbalimbali

TANGU nyakati za huko nyuma zaidi, historia ya wanadamu imekuwa yenye jeuri na vita vingi. Mungu alileta Gharika ya duniani pote siku za Noa kwa sababu “dunia ilipata kujawa na jeuri.” (Mwanzo 6:11-13, NW) Baada ya hapo Biblia na historia zina kumbukumbu la vita vingi vilivyopigwa hata kabla ya siku za Yesu. Kwa hiyo “vita na matetesi ya vita” havingekuwa jambo jipya kwa ulimwengu wa wanadamu.

Ili “vita na matetesi ya vita” hivyo viwe na maana kwa wanafunzi wa Yesu vingepasa kuwa tofauti kwa njia fulani yenye kuonekana wazi. Yeye aliendelea kueleza hivi: “Kwa maana taifa litainuka dhidi ya taifa, na ufalme dhidi ya ufalme: na kutakuwako njaa kubwa-kubwa, na magonjwa ya kipuku, na matetemeko ya ardhi, katika mahali pengi [mbalimbali]. Yote hayo ndiyo mwanzo wa huzuni mbalimbali.” (Mathayo 24:7, 8, Authorized Version; linganisha Luka 21:10,11.) Kwa hiyo halingekuwa shauri la kusikia tu habari za vita moja-moja vya hapa na pale. Sehemu hiyo ya ile ishara ingehusu mataifa mengi na falme nyingi. Ingekuwa vita yenye kujumlisha wote ndani!

Je! sisi tumeona vita ya namna hiyo? Ndiyo, na ilianza na kizazi kile cha mwaka wa 1914. Kwa kweli, tumeona vita viwili vya namna hiyo vyenye kuizunguka dunia yote wakati wa kizazi hiki. Kwamba namna hiyo ya vita ilikuwa jambo jipya katika maandishi ya kumbukumbu la historia ya kibinadamu inashuhudiwa na majina ambayo namna hizo za vita zilipewa na waandishi wa historia. Ya kwanza iliitwa ile Vita Kuu. Baadaye jina lilibadilishwa ikaitwa vita ya ulimwengu ya kwanza, na iliyoifuata ikaitwa vita ya ulimwengu ya pili. Vita ya ulimwengu ikawa jambo lenye kuanzia mwaka wa 1914.

Huzuni Mbalimbali Zisizo na Ulinganifu

Kulingana kikweli na utabiri wa Yesu, Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilikuwa “mwanzo wa huzuni mbalimbali.” Ni kama vile watangazaji wa kitabu The End of Order (Mwisho wa Utaratibu)’ wametaja katika jalada la kitabu hicho: “Vita ya ulimwengu ya kwanza na Mapatano ya Versailles yaliyofuata vilitokeza msukosuko ulio mbaya zaidi katika mwendo mrefu wenye matatizo makubwa-makubwa wa historia ya kisasa ya ulimwengu. . . .Badala ya kurudisha ulimwengu kwenye utaratibu, wajumbe waliokutana mwaka wa 1919 huko Paris na huko Versailles waliutumbukiza tena ulimwengu ndani ya machafuko yaliyo katika karne ya ishirini, na safari hii haungeweza kuondolewa tena humo. Ulikuwa ndio mwisho wa utaratibu.”

Ndani ya kitabu hicho, mwandikaji L. Mee, Mwana, anaendelea kueleza hivi: “Lakini, mwisho wa ile Vita Kuu wajumbe walielekeana na ulimwengu ukiwa vipande vipande, ulimwengu ulioonekana kuwa katikati ya mvunjiko mkubwa sana wa hali za kiroho, katikati ya mvunjiko wa miunganisho ya kale ya serikali mbalimbali na milki, katikati ya kuzorota kwa taratibu za kiuchumi, katikati ya ubepari wa karne ya kumi na tisa, katikati ya kutokea ghafula kwa misiba, katikati ya ghasia-ghasia za watu na kuuawa kwa watawala, katikati ya utawala wa ukatili na fujo-fujo, katikati ya uzembe na kukata tumaini, uchangamfu na hofu kubwa juu ya taratibu hiyo yenye matatizo makubwa kiasi cha kuipumbaza kabisa akili... . Badala ya kurudishia ulimwengu utaratibu, wao waliyachukua machafuko ya ile Vita Kuu, kisha . . . wakayatia muhuri yawe ndiyo hali ya daima ya karne yetu.”

