Washindi Wajapokabiliwa na Kifo
“Na kwa kushangaza Wanazi, [Mashahidi] pia hawangeweza kumalizwa. Kadiri walivyoonewa zaidi ndivyo walivyopata kuwa na nguvu zaidi, wakiwa wagumu kama almasi katika ukinzani wao. Hitler aliwaingiza katika vita vya kuwamaliza, lakini walidumisha imani yao. . . Maono yao ni jambo muhimu sana kwa wote wanaojifunza namna ya kuokoka chini ya mkazo mkali zaidi. Kwa sababu waliokoka.”—Maneno ya Dkt. Christine King, mwanahistoria, katika jarida Together.
MASHAHIDI WA YEHOVA wapaswa kuonwa katika historia ya karne ya 20 kuwa kikundi cha kidini ambacho kimedhulumiwa na kunyanyaswa zaidi kotekote duniani. Wamechukuliwa kimakosa na mara nyingi kutendwa vibaya kwa sababu tu ya kudumisha kutokuwamo kwao kwa Kikristo na kukataa kwao kujifunza vita au kupigana vita. Kutojiingiza kwao katika mambo yoyote ya kisiasa kumewaletea ghadhabu ya watawala wakatili katika nchi nyingi. Na bado, mmoja wa michango yao kwa historia ya sasa umekuwa ni rekodi yao ya kutokuwamo thabiti na ushikamanifu-madili imara.a
Mwanahistoria Mwingereza Arnold Toynbee aliandika hivi katika 1966: “Katika wakati wetu nchini Ujerumani kumekuwa na Wakristo wafia-imani waliotoa uhai wao badala ya kuabudu Utukuzo wa Taifa ulioenea sana uliowakilishwa huko na mungu-binadamu Adolf Hitler.” Mambo ya hakika yaonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa wengi miongoni mwa wafia-imani hao. Maono fulani yapasa kuonyesha jinsi walivyokabili mnyanyaso na hata kifo kwa sababu ya ushikamanifu wao wa maadili—na jambo hilo halikutokea wakati wa Unazi pekee. Katika sehemu nyingi za dunia, rekodi yao ya ushindi wajapokabiliwa na kifo ni imara na haina kifani.
Masimulizi ya Ananii Grogul wa Ukrainia
“Wazazi wangu walikuja kuwa Mashahidi wa Yehova wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilipokuwa ikiendelea katika 1942, nilipokuwa na miaka 13. Muda mfupi baadaye, baba yangu alikamatwa, akafungwa gerezani, na baadaye akahamishwa kupelekwa katika kambi za Sovieti katika Milima ya Ural. Nilipokuwa na miaka 15, katika 1944, wenye mamlaka wa kijeshi waliniita kwenye utumishi wa kujitayarishia kazi ya jeshi. Kwa vile tayari nilikuwa na imani thabiti kwa Yehova, nilikataa kujifunza vita. Kwa sababu hiyo nilihukumiwa miaka mitano gerezani, nikiwa na umri huo mdogo.
“Ndipo ukaja ule mwaka mgumu sana wa 1950. Nilikamatwa tena na kuhukumiwa kifungo cha kizuizi kwa miaka 25 kwa sababu ya utendaji wangu nikiwa Shahidi. Nilikuwa na miaka 21. Nilikaa katika kambi za kazi ngumu kwa miaka saba na miezi minne. Niliona watu wengi wakifa, wakiwa wamefura mwili kwa sababu ya njaa na kuchoka mno kutokana na kazi ngumu.
Baada ya kifo cha Stalin katika 1953, hali zilianza kubadilika, na katika 1957 wenye mamlaka walinifungulia nikatoka gerezani. Tena nilionja ‘uhuru.’ Lakini wakati huu wakanihamisha mpaka Siberia kwa miaka kumi.”
Kuteswa Kinyama kwa Dada Yangu
“Katika Siberia, niliungana tena na dada yangu wa kimwili, aliyekuwa tayari mgonjwa. Alikuwa amekamatwa majuma mawili kamili baada ya mimi katika 1950. Uchunguzi wa kesi yake uliendeshwa kwa njia isiyo ya kisheria kabisa. Walimfunga katika kifungo cha kukaa pekee na kisha wakaachilia panya wengi katika seli yake. Panya hao waliuma miguu yake na kutambaa juu ya mwili wake. Hatimaye, watesi wake walimlazimisha kusimama katika maji baridi yanayofika kifuani pake huku wakitazama maumivu yake makali. Alihukumiwa miaka 25 gerezani kwa sababu ya utendaji wake wa kuhubiri. Miguu yake yote miwili ilipooza, lakini angeweza kutumia mikono yake. Kwa miaka mitano walimweka katika hospitali ya kambi na hatimaye wakamsahau kana kwamba amekufa. Kisha wakamhamisha na kumpeleka kwa wazazi wetu, waliokuwa wamepelekwa uhamisho wa maisha yote katika Siberia mwaka wa 1951.”
Kurudi Ukrainia na Mnyanyaso Zaidi
“Katika Siberia nilikutana na Nadia, aliyekuja kuwa mke wangu na kuzaa watoto wetu. Hata katika Siberia tuliendelea na kazi ya kuhubiri. Niliaminishwa kazi ya kutokeza na kurudufisha vichapo vya Biblia. Kila usiku, ndugu yangu nami tulikuwa na shughuli nyingi katika chumba cha chini tukirudufisha Mnara wa Mlinzi. Tulikuwa na taipureta mbili na mashine ya kurudufisha ya kujitengenezea. Makao yetu yalipekuliwa mara kwa mara na polisi. Kila wakati hawakufaulu kupata kitu.
“Uhamisho wangu ukaisha. Nikiwa pamoja na familia yangu nikahamia Ukrainia, lakini mnyanyaso ukatufuata. Nilipewa mgawo wa kutumikia nikiwa mwangalizi asafiriye. Ilinibidi nifanye kazi ili kuruzuku familia yangu. Mara nyingi kila mwezi, washiriki wa Polisi wa Siri walikuja mahali pangu pa kazi na kujaribu kunisihi nikane imani yangu. Pindi moja nilihisi msaada wa Yehova kwa njia ya pekee sana. Walinikamata na kunipeleka katika ofisi za Polisi wa Siri katika Kiev, walikoniweka kwa siku sita. Wakati huo wote walijaribu kunishawishi kwa propaganda za kutokuamini kuwapo kwa Mungu. Kwa njia yao ya kutomhofu Mungu, walitoa maelezo juu ya Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vya Watch Tower Society. Mkazo ukawa mwingi sana. Nikiwa bafuni, nilikuwa nikipiga magoti na kububujika machozi, nikimlilia Yehova. Sikumlilia aniachilie huru bali anipe nguvu ya kuvumilia ili nisije nikasaliti ndugu zangu.
“Mkubwa wa polisi alikuja kuniona, na akiketi mbele yangu, akaniuliza kama nilisadiki kabisa kile nilichokuwa nikitetea. Nikamtolea ushahidi mfupi na kujulisha utayari wangu wa kufa kwa ajili ya kweli. Jibu lake lilikuwa: ‘Wewe ni mwenye furaha. Kama tu ningesadiki kuwa hii ndiyo kweli, ningekuwa tayari kukaa katika jela kwa miaka 3 au 5 na hata kusimama kwa mguu mmoja gerezani kwa miaka 60.’ Akiwa ameketi, akafikiri akiwa kimya kwa muda mfupi na kisha akaendelea kusema: ‘Lahusu uhai wa milele. Je! waweza kuwazia uhai wa milele wamaanisha nini hasa?’ Baada ya kunyamaza kwa muda mfupi akasema: ‘Enda nyumbani!’ Maneno hayo yalinipa nguvu nisiyotarajia. Sikuhisi njaa tena. Nilitaka tu kuondoka. Nilikuwa na uhakika wa kwamba Yehova ndiye aliyenipa nguvu.
“Katika miaka ya karibuni mambo yamebadilika katika ile iliyokuwa Muungano wa Sovieti. Sasa kuna vichapo vingi sana vya Biblia. Tunaweza kuhudhuria makusanyiko ya mzunguko na mikusanyiko ya wilaya, na tunashiriki katika njia zote za utendaji wa kuhubiri, kutia ndani huduma ya nyumba kwa nyumba. Kwa kweli, Yehova ametupatia ushindi yajapokuwa majaribu mengi!”
Ushikamanifu-Maadili Wajaribiwa Katika Afrika
Wakati wa miaka ya mwisho-mwisho ya 1960, Nigeria ilikumbwa na vita ya wenyewe kwa wenyewe yenye uharibifu mkubwa sana. Wakikabiliwa na hali ya wanajeshi wengi kuuawa, wanajeshi wa jimbo lililojitenga, lililokuja kuitwa Biafra, waliingiza kinguvu vijana katika jeshi lao. Kwa kuwa Mashahidi wa Yehova hawaungi mkono upande wowote wa kisiasa na wao hukataa kujihusisha katika vita, Mashahidi wengi katika Biafra walisakwa, wakatendewa kikatili, na kuuawa. Mmoja wa Mashahidi asema: “Tulikuwa kama panya. Ilitubidi tujifiche wakati wowote tuliposikia wanajeshi wakija.” Mara nyingi hakukuwa na wakati wa kujificha.
Asubuhi moja ya Ijumaa katika 1968, Philip, mhudumu wa wakati wote mwenye miaka 32, alikuwa katika kijiji cha Umuimo akihubiria mtu mmoja mzee-mzee wakati wanajeshi wa Biafra walipoingia uani katika jitihada ya kusajili wanajeshi.
“Unafanya nini?” akataka kujua kiongozi wa kikundi hicho. Philip akajibu kwamba alikuwa akiongea juu ya Ufalme wa Yehova unaokuja.
“Huu si wakati wa kuhubiri!” mwanajeshi mwingine akasema kwa sauti kubwa. “Huu ni wakati wa vita, na hatutaki kuona watu wanaojiweza wakizurura bila jambo la kufanya.” Kisha wanajeshi hao wakamvua Philip nguo na kumwacha akiwa uchi, wakafunga mikono yake, na kwenda naye. Israel, mzee Mkristo mwenye miaka 43 pia hakuweza kujificha. Alishikwa alipokuwa akitayarishia watoto wake chakula. Kufikia saa 8:00 alasiri, wanajeshi hao walikuwa wamekamata zaidi ya watu mia moja. Walilazimisha mateka wao kukimbia kilometa 25 kwenda kwenye kambi ya kijeshi katika Umuacha Mgbedeala. Wowote waliokimbia polepole walichapwa kiboko.
Israel aliambiwa kwamba angebeba bunduki kubwa ya kumimina risasi; na Philip angepewa mazoezi ya kutumia bunduki ndogo ya kumimina risasi. Walipoeleza kwamba hawangeweza kujiunga na jeshi kwa sababu Yehova anakataza jambo hilo, kamanda akaamuru kwamba wafungiwe. Saa 10:00 alasiri, wote walioandikishwa kwa nguvu, kutia na wale waliokuwa wamefungiwa, waliamriwa wapige foleni. Kisha wanajeshi hao wakaomba kila mtu atie sahihi karatasi iliyoonyesha kwamba anakubali kujiunga na jeshi. Ulipofika wakati wake wa kutia sahihi, Philip alirejezea maneno ya 2 Timotheo 2:3, 4 na kumwambia kamanda huyo: “Tayari mimi ni ‘askari mwema wa Kristo.’ Siwezi kupiga vita kwa ajili ya Kristo na wakati uleule nipige vita kwa ajili ya mtu mwingine. Nikifanya hivyo, Kristo ataniona kuwa msaliti.” Yule kamanda akampiga kichwani akisema: “Kuwekwa kwako kuwa mwanajeshi wa Kristo kumekomeshwa! Wewe sasa ni mwanajeshi wa Biafra.”
Philip akajibu: “Yesu hajanieleza kwamba kuwekwa kwangu nikiwa mwanajeshi wake kumekomeshwa, na kuwekwa kwangu kwaendelea mpaka nijulishwe.” Kwa hayo, wanajeshi hao walinyanyua Philip na Israel hewani na kuwaangusha chini. Wakiwa wamepigwa na bumbuazi huku wakitokwa na damu machoni, puani, na vinywani, hao wawili walikokotwa mbali.
Mbele ya Kikosi cha Kufyatua Risasi
Baadaye siku hiyo, Israel na Philip walijikuta mbele ya kikosi cha kufyatua risasi. Lakini wanajeshi hao hawakuwapiga risasi. Badala ya kufanya hivyo, waliwapiga kwa ngumi na kwa sehemu za nyuma za bunduki. Kisha kamanda wa kambi akaamua kuwachapa mpaka wafe. Aliwapa wanajeshi 24 mgawo huo. Sita wangemchapa Philip, na wengine sita wangemchapa Israel. Wanajeshi wengine 12 wangeleta viboko zaidi na kungojea zamu yao hao wengine wakichoka.
Philip na Israel walifungwa mikono na miguu. Israel aeleza: “Sijui tulipokea viboko vingapi usiku huo. Mwanajeshi mmoja alipochoka, mwingine alichukua mahali pake. Waliendelea kutuchapa muda mrefu baada ya sisi kupoteza ufahamu.” Asema Philip: “Mathayo 24:13, linalosema juu ya kuvumilia mpaka mwisho likaja akilini wakati wa kuteswa, na hilo lilinipa nguvu. Nilihisi uchungu wa kupigwa kwa sekunde chache tu. Ilionekana kama kwamba Yehova alikuwa ametuma mmoja wa malaika zake atusaidie, kama alivyofanya wakati wa Danieli. Kama si hivyo, hatungeokoka usiku huo mbaya sana.”
Wanajeshi hao walipomaliza, Israel na Philip walidhaniwa kuwa wamekufa. Mvua ilikuwa ikinyesha. Ilikuwa mpaka kesho asubuhi ndipo Wakristo hao wawili walipopata ufahamu. Wanajeshi walipoona kwamba bado walikuwa wangali hai, waliwaburuta na kuwarudisha ndani ya chumba walimofungiwa.
“Tayari Mnanuka Kama Maiti”
Kuchapwa kwao kuliwaacha wakiwa wekundu na wenye majeraha, huku majeraha yakijaa katika miili yao yote. Israel akumbuka: “Hatukuruhusiwa kuosha majeraha yetu. Baada ya siku kadhaa nzi walifurahia mlo wa mwili wetu bila kukoma. Kwa sababu ya mateso hayo, hatungeweza kula. Ilikuwa ni baada ya juma moja kwamba tungeweza kula kitu kingine mbali na kunywa maji.”
Kila asubuhi wanajeshi waliwachapa kwa kiboko—viboko 24 kila mmoja. Kwa ukatili, wanajeshi hao waliyaita mapigo hayo “kiamsha-kinywa” au “chai moto ya asubuhi.” Kila adhuhuri, wanajeshi hao waliwaleta kiwanjani wakabili jua kali mpaka saa 7:00 adhuhuri. Baada ya kuteswa hivyo kwa siku chache, kamanda aliwaita na kuwauliza kama wamebadili msimamo wao. Walisema la.
“Mtakufa katika seli yenu,” akasema kamanda huyo. “Kwa kweli, tayari mnanuka kama maiti.”
Philip akajibu hivi: “Hata tukifa, twajua kwamba Kristo tunayepigania, atatufufua.”
Waliokokaje wakati huo mbaya sana? Israel asema hivi: “Philip nami tulitiana moyo wakati wa jaribu letu lote. Mwanzoni nilimwambia, ‘usiogope. Hata hali iweje, Yehova atatusaidia. Kwa habari yangu, hakuna kitakachonifanya nijiunge na jeshi. Hata kama ni lazima nife, sitashika bunduki kwa mikono hii yangu.’” Philip alisema kwamba alikuwa na azimio ilo hilo. Wakiwa pamoja walikumbuka na kuzungumzia maandiko tofauti-tofauti.
Kamanda mpya aliamua kuhamisha walioandikishwa kinguvu karibu 100 kwenda Ibema, kambi ya mazoezi katika eneo la Mbano ambayo sasa ni eneo la Jimbo la Imo. Israel aeleza yale yaliyofuata kutukia: “Lori kubwa lilikuwa tayari, na walioandikishwa kinguvu wote walikuwa ndani. Mke wangu June, aliwakimbilia wanajeshi na kuwasihi kijasiri kwamba tusichukuliwe. Walipokataa kumsikiliza, alipiga magoti kando ya lori hilo, akasali, na kumalizia kwa kusema amen kwa sauti kubwa. Basi lori likaondoka.”
Twakutana na Mwanajeshi wa Kukodiwa Mwenye Huruma
Lori la Jeshi lilifika kambi ya Ibema alasiri iliyofuata. Mtu aliyeonekana kuwa kiongozi hapo alikuwa mwanajeshi kutoka Israeli. Alipoona jinsi Philip na Israel walivyokuwa wamepigwa na kudhoofika sana, aliwakaribia na kuwauliza ni kwa nini walikuwa katika hali hiyo mbaya sana. Walieleza kwamba wao ni Mashahidi wa Yehova na walikuwa wamekataa mazoezi ya kijeshi. Akiwa na hasira, aliwageukia maofisa wa jeshi waliokuwa hapo, “Kwa hakika Biafra itashindwa katika vita hii,” akasema. “Nchi yoyote inayopigana vita na ambayo inanyanyasa Mashahidi wa Yehova hushindwa bila shaka. Msiandikishe kinguvu Mashahidi wa Yehova. Shahidi akikubali kwenda vitani, ni sawa. Lakini akikataa, mwacheni.”
Daktari wa kambi aliuliza kama Mashahidi hao wawili walikuwa wamechanjwa na kupokea cheti cha tiba cha kuonyesha kwamba wanafaa vita. Kwa sababu hawakuwa wamekipata, yule mwanajeshi wa kukodiwa alikataa wasajaliwa wote na kuamuru kwamba warudishwe Umuacha.
“Enendeni Zenu, Mkamtumikie Mungu Wenu”
Baadaye, mke wa Israel na mama ya Philip waliamua kutembelea kambi ya Umuacha wakitumaini kupata habari yoyote. Walipokaribia, walisikia msukosuko katika kambi. Kwenye malango, mlinzi alisema: “Shahidi wa Yehova! Sala yako imejibiwa. Kikundi kilichochukuliwa siku tatu zilizopita kimerudishwa.”
Siku iyo hiyo, Philip na Israel walifunguliwa kutoka kambini. Kamanda akamwambia June: “Je! wajua kwamba sala uliyotoa ndiyo iliyofanya tusifaulu?” Ndipo akawaeleza Israel na Philip hivi: “Enendeni zenu, mkamtumikie Mungu wenu, na mwendelee kushika ushikamanifu wenu wa maadili kwa Yehova.”
Kwa habari ya Israel na Philip, walipona na wakaendelea na utendaji wao wa Kikristo. Baada ya vita, Israel aliingia katika huduma ya kuhubiri wakati wote kwa miaka miwili na ameendelea kutumikia akiwa mzee Mkristo. Phillip alitumikia akiwa mwangalizi asafiriye kwa miaka kumi na bado anatumikia katika kazi ya kuhubiri wakati wote. Yeye pia ni mzee wa kundi.
Kukataa Kuchangia Silaha
Zebulan Nxumalo na Polite Mogane ni wahudumu wawili wachanga katika Afrika Kusi-ni. Zebulan aeleza: “Jumapili moja asubuhi, kikundi kimoja cha watu kilikuja nyumbani mwetu na kudai Rand 20 (karibu dola 7 za U.S.) za kununua silaha. Kwa heshima tukawauliza warudi jioni hiyo, kwa sababu ratiba yetu ya Jumapili ilikuwa yenye shughuli nyingi mno tusiweze kuzungumzia jambo hilo wakati uo huo. Kwa kushangaza walikubali. Jioni hiyo, watu 15 walikuja. Sura zao zilionyesha kwamba walichukua jambo hilo kwa uzito sana. Baada ya sisi kujitambulisha kwa heshima, tukawauliza walitaka nini. Walisema kwamba walihitaji pesa za kununua silaha kubwa na zilizo bora zaidi wazitumie kukabiliana na kikundi cha kisiasa cha upinzani.
“Niliwauliza hivi: ‘Je! inawezekana kuuzima moto kwa petroli?’
“‘La, haiwezekani,’ wakajibu.
“Tukawaeleza kwamba kwa njia iyo hiyo, ujeuri ungeendeleza tu ujeuri na matendo ya kulipiza kisasi.
“Maneno hayo yalionekana kuudhi baadhi ya watu hao waliokuwapo. Dai lao likawa sasa tisho kubwa. ‘Mazungumzo haya yanapoteza wakati,’ wakasema kwa ukali. ‘Mchango huu wa lazima ni sharti ulipwe. Ama mlipe ama mkione cha-mtema-kuni!
“Kufikia wakati huo,” akumbuka Zebulan, “ambapo mambo yalikuwa yanaanza kuchacha, kiongozi wao akaingia. Alitaka kujua tatizo lilikuwa nini. Tukaeleza msimamo wetu, naye akasikiliza kwa makini. Tulitumia ujitoaji wao kwa itikadi zao za kisiasa kuwa kielezi. Tuliwauliza wangetazamia mwanajeshi aliyezoezwa kutoka chama chao aitikieje akikamatwa na kulazimishwa abadili msimamo wake. Walisema kwamba mtu kama huyo apaswa kuwa tayari kufia itikadi zake. Walitabasamu tulipowashukuru kwa jibu lao; hawakung’amua kwamba walikuwa wametupatia fursa nzuri ya kueleza msimamo wetu. Tulieleza kwamba sisi ni tofauti na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo. Tukiwa waungaji-mkono wa Ufalme wa Mungu, ‘katiba’ yetu inategemea Biblia, inayoshutumu aina zote za uuaji. Kwa sababu hiyo hatuwezi kutoa mchango hata wa senti moja wa kununua silaha.
“Kufikia wakati huu, mazungumzo yalipokuwa yakifikia upeo, watu wengi zaidi walikuwa wameingia nyumbani mwetu, hivi kwamba sasa tulikuwa tunasema mbele ya wasikilizaji wengi. Hawakujua kwamba tulikuwa tunasali kwa bidii kwamba mazungumzo hayo yawe na matokeo mazuri.
“Baada ya kujulisha wazi msimamo wetu, ukimya wa muda mrefu ukafuata. Hatimaye kiongozi wao akaeleza kikundi hicho hivi: ‘Wangwana, naelewa msimamo wa watu hawa. Kama tungetaka pesa za kujenga makao ya kutunzia wazee-wazee, au kama mmoja wa majirani wetu angehitaji pesa za kwenda hospitali, watu hawa wangetoa mchango kwa moyo wote. Lakini hawawezi kutupatia pesa za kuua. Mimi binafsi sipingi itikadi zao.’
“Basi, wote wakasimama. tukasalimiana na kuwashukuru kwa saburi yao. Jambo lililoanza kwa hali yenye kutisha ambalo labda lingetugharimu uhai wetu liliisha kwa ushindi mkubwa.”
Umati Wenye Ghasia Unaoongozwa na Makasisi
Kama ilivyosimuliwa na Shahidi Mpolandi Jerzy Kulesza:
“Kwa habari ya bidii na kutanguliza Ufalme, baba yangu Aleksander Kulesza alikuwa mfano mzuri wa kufuata. Kwake, utumishi wa shambani, mikutano ya Kikristo, na funzo la pekee na la familia yalikuwa mambo matakatifu. Wala dhoruba ya theluji wala baridi kali wala upepo mkali wala joto hazingeweza kumzuia. Wakati wa kipupwe alikuwa akivaa vifaa vya kuteleza juu ya theluji, angebeba mfuko wa vichapo vya Biblia, na kwenda katika maeneo ya mbali ya Polandi kwa siku kadhaa. Mara nyingi alikabili hatari nyingi, kutia ndani vikundi vyenye jeuri vya kupigana kwa kuvizia.
Nyakati nyingine makasisi walichochea upinzani dhidi ya Mashahidi, wakichochea umati wenye ghasia. Walikuwa wakiwadhihaki, kuwatupia mawe, au kuwapiga. Lakini walirudi nyumbani, wakiwa na furaha kwa kustahimili matukano kwa ajili ya Kristo.
“Wakati wa miaka hiyo ya kwanza ya baada ya Vita ya Ulimwengu 2, wenye mamlaka walishindwa kudumisha amani na utengamano nchini. Kulikuwa na ghasia na uharibifu. Polisi wa kawaida na wa siri walitawala wakati wa mchana, huku vikundi vya kupigana kwa kuvizia na magenge kadhaa wakitawala usiku. Wizi na unyang’anyi wa kutumia nguvu ukaenea sana, na mara kwa mara watu waliuawa. Mashahidi wa Yehova wasiokuwa na kinga walikuwa shabaha rahisi, hasa kwa vile baadhi ya vikundi hivyo vyenye kuongozwa na makasisi vililenga Mashahidi. Walitetea uvamizi wa nyumba zetu kwa kusingizia kwamba walikuwa wakitetea imani ya Kikatoliki ya mababu wao. Katika pindi kama hizo, walivunja madirisha, waliiba mifugo, na kuharibu mavazi, chakula, na vichapo. Walitupa Biblia nyingi ndani ya kisima.”
Kufia-Imani Kusikotarajiwa
“Siku moja katika Juni 1946, kabla hatujakutana ili kwenda kwa baiskeli katika eneo fulani la mbali, ndugu kijana, Kazimierz Kạdziela, alitutembelea na kuzungumza na baba yangu kwa sauti ya chini. Baba yangu alituambia twende katika eneo, lakini hakuja na sisi, jambo lililotushangaza. Tulisikia sababu baadaye. Tuliporudi nyumbani, tulisikia kwamba familia ya Kạdziela ilipigwa kikatili usiku huo uliopita, kwa hiyo baba yangu alikuwa ameenda kutunza akina ndugu na dada waliokuwa wamejeruhiwa sana.
“Baadaye nilipoingia chumbani walimokuwa wamelala, niliyoona yalinifanya nitokwe na machozi. Damu ilitapakaa kwenye kuta na darini. Watu waliofungwa kwa bandeji nyingi walikuwa wamelala vitandani, wakiwa wamebadilika rangi kwa kupigwa sana, walikuwa wamefura mwili, na kuvunjika mbavu na mikono na miguu. Ilikuwa vigumu kuwatambua. Dada Kạdziela, mama ya familia hiyo, alipigwa vibaya sana. Baba yangu alikuwa akiwasaidia, na kabla hajaondoka alitamka maneno yenye umaana sana: ‘Oh, Mungu wangu, mimi ni mtu mwenye afya nzuri na mwenye uwezo, na sijapata kuwa na pendeleo la kuteseka kwa ajili yako. Kwa nini jambo hilo limpate dada huyu mzee-mzee?’ Hakujua ni jambo gani lililomngojea.
“Jua lilipokuwa likishuka, tulirudi nyumbani kwetu iliyokuwa umbali wa maili mbili [kilometa 3]. Kikundi cha watu 50 hivi kilikuwa kimezingira nyumba yetu. Familia ya Wincenciuk ililetwa pia, kwa hiyo tulikuwa watu tisa. Kila mmoja wetu aliulizwa swali hili: ‘Je! wewe ni Shahidi wa Yehova?’ Tulipojibu ndiyo, tulipigwa. Kisha, wakipokezana zamu wawili kati ya watu hao wakatili walimpiga baba yangu huku wakimwuliza kama angeacha kusoma Biblia na kuihubiri. Walitaka kujua kama angeenda kanisani na kutubu dhambi zake. Walimdhihaki, wakisema: ‘Leo tutakutawaza uwe askofu.’ Baba yangu hakusema lolote, hata hakulia. Alivumilia mateso yao kwa ukimya kama kondoo. Asubuhi, dakika 15 hivi baada ya watesi hao wa kidini kuondoka, alikufa akiwa amepigwa sana. Lakini kabla ya wao kuondoka, walinichagua nipigwe. Wakati huo nilikuwa na miaka 17. Nilipokuwa nikipigwa, nilipoteza fahamu mara nyingi. Mwili wangu ulikuwa mweusi kutokea kiuno hadi juu kutokana na mapigo. Tulitendewa vibaya kwa muda wa saa sita. Kwa sababu tu ya kuwa Mashahidi wa Yehova!”
Utegemezo wa Mke Mwaminifu
“Nilikuwa miongoni mwa kikundi cha Mashahidi 22 waliokuwa wamewekwa kwa miezi miwili katika seli yenye giza ya ukubwa wa futi 100 za mraba [meta 10 za mraba]. Mwishoni mwa wakati huo, ugavi wa chakula chetu ulipunguzwa. Kila siku, tulipewa kipande kidogo cha mkate na kikombe kidogo cha kahawa chungu. Iliwezekana kulala chini kwenye simiti iliyokuwa baridi wakati tu mmoja alipoondolewa kwenda kuhojiwa wakati wa usiku.
“Nilifungwa gerezani kwa ajili ya utendaji wa Kikristo mara tano, jumla ya miaka minane. Nilitendewa kama mfungwa wa pekee. Kulikuwa na taarifa katika rekodi yangu ya binafsi kwamba: ‘Umkasirishe Kulesza sana mpaka apoteze kabisa tamaa yake ya kurudia utendaji wake.’ Hata hivyo, kila wakati nilipoachiliwa, nilijitoa kwa ajili ya utumishi wa Kikristo. Wenye mamlaka pia walifanya maisha yawe magumu kwa mke wangu Urszula, mabinti wetu wawili wachanga. Kwa mfano, kwa miaka kumi ofisa wa sheria alikuwa akinyakua sehemu ya mshahara wa mke wangu aliojipatia kwa jasho. Hiyo ilisemwa kuwa kodi juu yangu kwa sababu nilikuwa nikihariri vichapo vya Biblia vilivyopigwa marufuku. Tulinyang’anywa kila kitu isipokuwa vile vitu vilivyoonwa kuwa vya lazima maishani. Ninamshukuru Yehova kwa ajili ya mke wangu mjasiri, aliyevumilia kwa saburi pamoja nami mateso hayo yote na ambaye sikuzote alikuwa utegemezo thabiti kwangu.
“Tumeona ushindi wa kiroho hapa Polandi; sasa tuna ofisi ya tawi halali ya Watch Tower Society katika Nadarzyn, karibu na Warsaw. Baada ya miaka mingi ya mnyanyaso, sasa kuna Mashahidi zaidi ya 108,000, wakishirikiana na makundi 1,348.”
Kwa Nini Kuna Wafia-Imani Wengi Sana Hivyo?
Rekodi ya ushikamanifu-maadili wa Mashahidi wa Yehova katika karne hii ya 20 yaweza kihalisi kujaza mabuku mengi—maelfu wamekufa wakiwa wafia-imani au wamefungwa gerezani na kuteswa kinyama, kulalwa kinguvu, na kutekwa, katika nchi kama vile Malawi na Msumbiji, katika Uhispania chini ya Ufashisti, katika Ulaya chini ya Unazi, katika Ulaya ya Mashariki chini ya Ukomunisti, na katika United States wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Swali lazuka, Kwa nini? Ni kwa sababu viongozi wagumu wa kisiasa na kidini wamekuwa hawataki kustahi dhamiri zilizozoezwa kwa Biblia za Wakristo wanyoofu wanaokataa kujifunza kuua na ambao hawahusiki katika utendaji wowote wa kisiasa. Ni kama vile Yesu alivyosema ingetukia, kama inavyorekodiwa katika Yohana 15:17-19: “Haya nawaamuru ninyi, mpate kupendana. Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia.”
Mnyanyaso huo wote ujapotokea ulimwenguni pote, Mashahidi wa Yehova wameongezeka—kutoka 126,000 katika nchi 54 katika 1943 hadi kufikia karibu 4,500,000 katika nchi 229 katika 1993. Wamepata ushindi wajapokabiliwa na kifo. Wameazimia kuendelea na kazi yao ya pekee ya kufundisha ya kutangaza habari njema za Ufalme mpaka Yehova aamuru mwisho wa kazi hiyo.—Isaya 6:11, 12; Mathayo 24:14; Marko 13:10.
[Maelezo ya Chini]
a Ushikamanifu-maadili ni “kushikamana kabisa na kanuni za adili au mwenendo.”—The American Heritage Dictionary, Toleo la Tatu.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 6]
Kufia-Imani Katika Ujerumani
AUGUST DICKMANN alikuwa na miaka 23 wakati kiongozi wa polisi wa SS Heinrich Himmler alipoamuru apigwe risasi mbele ya Mashahidi wengine katika kambi ya mateso ya Sachsenhausen. Gustav Auschner, aliyejionea tukio hilo, aliripoti: “Walimpiga risasi Ndugu Dickmann na kutueleza kwamba sisi sote tungepigwa risasi kama hatungetia sahihi taarifa ya kukana imani yetu. Tungepelekwa katika shimo la mchanga tukiwa watu 30 au 40 kwa wakati mmoja, na sisi sote kupigwa risasi. Siku iliyofuata, polisi wa SS walituletea kila mmoja wetu kikaratasi cha kutia sahihi au tukikataa tupigwe risasi. Kama tu ungeona nyuso zao zenye huzuni walipoenda bila hata sahihi moja. Walitumaini kutuogofya kwa mauaji ya hadharani. Lakini tuliogopa zaidi kumkasirisha Yehova kushinda risasi zao. Hawakuwapiga risasi wengine wetu hadharani tena.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]
Kutoa Uhai
NYAKATI nyingine, ushindi ujapokabiliwa na kifo huenda ukahusisha kutoa uhai. Barua iliyopokewa kutoka Kundi la Nseleni, katika sehemu ya kaskazini mwa Mkoa wa Natal wa Afrika Kusini, yaeleza tukio lenye msiba: “Tunawaandikia barua hii kuwajulisha juu ya kifo cha ndugu yetu mpendwa Moses Nyamussua. Alikuwa na kazi ya kuchomelea na kurekebisha magari. Katika pindi moja aliulizwa na kikundi kimoja cha kisiasa achomelee bunduki zao za kutengenezwa nyumbani, jambo alilolikataa. Kisha katika tarehe 16 ya Februari, 1992, kikundi hicho kilikuwa na mkutano wa kisiasa, ambapo kilipigana na kikundi cha upinzani. Jioni ya siku iyo hiyo walipokuwa wakirudi kutoka vitani, walikutana na ndugu huyo akienda madukani. Hapo walimwua kwa mikuki yao. Sababu yao ilikuwa ni nini? ‘Ulikataa kuchomelea bunduki zetu, na sasa wenzetu wamekufa vitani.’
“Jambo hilo limeshtua sana ndugu zetu,” asema Ndugu Dumakude, mwandishi wa kundi. “Lakini” yeye aongezea, “tutaendelea na huduma yetu.”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 11]
Kufia-Imani Katika Polandi
KATIKA 1944, wakati majeshi ya Ujerumani yalipokuwa yakiondoka kwa haraka na mapigano yalikuwa yakikaribia mji mmoja katika sehemu ya mashariki ya Polandi, wenye mamlaka wa majeshi waliotwaa eneo hilo walilazimisha raia wachimbe mitaro ya kuzuia vifaru vya vita. Mashahidi wa Yehova walikataa kushiriki. Stefan Kieryło, Shahidi mchanga—aliyebatizwa miezi miwili tu iliyopita—alilazimishwa kufanya kazi katika kikundi fulani cha kazi lakini akachukua msimamo wa ujasiri wa kutokuwamo. Hatua kadhaa zilichukuliwa ili kuvunja ushikamanifu wake wa maadili.
Walimfunga akiwa uchi kwenye mti katika sehemu ya maji-maji ili aumwe na wadudu. Alivumilia hilo na mateso mengine, kwa hiyo waliachana naye. Hata hivyo, wakati ofisa mmoja wa cheo cha juu alipokagua kikundi hicho, aliambiwa kwamba kulikuwa na mtu ambaye kwa vyovyote vile hangetii amri yake. Stefan aliamriwa mara tatu achimbe mtaro. Hata alikataa kuchukua kolego ya kuondoa mchanga. Alipigwa risasi akafa. Mamia waliokuwa wakitazama walimjua binafsi. Kufia-Imani kwake kukawa ushahidi mkubwa kwa nguvu nyingi ambazo Yehova aweza kuandaa.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ananii Grogul
[Picha katika ukurasa wa 10]
Jerzy Kulesza