Hizo huzuni mbalimbali​—kifo cha kibinadamu na taabu iliyoanza na vita ya ulimwengu ya kwanza​—hazina ulinganifu katika historia ya kibinadamu. Vita vya kisasa vyenye kutumia vifaa vilivyotengenezwa kwa mashine​—vifaru, bunduki zenye kumimina risasi kama maji, ndege na nyambizi (sabmarini)—na pia uvumbuzi na matumizi ya gesi zenye sumu katika vita​—vilileta uharibifu katika sehemu zote za ulimwengu. “Sehemu kubwa ya kizazi ilikuwa imeuawa katika wanja za mapigano za Ulaya,” kinasema kitabu The End of Order. “Hakuna mtu aliyekuwa ameona mauaji ya mfano huo hapo kwanza: vifo vya askari waliouawa kila siku vilikuwa vingi mara kumi kuliko katika vile vya Vita Kati ya Raia za Amerika, mara 24 kuliko vifo vya Vita vya Napoleoni, mara 550 kuliko vifo vilivyotokea katika ile Vita ya Makaburu.”

Hata hivyo, Yesu alisema huo ungekuwa tu “mwanzo wa huzuni mbalimbali,” au “wa utungu.” Tafsiri nyingine zinayatafsiri maneno ya Yesu kuwa “mwanzo wa maumivu makali ya kuzaa.” (Jerusalem Bible; New Testament in Modern English ya Phillips) Mwanamke aliye karibu kuzaa anapatwa na maumivu yanayotukia kwa ukali wenye kuzidi kuongezeka. Yanazidi kutokea-tokea baada ya muda mfupi zaidi kadiri wakati unavyoendelea kupita. Vita ya Ulimwengu ya Kwanza na huzuni zayo ilikuwa mwanzo tu wa utungu.

Taabu Kubwa ya Ulimwengu Inaongezeka

Maumivu mengine yenye ukali mwingi zaidi yangefuata muda mfupi tu baada ya kutokea kwa Vita ya Ulimwengu ya Pili. Katika kitabu A Study of War Quincy Wright anaandika kwamba, “Jumla ya vifo vilivyotokana na upigaji vita na magonjwa yenye kuenezwa na vita kuhusiana na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza imekadiriwa kuwa zaidi ya milioni arobaini na vile vinavyohusiana na Vita ya Ulimwengu ya Pili ni zaidi ya milioni sitini. Vifo visivyopungua asilimia 10 katika ustaarabu wa kisasa vinaweza kuhusianishwa na vita moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja.”

Vifo vya raia vilikuwa vingi isivyo kawaida katika vita ya ulimwengu ya pili. Ni kama vile anavyoeleza Profesa Wright: “Kufa-njaa, kupigwa kwa makombora, kunyang’anya watu mali zao, na kuwatia maogopesho kuhusiana na uharibifu wa majiji mazima ni mambo yaliyotumiwa katika Vita ya Ulimwengu ya Pili ili kupinga umati wote wa adui na kuchukua maeneo yao. . . . Mambo yalifikia hatua ya kushambulia uhai wa mataifa mazima ya adui. Kujikaza sana kupata ushindi kulifanya serikali fulani-fulani zifikie hatua ya kuangamiza jumuiya nzima ya watu na haki zayo za umilikaji wa mali ili ziyachukue maeneo yao na kuyakaa.”

Taabu kubwa iliyosababishwa na kutupwa kwa makombora ya moto katika Dresden na Tokyo mwaka wa 1945, ambayo yaliua watu 235,000, ilifunikwa ikawa si kitu kwa kulinganishwa na maogopesho makubwa yaliyoletwa miezi michache baadaye na makombora mawili ya atomi yaliyoangushwa juu ya miji ya Hiroshima na Nagasaki. Maisha yaliyokuwa yakiangamizwa na makumi ya maelfu ya makombora yangeweza sasa kuangamizwa na kombora moja tu. Lakini sumu yenye kuua ya viini vilivyoenezwa hewani na mlipuko wa makombora yaliyoangushwa ndiyo inayoleta uharibifu mkubwa hata zaidi, ambao unaendelea mpaka siku yetu ya leo.

Likiandika habari za lile kombora moja tu la atomi lililoangushwa mjini Hiroshima, gazeti World Press Review la Juni 1982 linasema hivi: “Wale Wapanda Farasi Wanne wa Ufunuo walikuwa wamefunguliwa. Wenye bahati ni wale watu waliokufa katika mashambulizi ya kwanza​—wanaume, wanawake, watoto wa shule, vitoto vyenye nyuso za mviringo, na vitoto vilivyozaliwa juzi karibu 100,000. Wengi wa majeruhi wa ziada 100,000 walikuwa wakifa kwa maumivu makali kutokana na viungo vya mwili vilivyopasuka, kutokana na kuchomwa vibaya sana, au kwa kupatwa na ugonjwa wenye kuwaua polepole wa viini vilivyoenezwa katika hewa na mlipuko.” Maumivu makali ya taabu yakawa yakizidi kupata nguvu.

Amani Inaondolewa Duniani

Mtajo wa wale wale ‘Wapanda Farasi wa Ufunuo’ unapendeza kwa sababu unategemea masimulizi ya Biblia yanayotolewa katika sura ya sita ya kitabu cha Ufunuo. Hapo, mstari wa 4 unasema hivi: “Akatoka farasi mwingine mwekundu sana, na yeye aliyempanda alipewa kuiondoa amani katika nchi, ili watu wauane, naye akapewa upanga mkubwa.” Masimulizi hayo yalingana sana na ile sehemu ya ishara aliyoitoa Yesu juu ya taifa likipigana na taifa na ufalme na ufalme!

Kweli amani imeondolewa duniani. Ingawa wanahistoria wamefanya maandishi ya miaka iliyokuwa ya amani kabla ya mwaka wa 1914, hakujawa na mwaka hata mmoja wa amani tangu wakati huo. Watu walitumainia bure kwamba ile vita ya ulimwengu ya mwisho ingeingiza kipindi cha amani. Kitabu The Violent Peace (Amani Yenye Jeuri) kinasema hivi: “Amani iliyokuja mwaka wa 1945 haikuleta mwisho wa vita kama tulivyokuwa tumetumainia. Tangu wakati huo watu wamepigana katika karibu kila pembe ya dunia​—kutoka Ugiriki mpaka Vietnam ya Kusini, kutoka Kashmir mpaka Kongo​—na ghasia za kupinga serikali waziwazi zinaongezeka kwa wingi katika mataifa yale maskini ya ulimwengu.”

Hivi majuzi Idara ya Serikali ya United States iliripoti kwamba kumekuwako vita vya kimataifa na vya kiraia 130 tangu ilipomalizika Vita ya Ulimwengu ya Pili. “Karibu watu 701,600,000 kati ya idadi ya watu wa ulimwengu wanahusika katika vita vya namna mbalimbali,” linaripoti gazeti Toronto Star la Juni 13,1982. “Hiyo ni karibu mtu mmoja kati ya watu sita katika uso wote wa dunia, na hesabu hiyo inakaribiana sana na hesabu ya watu waliohusika katika kupiga Vita ya Ulimwengu ya Pili kwa njia ya moja kwa moja. Karibu askari 250,000 na raia kufikia 2,000,000 wanakufa katika [vita] hivi kila mwaka.”

“Vita na matetesi ya vita” vinaendelea kuongezeka, bila kupungua. Ni kama vile kitabu The Violent Peace kinavyosema: “Tangu [mwaka wa 1945] hawafanyi tena matangazo ya kwamba watapigana au kukomesha vita. Wao wanapigana tu. Kipindi chetu ni cha jeuri nyingi sana inayofanywa huku ikisingiziwa kwamba kuna amani.”

Je! kutakuwako utungu mwingine duniani pote ukiwa kwa namna ya vita ya ulimwengu ya tatu? “Sisi tunaishi katika ulimwengu unaotangulia vita wala si ulimwengu wa baada ya vita,” anasema Eugene Rostow, mkurugenzi wa Shirika la Uzuiaji wa Ongezeko la Silaha la United States. Hakika mataifa yamejitayarisha kwa ajili ya pigano la namna hiyo! Kwa sasa yanatumia karibu dola 1,000,000 (kama shilingi 13,000,000) kila dakika yakitayarisha silaha. Kati ya dola bilioni 550 zilizotumiwa katika matayarisho ya vita mwaka wa 1981, karibu dola bilioni 110 zilitumiwa kutayarisha silaha za nyukilia. Silaha za nyukilia ambazo zimewekwa akibani sasa zina uwezo wa uharibifu wa makombora ya atomi ulio mara milioni moja kuliko uwezo wa lile kombora lililoangamiza mji wa Hiroshima. Hakika amani imeondolewa duniani.​—Ufunuo 6:4.

Ushuhuda unaohusu vita katika nyakati zetu za kisasa unafanya shauri likatwe hivi: Sisi tunaishi kweli katika “siku za mwisho” za mfumo wa mambo ya sasa.

Hata hivyo Yesu hakutaja vita ya ulimwenguni pote halafu akaachia hapo tu. Yeye alitaja sehemu kadha za ile ishara ambazo zikitukia pamoja zingethibitisha wazi kabisa kwamba tunaishi katika wakati wa ‘kuwapo kwake na wa umalizio wa mfumo wa mambo.’

Sehemu hizo nyingine za ile ishara zitazungumzwa katika matoleo yatakayofuata ya gazeti hili.​—Mathayo 24:3-12; Luka 21:7-11.

[Blabu katika ukurasa wa 6]

“Vifo visivyopungua asilimia 10 katika ustaarabu wa kisasa vinaweza kuhusianishwa na vita moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja”

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Vita vya kimataifa na vya kiraia vinavyozidi 130 vimepigwa tangu mwisho wa Vita ya Ulimwengu ya Pili

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki